Friday, January 18, 2013

My article for newspaper: Jinsi ya kupamba kwa vioo


Jinsi ya kupamba  nyumba yako kwa kutumia vioo

Kwa uchache kila binadamu anapenda vioo. Huenda unajiuliza kama kuna sehemu nyumbani kwako ambayo hupaswi kuweka kioo. Kupata jibu la swali hili kwanza jiulize ni nini kinachooonekana  kwenye kioo hicho. Ni kitu ambacho unakipenda zaidi? Kama una kioo kinachotazamana na kabati lenye mrundikano wa vitabu basi ukiangalia kwenye kioo hicho unaona makabati mawili yenye mrundikano wa vitabu! Na vile vile kioo kinachotazamana na picha nzuri kitakuonyesha picha mbili nzuri.

Vioo vinaweza kufanya mwanga wa nje uje ndani na kuleta mng’ao ndani ya nyumba. Weka kioo kitazamane na dirisha na mara moja mahali panafunguka. Kioo pia kinaweza kusaidia kufanya sehemu nyembamba kuonekana pana. Weka kioo kwa jinsi ambayo kitanasa mwanga wa asili kutokea dirishani; kwa hiyo mwanga utadunda kurudi chumbani. Hii ni dondoo muhimu  kwa mapambo ya ndani kwa vyumba vyenye mwanga hafifu.

Sehemu mojawapo ya kuepuka vioo ni chumba cha chakula. Sijui yeyote ambaye angependa kujiangalia kwenye kioo wakati anakula. Mazingira ya nyumbani yawe yanafanikisha malengo yako. Chochote kinachokufanya usijisikie vizuri hakisaidii kufanikisha malengo hayo.

Swala la vioo kwenye chumba cha kulala ni la mtu binafsi.  Ingawa vioo ni muhimu kwenye chuma hiki ila sio vitazamane na kitanda. Ukubwa na mahali pa kuweka ni vitu muhimu vya kuzingatia. Ukuta uliotundikwa kioo kwenye chumba cha kulala mara nyingine unaweza kuondoa mazingira ya hisia kuwa chumba cha kulala ni kama mahali patakatifu. Ni nani anapenda kujiona sehemu kubwa ya mwili wake? Jaribu kufunika vioo vikubwa usiku ili kuleta usingizi mwororo.

Watoto ni wadadisi wa mazingira yao. Mara nyingi wanaogopeshwa na vivuli wanavyoona kwenye vioo usiku. Watoto wengi wanaogopa kuwa kwenye vyumba vyao hasa usiku kwa ajili ya vioo. Mara chache kufunika vioo vyote usiku inasaidia, vinginevyo ni vyema kuondoa vioo kwenye kuta za vyumba vya watoto na kuvitundika kwa ndani ya milango ya makabati ya nguo.

Vioo bafuni ni kawaida sana na vina kazi kwa hivyo watu wengi wala hawafikirii kama ni mapambo ya ndani. Hata hivyo vioo vinaweza kuongeza mapambo ya chumba chochote. Vioo vikubwa vinaweza kuwa vizito zaidi; vitundikwe kwa uangalifu.

Kuweka ama kutoweka kioo kitazamane na mlango wa mbele ni swali ambalo watu wengi wanajiuliza. Baadhi wanafikiri kuwa kioo kwenye ukuta unaotazamana na mlango wa mbele kinawachanganya wageni wanaokutembelea njia ya kuelekea; kwa hivyo watu hawa hupendelea kutundika picha kubwa na kuweka kioo upande mwingine wa ukuta ila sio kitazamane na mlango wa mbele. Kama utapenda kuweka kioo zingatia urefu wa yeyote aliyeko ndani ya nyumba yako na pia mgeni wako.

Cheki kuona kuwa vioo vyote ndani ya nyumba yako vimetundikwa katika urefu sahihi. Kioo kitundikwe kwa jinsi ambayo kichwa cha kila mtu ndani ya nyumba kitaonekana. (Watoto wadogo wanaweza kuwa na vioo kwenye vyumba vyao vya kucheza ambavyo vimetundikwa kwa urefu sahihi kuendana na wao.) Sio afya na hujisikii vizuri ukijiangalia kwenye kioo na kuona sehemu ya kichwa chako imekatika ama kichwa chote hakionekani kabisa. Watu wengi pia wanatundika vipaneli vya vioo vilivyoko kwenye fremu moja ambapo inakuwa ngumu kujiona kivuli kilichokamilika badala yake unajiona vipande vipande. Kama vile isivyo poa kujiona sehemu ya kichwa ikiwa imekatwa vile vile haipendezi kujiona vipande vipande. Kama una fremu ya vioo vya namna hii basi itundike itazamane na dirisha ambapo italeta hisia ya kuwa kama nayo ni dirisha la ukweli.

Kioo chenye ufa au kipande maeneo ya kati kinachokosekana kitakupa hisia ya wewe kuwa na ufa au chochote unachokiona kwenye kioo hicho. Unaweza kupenda kioo cha sanaa fulani lakini kama kivuli unachokiona  hakionekani vizuri basi hicho hakifai.
Tundika mfululizo wa vioo vitatu ama vitano vyenye urefu sawa, vyembamba kufanya ukuta mfupi kuonekana mrefu. Mfululizo huu unatengeneza mtindo wa kuvutia kwa kuonyesha sehemu tu ya chumba badala ya picha nzima. Kwa mtindo huu chagua ukuta ambao haupokei mwanga wa jua wa moja kwa moja ili kuepuka chumba kung’aa sana.

Yote kwa yote nia inachukua sehemu kubwa katika kupamba kwa vioo. Fikiria kabla ya kutundika kioo. Kwa nini unakitundika hapo? Ni nini kinaenda kuakisi. Kama vikiwekwa kwa mwamko na nia, vioo vinaweza kuwa mapambo mazuri sana ya nyumba yako.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 200023

Thursday, January 10, 2013

furahisha genge

kati ya hizi cover 2 nani kakutumbuiza?...

Wednesday, January 9, 2013

My article for newspaper: Nyumba yenye mpangilio


Jinsi ya kuwa na mpangilio na kuondoa mlundikano wa vitu katika nyumba yako

Unapohitaji kitu na ukakifuata mahali kinapotakiwa kiwe usipokikuta hapo unaweza kujisikia hasira, kuchanganyikiwa na hata kama ni katika uzalishaji ukapungua.  Hutakiwi kuwa mtaalamu wa mpangilio wa vitu ili kuweza kuwa na mipangilio mizuri zaidi mwaka huu. Haijalishi ni mpangilio kwenye kabati lako la nguo, chumba cha kulala, meza yako ya ofsini au hata kwenye akaunti yako ya barua pepe. Utajisikia vizuri utakapoweza kuchambua na kuweka vitu kwenye mpangilio.

Wengi wetu tunashawishiwa na vitu, matukio na watu ambao tuko karibu nao kwa hiyo inaleta mantiki kabisa kuanza kuweka mpangilio na kuondoa mlundikano kwenye chumba chako cha kulala. Ondoa vitu vyote ambavyo kwakweli havihusiki kwenye chumba hiki kwa mfano vifaa vya mazoezi, vitu vya ofisini na kadhalika. Usisahau kuondoa mlundikano mvunguni.

Weka mpangilio kwenye kabati lako la nguo.  Hatua ya kwanza ni kuondoa kila kitu. Hapo ndio utakapoweza kuona una nini. Vitu kwenye kabati lako hili vitakuwa kwenye makundi manne: vya kubaki, vya kugawa, vya kutupa (takataka) na vya kuhamishia eneo lingine yaani vile ambavyo havitakiwi kuwa kwenye kabati la nguo. Andaa maboksi na raki za viatu, na usisahau mifuko ya plastiki kwa ajili ya kuwekea vitu vya kugawa. Kuwa mkweli, je ni kweli kuwa unahitaji na kupenda kila kitu? Kama nguo, kiatu ama kitupio hujakiona, hujakihitaji au hujakivaa ndani ya  mwaka mmoja basi kitupilie mbali.

Kila nguo iliyoko kwenye kabati lako la nguo jiulize maswali matatu: Je inakutosha? Ulishaivaa miezi 12 iliyopita? Ina thamani ya kuifanya iwe kwenye kabati lako la nguo? Kama majibu ni hapana basi iweke kwenye fungu la kugawa.

Endelea na mchakato huo huo kwenye nguo na viatu vya mwenzi na watoto wako. Utakapomaliza zoezi hili utajikuta una mzigo mkubwa wa vitu vya kugawa na hata taka nyingi.

Vile vile kwenye ofisi yako iwe ni ofisi ya nyumbani au ya mahali pa kazi basi kama msemo wa safari inaanza kwa hatua moja tenga saa moja ya saa yako ya kazi kwa kupitia nyaraka moja moja. Amua ni ipi ya kutupa,  ni ipi ya kumwagiza mfanyakazi wa chini yako aifanyie kazi, ni ipi ya masjala na mwisho ni ipi ya wewe kuifanyia kazi mara moja. Jiwekee utaratibu wa kumeneji nyaraka zako. Kama unadhani hailipi kutumia muda wako fulani kuweka vitu kwenye mpangilio basi wacha uone ni vipi vitu vilivyolundikana vinaweza kukuvuruga katika maisha yako ya kila siku.

Kwenye droo za kabati lako la sebuleni. Je kumejaa daftari za zamani na vitabu vya jinsi ya kuendesha biashara vya nyakati ukisoma elimu ya juu na risiti za bili zilizolipwa miaka mingi iliyopita? Au pengine droo hizo zimejaa midoli na vigari vya watoto wako ambao sasa wako kidato cha pili? Ikiwa ni hivyo basi akili ni lazima ivurugike. Vitu visivyo kwenye mpangilio na uhitaji wa wakati husika vinakunyonya nguvu taratibu. Na hata kutafuta kitu kwenye mlundikano ni mbaya zaidi.

Ingia jikoni, hali ya jiko lako ndio hali ya afya yako. Kwahiyo ihurumie afya yako kwa kusafisha na kuweka mpangilio kwenye jiko lako! Safisha kwenye jokofu, punguza viporo vilivyoshamiri huko. Safisha jiko lenyewe, masufuria na vikaangio. Safisha kwenye madroo yote na ondoa chupa zote zisizohitajika.

Kama kawaida mlango wa mbele ni kivutio cha nyumba na ni eneo unaloanzia kupata nguvu unapoingia nyumbani. Zipe fahamu zako unafuu kwa kuweka mazingira ya mlango wa mbele kwenye mpangilio ili kuondoa msongo wa mawazo. Ondoa vitu kwenye mlango huo ambavyo kwakweli havitakiwi pale kwa mfano doo la uchafu, vyungu vya maua vyenye nyufa na kadhalika. Lete muonekano wa umaridadi kwenye eneo hili la mbele ya nyumba.

Tafuta njia ya kushughulika na barua na bili zinazokuja nyumbani ili zisisambae kila mahali. Droo dogo kwenye kabati lako la nguo linaweza kuwa suluhisho la kuhifadhi barua zako kama hamna nafasi eneo lingine.

Sababu ya watu wengi kutopenda kuweka vitu katika mpangilio na kuondoa vile visivyotumika sio ni kwa vile inahitaji nguvu na muda. Sababu ya ukweli ni kuwa mchakato mzima una hisia kama vile ni tiba, na ni zoezi linalohitaji stamina. Ila habari njema ni kuwa mara ufanyapo zoezi hili na kuweka mkakati na miundombinu ya kuwezesha vitu kutolundikana tena basi maisha yanakuwa rahisi kwako kwani utazungukwa na mazingira freshi na safi.

Zingatia kuweka mpangilio, kuondoa mlundikano ili kufanya maeneo mbalimbali ya nyumbani kama yalivyoainishwa hapo juu kuwa nadhifu kwa kuwa yameunganika na ustawi wako hapo nyumbani. Watafiti wa kisayansi  walishagundua kitambo kuwa mlundikano wa vitu humsababishia binadamu kutozingatia mambo na pia kuwa na uwezo mdogo wa kuchanganua mambo.

Makala hii imeandikwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23