Tuesday, December 23, 2014

My Article for Newspaper: Malengo ya 2015 Nyumbani Kwako

Mazingira ya nyumbani kwako yasaidie kufanikisha maazimio yako ya mwaka mpya
Ni wakati mwingine tena wa mwaka ambao wengi wetu wanapenda kufanya mabadiliko kwenye maisha yao. Je umeshafikiria mabadiliko ya mwaka mpya kwa ajili ya kiota chako? Japo mabadiliko haya yanajulikana na wengi zaidi kama maazimio, kwa kutia msisitizo zaidi makala hii itayaita malengo. Malengo yanatamkwa kwa kusisitiza wakati uliopo ni nini tamanio lako (kwa mfano kuamua kubadili mpangilio wa fenicha za sebuleni kwako ili kuwezesha kunogesha zaidi mazungumzo) wakati maazimio yanatamka ni nini ungependa huko mbeleni ya kuwa unaenda kufanya nini wakati ujao.
Mara nyingi malengo (au maazimio) ya mwaka mpya yanatupiliwa mbali hata kama nguvu za kutosha ziliwekwa ili kuhakikisha yanafanikiwa. Moja ya sababu za malengo kutofanikiwa ni mazingira ya nyumbani kwako kutosaidia kuwezesha mafanikio ya malengo hayo. Kama unataka kufanya mabadiliko ndani ya maisha yako bila kuhusisha mazingira yako kufanikiwa ni mbinde. Kwa maana ya kwamba kama unaweka malengo yako ya mwaka 2015 kwa ajili ya makazi yako na ukayaacha mazingira yalivyo, ni ngumu sana kubadili chochote. Hata matangazo kwa mfano ya kujikinga na maambukizi ya VVU yanaonyesha uhusiano kati ya maambukizi na mazingira fulani ambayo yanachochea maambukizi hayo.
Kanuni ya malengo kuwa na uhusiano na mazingira inahusika karibia katika kila kitu. Kama unataka mwaka huu uwe tofauti basi unatakiwa kuweka mazingira ya kuwezesha malengo yako.
Je mazingira yako yanakusaidia kupata kile unachokihitaji? Kwenye mazingira ya nyumbani kwako vitu ambavyo havijakaa mahali pake au vimekaa mahali ambapo havifanyi kazi yake au havitumiki tena vinakukwamisha kutimiza malengo yako hapo nyumbani. Tembelea kwenye makabati ya nguo na vyombo angalia kwa umakini kuona ni vitu gani vya kuhifadhi, vya kugawa ama vya kutupa. Fanya hivyo kwa nia ya kupata nafasi ya kile tu kitakachosaidia kufanikisha malengo yako.
Pengine lengo lako la mwaka mpya ni kutokula hovyo kwa nia ya kupungua uzito. Je mara zote unaingia nyumbani kwa kupitia mlango wa nyuma ambapo unaingilia moja kwa moja jikoni? Kumbuka kanuni kuwa unachokiona mwanzo kinagusa zaidi akili yako, kwa hiyo kama mara ungiapo ndani unakutana na jokufu, chakula na kadhalika utapata hamu ya kula hapo hapo.
Mahusiano mengi yanaweza kuboreshwa kwa mapambo ya nyumbani hasa katika swala la kuwasiliana. Je chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni mahali patakatifu kwa wawili? Hakikisha vitu kama taa, vimeza, na viti kwenye chumba hicho viko viwili viwili.
Au lengo lako mwaka mpya ni kuwa na wageni wengi zaidi nyumbani? Hakikisha basi mlango wa mbele unaonekana na kuna njia ya wazi ya kuingilia. Taa zinazomulika njia ya kuelekea mlango huo ziwe zinafanya kazi. Pitia mlango wa mbele kama mgeni mtarajiwa uone kama kila kitu kiko sawa. Je njia hiyo inakaribisha? Na sebule yako je nayo inavutia kwa ajili ya wageni wako wengi ambao unapenda kuwaalika nyumbani mwaka mpya ?
Kwa wale ambao azimio lao kuu la mwaka 2015 ni kupamba nyumba zao hakikisha unachagua rangi kwa umakini, fikiria mpangilio wa fenicha je zinawatendea haki watumiaji wa chumba husika. Angalia vitu ambavyo inabidi uvifanyie kazi ili kuboresha muonekano wa makazi yako. Kama kwa mfano sakafu ya sebule yako ni ya marumaru na unachoka kusugua na kusafisha kila siku na unakiri kuwa ni ngumu kuifanya iwe safi; basi weka zulia kubwa ambapo utasafisha kwa mashine ya upepo mara mbili au tatu kwa wiki.
Ikiwa unaazimia kutojaza vyombo vichafu kwenye karo basi mwaka ujao lenga kuosha chombo mara baada ya kukitumia. Na hata hakikisha wanafamilia wengine pia wanafanya hivyo.
Huenda kijani kinakubariki lakini huna eneo kubwa ya kuweza kuwa na bustani za ardhini. Otesha basi bustani za kwenye vyungu walau ukifungua pazia la chumba cha kulala kunapopambazuka ukutane na kijani. Azimia kupamba ndani mwako kwa maua freshi japo mara moja kwa mwezi.
Kweli, baadhi ya mabadiliko ya nyumbani kwako unaweza kuhitaji kutafuta msaada, lakini kuna mabadiliko mengi sana ambayo hayahitaji gharama lakini yanahitaji muda na nguvu ( na pengine kaujuzi)  kwahiyo kwa 2015 kwa nini usiazimie kupamba mwenyewe? Unaonaje? Ni azimio moja zuri kwa ajili ya makazi yako ambalo unaweza kutekeleza. Fanya usafi mkubwa ndani ya nyumba yako mara moja kwa mwezi ( weka tarehe kwenye kalenda yako na isismamie). Mwanamke unatakiwa upende usafi na usiwe mvivu. Shirikisha na wanafamilia wengine pia.
Hii inaweza isikubalike kwa baadhi ya watu ila ni mawazo binafsi kuwa azimia kila anayeingia ndani avue viatu mlangoni. Viatu vya wanawake vilivyo na visigino vya ncha kali mara nyingine vinakwaruza sakafu za marumaru na mbao na kuacha alama na vile vya wanaume baadhi vina soli zinazoacha rangi sakafuni na hivyo kufanya sakafu ionekane zee kuliko kawaida.
Mwaka huu lenga kuweka nyumba yako nadhifu kila mara kama vile unategemea mgeni wa heshima!

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa magari, nguo na mazulia; pia ana mapenzi makubwa ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christinesdaughter@yahoo.com

Monday, December 22, 2014

Laundry Talk: Umuhimu wa Kutumia Bleach


As ninafanya biashara ya dry cleaning na laundry nimeona kuwa hakuna mbaya nikiwa na share na wewe tips za mambo hayo. So kuna mambo elfu moja na moja kidogo ya kuongelea kuhusu usafi wa nguo tatizo nadhani ni muda mchache uliopo!

Naanza na kwanini tutumie bleach? Nyeupe zizidi kuwa nyuepe zaidi, inaondoa udongo na inaua vijidudu.


Zaidi ya maelezo ya kwenye chupa bleach inatakiwa kuchanganywa na maji kabla ya kusweka nguo endapo unafua kwa mkono, baadhi ya watu kwa kutojua wanaweka nguo kwanza halafu wanamimina bleach juu ya nguo, hii ni makosa as inaweza kuunguza nguo endapo utaimimina moja kwa moja juu ya nguo.

Of course, kama unatumia mashine una ile sehemu ya ku dispense bleach, kwa hivyo unamimina tu pale kwa maana hiyo huna haja ya kuchanganya maji na bleach manually.

Kabla hujatumia bleach kwenye nguo hakiksha kwanza unasoma label ya nguo, kwa ajili kuna baadhi zinasema kabisa "No Bleach" - kwa maana hiyo usitumie bleach kwenye nguo yenye label inayosema hivi.

Na usisahau kuwa kuna bleach za kutumia kwenye nguo za rangi pia ...watu wengi hawajui hili, kwa mfano unaona zile chupa za jik za rangi ya bluu? hizi ni kwa ajili ya nguo za rangi.

TAHADHARI wakati wa kutumia bleach - kuna dondoo mbalimbali zinatolewa kwa ajili ya kufua nguo zitakate zaidi kama vile kutumia limao, vinegar na kadhalika. Kuchanganya vitu hivi na bleach kunaweza kuzalisha kemikali zitakazoharibu nguo zako, ambapo usingependa litokee hili.

Sunday, December 21, 2014

...mjini tumekuja kutafuta maisha...

wakati wa sikukuu tunachapa lapa kama hivi...usisahau chimbuko lako mdau...watu wangu wadogo washasepa zao xmas hiyoooooo yaja...




Thursday, December 11, 2014

my article for newspaper: kuhifadhi taulo na ugeni

Jinsi unavyoweza kuhifadhi taulo za bafuni kwa ajili ya wageni watakaokutembelea msimu huu wa sikukuu.

Moja ya faida za kipindi cha sikukuu  ni fursa ya kufungua nyumba yako kwa wageni ambao hamjakaa pamoja mwaka mzima.  Kama utakuwa na wageni nyumbani msimu huu wa sikukuu, makala hii inakuhusu. Mahoteli yanafanya wageni wao wajisikie spesho kwa ajili wanafahamu jinsi ya kuwafanya wajisikie  nyumbani kwa kuwapatia mahitaji muhimu. Wewe pia unaweza wafanya wageni wako wajisikie kama wameshukia kwenye hoteli ya kitalii wanapokuwa nyumbani kwako, kwa ajili tu ya buduriko wanalopata wanapokuwa kwenye chumba au vyumba vyao vya wageni hapo kwako.

Ni  bafu chache zenye sehemu ya kutosha kwa ajili ya kuhifadhi taulo za wenyeji na wageni kwa wakati mmoja, na huenda unafikiria ni jinsi gani utahifadhi taulo za wageni wako watakapokutembelea. Lakini usijali kwani hata kama bafu lako ni dogo namna gani njia mojawapo kati ya hizi itakufaa kutundika ama kuhifadhi taulo za wageni wako.

Kuweka fimbo za kutundika taulo kwenye ukuta wa bafu ama nyuma ya mlango (uwe wa mbao kwa uimara) ni njia rahisi zaidi ya kuhifadhi taulo za bafuni. Fimbo hizi hazichukui nafasi kubwa na wala hazina marembo kwahivyo ni suluhisho tosha kuhifadhi taulo kavu na hata zile zenye unyevu. Fimbo za taulo zinaruhusu taulo kukauka kwa usafi zikiwa zimetundikwa kwa kukunjwa nusu. Fimbo za bafuni za kuwekea taulo zinasaidia mambo makubwa mawili: kwanza, zinaweka taulo kavu na safi kwa jinsi ambayo ni rahisi kuchukua na kutumia; pili, zinatandazwa taulo zenye unyevu na kuzifanya kukauka kirahisi, hivyo kuzuia kuota kwa ukungu.

Licha ya kufungwa bafuni fimbo za taulo zinaweza kufungwa pia jikoni kwa ajili ya kuwekea taulo za mkononi.

Muonekano wa fimbo za taulo ni kawaida sana. Ni fimbo iliyosimikwa ukutani ama nyuma ya mlango kwa kutumia mashine ya kutobolea ukuta na taulo huwekwa hapo, hutolewa kutumika na hurudishwa tena hapo baada ya kutumika kwa ajili ya kukauka. Ni muhimu fimbo hizi zimewekwa imara kwakuwa kama tujuavyo taulo zikiwa mbichi zinakuwa nzito na pia mara nyingine fimbo hizi hutumika na watoto kwa utundu wao wa kupenda kubembea kila wapoona panafaa, na pia wazee kujishikilia wakiwa bafuni. Kwahivyo siwezi kuacha kusisitiza kuwa fimbo za taulo ni lazima zifungwe kwenye ukuta wa tofali ama mlango wa mbao kwa ajili ya uimara.

Fimbo za taulo sizo tu zinazoweza kuhifadhi taulo kwa usafi na kuruhusu zile zenye unyevu kukauka. Kulabu (hook) za taulo, susu (rack) za kusimama wima, bangili na ngazi za taulo nazo ni njia nyingine za kuhifadhi taulo za bafuni. Bangili iliyotobolewa ukutani ambapo taulo kadhaa zinatundikwa ni maarufu sana siku hizi na kwenye maduka ya fenicha wanaziita bangili za taulo.

Ngazi za taulo ni chuma kingine kinachoonekana kama ngazi ndogo ambacho hutumika kuwekea taulo,  ni njia mojawapo ya kuhifadhi taulo za bafuni. Je una nafasi kwenye ukuta wa chumba cha kulala cha wageni wako ambapo unaweza kuweka ngazi hii? Ni kiasi cha kuishikilia na braketi juu ili isianguke na unaweza kuhifadhi kwa kutandaza taulo za kuogea. Uzuri wa ngazi ya taulo ukilinganisha na fimbo ni kuwa wakati kwenye fimbo unaweza kuweka taulo zisizozidi 2 kwenye ngazi ya taulo unaweza kuweka hadi taulo 6.

Lakini kuna njia nyingine ambazo hazitakufanya uusumbue ukuta wako ambazo zinaonekana za kimapambo zaidi kwa mfano kuweka susu ya kusimama inayojitegemea kama ile ya kutundika makoti ofsini. Kama chumba cha kulala cha wageni wako kina nafasi kidogo ya ziada basi simamisha susu ya koti kwa ajili ya kutundikia taulo za bafuni. Susu inaweza kutundikwa taulo kadhaa kwa wakati mmoja. Fikiria kuiweka sehemu ambayo inaingiza hewa au vinginevyo wageni wako wawe wanazigeuza mara kadhaa kuwezesha kukauka. Kama susu hii inatundika taulo za wageni tofauti tofauti basi wawe na taulo za rangi tofauti kwa kila mmoja. Hakuna anayependa kushirikiana taulo.

Badala ya ile susu ya kusimama kuna hii nyingine inayofanana na ya kuhifadhia chupa za mvinyo. Kama unataka wageni wako wajisikie kama wako kwenye hoteli yenye hadhi ya nyota tano nenda kistaili zaidi kwa kuhifadhi taulo zao safi zilizobiringishwa vizuri kwenye susu ya taulo. Susu za taulo zina muonekano wa kuvutia kwahivyo kwa upande mwingine ni kama pambo. Taulo safi zinabakia zimebiringishwa vizuri ndani ya susu hadi wakati wa kutumiwa, na hii inachukua nafasi kidogo kuliko ile ya kusimama. Kuhifadhi taulo kwa kutumia susu ya taulo inakubidi uwe ni mtu wa kutumia taulo mara moja tu na kulifua.

Kama ulijisikia kwamba bafu lako ni dogo kiasi kwamba huna mahali pa kuhifadhi taulo za wageni wako msimu huu wa sikukuu hatimaye leo umefahamu njia kadhaa za kuweza kuhifadhi na kutunza taulo wakati huo huo ukiwa unazitumia. Wekeza katika njia mojawapo kati ya hizi ilikurahisisha maisha bafuni sikuzote na hata msimu wa wageni.


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye anajishughulisha na usafi wa magari, mazulia na nguo aina zote; pia ana mapenzi makubwa ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda christines.daughter@yahoo.com au 0755 200023

...nothing happier than to watch them growing...







Wednesday, December 10, 2014

ideas za makabati ya bafuni

Kila mmoja wetu ana ladha na mahitaji mbalimbali tofauti na mwingine. Wakati baadhi yetu tukiamini kuwa muonekano wa sebule ndio kipaumbele namba moja kwenye makazi yetu, wengine wanajali zaidi ni kwa namna gani mabafu yao yanaonekana, kwahivyo makabati ya bafuni kwa watu hawa ni kitu muhimu zaidi kwao  kwa uzuri na kwa matumizi ya bafu.
Wenye nyumba wengi wanaona uhaba wa eneo la kuhifadhi vitu bafuni kama vile shampoo na vipodozi. Sasa basi yawezekana ulikumbuka hivi wakati wa ujenzi na hivyo kuwa na mababati yaliyojengewa humo humo. Vinginevyo yapo hata ya kusimama peke yake, kama makabati ya bafuni ni jambo muhimu kwako bado hujachelewa, pata mionekano ya makabati haya ambapo staili mojawapo yaweza kukuvutia.




Friday, December 5, 2014

....my babies....

ulishahudhuria msiba ambapo marehemu ana miaka 80 lakini ukashangaa jinsi wanae wanavyomwaga chozi...kumbuka usemi wa kiswahili kuwa mtoto kwa mama hakui...lol




Thursday, December 4, 2014

my article for newspaper: ubora wa tile za bafuni

Umuhimu wa kujali ubora wakati wa kununua marumaru za bafuni


Bila shaka kila mmoja anataka apate bidhaa au huduma kwa thamani ya hela aliyotoa wakati wa ujenzi wa nyumba yake, lakini chaguo la marumaru za bafuni inahitaji kuwa makini zaidi ya hilo. Katika makala hii nitakuwa na Mhandisi David ambaye atatujuza umuhimu wa kuzingatia ubora zaidi ya gharama wakati wa kununua marumaru za bafuni.

Unaweza kuwa umepata marumaru za bei nafuu, lakini zisizokuwa na kiwango. Marumaru za aina hii zitakugharimu kwa kiasi kikubwa muda wote utakaokuwa unaishi kwenye nyumba yako hiyo.
Linapokuja swala la marumaru za bafuni, malighafi, rangi, uimara, mtelezo, na usimikaji ni mambo muhimu zaidi ya kuzingatia, anasema David. Hakikisha kuwa unapata ushauri kwa fundi mwenye uwezo kabla ya kufikia kufanya uamuzi.

Marumaru za bafuni zipo za kuanzia maumbo madogo zenye nyongeza ya border za aina na michoro mbalimbali. Wajenzi wanatafuta marumaru za maumbo tofauti tofauti  kutoka umbo la pembe nne lililozoeleka hadi malighafi nyingine kama mawe ya asili na vioo. Wanapenda pia mabafu yao yawe na muonekano wa  kazi za sanaa zaidi, anasema David. Ila marumaru za bafuni zinafanya kazi kubwa, zinatakiwa kufanya mvuke usisambae vyumba vingine na kulinda kuta zisiharibiwe na ukungu na hali ya umajimaji. Zinatakiwa zizibwe vyema na grout maeneo ya miungio na ziwe na usalama kutembea juu yake zinapowkuwa zimeloa, anasema mhandishi.

Pamoja na mawe ya asili, marumaru bado zitabaki kuwa chaguo maarufu zaidi kwa ajili ya kuta na sakafu za bafuni. Marumaru ngumu zina rangi sawa kwenye unene wake wote, ingawa zina gharama zaidi, na hapa ndipo mnunuzi anapopaswa kuwa makini. Ujue kutofautisha kama unanunua marumaru zilizopakwa rangi kwa juu tu, na hizi ni zile nyepesi na bei yake iko chini. Aina hii ni kuwa baada ya muda si mrefu rangi inatoka kutokana na kukanyagwa mara kwa mara, kwa kuwa rangi imepakwa kwenye eneo la juu la marumaru kwa unene kiasi tu na sio unene wote. Hizi zilizopakwa rangi inakuwa eneo la juu tu mfano barafu kwenye mlima au kwenye keki! Hizi za aina hii zinafaa zaidi kwa mapambo pengine kutengenezea ua la ukutani lakini sio kwa kuhimili shurba za sakafu ya bafuni. Marumaru  ambazo zina rangi hiyo hiyo hadi ndani kwenye kiini na unene wote wa marumaru ni imara zaidi kwa matumizi ya sakafu ya bafuni.

Kwa hivyo muhimu zaidi ni kutumia marumaru hizi ngumu zenye rangi sawa kila mahali kwa ajili ya sakafu na kuchagua za bei rahisi zinazoendana na zile ngumu kwa ajili ya ukuta, anasema David. Usimikaji wa marumaru ni kazi ya sanaa kwahivyo inahitaji fundi mwenye uwezo nayo.

Zaidi ya kuweka marumaru bafuni unaweza kuweka pia jiwe la asili kama vile marble lakini iliyo ngumu. Ubora wa jiwe na usimikaji wake ni muhimu sana. Uwekaji wa jiwe la asili ni wa kitaalam. Kunaweza kuwa na shida ya kufitisha slabu kubwa ya jiwe hilo kwenye maeneo ya kutolea maji machafu na kuingiza maji safi,  na muhimu zaidi ya yote sio kila jiwe la asili linafaa kwenye mazingira ya mvuke na majimaji ya bafuni, anasema mhandisi. Mawe mengine ya asili yananyonya maji na mwishowe kuwa na mipasuko.

Marumaru zitaongeza thamaini ya nyumba yako, kwahivyo kuwa tayari kutumia muda na pesa. Kwa bafu la kisasa na muonekno wa kifahari chagua marumaru zenye rangi za mwanga kama vile nyeupe ukutani huku ukiweka miisho na mpangilio fulani  wenye mvuto kwa baadhi ya maeneo ya ukuta.
Haijalishi ni mtindo gani wa marumaru utakaochagua kwa ajili ya bafu lako, zingatia ubora na usimikaji wa kitaalam kabla ya kufanya maamuzi yoyote. Dondoo muhimu kuliko zote, kabla hujaanza kutengeneza bafu lako angalia thamani ya nyumba yako. Ubora wa bafu uendane na thamani ya nyumba. Kwa kuzingatia hilo utafanya uamuzi sahihi kwa kushirikisha wataalam watakaokufanya usijutie maamuzi yako hapo baadaye.


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

Thursday, November 20, 2014

my article for newspaper: jinsi ya kupamba bedroom

Jinsi ya kupamba chumba cha kulala

Kwa nyumba nyingi chumba cha kulala ni chumba binafsi zaidi. Ni chumba pia ambacho kina vitu vingi zaidi binafsi. Kinaweza kuwa kama kiota cha mahaba au mahali patakatifu pa kulala na kupumzika. Pia kinaweza kuwa chumba cha kuchangamka na kutuliza kwa watoto, kwa jinsi wanavyokuwa wakigundua kuwa wanamiliki chumba chao wenyewe.
Kupenda kufurahisha marafiki, majirani na wageni; wenye nyumba wengi wanamalizia nguvu zao kupamba vile vyumba vya kuonekana na hadhara ndani ya nyumba. Umefika wakati wa kuwa mchoyo na kuelekeza nguvu zako kwenye chumba cha kulala. Juu ya yote ni kuwa kabla ya kuoga kujiaandaa kutoka ni lazima kwanza utokee kitandani.
Kwanza kabisa anza na kitanda kwa ajii kitovu cha chumba chochote cha kulala ni kitanda. Ni wazi kuwa kitu cha kwanza cha kuzingatia kwenye kitanda itakuwa ni godoro, lakini usisahau ubao wa kichwani. Ni ngumu kudharau umuhimu wa sababu za kisaikolojia katika kupata usingizi mwororo. Hisia na hata muonekano wa kitanda chako wakati unapoingia humo inaweza kuelezea ni namna gani unavyojisikia wakati unapotoka humo.
Kwa upande wa sakafu chaguo zuri zaidi kwa ajili ya chumba cha kulala ni zulia na mara zote imekuwa hivyo. Hamna kitu kizuri kama kuamka na kuweka miguu yako kwenye sakafu ambayo inaelekea kuwa na hisia kama za kitandani kwa kupata joto lile lile mithili ya la kitandani. Wengine hupenda kuweka sakafu za marumaru na mbao lakini eneo la pembeni mwa kitanda wengi wanapenda kuweka zulia.
Wazo la mwanga katika chumba cha kulala kwa baadhi linadharauliwa. Taa zisizokuwa na maridadi na balbu za juu ya kichwa tu zimeanza kupoteza mvuto kwenye chumba cha kulala cha kisasa. Taa za vivuli za kuweka juu ya vimeza vya kando mwa kitanda na za ukutani za maridadi ndio zinaendana na wakati kwa chumba cha kulala, kwa ajili ya mwanga wa chumba hiki kwa matumizi ya wakati wowote iwe ni mchana, jioni au usiku. Taa ndogo zinaweza kuwekwa kwa ajili ya kutumia muda maalum ambapo hutaki kuwasha taa zote kwa mfano wakati wa kusoma au kushikisha kifungo.

Kwa vyumba vidogo vya kulala mara nyingi vinafaidika na uwepo na makabati ya nguo, madroo na shelfu kwa kusaidia kuhifadhi na kuweka mpangilio. Baadhi ya vitu vidogo dogo na nguo vinapoukuwa vimewekwa kwenye sehemu hizi za kuhifadhia, chumba kinaonekana nadhifu.

Mara nyingi rangi za mwanga  zinashauriwa zaidi kwenye chumba cha kulala kwa ajili zinaleta hisia ya mapumziko. Rangi za vitambaa vya malazi viendane na rangi nyingine hapo chumbani na hata zile za samani. Shuka za rangi na maua ya kuvutia zinunuliwe ili kuongeza uzuri wa chumba.
Komfota lenye rangi nzito litaendana na samani au ubao wa kichwani wa mbao. Hii pia ni kweli kwa mapazia.

Wakati huo huo kumbuka kuweka samani zenye ukubwa na wingi wa kuendana na ukubwa wa chumba. Kabla hujanunua samani hizo ni vyema kwanza kufahamu mpangilio wa sakafu na ukubwa uliopo.

Kutengeneza bajeti ni muhimu kwa mradi wowote wa maboresho ya nyumbani. Kujipa wastani wa gharama inayohitajika itakusaidia kuamua ni nini kinachoweza kufanyika na kipi si kipaumbele. Baadhi ya shughuli kwenye mradi huu unaweza kufanya mwenyewe, kwa baadhi itakubidi utafute mtaalam. Kama kipaumbele chako ni ukuta kwa mfano, basi unaweza kutafuta mtalam wa rangi akapaka, ilihali ukitandika zulia mwenyewe. Vyovyote utakavyoamua, ni wakati wa kufanya chumba chako kuwa chako tena.

Kupamba chumba cha kulala ni shughuli mojawapo ya maboresho ya nyumbani ambayo inaweza kuhuisha tena afya yako na mahali unapoishi.


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

...picha hizi za mapambo haya yamenitumbuiza...

Hii picha nimefurahishwa zaidi na jinsi ya kupamba kwa mto ya soseji. Angalia hilo sofa kati kaweka soseji na iliyokuwa sandwiched na square, so nice...


Hii fremu unaweza iweka jikoni hasa kama mlango wako wa jikoni ni wa kuingilia toka nje pia. Ni pambo na ukaribisho vilevile


 haya tena ni ubunifu tu

lovely

Kama unakaa nyumba ya ghorofa ona hapa chini ya ngazi unavyoweza kufanya mambo.

Monday, November 17, 2014

designs simple za majiko kwa wanaoanza familia

Kuna aina nyingi za majiko ambazo wewe mdada unayeanza familia unaweza kuchagua kulifanya jiko lako kuwa na mashiko na kufanya kazi iliyokusudiwa kwenye nyumba. Siku hizi imekuwa rahisi kupata mawazo kwa kuchungulia dondoo mbalimbali kwenye majarida, kudesa la jirani au rafiki, kuangalia video na mitandao mbalimbali kwa mfano unavyosoma hapa sasa.
Muonekano wa jiko kwa asilimia kubwa unachukuliwa na tile na makabati. Tile za floor na ukuta wa jiko, zipo za kumwaga, ni wewe tu kuamua rangi na muundo upi unataka na kwa finishing ipi. 
Kitu kingine  unatakiwa kuzingatia kwenye design ya jiko ni makabati. Hard wood eg mkongo, mninga ndio mambo yote na ni muhimu sana, usidanganyike kwa urembo wa soft wood kwani si lolote si chochote kwa jikoni. Jiko litolee gharama lidumu.
 hili kwa nyumba yako ya room 3 safi sana
 rangi za makabati nazo ni decoration
 tile za floo nimezipenda, na kuwa na kisehemu cha kulia kama nafasi inaruhusu si mbaya
 rangi zimenibamba ila tile za floor big nooo

Thursday, November 13, 2014

my article for newspaper: vioo vya mapambo

Boresha muonekano wa ndani ya nyumba kwa kuweka vioo vya mapambo.

Vioo vina kitu kwakweli ambacho ni maalum ndani yake. Vinakusaidia kukujulisha unaonekanaje na pia kukuwezesha kujiweka jinsi ambayo unataka uonekane. Zaidi ya haya maandalizi binafsi na kujiridhisha na muonekano wako kabla hujatoka, vioo vinasaidia pia kwenye kupamba ndani na hivyo kufanya muonekano wa nyumba kuwa maridadi na nadhifu zaidi kwa kila mgeni anayekutembelea.

Kama kuna pambo la ndani ambalo wenye nyumba hatakiwi kulikosa, basi ni kioo. Havitumiki tu kujiangalia unapoingia, bali vina mahadhi yake kwenye kuongeza staili ya chumba au muonekano wa kupagawisha kwa kumfanya mgeni kuduwaa. Sababu nyingine kuu hapa ni kuwa vioo vinaweza kuwa  na bajeti rafiki. Ni kweli kuwa kuna vioo ambavyo ni lazima viwepo nyumbani kwa matumizi kuwa watu wanahitaji ili kuhakikisha kuwa wanaonekana jinsi wanavyotaka kuonekana, lakini leo kwenye makala hii tunaongelea vioo kama mapambo ambavyo unaweka kwenye ukuta wa nyumba yako ili kuongeza staili na ukubwa.

Utagundua kuwa leo, sokoni kuna aina nyingi na tofauti za miundo na aina za vioo. Watengenezeaji wa vioo vya mapambo wanakuja juu kwa kuongeza ubunifu hasa wa fremu wanazofungia vioo hivi. Unaweza kuvipata vioo hivi vikiwa kwenye fremu ya kila malighafi unayohitaji kwa mandhari unaotaka kutengeneza.
Fremu nayo ni kigezo muhimu cha kioo kuwa kifaa cha mapambo. Unaweza kuagiza kioo kwa umbo unalotaka kwa mfano unaweza kuwa na kioo kwenye ukuta wa sebule ambacho kinatoa sura kwenye taswira nne kwa jinsi ambayo ukijitazama unaona uso nne zinazofanana.. Haijalishi staili unayotaka au bajeti uliyonayo, kuna uhakika wa kupata kioo ambacho ni sahihi kwa mradi wako.

Sababu ya kuweka vioo hivi ndani ya nyumba ni ukweli rahisi kuwa unataka kutumia ile hali ya kujiona ndani ya kioo kwa faida ya kimapambo. Baadhi wananunua vioo na kuvitundika kama sanaa nyingine za ukutani, kwa maana ya kuwa wanakitundika katikati ya picha na fremu nyingine, au wanakiweka kwenye ukuta ambao hauna kitu kingine ambacho kingefaa hapo. Hata hivyo unaweza kutumia vioo vya mapambo kuakisi mwanga na vifaa. Kwa mfano unaweza kuwa na ujia (corridor) ambao una mlango upande mmoja lakini mwingine hauna. Pambo lako hapo linaweza kuwa mmea wa kijani (uwe hai au mfu) pale kwenye ukuta usiokuwa na mlango pamoja na kioo. Kioo kitauakisi ujia kwa kuukuza uonekane mpana na mrefu. Kupamba kwa vioo kunafanya eneo dogo lionekane kubwa na mbinu hii inatumika na wataalam wengi wa ubunifu wa ndani nyumba.

Kupamba kwa vioo kunaongeza mwanga wa chumba. Chumba kilichopakwa rangi ya giza kinaweza kuonekana kidogo, kuongeza vioo kwenye kuta zake kutaboresha mwanga. Njia sahihi zaidi ya kuongeza mwanga wa jua bila kuongeza taa ni kufunga vioo vitazamane na madirisha. Vioo vinadaka mwanga wa jua toka dirishani na kuusambaza chumba kizima. Hii inaweza kuwa njia mojawapo pia ya kubana matumizi badala ya kuwasha taa mchana.

Kupamba kwa vioo vya mapambo hakuhitaji mtaalam. Mtu akiwa na vifaa vya toolbox anaweza kufunga vioo ukutani  na kutengeneza chumba chenye muonekano mzuri kwa gharama nafuu.
Chagua vioo vyenye maumbo ya kuvutia, pembe nne ni nzuri ila vioo vyenye maumbo yasiyozoeleka vinafanya umaridadi zaidi. Tafiti aina na maumbo mbalimbali ya vioo kabla hujamua ni vipi unataka.

Ili kukifanya chumba kisicho na uwiano kionekane kuwa nao, funga vioo vya mapambo ukutani. Vioo hivi viwekwe kuakisi vitu fulani kwenye chumba ili kufanya ionekane kama vitu hivi viko katika kila upande wa chumba, kwahivyo pale unapoingia uone kama chumba kina uwiano na ni kikubwa.

Baadhi ya wenye nyumba wanatamani waboreshe muonekano wa ndani wa nyumba zao. Marekebisho yana gharama kubwa, hata hivyo wewe mwenye nyumba usizime tamanio lako. Unaweza kunyanyua uso wa ndani ya nyumba yako kwa kutumia vioo vya mapambo badala ya marekebisho makubwa.. Mradi huu mdogo wa kunyanyua uso kwa kutumia vioo unaweza kukupa matokeo usiyotarajia. Kupamba kwa vioo ni moja kati ya njia nyepesi na rahisi za kuboresha muonekano wa ndani ya nyumba.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ni mjasiriamali  upande wa usafi wa nguo, mazulia na magari; pia ana mapenzi makubwa ya muonekano wa nyumba. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com



Saturday, November 8, 2014

tv cabinet ni moja kati ya post zangu iliyopendwa kuliko...

nakuongezea hapa dondoo chache za muhimu kabla hujanunua kabati la tv, twende kazi...
kabati hili ni moja kati ya fenicha ya msingi hapo sebuleni ambapo unakutana na marafiki zako, kula dinner na kuangalia tv. Wakati unapotaka kununua kabati la tv, ukubwa wa tv yako unahusu.
wakati wa kununua usifikirie tv tu. fikiria pia vitu vidogodogo ambavyo vinatakiwa kuwa hapo lakini vihifadhiwe, kwa mfano remote, kwahivyo nunua kabati lenye droo moja au mbili na hata likiwa pia na shelfu itakuwa poa zaidi.. kwahivyo kumbuka kuwa usifikirie tv tu.
la mwisho lakini si dogo unatakiwa uamue malighafi na rangi za kabati lako. kuna makabati mengi ambayo machoni yanavutia lakini kwa ubora si lolote si chochote. kwa swala la rangi hakikisha una research hadi uone kitu kinachokuvutia ndio ununue. Good luck!



super saturday na marafiki zangu wa ukweli...

hapa na pale leo na watu wangu wadogo...

 pozi la kibaunsa..sungusungu wangu
 pozi zikazidi hadi rafiki akalamba chini
akanyanyuka akijongea tartiiibu

Friday, November 7, 2014

njia rahisi kabisa ya kupamba sebule

kwa vile sebule ni sehemu muhimu ndani ya nyumba inahitaji kutupiwa jicho zaidi ya nyingine zote na ni lazima ipambwe kwa njia mbalimbali ili iwe na mvuto mbele ya kila mgeni anayekutembelea, na hii wala si ngumu.
kwanza kabisa weka fenicha zenye mvuto ambazo ni sofa, vimeza vya kando, kimeza cha kati, meza ya chakula na viti vyake.
weka taa maridadi na zenye mwanga wa kutosha kumulika sebule yote. weka taa za vivuli juu ya meza na sakafuni ili kuleta matokeo makubwa. kama wewe ni mshabiki wa wallpaper chagua ukuta wa tv ubandike, ning'iniza picha na fremu ukutani na hata vikapu vidogodogo vikiwa na maua ya kutengeneza.
weka vyungu vikubwa vya maua juu ya meza au sakafuni kwenye kona. weka kioo kikubwa katika ukuta wowote na upambe boda zake kwa fremu za kuvutia. unaweza pia kuweka sanamu kwenye kona na pembe za sebule yako.
mwisho kabisa usisahau kuweka pazia na fimbo za kuvutia.