Thursday, September 4, 2014

my article for newspaper: kuepusha wadudu ndani ya nyumba

Wakati baadhi ya watu wanaogopa wadudu, wengine wanaweza kuwa wanavutiwa nao. Lakini kitu kimoja ambacho wengi tutakubaliana ni kuwa wadudu makazi yao sio ndani ya nyumba. Si tu kuwa wanaleta mazingira hatarishi kiafaya, bali pia, ni rahisi tu ya kuwa wanaudhi, kuanzia mbu wanaokupigia mziki masikioni mwako, kukuuma na kukusababishia maradhi hadi kwa nyigu anayeweza kukusababishia kidonda.

Hata yule mende wa kawaida anaweza akasababisha mzio hasa kwa watoto, anasema dokta Emil.
Kuepusha wadudu ndani ya nyumba inaweza kuwa ni vita vilivyoshindikana. Bahati nzuri ni kuwa, kwa kufahamu ni nini kinachovutia wadudu ndani ya nyumba yako, unaweza kuanza kufanya mabadiliko ambayo yatawakimbiza kimya kimya.

Kama ilivyo kwa binadamu, wadudu nao wanahitaji chakula, maji na makazi ili kuishi. Kwa kukata usambazaji wa chakula chao na kuvuruga maeneo yao ya kujifisha, unaweza kupunguza tatizo la kuwa na wadudu ndani ya nyumba yako. Kata chanzo chao cha chakula kwa kuhakikisha kuwa vyakula vyote vinawekwa kwenye kontena zilizofungwa vizuri. Mabaki ya vyakula ndani ya nyumba yatupwe eneo moja tu ambalo ni ndoo ya uchafu  yenye mfuniko wa kujifunga wenyewe iliyopo jikoni. Ndoo hii imwagwe na kusafishwa kila siku baada ya kuosha vyombo vya chakula cha usiku. Futa michuzi na mabaki yoyote yanayoweza kuwepo maeneo ya wazi ndani ya nyumba. Osha vyombo punde mara baada ya kutumika. Pipa linalomwagwa uchafu nje nalo liwe na mfuniko.

Usisahau vyakula vya wanyama waliopo nyumbani kwako. Kwa mfano unafuga mbwa na una vyakula vyake vya unga umehifadhi stoo, unga huu unaweza kuvuta mende na sisimizi. Unaweza kuweka dawa za kuzuia wadudu kwenye stoo yako ya chakula cha wanyama unaofuga.
Vifaa vyote vya kuhifadhia mabaki ya vyakula ndani na nje ya nyumba viwe vinasafishwa kwa dawa za kuua wadudu mara kwa mara.

Kama vile mlango uliolokiwa unavyoweza kuwaweka wavamizi nje, mlango uliozibwa sahihi unaweza kuwazuia wadudu wasiingie ndani. Kuepusha wadudu wanaotambaa kuingia ndani kwa kupitia sehemu ya wazi mlangoni, weka kizuizi cha mpira au brashi chini ya mlango. Vizuizi hivi vinapatikana kwenye maduka ya vifaa vya ujenzi, anasema mseremala Simon.

Kumbuka kuwa mbinu zote hizi za kuziba chini ya mlango hazitafanikiwa kama mlango wenyewe utaachwa wazi. Kama una watoto ambao wanasahau kufunga mlango, fikiria kusimika vifunga mlango.
Wenye nyumba wengi wanategemea hewa safi ya nje iingie ndani kupitia milangoni na madirishani. Hii inaweza kuwa majaribu hasa wakati wa kiangazi. Bahati mbaya ni kuwa kiangazi ni wakati mbaya kwa vile mbu na wadudu wengine wengi wanavamia ndani ya nyumba. Kufurahia raha ya hewa safi bila kupata bughudha ya wadudu weka wavu wa kuzuia wadudu kama mbu kwenye madirisha na milango.

Eneo la nje ya nyumba linaweza kuwa linasababisha wingi wa wadudu ndani ya nyumba yako. Endapo mioto ya asili ni mingi na iko karibu sana na ukuta wa nyumba basi tegemea kuwa na mazalia makubwa ya wadudu na hivyo uwezekano wa wengi kujaribu kukimbilia ndani. Hii pia itakufanya hata wewe mwenye nyumba kushindwa kufurahia kukaa kuburudika nje ya nyumba yako, kwa hivyo njia nzuri ya kuepusha wadudu ndani ya nyumba ni kuhakikisha wanaondoka pia kwenye maeneo ya nje ya nyumba.

Majani yaliyorundikwa, matofali yaliyopangwa kwenye yadi yako na hayatumiki tena na mashimo ya maji taka yanafanya makazi ya wadudu mbalimbali. Maeneo haya ni sehemu za kujificha kwa wadudu kama mende nyoka na wengine wengi na hata panya. Mashimo ya maji taka yawe na mifuniko iliyoziba vizuri na mrundikano mwingine wowote uondolewe na utashangazwa ni kwa jinsi gani wadudu watakimbia na mazingira yako yatakavyovutia.

Baadhi ya wenye nyumba wanapendelea kutumia dawa za kupulizia kwa ajili ya kuua wadudu kama mbu na mende. Haijalishi ni njia ipi unatumia ili kuepusha wadudu kufanya makao ndani ya nyumba yako; njia kuu ya kuwafanya wakimbie ni kukata “mirija” wa kile kinachowavutia. Hii inamaanisha ni pamoja na kuondoa mrundikano, vyakula na vyanzo vya maji. Bila kuwa na rasilimali hizi, wadudu watakimbia kwako kuelekea nyumba ya pili na kukuacha ukiwa na amani.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com


No comments:

Post a Comment