Wednesday, June 15, 2016

Nani alijua matumizi mengine ya microwave?

Wengi wetu tunatumia kipasha chakula (microwave) kwa ajili ya kupasha chakula, lakini je unajua kuna kazi nyingi unazoweza kufanyia ndani ya microwave zaidi ya huu ulimwengu wa kupasha chakula tu? Nimetafiti kazi mbalimbali zinazoweza kufanyika ndani ya microwave na hakika zitakurahisishia maisha yako! Hata hivyo tukumbuke kuwa
microwave imekuwa maarufu kwa ajili ya kufanya kazi kwa haraka zaidi. Kwahivyo zaidi ya kupasha chakula, microwave inaweza kufanya yafuatayo:

·        Kuzuia machozi wakati wa kukata kitunguu. Kikate eneo la juu na chini (kuondoa mizizi) halafu kipashe kwenye microwave kwa sekunde 30. Kitoe na ndipo unaweza kukikata bila tone la chozi!

·        Unaweza ukaondoa kirahisi karatasi zilizobandikwa kwenye vyombo na vikontena kwa kupaka maji eneo lenye karatasi halafu unakiweka chombo ndani ya microwave kwa sekunde 20. Gundi yote inayeyuka na unaondoa hiyo karatasi/lebo bila usumbufu wowote tena bila kuacha alama kama ambavyo ungetoa kwa maji, sabuni na sponji wakati wa kuosha.

·        Wote tunajua kuwa asali inakuwa ngumu ikitulia. Ifanye irudi kuwa kimiminika chepesi tena kwa kuiweka ndani ya microwave ikiwa wazi bila mfuniko kwa dakika moja.

·        Unaweza kupika baadhi ya vyakula moja kwa moja kwenye microwave mara baada ya kuvimenya maganda yake. Jaribu kwa viazi mviringo. Vilevile pika bisi ndani ya microwave kwa dakika nne tu.

·        Kama unataka kupika maharage na hukukumbuka kuyaloweka usiku kucha – jaribu mbinu hii. Yaweke kwenye bakuli yakiwa yamefunikwa na maji na ongezea magadi soda halafu yapashe kwenye microwave kwa dakika 10 yatoe yaache yapoe kwa muda wa dakika 40, baada ya hapo yatakuwa tayari kwa kuunga mboga.

·        Unapata shida ya kupata juisi kutoka kwenye hizo ndimu au limao? Lipashe kwa sekunde 15 utashangaa itakavyokuwa rahisi kukamulika.

·        Unachukia kumenya vitunguu swaumu?  Vitie maji halafu vitoe viweke kwenye microwave kwa sekunde 20. Hali ya mvuke inasaidia ngozi kavu ya nje itoke haraka.

·        Unaweza kukausha viungo na mitishamba kwa ajili ya kuvihifadhi kwa muda mrefu kwa kuvikausha kwenye microwave. Anza na dakika 3, vitoe viangalie hadi ufikie kiwango cha ukavu unachohitaji.

·        Unateseka kuondoa maganda ya nyanya kwa kisu wakati unapotaka kupika? Ziweke ndani ya maji halafu pasha kwenye microwave kwa dakika tano. Zitoe ziache zikae kwa muda wa dakika mbili. Ngozi itaanza kusinyaa na kutoka kirahisi.

·        Unaweza kuyeyusha nyama na samaki zilizoganda kwa kutumia microwave. Chagua pale palipoandikwa defrost. Muda wa kuyeyusha unategemeana na uzito wa chakula, kama huna mizani kisia uzito wa unachotaka kuyeyusha. Microwave moja kwa moja itaseti muda baada ya wewe kuchagua kiasi cha uzito.

·        Matumizi mengine ya microwave ni pamoja na kuua vijidudu. Unaweza kuua vijidudu kwenye sponji la kuoshea vyombo kwa kuliweka kwenye macrowave likiwa limeloa. Litoe baada ya dakika 2.

Sina shaka kuwa hakika utakuwa unafurahia matumizi yako mapya ya microwave. Kama kuna ambayo unajua lakini sijaorodhesha hapa, tafadhali nijulishe nitapenda kusikia toka kwako.

Ni follow ig @vivimachange

No comments:

Post a Comment