Thursday, July 28, 2016

Ufuaji wa nguo za wanawake unazingatia aina ya nguo

 
Kujua ni lini nguo ya mwanamke ifuliwe inategemea aina ya nguo, anasema Bi Winnie Mamkwe ambaye ni mfuaji kwenye kituo cha kufulia nguo. Anaendelea kutujuza kuwa baadhi ya nguo zinaweza kuvaliwa mara kadhaa wakati nyingine zinatakiwa kufuliwa kila baada ya kuvaliwa mara moja. Tujielimishe kuhusu ufuaji nguo za wanawake kuanzia za ndani hadi
ofsini, ili kuzifanya zionekane mpya na za kuvutia wakati wote.

Nguo za ndani
Hizi ni pamoja na sidiria, chupi na zile za kubana tumbo/kutengeneza shepu. Kama hutoki jasho sana aidha kutokana na maumbile au hali ya hewa ya maeneo unayoishi na ulipo muda mwingi, sidiria inaweza kuvaliwa mara 3 hadi 4 kabla ya kufuliwa. Ila inahitaji kuachwa kwa masaa 24 bila kuvaliwa mara ya pili ili kuruhusu mipira kujirudi vizuri.

Endapo  mazingira ni ya jasho, ifue kila baada ya kuivaa mara moja. Namna unavyotunza sidiria zako ndivyo unapovaa inakupa muonekano wa ujana.

Ufuaji wa nguo za kutengeneza shepu unakaribia wa sidiria kwani zote zinavaliwa kugusana na ngozi, zinahitaji ufuaji wa mara kwa mara lakini bila kusahau umakini ili kufanya mipira ibaki imara. Chupi inatakiwa kufuliwa kila baada ya kuivaa.

Fulana na jeans
Fulana ni nguo ambayo inakamata mwili na haipishani sana na zile za ndani. Inanyonya jasho na mafuta yanayotoka mwilini na ndio maana nayo inapaswa kufuliwa kila baada ya
kuvaliwa mara moja. Unapofua fulana nyeupe usisahau makwapani ambapo uchafu ukiachwa unaweza kutengeneza rangi ya njano.

Jeans ni nzuri kuficha uchafu na madoa. Kama ni ya kushika mwili unaweza kuifua baada ya kuvaliwa mara 4 hata kama bado inaonekana safi. Kuepuka kupauka, fua na anika ukiwa umeigeuza nje kuwa ndani.

Blauzi
Blauzi inatakiwa kufuliwa baada ya kuvaliwa mara moja. Ila kama hutoi jasho sana au unaivaa tu masaa machache unaweza kuivaa tena kabla hujaifua. Epuka kuzidisha vipodozi vya makwapani kwani vinaweza kusababisha nguo kuchuja eneo hilo au kutengeneza doa.

Mavazi ya ofsini
Kama mavazi yako ya ofsini unayavaa katika ofisi ambayo ina viyoyozi, unaweza kuyavaa mara 2 hadi 3 kabla ya kuyafua, laa iwe umedondoshea lanchi mapajani kwa bahati mbaya. Mara zote tundika magauni, suruali au makoti ambayo umevaa kwa masaa 24 kabla ya kuvaa tena. Kwa mfano unaweza kuvaa gauni lako ofsini jumatatu halafu ukaliacha umelitundika na ukalivaa tena alhamisi. Kama utaona kuna umuhimu wa kupitisha pasi juu juu kuondoa mikunjo fulani basi fanya hivyo.

Makoti yanaweza kuvaliwa hata mara 4 kabla ya kufuliwa. Kuwa makini kuangalia maeneo yanaoonyesha uchafu kirahisi kama vile kwenye kola, mikononi na kwenye viwiko ili uwe na uhakika ni kusafi. Yaachie muda ya kupumua usivae mfululizo. Koti na suruali zinazofanana zifuliwe pamoja ili kuepuka moja kuchuja na mwenzake kubaki mpya.

Sweta
Sweta inayovaliwa juu ya nguo nyingine, unaweza kuivaa hadi mara 5 kabla ya kuifua. Ila kama unaivaa yenyewe na inagusana na mwili moja kwa moja, vaa mara moja au mbili tu baada ya hapo ifue.

Nguo za kulalia
Naamini unafahamu kuwa watu wote wanatokwa na jasho usiku. Fua pajama au nguo nyingine unayovaa wakati wa kulala kila baada ya kuivaa mara mbili hadi tatu. Kama unaoga muda ule kabla tu hujaingia kulala unaweza ukaivaa muda mrefu zaidi.

Nguo za mazoezi
Unapaswa kufua nguo zako za mazoezi kila baada ya kuzivaa mara moja. Unatokwa na jasho jingi na pia nguo hizi zinashika mwili kwahivyo ni rahisi kutoa harufu mbaya na pia kuhifadhi vijidudu.

Ushauri 0755 200023

No comments:

Post a Comment