Thursday, May 26, 2016

Namna ya kupanga vyakula ndani ya jokofu


Haishangazi jokofu kutoka kuwa katika hali ya usafi na mpangilio na mara moja kuhamia kwenye mvurugano na harufu mbaya za vyakula vilivyoharibika ambavyo hata havijulikani.

Lakini ni kwa namna gani katika maisha ya nyumbani unavyoweza kuanza mchakato wa kuweka mpangilio kwenye jokofu na friza? Kabla hatujaangalia hilo ni vyema tukakubaliana katika mambo matatu ambayo ni; si kila familia inanunua vyakula vingi vya
kuhifadhi kwa muda mrefu,  ukubwa wa familia unatofautiana kati ya moja na nyingine  kwahivyo wingi wa vyakula kwenye jokofu nao ni tofauti na jambo la tatu ni kwamba haya majokofu na friza yana miundo tofauti tofauti. La kwako linaweza kuwa tofauti kabisa na la yule.

 Baada ya kukubaliana hayo, sasa tuangalie dondoo hizi kadhaa nilizokuandalia ili kuwezesha na pia kuendeleza hali ya mpangilio ndani ya jokofu kwa ujumla, huku tukizingatia mambo hayo matatu hapo juu.

Sio kila chakula ni cha kuhifadhi kwenye jokofu
Ni vyema tutambue kuwa kuna vyakula ambavyo tunaweka kwenye jokofu kutokana tu na mazoea lakini kiuhalisia vinafaa kuhifadhiwa katika halijoto ya kawaida iliyopo hapo jikoni au stoo. Kuweka vyakula kwenye jokofu ambavyo havina sababu ya kuwekwa humo inaweza kuwa ni chaguo binafsi kutokana na kwamba jokofu lako lina nafasi ya kutosha kwasababu pengine una familia ndogo lakini jokofu ni kubwa, kwahivyo unaona tu kwanini usiweke na chakula fulani ndani yake.

Hifadhi pamoja vyakula vinavyofanana
Hii ni kanuni ya msingi ya mpangilio wowote ule, ili uweze kupata unachohitaji kwa haraka. Pale unapohitajika kuhifadhi chakula fulani ndani ya mfuko hasa kama ni kwenye friza iandike mifuko hiyo majina ya vyakula vilivyomo ndani. Weka ndani ya mifuko vyakula vya mbogamboga vilivyogandishwa. Wapo ambao wanagandisha mbogamboga kama vile nyanya, njegere mchicha na nyinginezo. Wakati huo huo ukikumbuka ukikumbuka kutenga sehemu ya nyama na mikate (ndio mikate ikigandishwa inakaa muda mrefu zaidi, unaitoa muda mfupi pale unapotaka kuanza kuitumia ndipo unahamishia kwenye jokofu yani sehemu isiyogandisha).

Vyakula vya maboksi na makopo vinafaa kuwekwa eneo la mashelfu wakati mbogamboga zisizogandishwa kama vile hoho, karoti, biringanya na kabichi vikipendeza kuwa kwenye droo ambazo kwenye miundo ya majokofu mengi ziko eneo la chini.

Vyakula vidogodogo kama vikopo vya maziwa mgando vinapendeza vikiwa ndani ya kikontena kwani inasaidia visianguke anguke au kusambaa kila mahali. Pia inakuwa rahisi kuchukua mara moja wakati ukihitaji kufanya hivyo na vilevile kugundua vilivyopita muda wa kutumia. Kama wewe na familia yako mnapendelea kununua maziwa yaliyo kwenye vikopo utakubaliana na mimi kuwa mara kadhaa kwenye kona nyuma ya jokofu  umeshakutana na ambayo yamepita muda wa kutumiwa. Unapokuwa umeyahifadhi pamoja inakuwa rahisi kung’amua.  Sasa basi, huenda wewe ni mpenzi wa  vikontena katika kuweka mpangilio, ni muhimu kuwa makini kuchagua ni wapi kwa kuvitumia kwa sababu vikiwa vingi vinaweza kuzuia nafasi ndani ya jokofu hasa kama jokofu hilo ni dogo.

Kila kiporo kiingize kwenye orodha ya mlo unaofuata
Ili kuzuia mrundikano wa viporo ndani ya jokofu, kabla ya kuandaa mlo mpya ni vyema kushirikisha kiporo cha mlo uliopita.

Tumia vyumba vidogovidogo jinsi ilivyokusudiwa
Watengenezaji wa majokofu wamefanya tafiti za kutosha na ndio maana wameweka vyumba mbalimbali vikubwa kwa vidogo kwa mfano sehemu za kuweka mayai, dawa, vinywaji vilivoko kwenye chupa na vingine nyingi. Kila kitu kinapokuwa eneo lake kwa mpangilio jokofu linakuwa nadhifu.

Weka majina ya vyakula kwenye mashelfu
Unaweza kutumia zile kalamu za kuandika na kufuta baadaye kuweka majina kwenye mashelfu hasa pale unapokuwa na friza refu kwenda juu lenye mashelfu juu mpaka chini. Mpishi atakapofungua kuchukua nyama ya ngombe, kuku au samaki majina yatamrahisishia shelfu la kwenda.


Je msomaji wangu ni zipi dondoo zako muhimu za kuweka mpangilio ndani ya jokofu au eneo lingine lolote ndani ya nyumba yako? Nishirikishe!

Nifuate instagram @vivimachange

No comments:

Post a Comment