Thursday, January 19, 2017

Namna ya kuweka mpangilio kwa dakika 15



Kama umeshagundua ni kwamba watu wengi wanajitetea kuwa hawana mpangilio ndani ya nyumba zao kwa ajili hawana muda wa kufanya hivyo. Na pengine hata wewe unayesoma hapa sasa hivi una sababu hiyohiyo. “Ooh napenda sana kuweka mpangilio na kuondoa mrundikano wa vitu lakini muda sina”.

Ni kweli watu wana pilika na
shughuli nyingi pengine ni kazini, au kwenye jamii, muda na familia au pia labda ni matukio ya kujifurahisha binafsi. Ndio maisha! Kwahivyo tunafanyaje sasa wakati tunapotaka kupangilia nyumba zetu lakini hakuonekani muwa na muda wa kutosha kufanya hivyo?

Kwanza kabisa tenga dakika 15 tu kila siku.
Haijalishi tuko na shughuli kiasi gani, karibia kila mmoja wetu anaweza kupata dakika 15 kwenye ratiba yake ya siku. Ndio inaweza kuwa ni kupunguza muda unaokuwa kwenye mitandao ya kijamii, au inaweza kumaanisha ni kuamka mapema dakika kadhaa kabla au kwenda kulala ukiwa umechelewa dakika kadhaa . Ila nikuambie ukweli kuwa kama unaweza kujitolea dakika 15 kila siku kwa ajili ya kuweka mpangilio, utapata matokeo makubwa baada ya kipindi fulani.

Hatua ya pili ni tengeneza orodha.
Chukua kalamu na karatasi na andika maeneo ambayo unatakiwa kuweka mpangilio. Na kama eneo unaona litahitaji zaidi ya dakika 15 basi ligawe katika maeneo madogodogo. Kwa mfano kama ni eneo la jikoni unaweza kuligawa katika maeneo madogo kama vile mpangilio kwenye jokofu, kwenye droo ya vijiko, kwenye kabati la vikontena na kadhalika.
Inawezekana maeneo mengine yakahitaji kupangiliwa zaidi ya mara moja.

Hatua ya tatu ni tegesha muda.
Kila siku kwenye zile dakika zako 15 chagua eneo moja kwenye orodha yako la kuweka mpangilio. Endapo dakika 15 zitaisha kabla hujamaliza na ukajikuta kwamba huwezi kuongeza dakika hata moja basi acha utamalizia kesho yake.

Hatua ya nne ni chambua ipasavyo.
Unapotumia dakika zako 15 kuweka mpangilio hakikisha unaangalia kila kitu kwa kina. Kwa mfano kama kuna vitu ambavyo vimevunjika, vina madoa au vimechakaa vitupe. Kama kuna kitu ambacho hutumii tena lakini kiko kwenye hali nzuri bado, kigawe. Tenga boksi kwa ajili ya hivi vitu vya kugawa na mara linapojaa peleka kwenye vituo vya watoto yatima au safirishia ndugu na majirani wa kijijini ambao kwa uchumi wao wanahitaji msaada huo.

Ni kweli kuwa saa nyingine moyo unakuwa mgumu kugawa vitu ambavyo vinafanya kazi vizuri lakini kumbuka kuwa kama hivitumii tena ukiendelea kuvihifadhi vitakusababishia mrundikano tu.

Hatua ya tano ni tenga eneo kwa kila kitu.                                                                        Utagundua kuwa ikiwa kila kitu kina eneo lake, ni rahisi sana kuweka vitu kwenye  mpangilio. Kwa ajili kinapokuwa kimetoka pale kilipotakiwa kuwa unachotakiwa ni kukichukua na kukirudisha hapo tu.

Haya sasa baada ya kupata elimu hii ya kutumia dakika 15 kila siku kuweka mpangilio ndani ya nyumba yako, je msomaji wangu uko tayari kufanya zoezi hili? Kama kweli mwaka huu unataka nyumba yako ianze kuwa na mpangilio nakushauri utumie elimu ya makala hii. Najua huenda unafikiri kuwa dakika 15 ni chache sana kuweza kufanya chochote lakini nakuambia jaribu na utaona matunda yake. Usisahau kurudi kunishukuru!


No comments:

Post a Comment