Monday, August 25, 2014

...marvelous monday...

marafiki zangu wa kweli wamerudi shule...


ukiniuliza best skill yangu ni ipi nitakujibu cleaning..yani iko moyoni. i love to make things and places spotless...

Thursday, August 21, 2014

my article for newspaper: makosa wakati wa kununua sofa


Makosa makubwa ya kuepuka wakati wa kununua sofa
Moja ya umuhimu wa makala kama hii ni kusaidia wadau kuchagua kilicho chema kwa ajili ya nyumba zao. Sofa ni fenicha ambayo muda mwingi wa maisha ya nyumbani unakuwa pale hivyo inatakiwa ikidhi viwango vya nyumba na maisha unayoishi. Kuhakikisha unapata sofa sahihi, epuka makosa haya makubwa unayoweza kufanya wakati wa kuinunua. Habari njema ni kuwa makosa haya yanaweza kuepukwa kama kutafanyika maandalizi kabla ya manunuzi. Makosa haya makubwa basi, ni yapi ambayo mara kwa mara wanunuzi wanayarudia?

Kusahau kupima ukubwa wa sebule yako

Unatakiwa kujua ukubwa wa chumba kabla ya kukua sofa ili kuwa na uhakika kuwa fenicha hiyo mpya itafiti. Usikimbilie kununua fenicha kabla ya kuwa na uhakika wa ukubwa wa chumba, zingatia itakavyokaa kwa kujali milango na madirisha.

Kama eneo husika kuna mwanga mwingi unaoingia zingatia rangi ya kitambaa kwani vipo vinavyopaushwa na jua. Sofa inatakiwa iendane na ukubwa wa chumba, isiwe kubwa sana wala kiduchu. Usitegemee kumbukumbu wakati ukiwa kwenye chumba cha maonyesho ya sofa, huwa inadanganya kuona kuwa sofa ni ndogo kwenye chumba hicho kwani eneo ni kubwa, pia sofa iwe na uwiano na fenicha nyingine sebuleni.

Kutokuwa makini na rangi
Je unafahamu kuwa rangi ya sofa inayoonekana kutokuwa na nguvu kwenye chumba cha maonyesho inaweza kuwa kinyume kwenye sebule yako? Nenda na mto wa sofa unaoupenda na kuutupia kwenye sofa unayotaka kununua ili kuona itakuwaje ndani mwako.

Mvinyo mwekundu unaenda kumwagika kwenye sofa zako, kama una wanyama wa ndani kama paka nao wanaenda kufanya mambo kwenye sofa yako, mwenza na watoto wanaenda kula bisi kwenye sofa zako; hata uwakataze mara ngapi. Kwa kuwa maisha halisi yanaendelea kila siku, unahitaji sofa ya kuweza kubeba madhila yote haya.

Kuchagua aina mbaya ya kitambaa cha sofa ni kosa la gharama. Chagua rangi na aina ya kitambaa kutokana na jinsi sofa inavyoenda kutumika. Kama sebule inatumika sana na ukanunua sofa ya kitambaa laini au rangi za mwanga, inaenda kuharibiwa hata kabla hujaifurahia. Rangi ya sofa iendane na fenicha, samani, rangi ya ukuta na taa.

Rangi nyeupe, maziwa au nyingine ya mwanga isiwe chaguao lako kama kwenye makazi yako kuna uwezekano wa tope na mikono michafu kufikia sofa. Siku zote chagua rangi ambayo unaipenda na unaweza kuishi nayo, usichague kwa kuangalia mitindo ya nyakati. Utaishi na hiyo rangi uliyochagua kwa miaka.

“Siwezi kukuambia ni mara ngapi nimefanya kazi na wateja ambao wanataka kubadili kitambaa cha sofa zao ambacho bado kiko vizuri bali ni kwa sababu tu wameichoka rangi yake”, anasema mtengeneza sofa Hamis Rajabu. Bahati mabaya ni kuwa haichukui muda kuchoka vitambaa vya maua maua, vyenye mistari mikali na vile vya rangi za giza, anasema Hamis. Ushauri wangu ni kuwa, chagua rangi ya kitambaa ambayo itashirikiana na rangi nyingi. Kama unapenda rangi nilizosema zinachosha mapema basi weka japo kwenye kiti kimoja cha pembeni lakini siyo kwa sofa nzima, anashauri Hamis

Kutokuomba ushauri kwa wauzaji
Ongea na watu wanaouza watakupa mawazo ambayo yatakupelekea kufanya maamuzi ya busara. Hata hivyo unamuizi wa mwisho ni wako ila unapenda kuwauliza wataalam usikie wanasemaje.

Kutofikiria sofa ina burudiko kiasi gani 
Utakubaliana na mimi kuwa mara nyingi unaweza kushindwa kupata usingizi kitandani, ila ukija kwenye sofa ukaegesha aidha ukiangalia muvi au kusoma kitabu haraka sana unapata usingizi. Ni muhimu kuwa sofa unayotaka kununua ikawa ya matumizi na burudani.

Kununua sofa kabla ya kuijaribu
Kama ambavyo sofa haitakiwi kuwa ndogo sana au kubwa sana kwenye chumba, vilevile isiwe ndogo sana au kubwa sana kwako. Kama ni mrefu, hakikisha ukikaa miguu yako itakaa vizuri. Kamwe usinunue sofa kabla ya kuijaribu, ikalie, ilalie, ijaribu kwa kila namna ambayo utaitumia nyumbani. Kama unapenda kupata usingizi wa mchana kwenye sofa hakikisha mikono yako iko vizuri kwenye sofa unayotaka kununua.

Haya ni makosa makubwa ya kuepukwa wakati wa kunua sofa. Endapo utafanya makosa haya utaishia kutoridhika  na sofa uliyonunua.
Tukutane wiki ijayo!


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

Tuesday, August 19, 2014

...vitu vizuri.... lunch yako leo

si mbaya ukaweka hapo paradodo...matunda muhimu...wanasema sio hadi uambiwe na d r

Thursday, August 14, 2014

my article for newspaper: maeneo tunayosahau kusafisha

 
Wakati ukiwa unasafisha makazi yako mwishoni mwa wiki hii, kumbuka kufanya usafi wa uhakika. Mara nyingi huwa tunasafisha maeneo na vitu vinavyoonekana. Makala hii itakujuza baadhi ya sehemu na vitu ambavyo kwa wengi ni rahisi kusahaulika kusafishwa na mwishoni utasema, ee kweli hapa huwa sisafishi.

Tunakumbuka kusafisha ndani ya jokofu, lakini je juu na chini yake? Ndani ni kwasababu huenda kila tunapofungua mlango wa jokofu harufu mbaya na macho yanatuashiria kuwa sasa ni wakati wa kusafisha. Juu ya jokofu kunabeba vumbi ambalo sio rahisi kuliona vinginevyo uwe ni mrefu sana. Nyuma na chini ya jokofu vile vile kunaweza kuwa kumebeba vumbi sawa na lile la juu. Na chini sio vumbi tu hata mabaki ya vyakula vinavyodondoka kwenye sakafu ya jikoni. Kinachotakiwa ni kusimama juu ya kiti na kusafisha juu  wakati kwa chini unachotakiwa ni kuomba mtu wa kukusaidia kulisogeza ili usiharibu sakafu yako kwa kuburuza. Jokofu likishakuwa limesogezwa, ni kiasi cha kufagia na kudeki.  Baada ya hapo lirudishe mahali pake.

Tunategemea feni majumbani mwetu kwa ajili ya kuleta mpepea wa ubaridi. Kwa kadri feni inavyotumika, ndivyo inavyojaa vumbi. Feni hasa za darini ni maarufu kwa kujaza tabaka la vumbi. Njia rahisi ya kuzisafisha ni kufuta kwa kutumia ufagio uwe wa kawaida au wa buibui uliofungiwa kitaulo kilicholoa kwenye brashi zake. Kulingana na majira na matumizi, feni zisafishwe walau mara moja hadi mbili kwa mwezi .

Ni kichekesho cha muda mrefu kuwa ndani ya nyumba sofa ndio eneo linalomeza vitu vidogodogo. Kwa sababu hii mito ya sofa (ile ya kukalia na kuegemea) inapaswa kuondolewa na ndani ya sofa kusafishwe. Japo kwa nyumba nyingi ndani ya sofa ni rahisi kusahaulika kusafishwa hadi pale vitu kama hereni, kalamu ama opener inapopotea ndio eneo hili linakumbukwa kua huenda mtoto kaficha humo. Kulingana na aina na ukubwa wa familia yako pengine huhitajiki kusafisha ndani ya sofa mara kwa mara. Usafi huu ujumuishe na kufua foronya za mito, ni kazi rahisi japo huwa inasahaulika.

Ndoo za taka za ndani ya nyumba zinaashiria kuwa zinahitajika kusafishwa ila pipa la nje linakosa kiashiria hiki kutokana na eneo lililopo. Ukiona jirani anaanza kuguna kila unapofungua pipa lako la nje la taka basi ni wakati wa kufikiria kulisafisha kiaina. Kwa kawaida mapipa ya taka ya nje yanahitaji kutupiwa jicho la usafi zaidi wakati wa kiangazi kuliko wa masika.

Kama una taa za vivuli ndani ya nyumba yako, kumbuka kusafisha kile kifaa kinachosababisha kivuli. Kuendana na jinsi kilivyotengenezwa iwe ni kwa kitambaa, kioo au plastiki zinaweza kusahaulika kufunguliwa na kusafishwa.

Majani ya mimea iliyooteshwa ndani ya nyumba husahaulika kufutwa vumbi. Haishangazi kukuta mmea wa ndani iwe ni nyumbani au mgahawani ukiwa na majani yaliyojaa vumbi.
Vipasha vyakula (microwave) vinachafuka sana ndani kwa kuwa wengi wanapasha vyakula ambavuo havijafunikwa. Uchafu huu wa matone ya michuzi unaorukia kwenye kuta za microwave hubaki na kukaukiana na ajili unapata moto kila vyakula vingine vinapopashwa. Haishangazi kukuta microwave ambayo kwa jinsi ilivyo ndani unapata ukakasi kupashia chakula.

Ingawa wengi hawana taabu ya kukumbuka kusafisha vioo iwe ni vya madirisha au vya kujitazama, kioo cha luninga ni eneo ambalo kwa wengi linasahaulika kusafishwa. Endapo luning hii inatumiwa na watoto wadogo ni rahisi kuona alama za vidole kwenye kioo pale inapokuwa imezimwa. Chukua muda kufuta vumbi luninga yako weekend hii ili kufanya kioo king’ae tena.

Vumbi linajikita kwenye vitabu. Chukua dasta kufuta vumbi vitabu vyako.

Ingawa tunaweza tusione uchafu na utando ulio kwenye vitasa vya milango ya nyumba zetu lakini upo. Na tunapovisafisha tunaweza tusihisi tofauti, lakini unajisikia vizuri kushika kitasa kisafi. Na zaidi ya yote kukinga nyumba yako na vijidudu vinavyotoka kwenye mikono michafu inayofungua milango kwa kushika vitasa hivi.
Ni nini na wapi unapofikiri watu wengi wanasahau kusafisha? Je kuna popote nimesahau?


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

Wednesday, August 13, 2014

bafu la wenza...

kwenye sanitary ware zetu hili sijaliona bado...au mdau wewe umelifuma wapi hili bongo?


Friday, August 8, 2014

wakati wa SNAPSHOTS...




house tour: Here's the $20M SoCal Mansion Kim and Kanye Just Bought

hebu tusafishe macho mdau tuone mambo hapa...
 wenye nyumba, kim & kanye
 ukifungua geti unakutana na muonekano huu wa mbele
 yasemekana ina vyumba 8 vya kulala
 vegetable garden nayo haijakosekana
 floor ni ya mbao...huenda baby north atalala hapa
kanye naye atakuwa anajilia raha za kisamaki hapa kwenye hii pool

Thursday, August 7, 2014

my article for newspaper: kusafisha vifaa vya kusafishia


Jinsi ya kusafisha vifaa vya kufanyia usafi

Hatusafishi vifaa vyetu vya kusafishia sio? Hata ukikataa, kubali tuu kuwa wengi hawasafishi. Wengi tunajua umuhimu wa kusafisha na kutunza vitu….ila vifaa vyetu vya kusafishia mara nyingi vinasahaulika. Haijalishi wewe ni msafi kiasi gani, haiwezekani kuweka nyumba safi kama vifaa vyako vya kusafishia havisafishwi! Makazi ya vijidudu vingi ni kwenye maeneo machafu. Angamiza vijidudu kwa kusafisha sponji na vifaa vyako vingine vya kusafishia!

Kwa sababu tu kinatumika kusafishia sio kuwa kinajisafisha chenyewe. Kiukweli vifaa vya kusafishia vinaweza kuwa makao ya uchafu, vijidudu, tope na harufu kama havitunzwi vizuri. Jinsi vifaa vinavyotunzwa ndivyo hela yako ya kununua vipya itakavyobaki mfukoni. Ufagio mchafu unachafua zaidi sakafu na pia uchafu huo unaweza kukwaruza sakafu yako. Mashine ya kusafishia kwa upepo ambayo haijasafishwa haifanyi kazi yake vizuri. Weka vifaa vyako katika hali ya usafi ili kuwa na matokeo mazuri.
Kuna ule usafi wa kawaida wa kusafisha vifaa vya kusafishia japo kwa sabuni na maji na kuviacha vikiwa safi tayari kwa kuanza usafi mwingine. Brashi za kusafishia bafuni zishafishwe kwa dawa za kuua vijidudu japo mara moja kwa mwezi. Brashi za kusugulia zaweza kusafishwa kwa maji na sabuni ya kawaida. Brashi zenye taka zilizojishikilia waweza kuchukua kijiti na kuondoa taratibu taka zote ziwe ni tope au nyuzi nyuzi.
Ndoo zako za kupigia deki usiziache zikiwa na uchafu wa aina yoyote hata kama ni maji yaliyotumika tayari. Ziache zikiwa kavu aidha kwa kuzigeuza juu chini.

Sponji la kuoshea vyombo uwe unaliosha kwa maji ya moto walau kila juma. Ikiwezekana hata kulichemsha jikoni itakubwa bora zaidi, wengine wanaenda hatua ya mbali zaidi ya kuliweka kwenye kipasha vyakula (microwave).  Ila kama utafanya hivi hakikisha sponji limeloa chepechepe kabla ya kuliweka kwenye microwave. “Asimilia 70 ya bacteria huishi kwenye sponji chafu”, anasema dokta Mbuya.

Tokea ukiwa mdogo, kulikuwa na kitambaa cha kufutia vumbi nyumbani. Ukichukua kitabu chenye vumbi unachukua kitambaa unakifuta. Vitambaa hivi vya kufutia vyumbi ambavyo wengi wetu wanaviita dasta vinapaswa kufuliwa kiumakini kama tunavyofungua nguo nyingine. Tofautisha kati ya vile vyenye uchafu mkubwa wa kudiriki kutengeneza utando na vile vyenye uchafu mwepesi.

Vichwa vya mop na madekio mengine vinapaswa kusuuzwa baada ya kufanyika usafi na kuachwa vikauke. Kabla ya kusuuza hakikisha kuwa unaondoa udongo wote, mchanga na hata majani yanayoweza kuwa yamejishikilia ndani. Sio sawa baadhi walivyozoea kuacha dekio linakanyagiwa mlangoni. Pale ni sehemu ya kuweka tandiko la mlangoni na sio dekio. Sabuni ya kawaida ya kufulia inatosha, huhitaji kuweka dawa za kusafishia kwenye vifaa hivi. Ila ni muhimu vikuke kwani vinaweza kutoa harufu ya uvundo.

Kusafisha mifagio..mmh ni wachache wanaofikiria kufanya hivyo! Unaweza kufungua ile sehemu ya brashi ukaitenganisha na fimbo na ukaiweka kwenye ndoo ukasafisha na brashi zako nyingine za kusafishia. Jambo la kuzingatia ni kuondoa matope kwanza kwa kuwa sehemu ya ufagio ya brashi ni maarufu kwa tope na uchafu uliojizunguishia kwenye vibrashi vyake.

Mashine za kusafishia kwa upepo zinatofautiana kiumuundo ila kuna dondoo kadhaa za kukuwezesha kuisafisha. Tafuta kama una kitabu ulichonunulia kitakuongoza jinsi ya kuisafisha. Hakikisha unamwaga mfuko wa kukusanya vumbi mara kwa mara. Kutegemea na jinsi unavyotumia mashine yako fua mfuko wa vumbi kila baada ya miezi mitatu. Uanike ili ukauke kabisa kwani ukiiurudisha ukiwa na unyevu utasababisha vumbi kufanya tope na hivyo kuiharibu mota kwa kuilazimisha ifanye kazi kubwa ya kusukuma kushindana na ukuta wa tope. Kama unasikia harufu ya vumbi inatoka ndani ya mashine yako ni kwa kuwa mfuko wa vumbi umejaa.

Ingawa hutumii mashine yako ya kufulia kwa kitu kingine zaidi ya nguo bado kuna wakati inakubidi ufungulie maji kuisafisha yenyewe bila kuweka nguo ndani.

Tumejuzana namna ya kusafisha vifaa vya usafi ambavyo tunatumia mara kwa mara nyumbani. Inaweza kuwa shughuli sahihi ya kufanya kwa muda wowote wa ziada ulio nao weekend hii!


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

alhamisi ya rasha rasha...

rasha rasha za leo za hapa na pale za kupunguza vumbi kwa tuliopo mazingira ya vumbi. hali ya hewa si joto wala baridi ni safi kabisa...