Wednesday, October 24, 2012

My article for newspaper: Unatokea ofsini kwenda kimnuso



Jinsi ya kuvaa ukiwa unatokea ofsini kwenda kwenye kimnuso

Ni saa kumi na moja jioni lakini sio muda wa kwenda nyumbani. Badala yake, kuna kimnuso na wanawake wengi walivyo ni tukio ambalo linaweza kukuacha ukihangaika juu ya nini huku duniani cha kuvaa kazini siku hiyo ili uunganishe na mtoko wako huo wa usiku.

Mbaya zaidi ni kuwa huna muda wa kwenda nyumbani kubadili ni lazima utokee kazini ulikokuwa umekaa mbele ya komptyuta moja kwa moja kwenye usiku wa tafrija na shampeni. Lakini kabla hujaumia kichwa zaidi, vitupio vinaweza kubadili kabisa muonekano wa vazi fulani kutoka muonekano wa kiofisi kwenda kwenye usiku wa sherehe.

Sasa ni wapi pa kuanzia? Anza siku yako kwa kuvaa sketi  fupi ya rangi yoyote na koti la rangi isiyofanana na sketi na kiblauzi ndani mwake. Usisahau mchuchumio wako kuonyesha umbile na urembo wako. Baada ya saa za kazi wakati wa kuelekea kwenye tafrija kama hutaweza kwenda nyumbani kubadili nguo unaweza kubaki na kiblauzi cha ndani ya koti na kuacha koti lako kwenye gari na beba pochi na sio ule mkoba mkubwa wa kazini.

Siri ya kuvaa nguo zile zile ila mionekano tofauti kutoka mchana kuingia usiku ni mpangilio wa  nguo na vitupio vyako. Changanya mavazi yako na vitupio kuendana na shughuli ya wakati husika ili mavazi yale yale yawe na mionekano tofauti. Jenga taswira mbalimbali kwa mfano kiatu hichi hicho ila na pochi tofauti tofauti inaonekanaje. Taswira ni msingi wa mafanikio yako.

Hereni zina nguvu kubwa ya kubadili muonekano wa mavazi ya kiofisi kwenda kwenye mg’ao wa muonekano wa usiku. Kama huwa huvai hereni kazini au unavaa vile vidogo sana basi usiku ni wakati wa kuvaa hereni kubwa zinazong’aa ambazo huwa zinabadilisha hata mavazi rahisi kabisa. Jaza shingo yako na mkufu au hata mtandio wenye rangi za kuwaka utabadili muonekano wa ofsini kuwa wa sherehe. Hii itasaidia kuleta mwanga na rangi usoni mwako na hivyo kubadili muonekano wako mzima. Kuendana na mtindo uliopo kuna wakati vidani, mikufu au shanga zinavaliwa zaidi ya mmoja na unaweza basi ukaongeza na bangili.

Pete kubwa yenye jiwe kubwa kati  iliyovaliwa kwenye kidole chochote inabadilisha muonekano wa kiofisi kuwa wa kisherehe zaidi. Pete hii moja tu inatosha usivae zaidi. Hakuna kitu kinachoonyesha unaelekea kazini kama mkoba wako. Mkoba unaweza kuharibu kabisa muonekano wako wa vazi la sherehe. Kwanye sherehe beba pochi (ile ndogo ambayo mara nyingi si ya kutundika) na weka vile vitu muhimu sana ambavyo ni lazma unavihitaji popote uwapo kama vile leseni ya udreva, pesa taslimu kidogo, kadi ya ATM, simu na funguo. Wakati wa kutoka kuelekea kwenye mnuso unaweza kufungia mkoba wako kwenye droo la ofsini na kuuchukua kesho yake. Kumbuka mkoba usiache kwenye gari kwani ni kishawishi kwa wezi wa kwenye magari.

Linapokuja swala la vipodozi, ukiwa unatokea ofsini kwenda moja kwa moja kwenye sherehe usijaribu kujipaka tena uso mzima. Badala yate tumia vichache tu kama lipstiki, ongezea mascara kidogo na kimguso cha poda kuondoa mngao kwemye uso wako na ongeza vipodozi kwenye mashavu.  Weka shedo za macho zenye rangi za silva na dhahabu. Vipodozi vya kwenye mashavu vizidi kidogo usiku kulinganisha na wakati wa kuwa ofsini.
Kwa nywele za chap chap chana ulizonazo kama ni fupi ama funga kifagio kama ni ndefu na kuongezea kibanio. Hizo hereni zako kubwa tayari zitakuwa zinashirikiana na nywele kuleta mvuto.

Mtandio ama skafu inasaidia sana kubadili muonekano wa mavazi toka siku ya kazi kwenda usiku wa kimnuso. Kwa ofsini funga kitambaa chako hicho shingoni wakati usiku  unaweza kufunga mtandio au skafu yako kiunoni kama mkanda.
Rangi zinaweza kuvalika kutokana na uamuzi wako ila nyeusi na nyeupe bado ni maarufu kwa wanawake. Vaa rangi kazini lakini zigeuze kuonyesha urembo wako nyakati za usiku.

Harufu yako ni muhimu kukamilisha muonekano wako mzima; inakupa utambulisho, wakati wa mchana tumia pafyum zenye ladha za maua ila usiku tumia pafyum yenye harufu kali zaidi kusisitiza utu wako.
Kama una mtoko utakaokugharimu kutokea ofisini moja kwa moja fuata dondoo hizi na zitakuongoza kupata muonekano wako wa kazini na usiku siku hiyo.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au  simu 0755 2000 23.





Sunday, October 21, 2012

ni kama jana tu

ukiona kitu kizuri cha kumfaa mwanao hata kama ni hapo miaka 10 ijayo usiache kumnunulia kwa ajili siku hazigandi. utashangaa mara anakitumia. nakumbuka baba mwenye nyumba alikutana na buti nzuri za mvulana kama wa miaka 12 akamchukulia mwanae wa miaka 2 watu wakamcheka na kumshangaa sana. lakini soon huyo kijana atazitinga..

Saturday, October 20, 2012

nikumbuke kwenye ufalme wako wa kuosha gari

tunapenda usafi. hutajutia hela yako. hatuna presha wala papara tunakusafishia gari yako tukiwa tumetuliza akili...karibu Ian CAR WASH survey karibia kabisa na pub le maarufu sana BRAJEC. tuonane weekend hii...xo

Friday, October 19, 2012

ukifanya haya utakuwa kwenye mahusiano yenye afya



Njia 3 za kufanya kuwa mahusiano mazuri zaidi
Mimi sio expati wa mahusiano. Ila nimegundua kuwa japo kila mahusiano ni ya kipekee na yanatofautiana ya kati ya  mtu na mtu kuna vitu vitatu ambavyo mahusiano yoyote yakivifuata vitaboresha uhusiano wa mtu na mwenzie.  Nakualika kujua hivi vitu vitatu tu: Kuwa mkweli. Kuwa tayari kukubaliana kutokubaliana . Kuwa tayari kukimbia.

Kuwa mkweli

Kutokuwa mkweli katika mahusiano ni sumu. Ni ngumu sana kukumbuka uongo wote uliowahi sema na ni nani ulimwambia. Kudanyanywa kunaumiza, Kuna faida nyingi ukiwa mkweli kwa patna wako. Kuna uhuru unaokuwa  ndani yake na ulinzi wa kujiamaini kuwa unaambiwa ukweli daima.


Kuwa tayari kukubali kutokubaliana


Inapokuwa ulikuwa singo kwa muda, una maono fulani kichwani kwako juu ya mambo fulani kuwa ndivyo unavyotaka yawe. Mara anakuja huyu mtu ambaye umempenda lakini ana mawazo tofauti na yako kwa labda kila unachotaka. Unajikuta inabidi ulegeze msimamo wako kiasi. Na unaona ni sawa tu. Lakini vinakuja vile vitu ambavyo unajisikia kabisa lazma viwe hivi na sio vile, unatakiwa kuwa na uhakika kuwa patna wako amekubaliana na wewe. Kwa hiyo ukiweza kulegeza msimamo kidogo na kuweka wazi kwa patna wako mnaweza kuja na solution ambayo itakuwa bora zaidi na wote mkaifurahia.


Kuwa tayari kukimbia


Fuata moyo wako. Unajua wakati mambo hayaendi sawa au jambo fulani patna wako alilofanya halileti heshima kwako. Ujue nini, unatakiwa ujipe raha mwenyewe. Kama unahisi kuwa hufurahii mahusiano yako ni sawa kukimbia hata kama ni kwa muda ili utulize kichwa uamue ni nini hasa unataka. Usijali watu watasema nini: chukua maisha yako mikononi mwako. Saa nyingine kujiondoa kwenye uhusiano ni kitu chema zaidi unachoweza kufanya kwako na kwa huyo mtu mwingine.

Tuesday, October 16, 2012

My article for newspaper: Miwani ya jua




Miwani ya jua ni zaidi ya kitupio cha mitindo
Ingawa umeshavaa tayari kuelekea kwenye mkutano au mtoko wako mwingine, unajisikia kuna kitu umekosa. Ni nini hicho? Ni hiyo miwani ya jua ambayo itakinga macho yako na jua na pia inaongeza mvuto wa muonekano wako.

Miwani ya jua inaimarisha afya na usalama wa jicho. Ni muhimu kuyapa macho yetu kipaumbele leo ili kuwa na uhakika wa ubora ule ule hapo uzeeni. Usitoke nyumbani bila ya  miwani yako ya jua hasa kwa siku ambayo jua ni kali. Kwa majira yote ya mwaka miwani ya jua inatakiwa kuwa sehemu ya kila siku ya maisha yako. Malaka hii itakujuza umuhimu wa miwani ya jua zaidi ya kuwa kitupio maarufu cha mitindo.

Miwani ya jua ina historia ndefu toka enzi za himaya ya Roma. Kutokana na kukua kwa teknolojia miwani hii nayo inabadilika kuendana na wakati.

Wavaaji leo wanajua miwani hii sio tu kitupio cha mitindo bali ni muhimu kwa afya ya macho yao kuyakinga na mionzi hatari ya jua ijulikanayo kama UV (Ultraviolet rays). Wengi wetu tunajua kuwa mionzi hii inaweza kusababisha saratani ya ngozi na matatizo mengine ya kiafya. Binadamu anaweza kuzuia yote hii kirahisi tu kwa kuvaa miwani sahihi ya jua ambayo inazuia mionzi ya UV hadi 100%. Tatizo ni kuwa huwezi kuona zuio hili kwa macho kwa kuwa ama limechanganywa au kuwekwa kama kingozi chembamba sana kwenye lensi. Njia ya kujua miwani ina zuio hili ni kwa kupima kwa kifaa maalumu au kusoma maelekezo yanayosema miwani ina zuio la UV kwa 100% au mingine imeandikwa UV 400.

Mitindo ndio inaamua ni miwani gani inaendana na wakati husika. Kutokana na kuwa na bei, staili na aina nyingi za miwani hii inaweza kuwa ngumu kwa mvaaji kuamua ni ipi anunue kutimiza kiu ya mitindo na kulinda afya ya macho yake. Wakati wa kununua zingatia vitu vikubwa vitatu ambavyo ni kinga ya jicho, ukivaa ujisikie huru na mtindo utakaokupendeza. Usidanganyike na rangi za lensi, ziwe kijani, nyekundu, kijivu na hata rangi ya udongo; zote zinaweza kufanya kazi kama ile ya lensi nyeusi. Zuio la UV liwe ni kigezo kikuu.

Chagua miwani kuendana na umbo la uso wako.  Kwa mfano kama umejaaliwa uso mnene, jitahidi kuepuka miwani itakayoonekana mikubwa sana au midogo sana. Vaa saizi ya kati na kama una uso wa pembe nne na hasa mataya makubwa epuka miwani yenye fremu nyembamba kwa ajili itafanya uonekane mpana sana. Kuna miwani inayowapendeza wenye sura ndefu na pia kuna inayowapendeza wenye sura pana ama za duara.

 Kama unavaa miwani ya jua wakati wa kuendesha chombo cha moto au kwenye kazi kama za bustani kwa mfano fikiria kununua yenye lensi imara zaidi na ambayo haivunjiki kurusha vipande vipande. Lensi inaweza kuwa ya kioo au plastiki au za kubadilika rangi kuendana na kiwango cha mwanga ni sawa tu ili mradi ziwe na zuio la UV. Fremu za rangi nyeusi na udongo zinampendeza walau kila mtu wakati zile za rangi rangi hazimpendezi kila mtu. Maelekezo ya uimara wa lensi utayapata kwenye duka ya muuzaji aliye mtaalamu na sio hiyo ya kununua mitaani. Hakikisha unajaribu miwani kabla hujainunua.
Wanawake wengi hawana uhakika jinsi ya kupaka vipodozi na miwani ya jua. Hii wala isiwe taabu. Oanisha rangi ya fremu za miwani yako na vipodozi utakavyotumia. Pia lensi nene zinafanya macho yawe makubwa kwa hiyo ukipaka wanja wa kope itasaidia kupunguza ukubwa wa jicho hivyo kuleta uwiano. Kwa vile miwani inalala maeneo ya nyusi hakikisha zimetindwa vyema na ukitaka zionekane zaidi basi ongezea wanja. Kope za kubandika zinaweza kugusa miwani na kuacha rangi ya maskara. Weka kope fupi na maskara isiwe nyingi kiasi cha kuweza kuchafua lensi za miwani. Usihisi kuwa unatakiwa kujaza vipodozi ili vionekane nje ya miwani. Wacha uzuri wa asili wa macho yako kwa kutumia vipodozi vichache.

Kuvaa miwani ya jua ndani ya majengo ni sawa kwa vile mvaaji ama anataka kuwa na mvuto au hataki kujulikana kwa sana kwa kila anayemfahamu.
Miwani ya wabunifu ni mizuri sana kimuonekano lakini sio kwamba ni ya kimuujiza kulinganisha na mingine. Kama chaguo lako la kuvaa miwani ya jua ni kwa ajili ya mitindo au ni kwa kukinga macho kutokana na jua, kumbuka kuwa haitakiwi kuwa ghali ili kufanya kazi iliyokusudiwa.

Kucheza salama, nunua miwani ya jua toka kwenye maduka yenye wataalam  ambayo unaweza kupata kwa bei ya kati ya elfu 20 hadi 50 na epuka kununua ya barabarani ambayo inaweza kuwa na zuio la UV lakini isiwe imara ya kudumu tuseme mwaka mzima. Kwa kawaida mtu anahitaji miwani ya jua moja tu. Usisahau watoto pia wanahitajika kuzuiwa macho yao yasiharibiwe na hii mionzi hatari ya jua.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au simu 0755 2000 23.