Thursday, November 28, 2013

My article for newspaper: Safisha mifereji

Masika yanaanza, safisha mifereji kabla haijasafisha mifuko yako



Kusafisha mifereji ya maji iliyojengewa kwenye nyumba (gutter) ni moja kati ya kazi muhimu za kufanya kipindi hiki ambacho masika yanaanza. Japo mara  nyingi huwa jambo hili inachukuliwa kijuu juu tu, kwa bahati mbaya wengi wetu tunasubiri hadi madhara yatokee ndio tunafikiria kusafisha mifereji ya nyumba zetu. Kuchelewa kuondoa majani ya miti yanayodondoka na kuingia ndani ya mifereji ya nyumba pamoja na vumbi kunasababisha matatizo makubwa mara mvua zinapoanza. Na hivyo kufanya kazi ya kusafisha iwe ngumu na kubwa zaidi. Majani yaliyoozea ndani ya mifereji pamoja na tope linalosababishwa na vumbi hukutana na maji ya mvua na kufanya tope kubwa zaidi linaloziba mfumo mzima wa usafirishaji maji ndani ya makazi yetu. 

Kama utasafisha mifereji ya maji kwenye makazi yako mara kadhaa kwa mwaka, hasa wakati wa miti kudondosha majani, usafishaji utakuwa rahisi. Mara moja pekee au kuacha kabisa, inaweza kuja kuwa kazi kubwa ambayo itakugharimu hela nyingi kwa shida zitakazotokana na kutosafisha huko.

Tatizo la mifereji iliyoziba ni kuwa maji ambayo yanasimama yanaharibu ukuta wa nyumba. Mifereji ya maji iliyojengewa kwenye nyumba yako imebuniwa kusukuma maji yaende chini kutoka kwenye paa yaende mbali na nyumba na msingi wake kwa ajili ya ukaukaji wa haraka wa maji maeneo yasiyohitajika kusimamisha maji au kuwa chepechepe. Maji yanayobaki yamesimama kwenye mifereji iliyoziba yanatafuta njia na kuweza kupenya kwa kupitia eneo lile ambalo ni dhaifu zaidi wakati yakijitahidi kuondoka, na hii inamaanisha kuwa yanaweza kukimbilia moja kwa moja kwenye ukuta na dari la nyumba yako.

Tatizo la kwanza kabisa la mifereji iliyoziba kwa majani na tope ni kuongezeka uzito. Hayo majani yaliyooza yakiloa, yananyonya maji ya mvua kama sponji na yanakuwa mazito haswaa. Mzigo huu unaweka msongo kwenye mifereji na vishikizo vyake na hii inaweza kuangusha mifereji toka kwenye nyumba. Mifereji iliyoanguka ni gharama kuweza kuirudishia tena, zaidi ya hayo taa au vioo vya dirisha vinavweza kuvunjika wakati mfereji ukiporomoka chini.

Maji yanayofurika kwenye mifereji yanaharibu rangi ya nyumba na pia michirizi ya maji inafanya alama kwenye kuta. Maeneo yenye mbao mirefeji ilikopita nako kunaozeshwa na maji yaliyoziba na kuanza kuvuja.
Msingi wa nyumba na sakafu zenye nyufa ni dalili nyingine pia za mifereji iliyoziba. Kama kwa kipindi kirefu maji hayataondoka kwenye msingi wa nyumba kuelekea sehemu yalikoelekezwa yanaweka kuangusha nyumba.

Sasa ni nini unachohitaji ili kufanya kazi hii ya kusafisha mifereji? Unahitaji vitu vichache kuendana na njia utakayochagua. Ila dhana kuu ni rahisi, ni kuchukua ngazi na kuvuta takataka toka kwenye mifereji. Unahitaji ngazi, ndoo ya kuwekea uchafu, mpira wa bustani na kama utapenda pia glavu.

Ondoa taka kutoka kwenye urefu wote wa mfereji na weka kwenye ndoo kwa ajili ya kwenda kutupa na baada ya hapo fungulia maji kwa kutumia mpira wa bustani ili kuondoa uchafu mdogo mdogo uliobaki. Hakikisha maji yanapita bila kikwazo na huu pia ni wakati mzuri wa kuona kama mifereji yako ina popote panapovuja kwenye kona au maungio. Kama kuna mahali panapovuja unaweza ukanunua silikoni ya kuzibia na kwa urahisi tu ukapaziba. Kumbuka kuwa maji yanatembea kufuata sehemu rahisi kupitia kwa hivyo ukiwa na mfereji unaovuja ni sawa tu na kuwa na mfereji ulioziba.

Kama unapenda sana unadhifu unaweza ukapaka nje ya mifereji yako rangi kufanya nyumba yako ionekane mwaa.
 
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa mazulia, nguo na magari; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Monday, November 25, 2013

hapa na pale

the dress is my own creation..mchanganyiko wa velvet na boda za kanga

kidali po...po

nimekutana na hii keki ya umbo la kibao cha nazi

My article for newspaper: TV Ukutani

Kabla hujaamua kufunga luninga ukutani zingatia mambo haya

Zile nyakati ambazo luninga ya kichogo kuwekwa juu ya meza au kabati la sebuleni zinaelekea ukingoni. Teknolojia imefanya luninga za kisasa zisikalishwe juu ya fenicha ili kupata muonekano angavu kutoka kila pembe. Luninga za kileo zina kipengele cha kuifunga ukutani kusaidia kuhifadhi eneo, kuboresha mambo na kuwezesha watu kuona vizuri kioo cha luninga yao.
Tunapozungumzia luninga za kufunga ukutani ni aina ya plasma na LCD. Kwa siku za karibuni luninga hizi zimekuwa ni chaguo maarufu zaidi kwa wenye nyumba wengi kutokana na kuwa na muonekano angavu, pembe pana za kutazama na wigo mpana wa rangi.

Moja kati ya jambo kubwa kabisa kuhusu kufunga luninga ukutani ni sio tu nafasi unayohifadhi ukilinganisha na kama ungeweka juu ya meza au kabati au shelfu bali pia ni muonekano nadhifu kwa mapambo yako ya ndani ya nyumba. Kwa mfano kama ulikuwa unaogopa kuwa luninga yako mpya itachukua eneo kubwa na hata nafasi ya kukaa kuongea na wageni wako kwenye mazungumzo yasiyohitaji kutizama luninga, unaweza kuweka kiti kimoja au viwili vya ziada chini ya ukuta ambao luninga imefungwa. Wewe na wageni wako mnaweza kukaa na kufurahia ushirika wa kila mmoja, lakini kama fenicha zako za sebuleni ziko kwenye mpanglio wa macho kuelekea kwenye luninga mpya yenye mvuto basi mazungumzo yenu yanaweza kukosa kitu fulani kwa akili kuzingatia zaidi muonekano wa luninga kuliko mazungumzo. Hata hivyo bado utakuwa na sofa au fenicha zilizopangwa kuelekeza macho kwenye luninga wakati utakapotaka kuongea huku ukitazama luninga.

Kwa maneno mengine, pia unaweza kuweka baadhi ya shelfu za vitabu au meza ya kahawa na kuacha nafasi ya kati wazi kwa kuweka kila fenicha yako ya kukalia karibia na ukuta ilikofungwa luninga, kama unataka chumba kiwe na muonekano wa thieta ya nyumbani.
Unaweza ukafikiri ni kupoteza hela lakini luninga hizi  za kufunga ukutani za plasma na LCD zina faida kwenye nyumba yako kwa hivyo usidharau. Teknolojia hii mpya sio tu kwa ajili ya muonekano angavu na mfumo bora wa sauti, ni kuwa hizi luninga za kioo kilicho flati na za kufunga ukutani zinawasaidia wenye nyumba wengi kutimaza upya nafasi ya sakafu iliyokuwa ikipotea, kwenye sebule, kwenye vyumba vya familia na hata kwenye vyumba vya kulala. Kufunga luninga ukutani ambayo inakufanya kuondokana na hilo kabati, meza ama shelfu la sebuleni inaweza ikaboresha sana nyumba yako kuliko hata hiyo luninga yenyewe.

Kuweza kufunga luninga ukutani unatakiwa kuwa na fundi anayejua jinsi ya “kucheza” na ukuta kwa maana ya kuutoboa au mseremala kuongeza mbao na fundi umeme wa kuunganisha waya za umeme na luninga na jinsi ya kuficha mrundikano wa waya na kebo. Kuna mambo muhimu ya kuzingatia kabla hujaamua kufunga luninga yako ukutani ambayo ni pamoja na kuamua ni ukuta upi unataka kufunga, waya zitakaa kaaje, muonekano, ukubwa na uzito wa luninga. Nyingi ya luninga hizi za plasma na LCD ambazo zinapendeza zaidi zikifungwa ukutani zina vifaa maalum vya kufungia ambavyo unatakiwa kununua kulingana na ukubwa na uzito wa luninga yako.

Katika kuamua ni wapi pa kufunga, fikiria ni wapi unapojisikia burudani zaidi wakati unapotazama luninga, unapendelea iwe juu ya usawa wa jicho ukiwa umekaa au iwe levo sawa na macho? Je unataka sauti kila mahali au ni eneo fulani tu la chumba. Kikawaida inatakiwa jicho lako liende katikati ya kioo cha luninga ukiwa umekaa. Unatakiwa kukaa raha mustarehe wakati ukitazama luninga. Pia, kuna uwezekano wa kuona picha  vizuri zaidi kichwa kikiwa wima kuliko kikiwa kwenye pembe. Kama unapendelea kuifunga luninga juu basi iweke kwa pembe ambayo itainama kuelekea chini.
Kaa kwenye hilo eneo unalopendelea kukaa kutizama luninga na angalia ukutani pale ambapo una mpango wa kufunga luninga yako. Je kuna mwanga unapiga kinyume na eneo hilo? Kama ndio je unaweza kurekebishika tuseme kwa kufunga pazia labda au kwa kusogeza taa ya kuhamishika. Mwanga kinyume na luninga unaweza kusumbua na hata kuharibu muonekano wa picha, kwa hiyo kabla ya kufunga luninga yako kuwa makini na vyanzo vya mwanga vya eneo unalotaka kufunga.

Fahamu kwa kina mahitaji yako ya burudani. Vyumba vya thieta za nyumbani kwa mfano, vinahitaji spika sahihi kwa sauti sahihi. Mahali pa kuweka spika napo panahusika kwa spika mbili au nne kuhitajika kuwekwa mbele ya luninga. Na nyingine mbili kwenye kona nyingine za maeneo ya kukaa.

Baadhi ya luninga ni nzito sana kufunga ukutani kwa hivyo kama nyumba yako ni ya zamani sana au haina kuta imara, utatakiwa kuiseti juu ya fenicha. Ukubwa pia unahusika kwenye kufunga luninga ukutani kwa ajili nati maalum vya kufungia vinaweza kufanya kazi kwa luninga zenye uzito na ukubwa fulani.  Haijalishi aina ya ukuta ilipofungwa, luninga inatakiwa iwe imefungwa imara kiasi cha kuzuia isianguke, na pia isicheze cheze hata kama iko karibia na mlango uliofunguliwa kwa nguvu. Kama huna uhakika na uimara wa kuta zako ni vyema kupata ushauri wa mtaalam.

Waya zinakaaje? Baadhi ya watu wanatoboa ukuta na kudumbukiza waya upande mwingine wa chumba ili kufanya chumba cha luninga kisiwe na mrundikano wa waya. Hata hivyo wengi wanapendeleaa kuwa na kila kitu yani luninga na waya kwenye chumba kimoja na kwa maana hiyo kuna jinsi ambayo fundi anaficha waya nyuma ya luninga iliyofungwa. Kuficha hizi waya inaweza kuwa ngumu au rahisi kutegemea na kiwango cha fundi cha utaalam na uvumilivu kwenye kufanya kazi yake. Ni vyema kufikiria jinsi ya kuficha/hifadhi waya zako kabla ya kuamua mahali pa kufunga luninga ukutani kwa kuwa kwa njia utakayochagua, eneo fulani la ukuta linaweza kufanikisha zaidi kuliko lingine.
“Luninga nyingi za flati hazina yale matundu ya kufungia ukutani yakiwa wazi— yanakuwa yamezibwa na vifuniko vya plastiki, unachotakiwa ni kuchukua bisibisi na kuyafungua”, anasema muuzaji Minja.

Walio wengi wanaweka luninga zao za plasma au LCD juu ya stendi au meza au fenicha nyingine. Lakini ni burudani gani iliyoko hapo? Moja ya jambo poa kuhusu kuwa na kuninga isiyokuwa ya kichogo ni uwezo wa kuifunga moja kwa moja ukutani! Luninga ya flati iliyofungwa ukutani ni mvuto wa mtazamaji. Pamoja na picha maridadi na sauti ya kiwango, luninga ya plasma au LCD inaleta mvuto na unadhifu wa muonekano wa chumba, hata hivyo nyaya na kebo za umeme zinazozagaa zinaweza kuharibu picha ya unadhifu ambao luninga za flati zilizofungwa ukutani zinasababisha.

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa mazulia, nguo na magari; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Thursday, November 14, 2013

My article for newspaper: Jinsi ya kuchagua rangi za dari



Inawezekana umekuwa na fikra ya kuwa dari sahihi ni dari nyeupe. Miaka mingi iliyopita dari halikuwa linahusika kwenye muonekano maridadi wa chumba. Ilikuwa tu kwamba ni dari. Ipo ipo tu huko juu, ikijisikia wivu kila wakati kuta nyingine zinavyopakwa rangi na yenyewe kuachwa kama ilivyo.

Katika kuchagua rangi za kupaka dari ya chumba, msanifu wa majengo bwana Haji anasema kanuni za msingi ni hizi: Dari ambazo zina rangi za mwanga kuliko za kuta zina hisia za kuwa juu wakati zile za giza zina hisia za kuwa chini. Kabla ya kuamua rangi unayotaka kupaka dari, fikiria vyanzo na kiasi cha mwanga chumba hicho kinachopokea wakati ule unaokitumia zaidi. Kwa mfano, mwanga wa jua unaogonga kwenye dari ya rangi ya pinki au bluu ya anga inaleta burudiko la nafsi. “Mwanga wa taa unaogonga kwenye dari ya rangi nyekundu ya nyanya inazaa mng’ao mkali,” anasema Haji.

Funguka na usidharau  uwezo ambao dari inaweza kuwa nao katika muonekano wa chumba. Kuna rangi ambazo zinaweza kukifanya chumba kiwe kikubwa, kidogo, rasmi au cha kawaida. Dari mara nyingi inasahaulika kuwa ni kama ukuta wa tano wa chumba. Wakati wa kubuni nyumba wenye nyumba wengi wanaweza wasifikirie kuwa muonekano na mtindo wa dari unahusu. Ukichagua rangi za mwanga zitafanya chumba kionekane kikubwa na ukichagua rangi za giza zitakifanya ionekane kidogo. Na mchanganyiko wa rangi uwe ni za mwanga au za giza una matokeo fulani juu ya hisia za ukubwa na udogo wa chumba.

Chumba cha sebule kikubwa chenye dari ndefu kinaweza kuleta hisia za kutokuwa na uwiano kwa kuwa sakafu na fenicha zinachukua chini ya nusu ya eneo, ikiacha eneo lilolobaki bila kitu. Rangi iliyopakwa kwenye dari ya aina hii inaweza kusaidia kuleta hisia za dari kuwa chini, inapumbaza jicho kuwa chumba ni kidogo na cha faragha zaidi. Kwenye chumba chenye fenciha chache za kutawanyika, dari zilizopakwa rangi zilizokolea inakuwa kitovu cha jicho, kuhamisha jicho kutoka kule kusikokuwa na vitupio.

Vyumba vidogo au vile vyenye dari fupi, vinaweza kuonekana na msongamano. Rangi za mwanga kwenye dari zinafanya vyumba hivi vionekane vikubwa. Kigezo kikuu cha kufanya nyumba ndogo ionekane kubwa ni kwa rangi za dari na kuta kutotofautiana sana. Kwa mfano, ukuta wa bluu iliyokolea na dari nyeupe haziwezi kufanikisha kuleta hisia za kukuza chumba. Lakini rangi kama njano isiyokolea ya ukuta na dari ya rangi ya maziwa zitawezesha chumba kionekane kuwa kikubwa, kuwa na mwanga na hewa.

Nyeupe mara nyingi inatumika kama rangi ya dari kwa kuwa inakubaliana na walau kila rangi kwenye gurudumu la rangi. Nyeupe juu ya kichwa ina tabia ya kupotea machoni kwa hivyo macho yanavutwa zaidi kwenye kuta na fenicha kuliko dari na kuwezesha sanaa zako za ukutani zionekane zaidi, na kama kuta hizo zina rangi za mwanga dari inaonekana iko juu, na pia kama kuta zina rangi isiyokolea zinaleta hisia ya chumba kuwa kikubwa.

Kwenye vyumba vinavyopokea mwanga wa jua kidogo, dari nyeupe inasaidia  kudaka huo mwanga kidogo na kuusambaza chumba kizima. Kama ilivyo kawaida ya rangi yoyote, rangi nyeupe inahitaji ushirikiano na rangi nyingine zilizoko hapo chumbani iwe ni ukuta, zulia, malazi, mbao ama pazia ili isijejisikia kama haipo mahali pake.

Kampuni zinazotengeneza rangi zina rangi nyeupe za aina tofauti tofauti, kuna ambazo ni za kupoa na kuna ambazo ni za kuwaka. Kwa hiyo chagua ambayo ungependa kuleta kwenye dari yako.
Vile vile kuna baadhi ya rangi  mbali na nyeupe ambazo kwa kuzitumia kwenye dari zinaweka kukufanya mara moja kubadili fikra zako kuhusu muonekano wa chumba. Baadhi yake ni bluu ya anga, njano ya siagi na pinki ya kitoto.

Vyumba vinavyokuwa na rangi sawa na ya kuta na dari vinasaidia dari kuchanganyika vema na eneo la chumba lililobaki. Kutegemea na rangi ulizochagua, hii inaweza kusaidia kufanya eneo liwe dogo au kubwa. Kwenye hivi vyumba vya kufanana kuta na dari unaweza ongeza utepe wa rangi ya mwanga na pia gusa yale maeneo ya kiusanifu, hii italeta mvuto kwenye chumba. Ni wapi unapoanzia na kumalizia kupaka rangi? Je mikanda ya dari unaipaka rangi sawa na dari lenyewe?

Kubadilisha rangi pale ukuta unapokutana na dari kutaelekeza jicho kwenye chumba badala ya darini. Pia muonekano wa rangi hauji tu toka kwenye rangi, unaweza kufikiri pia kuweka paa la vipande vya mbao.

Rangi unayochagua kupaka dari ya chumba inaweza kubadili kabisa hisia zako, lakini kuwa makini isizidi: kwa maeneo yale ya msingi ndani ya nyumba, ambayo watu wanakua mara nyingi, weka rangi ya dari isiyo kali ili usiwe unaichoka.
 
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa mazulia, nguo na magari; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Wednesday, November 13, 2013

una hitaji la kufuliwa nguo yako ya harusi?

waolewaji wengi wamekuwa wakikodi magauni ya harusi ambayo wakati mwingine hanahitaji marekebisho. sasa basi, kwakuwa wakodishaji wanakupa gauni safi na wewe hata kama kuna mahali unataka kurekebisha kwa kushikiza basi unatakiwa ulirudishe kama ulivyopewa. kama utahitaji kurekebisha gauni ina maana unalivaa mara mbili na kuwa utahitajika kulifua mara mbili. ya kwanza ni pale baada ya wewe kulijaribu na kumpelekea fundi kushikiza unapotaka kurekebisha au hata kama utashikiza mwenyewe. sasa hapa lazma gauni litachafuka, kwahivyo utahitajika kulifua tena baada ya kushikizwa na ufuaji huu ni tayari kwa kuvaa siku ya harusi. harusi ikiisha utalirudisha gauni ulikoazima na utahitajika kulifua tena. kwa hivyo mara nyingi waolewaji wanajikuta kutakiwa kufua gauni la harusi mara mbili. sasa basi baada ya hii stori ya kusisimua nakukaribisha uje kufua gauni lako la harusi Ian DC & Laundry. Hata ukupenda kuleta na hiyo taxedo mpya ya bwana harusi nayo tutakufulia, na hata marekebisho kama ya kupunguna urefu etc tutakufanyia.uchafu kwetu ni kama maziwa na asali. karaibuu
tunafua kwa uangalifu virembo yote vinabaki kama vilivyo.



Tuesday, November 12, 2013

Xmas hiyoo iko njiani yaja

anza kujikusanyia mapambo na kufikiria zawadi za sikukuu kama hivi...


hata ukimfungashia vimapochopocho ataona umemthamini

santa asisahaulike

vijibwa na xmas tree

vi bag kama hivi navyo waweza kuvifikiria kama zawadi. zawadi tu ndogo ndogo ila itaonyesha unajali. ila ukiona wa nini naye potelea mbali..naupenda huu wimbo...mchaga na taarabu...tumooo

rangi za xmas ni nyekundu na nyeupe. meza ya mahanjumati inang'aa u xmas

muonekano wa meza toka juu

chocolate nazo zimo

vidungurushi kibwena vya kupambia

Saturday, November 9, 2013

house tour

hebu tutembelee nyumba mojawapo ya majuu aka mamtoni aka ughaibuni aka etc etc. nyumba hii ina vyumba vitano vya kulala. twende pamoja kujipatia ideas za muonekano wa nyumba nje na ndani. naamini kuna wakati hata wabongo wanaweza kuwa huru kuonyesha makazi yao kama hivi na muda utakapofika nitakuletea hapa hapa..karibu msomaji
muonekano wa nje

mashallah boda zimekatiwa zikakubali

kwenye ujia. angalia vizulia unavyoweza kutupia kwenye corridor maarufu kama area rugs


bafuni
sebule

bedroom..rangi cream na pink zinaongeza mwanga

bedroom nyingine. wall paper na duvet zinaendana

master bedroom

dining room mmmh..

ofisi ya nyumbani

jiko lenye  kisehemu cha kulia


Friday, November 8, 2013

friday finest

watu wangu wadogo wameniambia hili pozi la picha linaitwa triangle..jamani. hapa lazima ucheke...

Thursday, November 7, 2013

My artice for newspaper: Uanzishaji na utunzaji wa bustani




Utaijua bustani yenye afya wakati unapoiona: laini, kama vile ni zulia la kijani limetandikwa chini, ukitembea humo hamna majani makavu yanayojaa miguuni kukufanya uchafuke miguu na viatu vyako. Sasa, kwa nini bustani yako haionekani hivyo? Kupata muonekano maridhawa wa bustani huenda ikatakiwa ubadili fikra zako, anasema mtaalamu na mbunifu wa bustani Hadija Adam. “Unajua jinsi wanavyosema utamu wa ngoma uingie ucheze? Vyema, unatakiwa ugeuke ukoka. Unatakiwa ufikiri ni nini ukoka unahitaji,” anasema Hadija. 
Vitu vya msingi anasema ni vya kawaida sana: jua, maji na mbolea. Ukishapata hivyo hapo ni furaha tu - kwako na kwa bustani yako.

Kuanzisha bustani mpya ni mchakato wa raha na changamoto pamoja. Inabidi maandalizi na mipango. Unatakiwa kuandaa eneo kwa kuondoa magugu yote na kujaza udongo kama itahitajika. Sasa hapa nikisema kujaza udongo kumbuka sio kila udongo unafaa. Bi Adam anasema hatua ya muhimu sana ambayo watu wengi wanaruka ni hii ya kujaza udongo. Ni muhimu sana kuweka udongo unaofaa na mbolea ya ng’ombe (sio ya kuku kwa kuwa ina tindikali kali kwa hivyo haifai kwa kuoteshea ukoka). Bi Hadija anashauri kama kiasi cha udongo ni robo tatu basi mbolea iwe robo. Katika kuchanganya na kusawazisha kwa kureki usilazimishe sana tambarare fuatilia ardhi ilivyo na mwelekeo wa maji ili usijesababisha kuweka dimbwi kwenye bustani yako wakati wa masika. Kuwa makini sana kwa kuwa ukishaotesha ukoka wako hutarudi nyuma tena na kuanza kung’oa kwa ajili ya makosa yaliyofanyika mwanzo.

Kuna aina nyingi za ukoka (majani) unazoweza kuotesha kwenye bustani yako. Nyingine ni laini na nyembamba sana (fikiria uwanja wa golfu na wa mpira wa miguu), wakati ukoka nyingine unaweza dhania umekanyaga nyasi kavu miguuni. Majani ni mengi na yanagundulika kila mwaka. Kwa majani haya yote hali ya hewa inachangia unawiri wake.

Hakuna swali ya kuwa kuweza kupata zulia zuri la ukoka lililofunga kila mahali kwa wakati mmoja ni kwa kuotesha mbegu kila mahali wakati wa mwanzo. Lakini hii inaweza kuwa gharama hasa kama unataka kufunga eneo kubwa. Badala yake unaweza kununua mbegu chache ukaotesha kitaku nawe ukaanza kujipatia mbegu zako kwenye kitalu hicho. Kumbuka hii ni kama kununua mbegu za kuweza kutosha eneo lako ni gharama sana. Kwa mfano, tukichukulia huu ukoka unaoitwa Canadian; mbegu za kujaa mfuko mmoja wa saruji zinauzwa kati ya elfu 30-40. Sasa kama eneo lako utahitaji mbegu mifuko hamsini kwa mfano, inaweza kuwa ni gharama kubwa kwako. Kwa hivyo nunua mifuko michache uoteshe kitalu uvune mbegu mwenyewe.

Sasa ukoka wako umeshaota na umeshafunga kila mahali na umerefuka kiasi ya kuwa unahitaji kuukatia. Inapokuja kwenye swala la kukata ukoka wa bustani wenye nyumba wengi wanashindwa kujua urefu sahihi. “Watu wengi wanakata ukoka wao kwa kuuacha mfupi sana, kitu ambacho kinayasababishia majani msongo,” anasema Bi Hadija. Anashauri usetie mashine  ya kukatia kwenye alama ya juu kabisa. Majani yakibaki marefu yanafanya mizizi ikue vizuri na pia inasaidia ardi isichomwe na jua la moja kwa moja na kuwa kavu kwani utaingia gharama ya kuongeza umwagiliaji. Na usiamini kuwa ukiacha majani yawe marefu ina maanisha kuyakata mara kwa mara kila baada ya muda mfupi, anasema Hadija. “Lakini hii ni uongo kabisa "kuna upotofu kwa watu wengi kuwa kama wakiyakata yakawa mafupi hautakata mara kwa mara, huu ni uongo; yanaota haraka mno kiasi kwamba hayakupunguzii muda wowote wa kukata tena.

Maji, maji, maji kila mahali. “Maji mara mbili kwa wiki ila maji mengi” kwa Hadija hii ndio kanuni ya msingi. Maji ya kuzama yanasaidia mizizi kupenya kina kirefu ardhini, wakati  maji kidogo kidogo kila siku yanasababisha vishina kukauka na kuzalisha majani makavu (ambayo ndio yanachafua miguu). Kumwagilia kwa kina pia kunafukuza wadudu wanaojishika kwenye majani. Kwa bustani mpya iliyooteshwa ukoka mwagilia maji mengi kila siku hadi mizizi ishike.

Bustani, hata ile unayoiona ina afya inahitaji chakula imara na hewa. Mara mbili au tatu kwa mwaka wakati wa masika wataalam wanashauri ndio wakati wa kuiwekea bustani mbolea. Kwa wakati huu mbolea ya kuku ndio inafaa zaidi hasa kuweza kutunza ule ukijani wa ukoka unaohitaji.

Magugu kwaheri, sio ajabu kuwa karibia kila bustani itakuwa na magugu. Njia nzuri ya kuangamiza magugu kwenye bustani ni kuchagua ukoka unaofunga kiasi kwamba utayazuia magugu kushamiri. Yale machache yatakayopenya dawa yake ni kuyang’oa.

Zingatia kanuni hizi za uanzishwaji na utunzaji wa bustani na kila mmoja atakuwa na furaha -- wewe na bustani yako.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa mazulia, nguo na magari; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk



morningwood

marafiki zangu wa ukweli asubuhi hii kijua kikiwachoma choma. yani huwa hawa watoto wakiwa mahali halafu mtu akauliza ni wa nani akijibiwa ni wa vivi huwa najisikia raha mno.furaha ya maisha yangu iko kwa hawa watu wangu wadogo

Saturday, November 2, 2013