Friday, February 28, 2014

Happy 6th birthday to my first miracle!

To Ian,
Thanks for being such an incredible son! You  are kind, respectful, powerful, and have a great sense of humor. You amaze me with your wisdom, your insight and your talent. Your father and I treasure the time we share together especially to see you growing day by day. Surely you are going to make a significant impact on our world. I am proud to call you my son. With no particular order, here are some of the best memories of you for the past 6 years:





Thursday, February 20, 2014

My article for newspaper: Kabla hujanunua microwave

Mambo unayotakiwa kufahamu kabla ya kununua microwave

Wanasema, “kama huwezi kuhimili joto, kaa mbali na jiko.” Microwave inakataa usemi huu wa zamani kwa kuweka joto mbali ukilinganisha na jiko lako la gesi, umeme, mkaa, kuni ama jiko lolote lile lingine. Teknolojia imefanya microwave isiwe tu kifaa cha kupashia chakula, bali kuiwezesha kumudu mahitaji ya mapishi mbalimbali. Kifaa hiki kinaweza kutumika kuchoma, kuoka, kuchemsha, kupasha, kuyeyusha na hivyo kufungua ulimwengu mpya kabisa wa mapishi rahisi kwako. Swali kuu:

Ni mambo gani unayotakiwa kufahamu kabla ya kunua microwave?
Hununui tanuri ya microwave kila mara kama unavyonunua vifaa vingine vya jikoni. Kabla hujaenda dukani kuna baadhi ya mambo ya kuzingatia. Ni vizuri kufikiria mambo haya kwanza na kulinganisha huduma zinazoweza kutolewa na microwave husika kwa hivyo kuwa na uamuzi wa busara.

Kununua microwave ni rahisi mno kwa ajili sokoni kuna wigo mpana wa  microwave zisizo za gharama kubwa. Unatakiwa ujue mahitaji yako kabla ya kuamua kuwa microwave fulani itakufaa. Zipo modeli zinazoweza kupika na kupasha kwa pamoja na zipo za kupasha peke yake. Fahamu ni chakula gani utakachoweza na usichoweza kupika kwa microwave. Microwave zina vipengele vinavyoelekeza haya yote. Hapa ni mambo ya kuzingatia kabla hujanunua.

Kama huitumii sana, uwezekano mkubwa ni kuwa unaitumia kwa kuyeyusha, kupasha au labda kuchoma bisi. Kwa maana hiyo huhitaji yenye vipengele vingi kwa hiyo usinunue ya namna hiyo!
Kama unapenda kupika na unathubutu kujaribu mapishi mbalimbali mapya kila siku, nunua microwave ya kisasa zaidi yenye vipengele vingi kuendana na mahitaji yako.

Je kuoka ni pendeleo lako na unapenda kuchoma sandwich, vitafunwa mbalimbali na pia kuoka keki? Micowave ambayo inaweza kufanya yote haya ni wazo zuri jikoni kwako.
Kama watoto wako wadogo pia watatumia microwave unayotaka kununua basi vipengele vya urahisi wa matumizi na usalama ni muhimu zaidi.

Je, matumizi ya nishati ya microwave unayotaka kununua yakoje? Wati kubwa zitapika chakula haraka ziadi. “Microwave nyingi zinahitaji nishati ambayo inaangukia kati ya wati 600 hadi 1500,” anasema Ali Maftaha ambaye ni meneja mauzo wa duka la vifaa vya jikoni. Vyakula vilivyobainishwa kuwa vinafaa kupikiwa kwenye microwave husika vinatumia nishati ya angalau wati 800 ili viweze kuiva sawasawa.

Ni wapi unapoenda kuweka microwave yako? Modeli za kuweka juu ya kaunta za jikoni ni maarufu zaidi – unachomeka tu kwenye umeme na kuanza kutumia. Microwave za kujengea zinahitajika kusimikwa kwa utaalamu, na kwa ujumla zina nguvu zaidi  na vipengele vingi zaidi. Kwa hivyo kuwa na ukakika ni wapi utaweka microwave yako kabla ya kuinunua. Kwa mfano hizi za kuweka juu ya kauta panahitjika nafasi ili kuifikia kirahisi kurahisisha matumizi.

Utashangazwa na vipengele ambavyo microwave inavyo. Kipo kipengele cha vyakula vya kupika kutokana na microwave kusoma hisia ya kiwango cha moto kitakachohitajika kwenye tanuri kutokana na mvuke unaozalishwa na chakula kinachopikwa. Vyakula vya kupika kwa programu vinaanza kupikwa kwa mguso mmoja tu: unaingiza chakula, unakiambia kifaa ni nini unapika, na kinaanza kupika. Microwave nyingi zina sehemu zilizosetiwa automatiki kwa kupika vyakula kama bisi na supu. Zinachagua zenyewe kiasi cha moto na muda utakaotumika.

Kuna kipengele cha kuyeyusha. Kwa mfano nyama imeganda na huna muda wa kuisubiri iyeyuke yenyewe. Microwave zote zina kipengele hiki, anasema Maftaha. Kipengele hiki nacho ni bora ukachagua microwave yenye kile cha automatiki ambapo utahitajika kuyeyusha kwa kubonyeza tu aina na uzito wa chakula. Microwave yenyewe ndio inachagua kiwango cha moto na muda utakaotumika kuyeyusha.

Kipengele kingine cha muhimu sana cha kuangalia kwenye microwave unayotaka kununua ni loki ya watoto. Hasa kama una watoto wa umri wa kutoweza kuitumia. Loki ya umeme (kama vile kubonyeza kitufe fulani) kitasaidia kuwazui wasiharibu kwa kuwasha tanuri kwa bahati mbaya.

Nunua microwave kwa kuzingatia ukubwa wa familia yako. Kwa jinsi familia ilivyo kubwa ndivyo microwave inatakiwa iwe kubwa. Kwa mfano hakikisha bakuli unalotumia litatosha kwenye tanuri ya microwave unayotaka kununua.

Mwisho kwenye mambo haya ya kuzigatia usisahau urahisi wa kusafisha microwave yako. Modeli za microwave ambazo zimetengenezwa kwa jinsi ambayo ndani hakunasi vyakula ni rahisi kusafisha.

Baadhi ya watu wanaogopa kutumia microwave kwa ajili wanaamini kuwa zinabadilisha kemikali ya asili ya chakula au zinasababisha uvimbe kutokana na mionzi.. Hata hivyo jambo hili limekataliwa na watafiti wengi. Mionzi inaweza kupenya pale tu mlango wa microwave unapokuwa umepasuka au haufungi vizuri, anasema mkemia Enos Kwai. Hata kama  ni kwa sababu hiyo, kuvuja kwa mionzi kunakuwa ni kidogo mno kuweza kusababisha tatizo lolote la kiafya.

Akili bora kabisa zinanolewa jikoni Miili bora kabisa ya mazoezi inalishwa hapa pia. Ni hii sehemu ambayo harufu nzuri zaidi ndani ya nyumba zinakotoka. Kutoka kwa bibi yako hadi kwa mama yako, ladha ya chakula kilichoandaliwa nyumbani sio cha mtu yeyote kusahau utamu wake. Unatamani hata kupika chakula hicho kwa mapishi mbali mabli lakini huna muda wa kutosha mikononi mwako. Jitwalie microwave ya vipengle mbalimbali viwe ni kupasha, kupika, kuoka, kuyeyusha na kuchoma leo ili ikurahisishie mambo.


Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange.  Vivi ni mjasiriamali  upande wa usafi wa nguo, mazulia na magari; pia ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa nyumba. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

house tour: njia mbali mbali za kurembesha sakafu kwa tile

pambo la kati 

waweza weka boda kama hivi

waweza pishanisha rangi mbili

Wednesday, February 19, 2014

NEWS: Serikali yaingiza sokoni nyumba 130

NYUMBA 130 kati ya 851 zilizojengwa Dar es Salaam eneo la Bunju A katika mradi
maalum wa ujenzi wa nyumba za watumishi wa umma, zimefikia hatua ya kukamilishwa.
 
Kutokana na mafanikio hayo, Serikali imeuagiza Wakala wa Barabara (Tanroads)
kujenga barabara katika eneo ambalo mradi huo unatekelezwa, ili kuwapunguzia
watumishi wa Serikali gharama.
Gharama za nyumba hizo zinaanzia Sh milioni 30 kwa nyumba ya vyumba vinne vya kulala hadi Sh milioni 140 kwa nyumba za ghorofa.
Mtendaji Mkuu wa Mradi kutoka Wakala wa Majengo (TBA), Elius Mwakalinga amesema
hayo jana Dar es Salaam wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa
Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli aliyefanya ziara ya ghafla katika eneo hilo.

Akiwasilisha ripoti hiyo, Mwakalinga alisema nyumba hizo ni sehemu ya nyumba
1,400 zitakazojengwa Dar es Salaam katika mwaka wa fedha 2013/2014 ukihusisha
ujenzi wa nyumba 2,500 katika mikoa 12 ya Tanzania Bara.
Alisema Wakala umepanga kuanza kuuza nyumba 155 kwa njia ya mkopo ingawa hadi
sasa watumishi 3,000 wameomba kuuziwa nyumba hizo.
“TBA imeandaa vigezo vitakavyozingatiwa kuuziwa nyumba ambavyo ni muda wa
mtumishi kazini, umuhimu wa kazi anayofanya mtumishi kulinganisha na eneo ilipo
nyumba husika, maombi ya muda mrefu na mahitaji ya haraka,” alisema Mwakalinga.

Alisema vigezo vingine ni pamoja na ulemavu, mjane, mgane au familia yenye mzania mmoja, uwezo wa mtumishi kulipa deni lote kwa wakati, malipo ya awali na mtumishi anayekaribia kustaafu na mafao yake yanatosha kulipia nyumba.
Hata hivyo alisema TBA imeanzisha kikosi cha Brigedia ya Ujenzi, ambacho kimeunda vikosi saba vitakavyojenga nyumba ambapo vikosi sita vitajenga nyumba za chini
hadi za ghorofa moja, na kikosi kimoja kitajenga nyumba za ghorofa hadi nane
lengo likiwa ni kukamilisha ujenzi wa nyumba 10,000 zinazotakiwa nchini.
Akizungumza katika ziara hiyo, Magufuli aliitaka TBA kutopandisha ghama za nyumba hizo na ikiwezekana ziendelee kushuka huku akiomba kuangaliwa kwa kodi ya
kuingiza vifaa hivyo vya ujenzi, ili kuwezesha ujenzi huo kukamilika na kuuzwa kwa gharama stahiki.
Kuhusu ujenzi wa barabara, aliiagiza Tanroads kutumia fedha za Mfuko wa Barabara katika ujenzi wa barabara katika eneo ambalo mradi huo unatekelezwa lengo likiwa ni kuendelea kuwapunguzia mzigo wa gharama watumishi wa Serikali.
“Wakati Tanzania inapata uhuru kulikuwa na nyumba 6,000 peke yake ambazo zilikuwa hazitoshi na hadi sasa suala la makazi ni gumu kwani watu milioni tatu wana
upungufu wa makazi,” alisema Dk Magufuli.

CHANZO: HABARILEO

house tour: mansion la Khloe Kardashian huko California

the reality TV star is asking $5.5million for her mediterranean-style villa which she shared with her soon-to- be ex-husband Lamar Odom.

hebu tuvinjari ndani na sie tujionee
ukiingia tu unakutana na muonekano huu

living room

dining room

jiko

stairwell

bedroom

bathroom


office ya nyumbani

patio
pool
muonekano wa nyuma

Monday, February 17, 2014

house tour: umuhimu wa paving blocks kwenye makazi yetu

dunia 'mzima' imepasisha paving blocks kama njia nambari moja ya kukausha maji fasta nje ya nyumba
maji hapa hayasimami ng'oo. super drainage..

fundi lazima ahakikishe anatafuta slope (ndio maana hizo mbao ziko hapo) kuelekeza maji kunakotakiwa

halafu kushindilia. hicho kimashine cha kushindilia huwa kinakodishwa kwa siku

fundi akichemka slope maji yanabaki yamesimama kati kama hivi. 

vitu vizuri: hawa watu hawa...

"asilimia asilimia" ya furaha ya maisha yangu ni hawa..je wewe mdau?

Friday, February 14, 2014

my everyday life

nimetoka kumchukua mtu wangu mdogo shule na huko nimekutana na jambo lililonigusa mno. mdau jambo hilo ni kuwa baada ya kugeuza shingo yangu nimemwona mwanafunzi mvulana mdogo wa miaka kati ya 3-4 anaingia kwenye gari na magango mikono yote miwili. Eeh Mungu, nikajisemea hebu subiri dakika moja. nikaamua kumwuliza mwalimu kulikoni mwanafunzi huyo mdogo hivyo kutembelea magango. 
mwalimu akaniambia kuwa mzazi wa huyo mtoto anasema kuwa mtoto wake alizaliwa mzima na akatembea vizuri kama watoto wengine ila baadaye kuna sindano aliyochoma ndiyo iliyosababisha miguu yake kukosa nguvu ndio maana anatembelea magango. kusema kweli nilivyomwona mtoto mwenyewe keshazoea miguu yake hiyo ya ziada kwa hivyo anacheka na yuko anafurahia kama watoto wengine tu. 
sasa mdau wangu kutokana na hili hatuwezi kumhukumu yeyote kuwa ndio mwenye kosa lililomsababishia huyu mtoto awe melemavu maisha yake yote ila nilichojifunza ni kuwa ni vyema kuhakikisha kuwa mtoto wako mdogo anapoumwa ni vyema kumpeleka kwa daktari wa watoto (pediatrician) na hata ukiweza nenda extra mile kwa kupata referal ya daktari unayetaka kumpelekea mtoto wako kabla ya kumpeleka. ni hayo tu mdau ila moyo wangu kweli umesoneneka. tusisahau kumshukuru Mungu kila siku kwani kiburi cha uzima kinawafanya wengi wamsahau. 

Uwe na valentine njema!

Thursday, February 13, 2014

my article for newspaper: kabla hujanunua jiko..

Mambo muhimu ya kuzingatia kabla ya kununa jiko

Umeamua kuwa kwenye vifaa vyako vya  jikoni vya zamani vinaondoka vipya vinaingia. Au labda unaanza mwanzo kabisa kwa kuwa ni jiko ama nyumba mpya. Kwa sababu yoyote ile ya uamuzi wako wa kununua jiko jipya makala hii itakufahamisha mambo muhimu ya kuzingatia kabla hujaingiza mikono yako mfukoni kutoa hiyo hela yako uliyopata kwa jasho.

Kwanza tuwekane sawa kuwa kwa lengo la makala hii, jiko litamaanisha kifaa kizima kinachotoa moto kwa ajili ya kupikia chakula. Jiko hili litakuwa na pande mbili ambapo upande wa kwanza wa jiko ni pale panapobandikwa sufuria na tutapaita stovu na wa pili ni pale pa kuokea na tutapaita tanuri. Kwa maana hiyo jiko linakuwa ni kifaa chote cha kutoa moto wa kupikia na sio chumba kizima cha jiko. Kwa ufafanuzi huo sasa tunaweza kuendelea.

Kununua jiko jipya ni uamuzi muhimu. Jiko jipya (au lililotumika) linaweza kuwa bei kubwa, na litaleta mabadiliko kwenye shughuli zako za mapishi na linagusa pia mapambo ya nyumba yako. Kuna mambo kadhaa ya kuzingatia wakati wa kuchagua jiko ambayo ni pamoja na ukubwa, nishati itakayotumika, umaridadi na bajeti. Baada ya kujichunguza, kutafakari na kulinganisha majiko yaliyopo sokoni, unaweza kuchagua jiko sahihi kwa ajili ya chumba chako cha jiko.

“Mambo ya kuzingatia kabla ya kununua jiko jipya mara nyingi yanategemea na kama unanunua  jiko kwa mara ya kwanza au hapana,” anasema Nassoro Ali, muuzaji msaidizi wa duka la vifaa vya nyumbani. “Kama ulishanunua jiko kabla, kwa kawaida walau utakuwa na mawazo ya ziada juu ya ni kitu gani hasa unatafuta,” anasema. Ali anasema kuwa watu wanaonunua majiko yao ya kwanza “hasa kwa uchumi huu,” wanaamua  tu kukimbilia modeli za bei rahisi zilizopo.

Ali anasema kuwa kwanza unatakiwe ujue kuwa utaweza kumudu chanzo kipi cha nishati kwa ajili ya jiko lako, je ni gesi au umeme. Baadhi ya wanunuzi wanamudu vyote. Hata hivyo, Ali ameongelea modeli mpya za majiko zilizopo ambazo zina stovu za gesi juu na tanuri ya umeme chini. “Wanunuzi wangu wengi wanapenda kupikia stovu za juu za gesi na kuwa na matokeo mazuri zaidi ya kuoka kwenye tanuri ya umeme. Modeli hii yenye kutumia nishati za aina mbili inakupa kilicho bora kwa dunia zote mbili,” anasema.

Kama unanunua jiko kwa mara ya kwanza, kitu cha muhimu zaidi kuzingatia ni ukubwa ili lifiti vizuri jikoni kwako. Ali anasema kuwa ukubwa wa kawaida zaidi kwa jiko la nyumbani ni upana wa inchi 30, ila kuna modeli nyingine ndogo hadi upana na inchi 26 na kubwa hadi upana wa inchi 48. Kama unaondoa jiko la zamani ili uweke jipya, ni vizuri zaidi kununua jiko la ukubwa uleule ili kuepuka gharama za marekebisho mapya ya kaunta na kabati zilizo jirani na jiko. Kama ni jiko jipya basi unaweza kununua jiko la ukubwa wowote kuendana na ukubwa wa chumba na ladha binafsi. Hakikisha fundi anayekujengea chumba chako cha jiko anakupa vipimo sahihi kabla ya kununua jiko jipya.

Kitu kinachofuata cha kuzingatia, anasema Ali, ni mtindo wako wa mapishi. Je unataka jiko lenye zile stovu tu kama huvutiwi na kuoka? Je unataka jiko lako liwe la stovu mbili, nne au tano? Idadi ya stovu itategemea na ni watu wangapi mara kwa mara unawapikia, vyakula unavyopendelea kupika na kama unafurahia kuoka vyakula.

Vyakula vingi vya mapishi ya kukaanga na kuchemsha vinafaa zaidi kupikiwa kwenye stovu ya gesi kwa kuwa ni rahisi kudhibiti kiasi cha moto. Pia ule muonekano wa moto unaleta hisia halisi ya mapishi na pia visahani vya stovu havichukui muda kupoa. Wataalamu wanasema tanuri la umeme kwa ajili ya kuoka linafaa zaidi kwa kuwa umeme unaleta joto lenye uwiano. Ila hala hala zile koili zinashika moto kwa muda mrefu hata baada ya kuzimwa kwa hivyo umakini mkubwa unahitajika!

Amua kama unahitaji jiko la kujengea ndani kwa ndani ama la kusimama peke yake. Stovu na tanuri la kujengea humo humo ni mtindo unaowezesha kuhifadhi nafasi na pia ni muonekano wa kisasa zaidi, ila linaweza kuwa gharama kusimika, kutengeneza ama kurudishia. Majiko ya kusimama peke yake ni bei rahisi zaidi na yanapatikana kwa wingi. Maamuzi yako juu ya kipendele hiki hayatategemea tu bajeti na muonekano bali pia usanidi wa chumba cha jiko lako. Ijulikane pia kuwa haya ya kusimama peke yake yanaweza kujengewa ila ukarabati wake unahitaji matengenezo makubwa.

Zingatia umaridadi wa jiko lako. Majiko yanakuja kwa rangi mbali mbali kama nyeupe, nyeusi, silva ya kutoshika kutu na rangi nyingine nyingi. Fikiria rangi za chumba chako cha jiko na vifaa vyako vingine hapo jikoni labla ya kuamua ununue jiko la rangi gani.

Baada ya hayo yote sasa ni wakati wa kuanza kupiga misele kwenye maduka ya wauzaji wa majiko ya nyumbani. Kuna makampuni lukuki ya nje yanayotengeneza majiko, fanya utafiti wa jiko, lifungue uone mlango wa tanuri unafungukaje. Angalia koili na shelfu zikoje. Muulize muuzaji maswali, omba vipeperushi na majarida yanayooneysha jiko litakavyoonekana baada ya kusimikwa nyumbani kwako. Kama una dishi la kuokea ama kikaangio ukipendacho sana nenda nacho unajaribu kitaaje kwenye jiko unalotaka kununua.

Ukiweza kufanikisha haya yote naamini utapata jiko la ladha na mfumo wako wa maisha. Mpishi anafurahia kufanya kazi yake kwenye jiko linalokidhi viwango.


Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange.  Vivi ni mjasiriamali  upande wa usafi wa nguo, mazulia na magari; pia ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa nyumba. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

vitu vizuri...ama kweli huyu ni first lady wa fashion





Monday, February 10, 2014

News Zuhusuzo Makazi/Nyumba: Mhh

Wakazi wakiri kula kinyesi bila kujua wilayani Karagwe

Karagwe. Baadhi ya wananchi wa  Kijiji cha Kafunjo, Kata ya Kiruruma, wilayani Karagwe, mkoani Kagera, wamesema wamekuwa wanakula kinyesi bila kujua kutokana na kutokuwa na vyoo bora.

 Wakizungumza kwenye mkutano wa hadhara kijijini hapo  mwishoni mwa wiki iliyopita, baada ya kutembelewa na Ofisa wa Afya kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu Wilaya ya Karagwe, kuwaelimisha jinsi ya ujenzi wa vyoo bora na matumizi yake.

Mmoja wa wakazi hao,  Renatus Kanyabuhura alisema kutokana na kutokuwa na vyoo bora, walikuwa wakila kinyesi kwa sababu walikuwa wakitoka chooni bila kunawa mikono na kuvuta sigara huku  wengine kula matunda.
“Kutokana na kutokuwa na vyoo bora, unakuta nzi wanaotoka chooni wanatua kwenye chakula na huku mlaji anaendelea, jambo linalojionyesha tunakula kinyesi,” alisema Kanyabuhura.

Naye Ofisa wa Afya, Moses Aligawesa alisema magonjwa mengi yanatokana na matumizi mabaya ya vyoo na kula kinyesi kwa njia tofauti.


Aligawesa alitaja magonjwa yanayotokana na kula kinyesi kuwa ni, kipindupindu, kuhara, kichocho, safura (minyoo) na kwamba,  magonjwa hayo yanaathiri kila mmoja kuanzia familia, kijiji, kata hadi taifa. Alisema choo bora ni shimo lenye urefu wa futi 12 na kuendelea, kinachosafishika, kuezekwa   bila kusahau kunawa mikono kwa kutumia maji na sabuni.


Sunday, February 9, 2014

News Zihusuzo Makazi/Nyumba: Wasanii watakiwa kuchangamkia nyumba

MWENYEKITI wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Profesa Penina Mlama ametoa mwito kwa wasanii kuchangamkia kuchangia ujenzi wa nyumba unaoratibiwa na Mtandao wa Wasanii Tanzania (SHIWATA) ili kujiandalia makazi.
Akizungumza baada ya kutembelea mradi wa ujenzi wa nyumba za wasanii katika kijiji cha Mwanzega, Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, Profesa Mlama alisema makazi ni sehemu ya maisha ya binadamu hivyo wasidharau mradi huo ni faida kubwa kwao.
Alisema nyumba ambazo ameziona ni nzuri, imara na zinauzwa bei ya chini ambayo huwezi kuzipata sehemu nyingine yoyote nchini na kuongeza kuwa kujenga kwa lengo la kuishi pamoja, kunatoa fursa ya wasanii kubuni njia nyingine ya kuanzisha miradi mbalimbali.
Profesa Mlama alitaka Shiwata isikate tamaa, bali iendelee kuwashawishi wasanii wajiunge na kuchangia ujenzi wa nyumba ili baadaye wasitafute visingizio kuwa hawakupewa fursa hiyo.
Naye Katibu Mtendaji wa Basata, Godfrey Mngereza alisifu Shiwata kubuni njia ya kuwasaidia wasanii kupata makazi na kuahidi kuwa baraza hilo litatoa ushirikiano na kutoa ushauri kila unapohitajika.
Mwenyekiti wa Shiwata, Cassim Taalib alisema mpango wa ujenzi wa nyumba za wasanii utaendelea kote nchini na kuwataka wasanii waungane kufanya kazi zao kwa pamoja.
Alisema mpaka sasa nyumba 38 zimekabidhiwa kwa wasanii waliochangia ujenzi katika kijiji cha Mwanzega Mkuranga na nyingine 21 zinatarajiwa kukabidhiwa mwezi ujao.
Shiwata mbali ya kusimamia ujenzi wa nyumba hizo, inasimamia matamasha ya wasanii wachanga, kuendesha makongamano ya kupambana na kuzuia dawa za kulevya na kutoa elimu na maadili kwa wasanii.
Chanzo cha habari hii ni kutoka magazetini


News Zihusuzo Makazi/Nyumba: Wakazi waomba ulinzi


WAKAZI wa kijiji cha Kidago katika Halmashauri ya wilaya ya Morogoro
ambao walivunjiwa makazi yao kwa kile kinachodaiwa kuvamia shamba la
mwekezaji Martin Shem, wameiomba serikali na vyombo vya usalama mkoani
Morogoro kuwawekea ulinzi.
Wamesema hali hiyo inatokana na kupokea vitisho kutoka kwa mwekezaji
huyo, hali inayowafanya waishi kwa wasiwasi. Januari 10 mwaka huu kaya
45 zenye wakazi 180 katika kijiji hicho walivunjiwa makazi yao kwa amri
ya Mahakama kwa madai ya kuvamia shamba la mwekezaji huyo.
Wakizungumza katika mkutano wa hadhara mara baada ya kutembelewa na
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera, wakazi wa hao wamemuomba
kamishna wa ardhi nchini kushughulikia kwa haraka mgogoro uliopo katika
shamba namba nne ili iweze kujulikana nani mwenye haki ya umiliki.
Kwa upande wake mkuu wa Mkoa wa Morogoro aliwataka wakazi wa kijiji
hicho kutokuwa na wasiwasi na kuwataka waishi kwa amani kwani jambo hilo
serikali inalishughulikia.
Aidha aliwataka wakazi hao kuendelea na shughuli za kilimo katika
shamba hilo wakati Serikali ikiendelea na utaratibu wa kuirudisha ardhi
hiyo mikononi mwa wananchi hao.
Awali katika kikao cha wadau wa ardhi pamoja na makamishna wa ardhi
kilichofanyika mkoani hapa, Naibu Waziri wa Ardhi, George Simbachawene
alishangazwa na kitendo cha mwekezaji huyo kuvunja makazi ya wananchi
hao na hivyo kuziagiza mamlaka husika kushughulikia suala hilo ili
kuondoa mgogoro uliopo.
Mgogoro wa shamba hilo lenye ukubwa wa ekari 1,080 ulianza tangu mwaka 1999 ambapo hadi sasa haujapatiwa ufumbuzi.

Thursday, February 6, 2014

My article for newspaper: Sinki la jikoni

Jinsi ya kupata sinki la jikoni litakalokufaa

Jiko linaweza kuwa moyo wa nyumba lakini sinki ndilo linabeba dhamana kubwa ya kazi ya jikoni. Hii ni kwa sababu ndani ya sinki ni mahali pekee panapotumika kwa shughuli  ya mwanzo na ya mwisho kwa chochote kinachofanyika jikoni. Ni mahali panapotumika zaidi wakati wa kuanza kupika na kumalizia kusafisha baada ya kupika. Sinki ni kiungo muhimu kwa jiko lolote. Linakuwezesha kufanya shughuli kadhaa kama vile kuosha vyombo, kujaza sufuria maji na kuosha mikono yako. Pia ni muhimu kwa muonekano wa jiko na linafanya chumba cha jiko kionekane maridadi.
Ingawa sinki imara linaweza kudumu hadi miaka 15 lakini huwa linachakaa, anasema muuzaji Awadh Hafidh. Rangi yake kwa mfano yale masinki ya rangi ya bati laini lisiloruhusu kutu inaanza kufifia, na kuvujisha maji kwa kuudhi kunaanza kutokea baadhi ya maeneo. Na kama unafikria marekebisho ya jiko ni busara kubadilisha sinki na bomba zake.

Masinki ya jikoni sokoni yapo ya maumbo mbalimbali ila aina kuu mbili za kawaida sana ni masinki yenye karai moja na yale yenye karai mbili. Sinki la karai moja linakupa karai pana zaidi. Hili linafaa zaidi kama utakuwa na vyombo vingi vya kuosha kwa wakati mmoja na masufuria yanayotumika kwenye jiko husika ni makubwa. Sinki lenye karai mbili za pembe nne zilizolingana ukubwa linafaa zaidi kwa kuoshea na kusuuzia vyombo hasa kama unaosha kwa mikono. Kwa hivyo unatakiwa kujua ukubwa wa chumba cha jiko lako na jinsi utakavyolitumia sinki lenyewe. Umbo na ukubwa wa sinki ni muhimu, na wakati unapoangalia ukubwa wa sinki tupia jicho kwenye kina chake pia. Kutegemea na matumizi ya jiko, sinki lenye kina kirefu ni bora zaidi kwa kuoshea vyombo na masufuria.

Watengenezaji wanazalisha sinki za jikoni zilizotengenezwa kwa vifaa na mitindo mbali mbali kutoka bati la kung’aa lisiloshika kutu hadi vifaa kadhaa vya kisasa zaidi, anasema Awadh. Pia sinki la jikoni ni mojawapo kati ya kifaa cha bei rahisi kinachojumuika kwenye ujenzi wa jiko. Ingawa kuna masinki ya jikoni za kifahari ya bei kubwa, kuna utajiri wa masinki mengi ya jikoni ya bei nafuu.

Cha muhimu msomaji ni kujipatia sinki imara ambalo halitatikisa bajeti yako. Kwa kuwa sinki hili linauzwa pekee kama lilivyo bila kujumuisha bomba, basi katika hatua itakayofuata utaweza kujichagulia bomba la sinki la jikoni la rangi na staili unayopenda.
Mara unapochagua umbo na ukubwa wa sinki unalotaka kuendana na mahitaji yako, uamuzi wako unaofuata ni kuamua juu ya vifaa mbalimbali vilivyotumika kutengenezea sinki hilo iwe ni bati lisiloshika kutu au enameli. Aina ya kifaa kilichotengenezea sinki utakachochagua kati ya hizi mbili itategemea zaidi na ladha binafsi na mfuko wako.

Masinki ya bati lisiloshika kutu ndio ya kawaida zaidi kwa ajili ya jikoni. Ni gharama nafuu, yanadumu na rangi yake ya silva inaendana sana na vifaa na vyombo vingine vya jikoni. Wakati unanunua sinki la aina hii chagua lile la bati nene kwani litadumu zaidi. Sinki la bati nene limetulia kwa hivyo kupunguza hata kelele za vyombo na kufanya mchakato wa kuandaa chakula kuwa wa kimya kimya.

Usisahau kuzingatia vitu vya ziada ambavyo huenda ukahitaji viwepo kwenye sinki lako la jikoni kwa mfano pampu ya sabuni. Baadhi ya masinki yatakuwa na alama hizo wakati mengine hayana.
Nakutakia uchaguzi mzuri wa sinki lako la jikoni.


Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange.  Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa nguo, mazulia na magari; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Wednesday, February 5, 2014

utathubutu ipi?

rangi hizi za kuta ni za kipekee ambazo huenda mtu mmoja ukazipenda sana na mwingine akazichukuia sana na mwingine hata asithubutu. hebu cheki vyumba hivi ufikirie kwa ni wewe ingekuwaje..
orange

bright yellow

nyeusiii


bathroom ya orange

oops! olive green

purple

Monday, February 3, 2014

wakati ni ukuta...du! du!

basi asubuhi hii nilikuwa naperuzi picha nikakutana na hii ya muongo mmoja uliopita niliyopiga asubuhi ya graduation yangu katika mishemishe za kutafuta sehemu ninayotakiwa kukaa kule engineering enzi hizo. basi nilitinga hicho kimtoto cha joho wacha watu washangae kudhania kuwa ni kitambaa kimeshonewa kwenye hicho kisweta..kumbe walaa ni mbwembwe tu......furahia jumatatu yako usikubali iwe bluu na wala usiruhusu mtu asikuibie furaha yako