Thursday, August 30, 2012

My Article for Newspaper: Viatu vinaweza kukutoa au kukuangusha!


Viatu vinaweza kukutoa au kukuangusha!

Kwa kawaida binadamu anapenda anachovaa miguuni hivyo kujua kanuni za jinsi ya kuvaa michuchumio, buti, flat na mkuki moyoni itakusaidia kununua kwa busara na kuvaa aina mbalimbali za viatu kuendana na mwili wako.
Viatu ni kiambatanisho cha mitindo kipendwacho sana na vinaweza kutoa ushuhuda kuhusu mvaaji awe ni mtu maarufu au sio. Viatu vinavyoonekana vizuri sana kwenye shelfu la duka la muuzaji vinaweza visikufae kutokana na mwili wako, baada ya kuviweka miguuni ndio unapoweza kufanya uamuzi.  Kutochagua sahihi wakati kuna viatu kibao itakua mbaya sana. Ni vizuri kujiangalia muonekano mzima toka utosini hadi kidole cha mguu kwenye kioo kirefu na kuona ni nini wataalamu wanasema juu ya viatu vitakavyokufaa.

Viatu vya wanaume vimegawanyika katika makundi mawili. Buti za ngozi na viatu kwa ajili ya kuvaa kila siku. Hii ndio mitindo ya viatu vya wanaume.

Haipingiki kuwa viatu ni mojawapo ya kitu kinachomgusa mtazamaji kwenye muonekano wa mvaaji. Haijalishi kuwa mguso ni hasi au chanya ila viatu ni kivutio cha mitindo kwa vizazi vyote. Baadhi tunaamini kuwa viatu  ndio vinaleta muonekano mzima wa utofauti  kwa waigizaji, wanasiasa, wanahabari na watu wote wanaoonekana mara kwa mara katika macho ya jamii. Ni ukweli kuwa viatu fulani fulani vinatoa tamko mvaaji ni mtu gani hasa kama mbunifu wa viatu husika atakuwa anajulikana pia. Tumeona na kusikia jinsi viatu vya mbunifu Christian Louboutin maarufu kama CL au Loubs vinavyowatamanisha watu wengi maarufu duniani kote. Viatu hivi vina soli ya rangi nyekundu ambayo kwa furaha ya kuvipata mvaaji akiweza kuvinunua anapiga picha akiwa kanyanyua mguu kuonyesha soli. 

Ndio, viatu vinaweza kufanya mavazi yakawa rasmi au sio rasmi. Kama una kifundo cha mguu chembamba una bahati kwani kwenye ulimwengu wa viatu utavipata vya kila aina na kila uzuri. Kila kitu kuanzia sketi fupi na mchuchumio hadi sketi ndefu na sandali vitakutoa bomba.
Viatu virefu vinene, maarufu kama magogo kwa miguu membamba vinaweza kuonekana kama vinamzidi mvaaji nguvu, jicheki uridhike kabla hujaamua kuvaa staili hii.

Kama miguu yako ni mifupi na myembamba kitu muhimu sana cha kukumbuka ni urefu. Hii ina maana kuwa unahitaji viatu virefu bila kambakamba. Nimesema bila kambakamba ili kusiwe na kitu chochote cha kugawanya mguu wako, isipokua tuu vile viatu maarufu kama sandali za  gladiator ambazo zinawapendeza wenye vifundo vidogo vya miguu. Kama unataka kujisikia huru unaweza kuvaa viatu flat ila na gauni lenye urefu wa kuvuka magoti. Vinginevyo miguu yako itaonekana mifupi zaidi. Viatu vilivyo wazi nyuma na vile virefu vilivyo slimu vitasaidia kufanya miguu  mizuri mifupi minene kuonekana mirefu.

Wanawake wenye vifundo vya miguu vinene wafikirie mara mbili kabla ya kuamua kuvaa viatu vilivyochonga vidoleni. Viatu vya duara mbele vitawapendeza zaidi. Pia viatu vyenye rangi iliyokolea na kisigino cha wastani vitapeleka macho ya mtazamaji kwenye viatu zaidi na kuyaondoa  kwenye kifundo hivyo kuleta uwiano kwenye muonekano mzima wa mguu wa mvaaji. Kwa wenye miguu yenye vifundo vinene viatu vya kamba kamba za kuzungushia mguu mzima viepukwe. Viatu vya kisigino cha wastani na vilivyo wazi vidoleni vitafaa zaidi kuliko vile vya flat na kuzibwa kotekote.

Kama una umbile refu na kifundo chako cha mguu ni chembamba basi umebahatika! Kila aina ya kiatu kutoka flat za kuziba kotekote hadi michuchumio ni kwa ajili yako. Angalia usisitize viatu vya kuchongoka vidoleni na hata buti za kisigino kirefu ambazo pia ni nzuri kwa wanawake wafupi.

Kwenye tukio maalumu kila mhudhuriaji anapenda kuonekana na viatu vya kisasa kwa hiyo vaa viatu sahihi kwa mwili wako. Neno moja: Haijalishi una mwili gani miguu ya aina gani, michuchumio mara zote itakufanya uonekane mrefu na mwembamba – unahitaji nini tena cha zaidi!
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange 0755 2000 23

No comments:

Post a Comment