Thursday, May 21, 2015

Tanzania ni Nchi Inayoongoza kuwa na Wakimbizi Wengi Barani Afrika

TANZANIA inaongoza kwa kuwa  na wakimbizi wengi barani Afrika ambapo inakadiriwa kwa sasa wapo 70,000 ikifuatiwa na Rwanda yenye wakimbizi 26,000.

Aidha,
Jimbo la Kivu Kusini katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ni la tatu likiwa na wakimbizi 9,000.

Inakadiriwa kuwa zaidi ya wakimbizi 105,000 walikimbia nchini Burundi na kwenda kutafuta hifadhi nchi jirani kutokana na mgogoro wa kisiasa unaoendelea nchini humo.

Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) nchini Tanzania, Damien Thuriaux.

Alisema, IOM kwa kushirikiana na Serikali za mikoa nchini pamoja na Umoja wa Mataifa  wamefanikiwa kuwaokoa wakimbizi wapatao 50,000 toka nchini Burundi waliokuwa katika kijiji kidogo cha Kagunga mpakani mwa Tanzania na Burundi.

Alisema, wakimbizi hao walikuwa wakichukuliwa katika kijiji hicho kwa usafiri wa mashua upande wa Tanzania, Ziwa Tanganyika ambapo mashua mbili zilikuwa zikibeba wakimbizi 600 kila siku na kusafiri umbali wa kilomita 60 kutoka Kagunga hadi Kigoma.

Sehemu ambayo wakimbizi 1,500 hukimbia kila siku kutoka Burundi kutokana na ghasia za kisiasa zinazoendelea.

Alisema, baadhi ya wakimbizi wamekuwa wakitembea umbali wa kilomita 170 na kufika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu ambapo IOM na washirika wake wamekuwa wakitoa misaada ya usafiri wa mabasi na malori.

Alisema, katika zoezi hilo wameweza kusaidiwa na serikali ya Tanzania.

"Mchakato unaoendelea sasa ni kuendelea kutoa misaada ya kibinadamu kwa wakimbizi hao, kwa kuwa sasa kuna msongamano mkubwa wa wakimbizi katika Kijiji cha Kagunga, ambapo wakimbizi wanasubiri usafiri wa mashua ili waweze kutoka na kuingia nchini Tanzania," alisema.

Alisema, watu 1,500 kuhamishwa kila siku kwa kutumia mashua ni idadi kubwa ambayo inaweza kuchukua zaidi ya mwezi mzima kuwaokoa wakimbizi hao.
MAJIRA

PICHA: RFI

No comments:

Post a Comment