Wednesday, December 19, 2012

My article for newspaper: Chumba cha kulia chakula wakati wa sikukuu


Wakati wa sikukuu ni wa kula na kunywa; weka chumba cha chakula tayari.

Chumba cha kulia chakula ni mahali ambapo familia hukutana na kula chakula huku wakishirikishana kila mmoja juu ya mwenendo wa siku yake ulivyokuwa. Sikukuu kadhaa zikiwa njiani zaja wengi wetu tunajua kuwa ni wakati wa kufurahi na jamaa zetu kwa kula na kunywa.

Kimsingi, wakati wa sikukuu unapaswa kuwa ni wa kusheherekea na kujumuika kwa wakati maalum na wapendwa wetu. Lakini kutokana na orodha ndefu ya mambo ya kufanya, zawadi za kununua, wageni wa kukarimiwa, mipango ya safari, wakati wa sikukuu kweli unaweza kuzalisha msongo wa mawazo. Kwa hiyo iwe unaalika familia kadhaa  pamoja au unapamba chumba chako cha kulia chakula kwa ajili ya watu wawili, makala hii itakupa dondoo chache za jinsi ya kufanya sikukuu yako iwe njema.

Kwanza panga mapema, usisubiri hadi dakika ya mwisho. Lakini ni nani asiyekaa hadi dakika ya mwisho na kuanza kuweka mipango siku hizi? Hata hivyo ni wazo zuri kuanza kuangalia kwenye stoo yako ni nini unacho na ni nini bado kinafanya kazi toka mwaka jana. Halafu tayarisha orodha ya nini unahitaji ili utakapoenda madukani kununua unajua moja kwa moja mahitaji yako.

Tafuta nafasi kwenye chumba chako cha kulia chakula kwa ajili ya mapambo. Kwa mfano ongeza ladha ya sikukuu kwa kufunga utepe wa rangi za sikukuu nyuma ya viti vya meza ya chakula. Usijaze mapambo ya sikukuu kwenye kila kitu kilicho chumba cha kulia chakula, na wala usitoe vifaa vyako vingine unavyotumia kila siku kwa ajili ya mapambo ya sikukuu. Ila badilisha muonekano wa kila siku kwenda kwenye wa kisikukuu sikukuu kwa mfano ondoa picha za kila siku na badala yake pamba kwa picha za msimu wa sikukuu. Kumbuka kutengeneza sehemu ya kati ya mapambo yako. Usisambaze mapambo kila eneo la chumba.

Sehemu ya kati ya mapambo ni ile inayoonekana zaidi kwa mfano kwenye chumba cha chakula sehemu hiyo itakuwa ni meza ya chakula. Meza ya chakula ndio fenicha kuu kwenye chumba cha kulia chakula. Inachukua nafasi kubwa zaidi na ndio inayotoa picha kamili ya muonekano wa chumba chote. Pamba meza hii wakati wa mlo wa sikukuu kwa vitu vya msingi kama kitambaa cha meza, napkini na bakuli la matunda.  Tupia kitambaa cha kupitia eneo la kati tu kisichofunika meza yote ili kuweza kuacha uzuri wa meza uonekane. Meza iliyopambwa vizuri ni msingi wa mlo wenye kumbukumbu.

Kosa moja kubwa ambalo watu wengi wanafanya ni kuremba mno pambo la kati la kwenye meza. Pambo hili kwa makosa linafanywa kuwa kubwa sana kiasi kuwa wageni wa upande mmoja wa meza hawaonani na wale wa upande wa pili hivyo linawagawa pande mbili na hivyo kupelekea kugawa mazungumzo ya wageni wako. Weka pambo la kati lililo dogo. Kitambaa cha meza kisaidie kuelekeza macho kwenye pambo la kati na sio kishindane na  pambo hilo kwa hivyo weka kitambaa kisicho na mbwembwe nyingi.  Angalia usipoteze nguvu nyingi kwenye kupamba na ukashindwa kufurahia sikukuu.

Meza za chakula kwa matumizi ya nyumbani ziko kwa ukubwa na maumbo tofauti tofauti kuendana na idadi ya watu kwa mfano zipo za watu wanne na hadi hata watu kumi na mbili. Meza hizi hasa zile za mbao ngumu zinauzwa gharama kubwa kwa hivyo kabla hujanya manunuzi hakikisha unanunua itakayokidhi mahitaji yako.
Kwa ujumla chumba cha kula chakula kilichokamilika kwa uchache kinatakiwa kiwe na fenicha ambazo ni meza, viti na kabati la pembeni. Kuendana na ukubwa wa chumba fenicha hizi zinaweza kuzidi lakini zisipungue. Kazi ya kabati la pembeni ni kuhifadhia vyombo vya ziada, vitambaa vya meza na pia juu yake panatumika kama sehemu ya kuwekea mabakuli ya vyakula na/au kuwekea  mapambo na mishumaa. Kioo cha ukutani juu ya kabati hili kitasaidia kuakisi mwanga na kuonyesha kama eneo ni kubwa kuliko kiukweli lilivyo.

Taa maalumu ya kuning’inia juu ya meza ya chakula ni lazima. Taa hii iwe na ukubwa sahihi kuendana na ukubwa wa chumba na pia muonekano wake uoane na mapambo mengine yaliyopo eneo hilo.

Wakati wengi wetu tukifikiria chumba cha kulia chakula tunafikiria meza, viti, kabati na taa kuna kitu ambacho kina umuhimu sawa na hivi nacho ni pazia. Zaidi ya fenicha zote ngumu zinazojaza chumba hiki ni muhimu kuwa na vitambaa ambavyo vinaleta hali ya ulaini. Kwa hiyo kama huna utamaduni wa kuweka pazia kwenye chumba chako cha kulia chakula, inalipa kuanza kufikiria kufanya hivyo.

Ni rahisi kuchoshwa na hekaheka na shamrashamra za sikukuu, lakini usisahau sehemu muhimu sana ya sikukuu ni kuona wapendwa wako, kuwa na wakati mzuri pamoja na kuhesabu baraka zenu !!

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23

No comments:

Post a Comment