Wednesday, December 5, 2012

My article for newspaper: Fanana na mazingira yako



Fanana na mazingira ya nyumbani kwako
Kila mtu anachagua ni vipi anataka mazingira ya nyumbani kwake yawe. Ingawa tunaweza tusijali kuhusu uchaguzi huo lakini mazingira yetu ni dili kubwa kutuhusu. Una nafasi ya kutengeneza mazingira ambayo yatarahisisha maisha yako ama yatayafanya  yazidi kuwa magumu.

Kuna kanuni ya kwanza ya msingi kuwa katika kila kitu kilichopo kwenye eneo linalokuzunguka kina nguvu fulani iwe kitu hicho kina uhai ama hakina. Ni kama watu wa kale walivyoamini kuwa kila kitu kina uhai. Kanuni ya pili ni kuwa kila kitu kwenye mazingira yetu kinahusiana na kitu kingine. Inawezekana kwa mtizamo wa kiroho au wa kisayansi. Na kanuni ya tatu ni kuwa kila kitu kinabadilika kila wakati.

Sasa basi kama kila kitu kwenye mazingira yako kina uhai na kimeunganishwa na wewe basi mabadiliko yakitokea kwenye eneo lako nawe unaguswa. Mazingira yako yanakugusa nawe unayaakisi. Hii ni kama usemi kuwa kila kitu kwenye mazingira yako kinaongea na wewe. Je vitu vya mazingira yako vinasema yale ambayo unapenda kusikia, je vinakusaidia kupata kile unachotaka kupata katika maisha.

Fikiria jinsi unavyoingia nyumbani kwako na kukumbuka usemi kuwa unachokutana nacho mwanzo kinakugusa zaidi . Kama unaingilia varanda iliyojaa makorokoro kila mara unapoingia nyumbani kuna uwezekano mkubwa wa kuchoka hapo hapo nje hata kabla hujafika ndani. Vilevile kama unatembea kuelekea karibia na kizuizi unaanza kujifikiria kuwa inahitaji nguvu kupita pale. Pia kama unafungua mlango wa ofisi asubuhi na kukutana na meza iliyojaa nyaraka, unaweza kujisikia kama siku yako tayari imejaa na hakuna nafasi ya kuanza kitu kipya kwa siku hiyo.

Tembelea kila chumba nyumbani kwako. Je kuna kitu kinakuambia kuwa maisha ni mazuri na yamejaa fursa? Au una picha usiyoipenda, fenicha ambayo haijakaa sawa au rangi ya ukuta ambayo inakupa ukakasi kuitazama? Kila mara unapooana vitu kama hivi, unapotembelea chumba hiki unapata ujumbe hasi. Hata kama akili yako itazoea kuona hivyo lakini dhamira itakuwa inakereka.

Mkusanyiko wa picha unaweza kuwa chanjo cha ujumbe hasi. Hakikisha ni za kumbukumbu na hisia nzuri za watu hao kwako. Zinaweza kuwa ni picha nzuri sana kwa kuonekana kwa macho lakini kama mojawapo inakukumbusha tukio au wakati wa huzuni basi iondoe.  Weka zile zinazokufanya uwe na tabasamu. Watu mara nyingi wana picha kwenye kuta zao kwa sababu tu hawana kitu kingine cha kuweka hapo na sio kwamba ni kwa kuwa wanakipenda kilichopo. Sanaa ukutani inaweza kuwa nzuri sana ila kama ukiitazama haikubariki haina faida kwako. Badala yake inakupa ujumbe hasi na kukunyonya nguvu kila unapoiona. Ni vyema kuiondoa na kuacha nafasi kwa kitu ambacho kinakupa mtizamo chanya katika maisha.

Kuchukua hatua hii mbele zaidi, fikiria ni nini unakipenda kwenye maisha. Mfano mzuri ni mtu anayetaka kuwa na uhusiano. Mara nyingi picha atakazoweka nyumbani kwake na hasa chumba cha kulala ni za akiwa singo. Chumba hicho kitakuwa na taa moja tu ya kivuli na hata kimeza cha kando kimoja. Vyote hivi vinatoa ujumbe kuwa mhusika hana mtu. Badala ya vitu vilivyopo kwenye seti kwa mfano picha yenye watu wawili, na taa mbili za vivuli vinaleta alama za mahusiano.

Mazingira ya mahali unapoishi yanahusika katika kila eneo la maisha yako. Kama unahitaji akili tulivu hakikisha kuwa mazingira yako hayakupi kinyume na matakwa yako kwa kuwa na vitu ambavyo haviko mahali pake. Pia kama unataka kuwa mbunifu zaidi angalia kama je kuna nafasi zaidi ya kuweza kuwa hivyo? Kama unahitaji miundo mbinu safi je njia ya kuendea mlangoni kwako ni wazi, safi na inakaribisha?
Unavyotembea kwenye mazingira ya nyumbani kwako angalia kila kitu kwa jicho la ziada. Ondoa kila kitu ambacho huwezi ukasimama na kushuhudia kuwa unakipenda na ni kitu ungependa kuwa nacho. Unaweza usiwe na kiti kingine cha kuweka kwenye hiyo sehemu ulipotoa kile usichokipenda, lakini kama kinakuletea tukio la huzuni badi potelea mbali kitoe tu. Kinaziba kile unachokipenda na pia hicho usichokipenda kinakuletea hisia mbaya. Kwa kuamini utapata kingine unatengeneza uwezekano. Kuwa makini na hivyo vitu vinavyoongea na wewe furaha na kuvipa nafasi ya heshima nyumbani kwako.

Katika nyakati hizi za mihangaiko mingi, ni muhimu kuwa mazingira yako hayakuongezei vikwazo kwenye dunia yako. Hii inahusu hata taarifa za habari kwenye matukio ya mauaji, ajali na mengi ya kutisha. Fuatilia ni nini kiko kwenye vyumba vya watoto. Kama mazingira ya vyumba vyao yanaongea amani, watakua wakijifunza amani.
Kwa kuwa makini na kila kitu kwenye mazingira yako unatengeneza makazi ambayo yanafanana na wewe kwa kukupa ujumbe chanya na zenye kukutia nguvu. Kuwa kitu kimoja na makazi yako unakuwa na mtizamo chanya zaidi katika maisha. Mtazamo chaya unagusa kila kitu kwenye maisha yako. Yasikilize mazingira yako.

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23

No comments:

Post a Comment