Friday, May 5, 2017

Njia 7 za kupendezesha meza ya chakula

Ndani ya nyumba kuna meza za aina nyingi kama vile meza ya kahawa, meza ya kwenye korido, meza ndogo za pembeni mwa makochi na  pembeni mwa kitanda bila kusahau meza ya kuvalia na pia wapo baadhi wenye meza katikati ya jiko. Kati ya meza hizi zote meza ya chakula ndio ina changamoto kubwa katika kuipendezesha kuliko hizi nyingine. Hii ni kwasababu ya
umuhimu wake kuwa pamoja na kwamba wewe mwenye nyumba au mkaaji unataka meza yako ipendeze lakini wakati huo huo ikitumika kulia chakula.

Makala hii itakujuza njia kadhaa za kupendezesha meza ya chakula bila kubughudhi kazi yake kuu ambayo ni watu kukaa na kula chakula.

Kwanza kabisa katika kufahamu njia za kupendezesha meza hii ni vyema ufahamu kuwa kuna maumbo matatu yaliyozoeleka zaidi ya meza za chakula. Maumbo hayo ni meza za pembe nne, za yai au za umbo la duara. Unapopendezesha meza ni muhimu sana kuzingatia umbo lake. Kwa mfano trei la duara litaendana na kupendezesha zaidi meza ya duara na sio ya pembe nne.

Njia ya kwanza ni kwa kutumia usemi ambao sisi wapendezeshaji tunaita ni nguvu ya vitu vitatu. Vesi tatu, tepe tatu au mabakuli matatu yaliyowekwa maua au matunda yawe ni makavu au hai  yakisambazwa katikati ya meza yanaipendezesha na wala hayabughudhi walaji wakati wa chakula.

Njia ya pili ni kwa kuweka trei katikati ya meza. Trei hilo unaweza ukalibebesha vitu vidgodogo kama vile kichupa cha kuhifadhia chumvi ya mezani, vijiti vya kuondoa nyama katikati ya meno na kiungo chochote ambacho hakihitaji kuwekwa kwenye jokofu lakini kinatumika wakati wa kula.

Njia ya tatu ni kwa kuweka mishumaa mwili pamoja na  stendi/vibebeo vyake kwenye kila upande wa meza.

Njia ya nne ni kwa kutandika utepe wa meza na kuweka bakuli lenye mipira midogo ya mapambo hapo katikati ya meza.

Njia ya tano ni kwa kutumia mati za kuwekea sahani. Mati hizi zinatumika wakati wa kula lakini baada ya hapo meza inafutwa vizuri na zinarudishwa hapohapo mezani zinakaa muda wote kuwe na mlo au kusiwe na mlo.

Njia ya sita ni kuweka pambo lolote lenye umbo la chombo au chakula au tunda. Kwa mfano kuna mapambo ya seramiki yaliyotengenezwa mfano wa birika au tunda kubwa kama boga na kadhalika. Pambo la namna hii ni kwa ajili ya kuweka kwenye meza ya chakula.

Njia ya saba ni ile ambayo ni ya kale ya kutandika kitambaa cha meza. Ingawaje bado kuna wanaotumia njia hii wengi wanaona kama vile inaficha uzuri wa meza. Kwahivyo utakuta wenye nyumba wengi wenye meza za kuvutia aidha wanatumia kitambaa wakati wa chakula tu lakini baada ya hapo kinaondolewa na meza kupambwa kwa kutumia moja kati ya hizi njia nyingine.

Msomaji wangu hizo ni baadhi ya njia za kupendezesha meza ya chakula, usikubali ya kwako ibaki shaghalabaghala badala yake tumia njia moja ua mbili kati ya hizo.

No comments:

Post a Comment