Friday, December 14, 2012

My article for newspaper: Maazimio ya mwaka mpya kwa makazi yako


Mazingira ya nyumbani kwako yasaidie kufanikisha maazimio yako ya mwaka mpya

Ni wakati mwingine tena wa mwaka ambao wengi wetu wanapenda kufanya mabadiliko kwenye maisha yao. Je umeshafikiria mabadiliko ya mwaka mpya kwa ajili ya kiota chako? Japo mabadiliko haya yanajulikana na wengi zaidi kama maazimio, kwa kutia msisitizo zaidi makala hii itayaita malengo. Malengo yanatamkwa kwa kusisitiza wakati uliopo ni nini tamanio lako (kwa mfano kuamua kubadili mpangilio wa fenicha za sebuleni kwako ili kuwezesha kunogesha zaidi mazungumzo) wakati maazimio yanatamka ni nini ungependa huko mbeleni ya kuwa unaenda kufanya nini wakati ujao.

Mara nyingi malengo (au maazimio) ya mwaka mpya yanatupiliwa mbali hata kama nguvu za kutosha ziliwekwa ili kuhakikisha yanafanikiwa. Moja ya sababu za malengo kutofanikiwa ni mazingira ya nyumbani kwako kutosaidia kuwezesha mafanikio ya malengo hayo. Kama unataka kufanya mabadiliko ndani ya maisha yako bila kuhusisha mazingira yako kufanikiwa ni hatihati. Kwa maana ya kwamba kama unaweka malengo yako ya mwaka 2013 kwa ajili ya makazi yako na ukayaacha mazingira yalivyo, ni ngumu sana kubadili chochote. Hata matangazo kwa mfano ya kujikinga na maambukizi ya VVU yanaonyesha uhusiano kati ya maambukizi na mazingira fulani ambayo yanachochea maambukizi hayo.

Kanuni ya malengo kuwa na uhusiano na mazingira inahusika karibia katika kila kitu. Kama unataka mwaka ujao uwe tofauti basi unatakiwa kuweka mazingira ya kuwezesha malengo yako.
Je mazingira yako yanakusaidia kupata kile unachokihitaji? Kwenye mazingira ya nyumbani kwako vitu ambavyo havijakaa mahali pake au vimekaa mahali ambapo havifanyi kazi yake au havitumiki tena vinakukwamisha kutimiza malengo yako hapo nyumbani. Tembelea kwenye makabati ya nguo na vyombo angalia kwa umakini kuona ni vitu gani vya kuhifadhi, vya kugawa ama vya kutupa. Fanya hivyo kwa nia ya kupata nafasi ya kile tu kitakachosaidia kufanikisha malengo yako.

Pengine lengo lako la mwaka mpya ni kutokula hovyo kwa nia ya kupungua uzito. Je mara zote unaingia nyumbani kwa kupitia mlango wa nyuma ambapo unaingilia moja kwa moja jikoni? Kumbuka kanuni kuwa unachokiona mwanzo kinagusa zaidi akili yako, kwa hiyo kama mara ungiapo ndani unakutana na jokufu, chakula na kadhalika utapata hamu ya kula hapo hapo. Tumia mlango wa mbele ambapo utaona kitu tofauti mara uingiapo ndani - kitu ambacho hakitakufikirisha kula.

Mahusiano mengi yanaweza kuboreshwa kwa mapambo ya nyumbani hasa katika swala la kuwasiliana. Je chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni mahali patakatifu kwa wawili? Hakikisha vitu kama taa, vimeza, na viti kwenye chumba hicho viko viwili viwili.
Au lengo lako mwakani ni kuwa na wageni wengi zaidi nyumbani? Hakikisha basi mlango wa mbele unaonekana na kuna njia ya wazi ya kuingilia. Taa zinazomulika njia ya kuelekea mlango huo ziwe zinafanya kazi. Pitia mlango wa mbele kama mgeni mtarajiwa uone kama kila kitu kiko sawa. Je njia hiyo inakaribisha? Na sebule yako je nayo inavutia kwa ajili ya wageni wako wengi ambao unapenda kuwaalika nyumbani mwakani?

Kwa wale ambao azimio lao kuu la mwaka 2013 ni kupamba nyumba zao hakikisha unachagua rangi kwa umakini, fikiria mpangilio wa fenicha je zinawatendea haki watumiaji wa chumba husika. Angalia vitu ambavyo inabidi uvifanyie kazi ili kuboresha muonekano wa makazi yako. Kama kwa mfano sakafu ya sebule yako ni ya marumaru na unachoka kusugua na kudeki kila siku na unakiri kuwa ni ngumu kuifanya iwe safi; basi weka zulia kubwa ambapo utapitisha mashine ya kunyonya mchanga mara mbili au tatu kwa wiki.
Ikiwa unaazimia kutojaza vyombo vichafu kwenye karo basi mwaka ujao lenga kuosha chombo mara baada ya kukitumia. Na hata hakikisha wanafamilia wengine pia wanafanya hivyo.

Huenda kijani kinakubariki lakini huna eneo kubwa ya kuweza kuwa na bustani za ardhini. Otesha basi bustani za kwenye vyungu walau ukifungua pazia la chumba cha kulala kunapopambazuka ukutane na kijani. Azimia kupamba ndani mwako kwa maua freshi japo mara moja kwa mwezi.
Kweli, baadhi ya mabadiliko ya nyumbani kwako unaweza kuhitaji kutafuta msaada, lakini kuna mabadiliko mengi sana ambayo hayahitaji gharama lakini yanahitaji muda na nguvu ( na pengine kautaalamu)  kwahiyo kwa 2013 kwa nini usiazimie kupamba mwenyewe? Unaonaje? Ni azimio moja zuri kwa ajili ya makazi yako ambalo unaweza kutekeleza. Fanya usafi mkubwa ndani ya nyumba yako mara moja kwa mwezi ( weka tarehe kwenye kalenda yako na isismamie). Shikrikisha na wanafamilia wengine pia.

Hii inaweza isikubalike kwa baadhi ya watu ila ni mawazo binafsi kuwa azimia kila anayeingia ndani avue viatu mlangoni. Viatu vya wanawake vilivyo na visigino vya ncha kali mara nyingine vinakwaruza sakafu za marumaru na mbao na kuacha alama na vile vya wanaume baadhi vina soli zinazoacha rangi sakafuni na hivyo kufanya sakafu ionekane zee kuliko kawaida.

Mwaka ujao lenga kuweka nyumba yako nadhifu kila mara kama vile unategemea mgeni wa heshima!

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23

Wednesday, December 5, 2012

My article for newspaper: Fanana na mazingira yako



Fanana na mazingira ya nyumbani kwako
Kila mtu anachagua ni vipi anataka mazingira ya nyumbani kwake yawe. Ingawa tunaweza tusijali kuhusu uchaguzi huo lakini mazingira yetu ni dili kubwa kutuhusu. Una nafasi ya kutengeneza mazingira ambayo yatarahisisha maisha yako ama yatayafanya  yazidi kuwa magumu.

Kuna kanuni ya kwanza ya msingi kuwa katika kila kitu kilichopo kwenye eneo linalokuzunguka kina nguvu fulani iwe kitu hicho kina uhai ama hakina. Ni kama watu wa kale walivyoamini kuwa kila kitu kina uhai. Kanuni ya pili ni kuwa kila kitu kwenye mazingira yetu kinahusiana na kitu kingine. Inawezekana kwa mtizamo wa kiroho au wa kisayansi. Na kanuni ya tatu ni kuwa kila kitu kinabadilika kila wakati.

Sasa basi kama kila kitu kwenye mazingira yako kina uhai na kimeunganishwa na wewe basi mabadiliko yakitokea kwenye eneo lako nawe unaguswa. Mazingira yako yanakugusa nawe unayaakisi. Hii ni kama usemi kuwa kila kitu kwenye mazingira yako kinaongea na wewe. Je vitu vya mazingira yako vinasema yale ambayo unapenda kusikia, je vinakusaidia kupata kile unachotaka kupata katika maisha.

Fikiria jinsi unavyoingia nyumbani kwako na kukumbuka usemi kuwa unachokutana nacho mwanzo kinakugusa zaidi . Kama unaingilia varanda iliyojaa makorokoro kila mara unapoingia nyumbani kuna uwezekano mkubwa wa kuchoka hapo hapo nje hata kabla hujafika ndani. Vilevile kama unatembea kuelekea karibia na kizuizi unaanza kujifikiria kuwa inahitaji nguvu kupita pale. Pia kama unafungua mlango wa ofisi asubuhi na kukutana na meza iliyojaa nyaraka, unaweza kujisikia kama siku yako tayari imejaa na hakuna nafasi ya kuanza kitu kipya kwa siku hiyo.

Tembelea kila chumba nyumbani kwako. Je kuna kitu kinakuambia kuwa maisha ni mazuri na yamejaa fursa? Au una picha usiyoipenda, fenicha ambayo haijakaa sawa au rangi ya ukuta ambayo inakupa ukakasi kuitazama? Kila mara unapooana vitu kama hivi, unapotembelea chumba hiki unapata ujumbe hasi. Hata kama akili yako itazoea kuona hivyo lakini dhamira itakuwa inakereka.

Mkusanyiko wa picha unaweza kuwa chanjo cha ujumbe hasi. Hakikisha ni za kumbukumbu na hisia nzuri za watu hao kwako. Zinaweza kuwa ni picha nzuri sana kwa kuonekana kwa macho lakini kama mojawapo inakukumbusha tukio au wakati wa huzuni basi iondoe.  Weka zile zinazokufanya uwe na tabasamu. Watu mara nyingi wana picha kwenye kuta zao kwa sababu tu hawana kitu kingine cha kuweka hapo na sio kwamba ni kwa kuwa wanakipenda kilichopo. Sanaa ukutani inaweza kuwa nzuri sana ila kama ukiitazama haikubariki haina faida kwako. Badala yake inakupa ujumbe hasi na kukunyonya nguvu kila unapoiona. Ni vyema kuiondoa na kuacha nafasi kwa kitu ambacho kinakupa mtizamo chanya katika maisha.

Kuchukua hatua hii mbele zaidi, fikiria ni nini unakipenda kwenye maisha. Mfano mzuri ni mtu anayetaka kuwa na uhusiano. Mara nyingi picha atakazoweka nyumbani kwake na hasa chumba cha kulala ni za akiwa singo. Chumba hicho kitakuwa na taa moja tu ya kivuli na hata kimeza cha kando kimoja. Vyote hivi vinatoa ujumbe kuwa mhusika hana mtu. Badala ya vitu vilivyopo kwenye seti kwa mfano picha yenye watu wawili, na taa mbili za vivuli vinaleta alama za mahusiano.

Mazingira ya mahali unapoishi yanahusika katika kila eneo la maisha yako. Kama unahitaji akili tulivu hakikisha kuwa mazingira yako hayakupi kinyume na matakwa yako kwa kuwa na vitu ambavyo haviko mahali pake. Pia kama unataka kuwa mbunifu zaidi angalia kama je kuna nafasi zaidi ya kuweza kuwa hivyo? Kama unahitaji miundo mbinu safi je njia ya kuendea mlangoni kwako ni wazi, safi na inakaribisha?
Unavyotembea kwenye mazingira ya nyumbani kwako angalia kila kitu kwa jicho la ziada. Ondoa kila kitu ambacho huwezi ukasimama na kushuhudia kuwa unakipenda na ni kitu ungependa kuwa nacho. Unaweza usiwe na kiti kingine cha kuweka kwenye hiyo sehemu ulipotoa kile usichokipenda, lakini kama kinakuletea tukio la huzuni badi potelea mbali kitoe tu. Kinaziba kile unachokipenda na pia hicho usichokipenda kinakuletea hisia mbaya. Kwa kuamini utapata kingine unatengeneza uwezekano. Kuwa makini na hivyo vitu vinavyoongea na wewe furaha na kuvipa nafasi ya heshima nyumbani kwako.

Katika nyakati hizi za mihangaiko mingi, ni muhimu kuwa mazingira yako hayakuongezei vikwazo kwenye dunia yako. Hii inahusu hata taarifa za habari kwenye matukio ya mauaji, ajali na mengi ya kutisha. Fuatilia ni nini kiko kwenye vyumba vya watoto. Kama mazingira ya vyumba vyao yanaongea amani, watakua wakijifunza amani.
Kwa kuwa makini na kila kitu kwenye mazingira yako unatengeneza makazi ambayo yanafanana na wewe kwa kukupa ujumbe chanya na zenye kukutia nguvu. Kuwa kitu kimoja na makazi yako unakuwa na mtizamo chanya zaidi katika maisha. Mtazamo chaya unagusa kila kitu kwenye maisha yako. Yasikilize mazingira yako.

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23

Friday, November 30, 2012

shape ya hizi nail polish mmmmhh!

kweli biashara yahitaji mbinu nyingi. najiuliza hizi nail polish zinahusiana vip na makalio..

Tuesday, November 27, 2012

My article for newspaper: Mlango wa mbele

Mlango wa mbele ni kivutio cha nyumba

Mlango wa mbele wa nyumba yako ni kielelezo chako. Mlango huu zaidi ya kuleta mvuto wa nyumba pia unakuhuisha mara uingiapo nyumbani.

Mlango wa mbele ni moja ya vitu vya mwanzo watu wanavyoona kuhusu nyumba. Rangi, staili na hali yake ni sehemu kubwa ya jinsi nyumba inavyoonekana kwa nje. Mlango huu una kazi ngumu ya kufanya nje kuwe nje na ndani kuwe ndani. Unapata adha ya unyevu, jua, upepo na hata vumbi na kama umetengenezwa kwa mbao kuna uwezekano wa kusinyaa na kuvimba kuendana na hali ya hewa ya majira ya mwaka. Hali hii inafanya mlango kuwa mgumu kufunguka nyakati nyingine au kupiga kelele. Njia nzuri ya kuzuia ni kuhakikisha mlango umepakwa dawa sahihi za kuzuia hali hii kabla ya kuujengea kwenye nyumba.

Mlango wa mbele wa nyumba unaweza kuwa wa mbao, chuma ama glasi. Vyovyote uwavyo uangalizi wa mara kwa mara unahitajika ili kuufanya uonekane maridadi kila wakati. Kama mlango unapigwa na jua la moja kwa moja hakikisha unaupaka  rangi au finishi inayonyonya miale ya jua ili kufanya rangi yake idumu muda mrefu.

Kaya nyingi zimefanya mlango wa mbele kuwa rasmi kwa maana ya kwamba unatumika zaidi na wageni. Kutokana na kuwa hautumiwi mara kwa mara ni muhimu kuhakikisha kuwa unafanya kazi jinsi inavyotakiwa. Swali ni kuwa ni kwanini watu wengi hawatumii mlango wa mbele mara kwa mara? Ni kama vile mlango huu umewekwa kwa ajili ya wengine na wanafamilia hawastahili kuutumia wao wenyewe ambapo wengine hao huja na kuutumia mara chache kwa mwaka. Wakati mwingine hata marafiki na majirani wakija nyumbani, wanatumia mlango wa nyuma au wa pembeni ila sio wa mbele. Matokeo yake mlango wa mbele unakaa tu bila kutumika.

Watu wengi wanaingia ndani mwao kwa kupitia mlango wa nyuma ambao labda umeunganika na varanda iliyojazwa vitu vingi ama hata pengine umeunganika na gereji. Ule usemi wa unachokiona mwanzo kinadumu zaidi ni muhimu sana hapa. Kama unaingia ndani ya nyumba kupitia mlango wa nyuma uliojaa makorokoro na vifaa vya miradi ambayo haijakamilika au hata vifaa vya bustani moja kwa moja utajisikia kuchoka hata kabla hujafika ndani. Nyumbani kwako panatakiwa kuwa himaya yako. Jipe raha kwa kupitia mlango wa mbele, hata kama inamaanisha kuegesha gari yako kwanza halafu unazunguka mbele. Utashangaa ni vip utakavyohuisha nafsi yako!

Mlango wa mbele unasema mengi kuhusu watu wanaoishi kwenye nyumba husika. Kuna watu eneo la ndani la mlango huu linatumika kama stoo. Mlango wa mbele uliozibwa kwa ndani ni alama kuwa wenye nyumba hawataki mtu apitie mlango huo.
Kwa kawaida kitu kinachokuvutia kinakuhamasisha na hivyo kukuongezea nguvu mwilini. Kama mlango wa mbele unakuhamasisha ina maana nguvu inazalishwa. Kama huo mlango huupitii hata mara moja kwa mwezi basi hamna nguvu.

Mazingira ya mlango wa mbele kwa nje ni muhimu sana. Je ni rahisi kuuona mlango uko wapi na kuna njia nyepesi ya kuufikia? Je maua na mimea ya eneo lile imepunguzwa kuufanya mlango uonekane? Jicho linavutwa kuutazama na ni nini hasa kinachokuvutia ukitazama maeneo ya nje ya mlango wa mbele wa nyumba yako? Mlango wako huo unavutia vile ambavyo unasema unapenda katika maisha? Njia ya kueleweka kupitia mlango wa mbele, rangi za kuvutia au mapambo, ni hatua za kwanza kukuwezesha kutumia mlango huo na hivyo kujiongezea nguvu ya kusonga mbele na maisha. Weka eneo la mlango safi na huru, kwa ndani pasiwe stoo na mwisho utumie mlango huu. Kama bado unashawishika kuwa ni usumbufu kutumia mlango wa mbele kwa kila siku basi amua kuutumia japo mara moja kwa wiki. Ukiwa unajua kuwa unajiongezea nguvu kwa kutumia mlango huo.

Kwavile  imeonekana kuwa kaya nyingi hazitumii mlango wa mbele kila siku, basi ni vyema kuhakikisha na kucheki mara kwa mara kuwa mlango unafanya kazi vyema na hata eneo lake ni safi kwa ajili ya ukaribisho rasmi wa wageni. Usianze kuondoa buibui, vumbi na mavi ya mijusi kwenye mlango wako huo mbele ya mgeni wakati wa kumfungulia. Fanya hatua ya mwanzo ya mgeni anayekutembelea kuwa ya kumbukumbu. Pia hakikisha kuwa kile kizulia cha mlangoni ni kisafi.

Macho yanafurahia kuona vitu vizuri, mlango wako wa mbele ni moja ya pambo la kwanza kabisa wageni wanaloona wanapofika nyumbani. Mlango wako uvutie na uoane na mapambo yako mengine ya nje ya nyumba. Mlango huu pia unakulinda unapokuwa ndani, kwa hiyo unatakiwa kuwa imara.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 200023

Wednesday, November 21, 2012

What I do best..



My client Monica wearing dress designed by Vivi. We can work together to get the outfit you need..Karibuuu

My article for newspaper: Master bedroom



Chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni kama mahali patakatifu

Chumba hiki ni kile cha  baba na mama wa familia – ni koloni lao hapo nyumbani kama wengine wanavyoweza kusema. Wazazi mkiwa ndio nguzo ya familia basi mnahitaji chumba cha kipekee. Mnaokaa kwenye chumba hiki ndio mnaolipa bili na kufanya kazi kwa bidii ili mfanikiwe kwenye hilo. Kwa nini chumba chenu kisiwe maalumu? Wakuu wa familia mnastahili chumba hiki!

Je wewe mkuu wa familia unakipenda chumba chako cha kulala? Chumba hiki kiwe kama mahali patakatifu kwa wanandoa au yeyote anayelala mle. Ni nini cha kwanza unachokiona mara baada ya kufungua mlango wa chumba hiki, na ni nini unachokiona cha kwanza mara baada ya kufungua macho asubuhi. Chumba hiki kiwe ni sehemu huru pasipo na usumbufu kama wa kufua, kompyuta au midoli ya watoto. Midoli imekuwa ni tatizo kwenye chumba cha kulala hasa kwa wazazi wanaokimbia mchakamchaka wa maisha ya kila siku. Midoli inaishia chumba cha wazazi na hata kitandani.  Kuwa wazi  na kuweka mipaka juu ya chumba hiki na hata midoli ya watoto isijazane chumbani kwako na kitandani. Kwa ujumla watoto wawe na sehemu ya kucheza na kuweka midoli yao. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni cha watu wazima ndani ya familia.

Fenicha kuu kwenye chumba hiki ni kitanda. Kimsingi, kitanda kina lengo moja kuu: ni kufagilia usingizi wenye afya. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia kinahitaji kitanda chenye kukidhi vigezo vya usingizi bora. Kama matangazo tuseme ya magodoro yanavyoonyesha ni kuwa tunatumia theluthi moja ya maisha yetu kulala. Sasa kwa nini godoro, malazi na fremu ya kitanda visiwe maalumu. Kuna njia nyingi ya kupata kitanda bora kwa bajeti yeyote. Kitanda chenye fremu ya chuma tuu kilichosogezwa karibia na ukuta hakikidhi vigezo. Kila kitanda kinahitaji bodi la kichwani (makala zijazo tutaongelea umuhimu wa bodi hili) ambayo yanapatikana kwa saizi na mitindo mbalimbali.

Kwakuwa msisitizo wa chumba hiki ni kwa wanandoa kama kuna sehemu kubwa weka sofa au viti viwili vya kukalia badala ya kimoja. Mara zote fikiria vitu kwenye seti. Kama wewe ni mwanaume au mwanamke uliye singo lakini ndio mkuu wa familia weka picha ya peke yako kusisitiza utambulisho wako kuwa huna mtu. Kama mnaolala humo mko kwenye mahusiano basi mambo ni kwa seti kama vile taa za vivuli mbili, vimeza vya kando viwili na hata kama mishumaa basi miwili.  Kumbuka unatengeneza mandhari ya kupumzika na kuondoa msongo wa mawazo wa siku nzima. 

Chagua sanaa inayoelezea uhusiano wenu iwe ni picha ya ngalawa, ndege au hata maneno ya kimahaba. Sio sawa kuweka picha za marafiki, mababu na hata wanafamilia wengine kwenye chumba hiki. Tatizo ni kuwa chumba kinaanza kuonekana kinguvu kimezidiwa na vitu. Watu wote hawa wana haja gani chumbani kwako. Pambeni chumba cha kulala kwa picha zenu nyie wanandoa mnaolala humo.

Epuka rangi za kukolea sana kwa mfano kama ukiweka pazia za damu ya mzee au bluu ya weusi inaweza kuwa tabu kuamka asubuhi kuwahi kutafuta rizki. Kanuni inasema kuwa mlango usiwe mstari mmoja na kitanda, kwa maana ya kuwa ukiwa umelala kitandani uuone mkango lakini ukifungua mlango macho yasione kitanda moja kwa moja. Mlango ukiwa namna hii unawapa walalaji kujiamini zaidi kuwa wanamiliki chumba na usingizi unakuwa mwororo.

Vifaa vya umeme leo hii ni changamoto kwenye chumba cha kulala. Kompyuta, luninga na vifaa vingine vya umeme vinatuzunguka na kutunyonya nguvu kwa  kuleta nguvu ya uvutano mithili ya sumaku ambayo baadaye inaleta msongo wa mawazo. Ili kupumzisha mwili na kuuweka katika afya njema basi ni vyema kuwa mbali na vifaa vya umeme chumba cha kulala. Kama hamna jinsi kuwa ni lazima vifaa hivi viwepo chumbani basi sio tu vizime na kuacha vijitaa vinawaka bali chomoa kabisa kwenye umeme wakati wa kulala.

Kumbuka kuwa kila kitu kwenye nyumba tunazoishi kinatupa ujumbe. Chumba chako cha kulala wewe mkuu wa familia kinakupa ujumbe gani? Je kinakukumbusha majukumu yote unayohitajika kukamilisha au kinakupa hisia za utulivu na kukukaribisha kupumzika? Je kinakushawishi kuwasha luninga au kinakuleta kwenye faragha? Je kinaongeza msongo wa mawazo kwenye maisha yako? Au kinakupa pumziko la nafsi hata kama uko singo? Kama ndio basi umetengeneza chumba cha kulala ambacho ni kama mahali patakatifu.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni tuwasiliane kwa barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23