Thursday, September 25, 2014

my article for newspaper: jiko safi ukiendelea kupika


Baadhi ya siku unaweza kushangaa kama kupika kunalipa kwa nguvu yote inayotumika. Kweli, unaweza kuweka mlo kabambe mezani, lakini jiko lako likaishia kuwa chafu mno kwa, mrundikano wa vyombo vichafu. Unaweza ukawaza kuwa inaenda kuchukua muda mwingi kusafisha kuliko kula!

Kanuni kuu ya jiko kuwa safi wakati ukiendelea kupika, ni kuanza na jiko safi. Kwa njia hii uchafu unaokuogopesha ni ule unaotengeneza wakati wa kupika tu. Kwa mazoea wengi wanajitahidi kuacha jiko safi kabla ya kwenda kitandani kila ifikapo usiku. Vyombo visafi vinawekwa kabatini, vile vichafu vinaoshwa, viporo vinawekwa kwenye vikontena na kuwekwa ndani ya jokofu, ndoo ya uchafu inamwagwa na kwa namna hiyo hakuna uchafu unaobaki jikoni.
.
Siri ya kufanya jiko liwe safi wakati unapoendelea kupika ni kuosha kadri vinavyochafuka. Nadhani hakuna njia nzuri zaidi ya kusisitiza hili. Kama wali unaendelea kuiva kwa dakika 20, una muda wa kusafisha. Kama kuna muda wa kusubiria chakula kiive, basi kuna muda wa kusafisha. Inashangaza jinsi tunavyodharau hizi dakika 10 (au zaidi!) ambazo zingeweza kurahisisha kazi yetu ya kusafisha hapo baadaye. Safisha kwanza, na utakuwa na muda wa kupumzika na kufurahia chakula chako baadaye.

Pimia vyakula ndani ya sinki, na rudisha kila kitu mahali pake baada ya kukitumia ili kaunta isishamiri vitu. Jitihidi kuwa unafanya maandalizi yanayotakiwa kabla ya kuwasha jiko. Kama unatumia kikombe au kijiko cha kupimia, hakikisha unakisuuza papo kwa hapo mara baada ya kukitumia. Futa vyakula kwenye kaunta kila vinapowagika, hii itasaidia kuzifanya kaunta zako zisiwe vululu vululu na kukusababishia kazi kubwa ya kusafisha baadaye. Hii pia inasaidia kuwa na eneo la kutosha kufanyia kazi. Nyanya ndio kiungo kinachochafua zaidi kaunta. Haiepukiki kupata matone ya nyanya ukutani na hata juu ya stovu. Kufuta punde kwa kitambaa cha unyevu kunasafisha mara moja, kwa ajili tone halijakomaa. Kwa chakula ama kiungo chochote kile kilichomwagika jikoni mwako safisha kabla hayijakaukia kwenye eneo husika. Itasaidia kuokoa muda na machukizo baadaye.

Hifadhi vifaa na vyakula unavotumia mara kwa mara maeneo ya karibu na safisha makabati yako ya jikoni na jokofu kwa msimu. Kwa namna hii hutakuwa na haja ya kuondoa vitu vyote kabatini kwa ajili ya kutafuta kitu kimoja unachohitaji.

Wakati unapopika tumia vyombo vichache. Kwa mfano, wakati unapotaka  kumenya viazi badala ya kumenyea maganda kwenye chombo, tumia mfuko au gazeti mbapo utabeba na kutupa moja kwa moja kwenye ndoo ya taka na hivyo kupungukiwa na chombo cha kuosha.

Kwa siku zile ambazo una muda mchache sana, pika vyakula rahisi ambavyo havihitaji kutumia sufuria na vikaangio vingi. Fanya mapishi ambayo chakula zaidi ya kimoja kinapikiwa kwenye sufuria moja, mifano ni mchemsho na mbogamboga.

Endapo utakuwa na mapishi kwa ajili ya wageni kadhaa nyumbani, basi gawa kazi yako. Fikiria ni nini unaweza kuandaa usiku mmoja kabla ya ugeni wako. Hii itasaidia kufanya maandalizi na kujikuta baada ya tukio ukiwa na vyombo vichache vya kusafisha. Kama utapika maharage kwa mfano, unaweza kuyasafisha na kuloweka usiku. Halafu unayaacha yamekaa kwenye jokofu, hadi kesho yake wakati wa kuyapika.

Kupunguza mrundikano kwenye kaunta inafanya wepesi wa kusafisha jiko lako. Unavyokuwa na vitu vingi kwenye kaunta ndivyo inavyokupasa kuvisogeza vyote kabla ya kusafisha na hii inakupa kazi kubwa. Baadhi ya watu kanuni ni kuwa, hakuna kifaa chochote kukaa juu ya kaunta vinginevyo kiwe ni kile tu kinachotumika kila siku kwa mfano kipashio cha chakula. Vingine vyote kama visagio na kadhalika vinahifadhiwa kabatini hadi wakati wa matumizi ndipo vinapotolewa. Usipende vijiko na visu vyako vikae juu vikibeba mafuta mafuta na vumbi. Viweke kwenye droo lililo karibu na stovu, ili unapovihitaji iwe rahisi kufungua na kuchuka. Havina haja ya kuwa juu ya kaunta na kula eneo lako la kazi.

Hizi ni baadhi ya njia za kukuwezesha kuweka jiko safi wakati ukiendelea kupika. Je, wewe msomaji wangu ni kwa namna gani unaweka jiko lako safi wakati ukiendelea kupika? Nitafurahi kusikia toka kwako!


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

6 comments:

  1. Kaunta yangu ya jikoni imemwagikiwa na mafuta ya kupikia. Nitumie sabuni gani kuondoa mafuta hayo kwani kila ninaposafisha hayatoki

    ReplyDelete
  2. kaunta yako hiyo imetengenezwa kwa malighafi zipi?

    ReplyDelete
  3. Yeah, kwa kaunta ya marble sabuni yoyote yenye lemon itaondoa mafuta. Ila kwa baadhi ya watu wanakosea wanapoona sehemu moja ya jiwe la marble iko tofauti na nyingine na hudhani ni kitu kama mafuta yamemwagikiwa eneo hilo. Ukweli ni kuwa mawe haya hayafanani kila mahali kwenye jiwe zima. Kioo cha marble kinavyoteleza sio rahisi mafuta yakazama ndani hadi kushindwa kusafishika kwa sabuni sahihi.

    ReplyDelete
  4. Asante kwa ushauri. Nimekuelewa vizuri

    ReplyDelete