Thursday, June 5, 2014

my article for newspaper: bustani za kwenye vyungu

Mwongozo wa bustani za maua za kwenye vyungu
Hata kama una eneo dogo kiasi gani lakini unapenda bustani za maua, unaweza ukatimiza tamanio lako hilo kwa kutengeneza bustani za maua za kwenye vyungu.
Au pengine labda una eneo la kutosha kuwa na bustani ya ardhini lakini bado kuna yale maeneo kama ukutani, ndani ya nyumba au kwenye varanda ambapo ungependa kuwa na maua, basi suluhisho ni bustani za kwenye vyungu.

Bustani hizi zinakuwezesha kutengeneza bustani maalum kwa ajili ya eneo lolote. Unaweza kuotesha humo maua yako ya upendeleo ambayo usingependa kuotesha kwenye eneo kubwa la bustani ya ardhini kwani labda yatamezwa na mimea mingine iliyopo kwenye bustani husika. Mtunza bustani wa bustani za kwenye vyungu kikomo chake ni ubunifu wake pekee, anasema landscaper Aisha Idd.

Kwenye makala hii bi Aisha atatufunza jinsi ya kuchagua vyombo vya kuoteshea, uwekaji wa mbolea, udongo na umwagiliaji wa bustani zako bila kusahau maua yanayofaa kuotesha kwenye vyungu na mengine mengi!
Baadhi ya vyombo vinavyoweza kutumika kwenye bustani za kwenye vyungu ni vyungu vidogo vya kuning’iniza na vile vikubwa vya kuweka chini pamoja na maboksi ya mbao.                                                                                                                                       

Aisha anatupa mwongozo wa namna ya kuchagua vyungu kwa ajili ya bustani yako hiyo. Anasema epuka vyungu vyenye midomo myembamba. Pia vyungu vya plastiki nyembamba sana vinaweza kuharibiwa na jua na vitafanya ua lililoko ndani kukaukiwa na maji mara kwa mara. Kama utachagua vyungu vya udongo fahamu kuwa udongo unapitisha maji hivyo kiasi cha mji kitakuwa kinapotea kupitia kuta za chungu. Vyungu vya seramiki na saruji ndio vizuri zaidi kwenye kuhifadhi maji ila vinatakiwa kuwa na matundu kadhaa.                                                                                                                                    

Maboksi ya mbao huenda yakaoza, mbao nyekundu na za aina ya cedar huwa haziozi na zinaweza kutumika bila tatizo. Maboksi ya mbao zilizowekwa dawa ya kuzuia kuoza au kuliwa na wadudu si mazuri kwani kemikali zlizopo kwenye dawa hizo huwa zinaweza kuunguza maua. Uzuri wa mabokisi ya mbao ya kuoteshea maua ni kuwa yanaweza kutengenezwa kwa umbo na ukubwa utakaofiti eneo linalohitajika kuwekwa.

Vyungu viwe na ukubwa wa wastani kwani vikiwa vidogo sana vitazuia mizizi ya mmea kutambaa vizuri na pia huwa vinakauka maji mapema sana. Ukubwa na idadi ya mimea inayooteshwa itatokana na ukubwa wa chungu kitakachotumika. Maua yenye mizizi inayoenda chini inahitaji vyungu virefu. Hakikisha kuwa vyungu vyako vinapitisha maji vizuri na tandika magazeti chini ili kuzuia udongo usiwe unakimbia chungu wakati wa kukimwagilia. Sasa utajiuliza hayo magazeti si yataloa? Ni kweli ila hata kama yakiloa yatatengeneza kizuizi chini kwani hama tujuavyo ni kuwa karatasi haiozi. Kwa upande wa vyungu vidogo vya kuning’iniza hakikisha ya kuwa hutundiki kwenye ukuta wenye jua la moja kwa moja kwani vitakuwa vinakaukiwa maji mara kwa mara.

Hakikisha kuwa chombo chako cha kuoteshea bustani za kwenye vyungu kinapitisha maji mapema lakini kinahifadhi unyevu wa kutosha kuweka mizizi katika hali ya maji. Mboji inafanya udongo mzuri sana wa kwenye vyungu. Ila ni muhimu kujua hitaji la mmea kwani usijezidisha udongo wenye mbolea kali, na pia mbolea nyingine kama ya kuku ina tindikali sana kwahivyo inahitaji maji kwa wingi pindi unapoiweka. Kadri utakavyokuwa unamwagilia mmea wako ndivyo utkavyokuwa unaweka mbolea kwani huwa maji yanaondoa baadhi ya vimeng’enyo. Pia kuna mbolea za dukani za maji maji ambazo waweza tumia kwa kupata maelezo ya kitaalam toka kwa wauzaji.

Umwagiliaji wa bustani yako ya kwenye vyungu ufanyike pale mmea unapohitaji maji kwa maana ya ikiwa dalili za hali ya kunyong’onyea zitaanza kujitokeza. Baadhi ya mimea inaweza kuvumilia na inahitaji ukame kiasi kwamba ukiimwagilia mara kwa mara unaisababishia kuwa na unyevu wakati wote kwa maana hiyo itakufa. Ielewe mimea uliyo nayo, anasema Aisha. Kuna mimea mingine ya kwenye vyungu kwa mfano, kama iko ndani ya nyumba inaweza kumwagiliwa vikombe viwili tu kwa juma zima. Kumwagilia kuwe ni hitaji na sio jambo la kila wakati na kanuni kuu ya kujua kuwa mmea unahitaji maji ni kujaribu udongo wake. Kama inchi moja au zaidi ya udongo ni mkavu basi mwagilia.

Kwenye mazingira ya uwazi, mimea ya kwenye vyungu inapoteza maji mapema. Wakati wa kiangazi bustani zilizowekwa kwenye mazingira haya huenda zikahitaji kumwagiliwa kila siku.   Sasa basi, ni muhimu kufahamu kuwa sio kila maua au mmea unafaa kuoteshwa kwenye vyungu. Mimea inayokubalika zaidi kwa bustani hizi ni ile yenye mizizi michache na mifupi. Pindi uendapo kwenye bustani za wauza maua zilizojaa maeneo mengi kando kando ya barabara kuu watakufahamisha.                             

Umaarufu wa bustani za kwenye vyungu umetisha.

Mimea kwenye vyungu inaonekana kila mahali, kutoka kwenye makazi ya watu hadi maofisini, mahotelini, kwenye ma mall na hata barabarani. Udongo mbaya au hakuna eneo la kuweka bustani sio kisingizio tena cha kutokuweza kufurahia kijiraha cha kuwa na bustani!

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Friday, May 30, 2014

my article for newspaper: jinsi ya kufanana na mazingira yako

Jinsi ya kufanana na mazingira ya nyumbani kwako

Kila mtu anachagua ni vipi anataka mazingira ya nyumbani kwake yawe. Ingawa tunaweza tusijali kuhusu uchaguzi huo lakini mazingira yetu ni dili kubwa kutuhusu. Una nafasi ya kutengeneza mazingira ambayo yatarahisisha maisha yako ama yatayafanya  yazidi kuwa magumu.

Kuna kanuni ya kwanza ya msingi kuwa katika kila kitu kilichopo kwenye eneo linalokuzunguka kina nguvu fulani iwe kitu hicho kina uhai ama hakina. Ni kama watu wa kale walivyoamini kuwa kila kitu kina uhai. Kanuni ya pili ni kuwa kila kitu kwenye mazingira yetu kinahusiana na kitu kingine. Inawezekana kwa mtizamo wa kiroho au wa kisayansi. Na kanuni ya tatu ni kuwa kila kitu kinabadilika kila wakati.

Sasa basi kama kila kitu kwenye mazingira yako kina uhai na kimeunganishwa na wewe basi mabadiliko yakitokea kwenye eneo lako nawe unaguswa. Mazingira yako yanakugusa nawe unayaakisi. Hii ni kama usemi kuwa kila kitu kwenye mazingira yako kinaongea na wewe. Je vitu vya mazingira yako vinasema yale ambayo unapenda kusikia, je vinakusaidia kupata kile unachotaka kupata katika maisha.

Fikiria jinsi unavyoingia nyumbani kwako na kukumbuka usemi kuwa unachokutana nacho mwanzo kinakugusa zaidi . Kama unaingilia varanda iliyojaa makorokoro kila mara unapoingia nyumbani kuna uwezekano mkubwa wa kuchoka hapo hapo nje hata kabla hujafika ndani. Vilevile kama unatembea kuelekea karibia na kizuizi unaanza kujifikiria kuwa inahitaji nguvu kupita pale. Pia kama unafungua mlango wa ofisi asubuhi na kukutana na meza iliyojaa nyaraka, unaweza kujisikia kama siku yako tayari imejaa na hakuna nafasi ya kuanza kitu kipya kwa siku hiyo.

Tembelea kila chumba nyumbani kwako. Je kuna kitu kinakuambia kuwa maisha ni mazuri na yamejaa fursa? Au una picha usiyoipenda, fenicha ambayo haijakaa sawa au rangi ya ukuta ambayo inakupa ukakasi kuitazama? Kila mara unapooana vitu kama hivi, unapotembelea chumba hiki unapata ujumbe hasi. Hata kama akili yako itazoea kuona hivyo lakini dhamira itakuwa inakereka.

Mkusanyiko wa picha unaweza kuwa chanzo cha ujumbe hasi. Hakikisha ni za kumbukumbu na hisia nzuri za watu hao kwako. Zinaweza kuwa ni picha nzuri sana kwa kuonekana kwa macho lakini kama mojawapo inakukumbusha tukio au wakati wa huzuni basi iondoe.  Weka zile zinazokufanya uwe na tabasamu. Watu mara nyingi wana picha kwenye kuta zao kwa sababu tu hawana kitu kingine cha kuweka hapo na sio kwamba ni kwa kuwa wanakipenda kilichopo. Sanaa ukutani inaweza kuwa nzuri sana ila kama ukiitazama haikubariki haina faida kwako. Badala yake inakupa ujumbe hasi na kukunyonya nguvu kila unapoiona. Ni vyema kuiondoa na kuacha nafasi kwa kitu ambacho kinakupa mtizamo chanya katika maisha.

Kuchukua hatua hii mbele zaidi, fikiria ni nini unakipenda kwenye maisha. Mfano mzuri ni mtu anayetaka kuwa na uhusiano. Mara nyingi picha atakazoweka nyumbani kwake na hasa chumba cha kulala ni za akiwa singo. Chumba hicho kitakuwa na taa moja tu ya kivuli na hata kimeza cha kando kimoja. Vyote hivi vinatoa ujumbe kuwa mhusika hana mtu. Badala ya vitu vilivyopo kwenye seti kwa mfano picha yenye watu wawili, na taa mbili za vivuli vinaleta alama za mahusiano.

Mazingira ya mahali unapoishi yanahusika katika kila eneo la maisha yako. Kama unahitaji akili tulivu hakikisha kuwa mazingira yako hayakupi kinyume na matakwa yako kwa kuwa na vitu ambavyo haviko mahali pake. Pia kama unataka kuwa mbunifu zaidi angalia kama je kuna nafasi zaidi ya kuweza kuwa hivyo? Kama unahitaji miundo mbinu safi je njia ya kuendea mlangoni kwako ni wazi, safi na inakaribisha?

Unavyotembea kwenye mazingira ya nyumbani kwako angalia kila kitu kwa jicho la ziada. Ondoa kila kitu ambacho huwezi ukasimama na kushuhudia kuwa unakipenda na ni kitu ungependa kuwa nacho. Unaweza usiwe na kiti kingine cha kuweka kwenye hiyo sehemu ulipotoa kile usichokipenda, lakini kama kinakuletea tukio la huzuni bado,  potelea mbali kitoe tu. Kinaziba kile unachokipenda na pia hicho usichokipenda kinakuletea hisia mbaya. Kwa kuamini utapata kingine unatengeneza uwezekano. Kuwa makini na hivyo vitu vinavyoongea na wewe furaha na kuvipa nafasi ya heshima nyumbani kwako.

Katika nyakati hizi za mihangaiko mingi, ni muhimu kuwa mazingira yako hayakuongezei vikwazo kwenye dunia yako. Hii inahusu hata taarifa za habari kwenye matukio ya mauaji, ajali na mengi ya kutisha. Fuatilia ni nini kiko kwenye vyumba vya watoto. Kama mazingira ya vyumba vyao yanaongea amani, watakua wakiwa wanajifunza amani.

Kwa kuwa makini na kila kitu kwenye mazingira yako unatengeneza makazi ambayo yanafanana na wewe kwa kukupa ujumbe chanya na zenye kukutia nguvu. Kuwa kitu kimoja na makazi yako unakuwa na mtizamo chanya zaidi katika maisha. Mtazamo chaya unagusa kila kitu kwenye maisha yako. Yasikilize mazingitra yako.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Thursday, May 22, 2014

my article for newspaper: jinsi ya kuhifadhi vyombo makabatini

Jinsi ya kupanga vyombo kwenye makabati ya jikoni

Je vyombo vyako vinataka kuporomoka wakati ukifungua makabati ya jikoni? Kama ndivyo basi ni wakati wa kupanga na kuhifadhi upya na makala hii ni sahihi kwako.  Njia bora zaidi ya kupangilia vyombo na vifaa kwenye makabati yako ya jikoni ni kufikiria ni kwa vipi unavitumia vyombo vyenyewe. Ni vyombo na vifaa vipi unajikuta ukivitumia kila siku, na ni vipi vinakaa tu kabatini. Tosa vile ambavyo unaweza kuendesha shughuli zako za hapo jikoni bila kuwa navyo na elekeza nguvu kwenye kufanya makabati yako yaonekane yanafanya kazi, masafi na yana mvuto. Mara utakapopanga ndani ya makabati yako basi utajisikia furaha tena kuingia jikoni.

Ili kuweza kufanikisha zoezi la kuhifadhi vyombo kwa unadhifu kwenye makabati yako ya jikoni kwanza kabisa ondoa kila kitu kwenye makabati. Ni rahisi kuanza mradi wowote wa kupanga upya kwa kuanza na eneo safi, na kwa makabati ya jikoni ni hivyo hivyo. Songa mbele na toa kila kitu kwenye makabati kuanzia sahani, glasi, vikombe, sufuria, vikaangio na kila kitu kingine chochote ulichohifadhi kwenye makabati yako hayo. Panga kila kitu juu ya kaunta zako za jiko au hata kama una meza ya jikoni ili kuweza kutathmini ni nini unacho na ni kipi unahitaji. Kuondoa vile usivyohitaji kutasaidia kuondoa mrundikano hivyo kukuwezesha kuhifadhi vyema vile unavyohitaji. Na kama utajigungua kuwa kuna chombo ama kifaa unakihitaji lakini huna basi hakikisha unakinunua kwanza kabla ya kuweka mpangilio wako. Kama ukisubiri itakuwa ngumu kupata eneo la kukihifadhi baadaye.

Fikiria kugawa vyombo vya zamani na vile usivyohitaji kwa wanaohitaji zaidi, au hata kupeleka kwenye mnada wa vyombo vilivyotumika endapo viko katika hali nzuri. Kufahamu kuwa vifaa vyako vya zamani vinaenda kwenye jiko lingine itakupa amani zaidi ya kuvitupa tu bila mpangilio.

Futa makabati yako ambayo hayana chombo chochote kuanzia juu hadi chini. Tumia sabuni nzuri za kusafishia pamoja na kitambaa cha kufutia na safisha kila mahali hadi kwenye milango yote ile ya mbao na hata kama ya kioo ipo. “Kama utataka kutumia kemikali za kusafishia,tumiavinega iliyochanganywa na maji kidogo,” anasema Bi Mwajuma Issa ambaye ni mmiliki wa kampuni ya kufanya usafi majumbani.  Kemikali hii ya asili ya kusafishia imefanikiwa sana kwenye makabati ya jikoni ila kama makabati yako yametengenezwa kwa mbao ambayo haijapakwa rangi basi hakikisha unatumia sabuni za kusafishia ambazo hazitaharibu mbao. Kwa namna hii unaweka makabati yako tayari kwa ajili ya mpangilio mpya wa vyomba na vifaa vingine vya hapo jikoni. Kusafisha makabati yako kwa mtindo huu kutaangamiza makazi ya wadudu na kufanya nyombo, vifaa na vyakula utakavyohifadhi humo kuwa freshi.

Nunua vihifadhio vya kukusaidia katika mpangilio wa jikoni kama vile vitrey vinavyotumika kuweka baadhi ya vyakula vikavu kama vitunguu na viungo , kitufe cha visu kwa ajili ya kuhifadhia visu vingi kwa wakati mmoja na pia kurahisiha matumizi na vitu vingine vidogodogo kama vya kuwekea vijiko kadhaa na uma ambazo zinatumika kila siku. Kwa kawaida vihifadhio hivi husimamishwa kwenye kaunta za jiko. Pia makontena kwa ajili ya kuhifadhia vyakula kama mchele, unga na sukari vitakusaidia kuweka mpangilio jikoni

Baada ya kabati kukauka unyevu wote sasa ni wakati wa kutandika karatasi za kwenye makabati ya vyombo kabla ya kupanga vyombo vyako. Sasa una makabati yako yakiwa masafi na yameshatandikwa, ni wakati wa kufikiri ni kwa namna gani unataka kuweka mpangilio wa vyombo unavyotaka kuhifadhi ndani. Tathmini hivyo vyombo na vifaa unavyotaka kuhifadhi. Weka kila chombo kwenye kundi lake kutokana na aina ya chombo. Wakati wa kupanga makabati ya jikoni inaleta mantiki kupanga vyombo vinavyoendana pamoja.

Hifadhi vyombo vya thamani na kuvunjika kwenye kabati za juu ya kaunta ambapo ni ngumu kwa watoto kufungua na kuvunja.
·         Hifadhi pamoja vyombo vya kuvunjika kama vile glasi za kunywea maji, glasi za juisi na glasi nyingine zozote za matumizi ya kila siku.
·         Hifadhi pamoja glasi za mvinyo na shampeni.
·         Hifadhi pamoja sahani zako za kuvunjika na mabakuli. Ila hapa ieleweke vizuri kuwa sio sawa kuweka sahani na mabakuli kwenye mstari mmoja kama njia ya kuhifadhi nafasi kwani inaweza kusababisha kuvunjikiana.
·         Tofautisha sahani na bakuli za matumizi ya kila siku na zile za matumizi ya msimu.
·         Kama makabati yako ya jikoni yana milango ya kioo fikiria ni vyombo vipi ungependa vionekane kwa nje kwani makabati haya ni kwa matumizi na umaridadi.

Hifadhi sufuria na vikaangio kwenye kabati za chini karibia na jiko. Kila mmoja ana jiko la tofauti, lakini kwa mara nyingi makabati ya chini (chini ya kaunta) ndio sahihi kwa sufuria na vikaangio. Vyombo hivi huwa ni vizito na mara nyingi kuokoa nafasi sufuria moja inaingizwa ndani ya nyingine kuendana na ukubwa kwa hivyo inaleta mantiki kuvihifadhi eneo ambalo haitakuwa na haja ya kuvitoa tokea juu. Zile sufuria na vikaangio unavotumia mara kwa mara viweke karibia na mlango ili kuchukua kirahisi na zile ambazo unatumia kwa nadra zihifadhi mwishoni  mwa makabati. Pia unaweza kuona ni rahisi kuhifadhi sufuria na vikaangio vya kutumika mara kwa mara kwenye raki yake inayoning’inizwa ukutani mbele ya makabati yako. Hii inasaidia kuning’iniza kila moja peke yake badala ya kubebana.

Panga vijiko, uma na visu vya ziada kwenye droo flati,ukiwa umegawanyisha kila kimoja kwenye mahali pake. Vile vinavyotumika mara kwa mara hifadhi kwenye kihifadhio cha vijiko na uma kilichowekwa juu ya kaunta na kitufe cha visu. Pia weka droo moja la flati kwa ajili ya kuhifadhi vitambaa na vitaulo vya kufutia vyombo.

Tafuta eneo kwa ajili ya kuhifadhia vifaa kama blenda na tosta ambapo vile ambavyo unatumia kila siku waweza hifadhi juu ya kaunta. Kama blenda ni ya juisi ambayo inatumika mara chache kwa juma basi hifadhi kwenye kabati

Hifadhi sabuni na vifaa vya kusafishia ndani ya kabati lililo chini ya sinki.

Sasa umemaliza kuhifadhi vyombo kwenye kabati zako za jikoni, zicheki mara kwa mara kuhakikisha kuwa bado vyombo na vifaa vyako vipo kwenye mpangilio uliochagua. Unaweza kuwa unaweka vidonge vya kuua wadudu kama mende mara moja kila baada ya miezi sita.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Sunday, May 18, 2014

super sunday...

maisha ni haya haya wajameni...ha ha haaa...tuendako baada ya hapa hakuna uzoefu kwa hivyo enjoy hapa hapa kwa sana kadri uwezavyo.....




Tuesday, May 13, 2014

pilika mitaani nikakutana na showroom iliyonitumbuiza..

showroom ilinivutia nikapiga picha kwenye hii dressing table.
imetengenezwa kwa mdf ila miguu ni mkongo

ki kiti cha dressing table
TV cabinet

Sunday, May 11, 2014

happy mothers day from my son

wala sikuwa aware...kesho shule nikamwambia mtu wangu mdogo do your homework..nikashangaa ananitolea na kikadi cha mothers day...shule hizi...nami nasema happy mothers kwa wamama wote wasomaji wangu... 


Thursday, May 8, 2014

my article for newspaper: mpangilio wa chumba cha kulala cha wakuu wa familia

Huenda wewe na mwenza wako mnaishi maisha yenye kazi nyingi (busy) ambayo mara nyingi yanapingana na kuwa na muda mzuri wa kukaa pamoja. Hakika mnajua hisia zenu zinavyokuwa kwa ajili ya kukosa muda huo muhimu. Ndio maana ni vyema kuwa na chumba cha kulala ambacho mkiwa pamoja kama wanandoa itawezekana kufurahia ule muda mchache mnaokuwa pamoja. Kwa lengo la makala hii chumba cha wakuu wa familia ni kile cha  baba na mama wa familia – ni koloni lao hapo nyumbani kama wengine wanavyoweza kusema. Wazazi mkiwa ndio nguzo ya familia basi mnahitaji chumba cha kipekee. Mnaokaa kwenye chumba hiki ndio mnaolipa bili na kufanya kazi kwa bidii ili mfanikiwe katika hilo. Kwa nini chumba chenu kisiwe maalumu? Wakuu wa familia mnastahili chumba hiki!

Je wewe mkuu wa familia unakipenda chumba chako cha kulala? Chumba hiki kiwe kama mahali patakatifu kwa wanandoa au yeyote anayelala mule. Chumba kiheshimiwe kisiwe ni ofisi ya nyumbani. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni sehemu ya kupumzika hivyo vitu kama kompyuta havina nafasi kwenye chumba hiki. Ni nini cha kwanza unachokiona mara baada ya kufungua mlango wa chumba hiki, na ni nini unachokiona cha kwanza mara baada ya kufungua macho asubuhi. Chumba hiki kiwe ni sehemu huru pasipo na usumbufu kama wa kufua, ndoo za maji, kompyuta au midoli ya watoto. Chumba hiki sio stoo!                          

Midoli imekuwa ni tatizo kwenye chumba cha kulala hasa kwa wazazi wanaokimbia mchakamchaka wa maisha ya kila siku. Midoli inaishia chumba cha wazazi na hata kitandani.  Kuwa wazi  na kuweka mipaka juu ya chumba hiki na hata midoli ya watoto isijazane chumbani kwako na kitandani. Kwa ujumla watoto wawe na sehemu ya kucheza na kuweka midoli yao. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni cha watu wazima ndani ya familia.

Fenicha kuu kwenye chumba hiki ni kitanda. Kimsingi, kitanda kina lengo moja kuu: kufagilia usingizi wenye afya. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia kinahitaji kitanda chenye kukidhi vigezo vya usingizi bora. Kama matangazo tuseme ya magodoro yanavyoonyesha ni kuwa tunatumia theluthi moja ya maisha yetu kulala. Sasa kwa nini godoro, malazi na fremu ya kitanda visiwe maalumu. Kuna njia nyingi ya kupata kitanda bora kwa bajeti yeyote. Kitanda chenye fremu ya chuma tuu kilichosogezwa karibia na ukuta hakikidhi vigezo. Kila kitanda kinahitaji bodi la kichwani (makala zijazo tutaongelea umuhimu wa bodi hili) ambayo yanapatikana kwa saizi na mitindo mbalimbali.

Kwa kuwa msisitizo wa chumba hiki ni kwa wanandoa,  kama kuna sehemu kubwa weka sofa au viti viwili vya kukalia badala ya kimoja. Mara zote fikiria vitu viwili viwili. Kama wewe ni mwanaume au mwanamke uliye singo lakini ndio mkuu wa familia weka picha ya peke yako kusisitiza utambulisho wako kuwa huna mtu. Kama mnaolala humo mko kwenye mahusiano basi mambo ni kwa seti kama vile taa za vivuli mbili, vimeza vya kando viwili na hata kama mishumaa basi miwili.  Kumbuka unatengeneza mandhari ya kupumzika na kuondoa msongo wa mawazo wa siku nzima. 

Chagua sanaa inayoelezea uhusiano wenu iwe ni picha ya ngalawa, ndege au hata maneno ya kimahaba. Sio sawa kuweka picha za marafiki, mababu na hata wanafamilia wengine kwenye chumba hiki. Tatizo ni kuwa chumba kinaanza kuonekana kinguvu kimezidiwa na vitu. Watu wote hawa wana haja gani chumbani kwako. Pambeni chumba cha kulala kwa picha zenu nyie wanandoa mnaolala humo.
Chumba hiki kamwe kisiwe na mrundikano, weka kero za maisha ya kila siku mbali na mahali hapa patakatifu. Kama kabati lako la nguo limefurika, punguza ubakize zile ambazo haswa unazivaa. Pia fikiria kupunguza kiasi cha fenicha ili kuwe na nafasi chumba kisionekane kusongamana. Sakafu ionekane peupe isijazane vitu.  

Zingatia kile unachokiona kwanza mara baada ya kuingia chumba chako cha kulala. Kanuni inasema kuwa mlango usiwe usawa mmoja na kitanda, kwa maana ya kuwa ukiwa umelala kitandani uuone mkango lakini ukifungua mlango macho yasione kitanda moja kwa moja. Mlango ukiwa namna hii unawapa walalaji kujiamini zaidi kuwa wanamiliki chumba na usingizi unakuwa mwororo.
Vifaa vya umeme leo hii ni changamoto kwenye chumba cha kulala. Kompyuta, luninga na vifaa vingine vya umeme vinatuzunguka na kutunyonya nguvu kwa  kuleta nguvu ya uvutano mithili ya sumaku ambayo baadaye inaleta msongo wa mawazo. Ili kupumzisha mwili na kuuweka katika afya njema basi ni vyema kuwa mbali na vifaa vya umeme katika chumba cha kulala. Kama hamna jinsi kuwa ni lazima vifaa hivi viwepo chumbani basi sio tu vizime na kuacha vijitaa vinawaka bali chomoa kabisa kwenye umeme wakati wa kulala.

Kumbuka kuwa kila kitu kwenye nyumba tunazoishi kinatupa ujumbe. Chumba chako cha kulala wewe mkuu wa familia kinakupa ujumbe gani? Je kinakukumbusha majukumu yote unayohitajika kukamilisha au kinakupa hisia za utulivu na kukukaribisha kupumzika? Je kinakushawishi kuwasha luninga au kinakuleta kwenye faragha? Je kinaongeza msongo wa mawazo kwenye maisha yako? Au kinakupa pumziko la nafsi hata kama uko singo? Kama ndio basi umeweka mpangilio wa chumba cha kulala ambacho ni kama mahali patakatifu.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

nukuu ya leo: mapenzi & maudhi

"mapenzi yakiwa na maudhi ndio yanaota mizizi"

Wednesday, May 7, 2014

nukuu: kasheshe homa ya dengue...

“Kwa ufupi, mbu sasa ni hatari kuliko ilivyokuwa awali kwa sababu hawa wanaoambukiza homa ya dengue huuma wakati wa mchana, tofauti na wale wanaoambukiza malaria ambao huuma usiku na watu walikwishajua kujikinga kwa chandarua au dawa,


Thursday, April 24, 2014

my article for newspaper: garden entrance


Jinsi ya kutengeneza na umuhimu wa eneo la kuingia kwenye bustani
Eneo la kuingia kwenye bustani ya maua ni kiungo muhimu cha bustani ya nyumba yako. Ni eneo sahihi la wewe mwenye bustani kuonyesha ladha na ubunifu wako binafsi.
Muonekano wa kuvutia wa eneo hili sio tu unaboresha muonekano wa bustani bali pia ni ishara kwa wageni wako kuwa wameshafika bustanini.  Eneo hili ni kama linasema“hapa ndio mahali panapoanzia bustani yangu ya nyumbani,” anasema mbunifu wa bustani Bi Tatu Mbegu.
Kuna staili nyingi tofauti za eneo la kuingia kwenye bustani au sehemu nyingine ya nje ya nyumba. Katika makala hii mbunifu Tatu Mbegu anakushauri aina hizi mbalimbali na ndipo utakapoweza kuamua ni ipi itafaa kwenye bustani yako.

Sehemu ya kuingia kwenye bustani inaweza kuwa eneo rahisi tu kwa mfano mawe mawili yaliyowekwa mkabala katika eneo hilo, vyungu vya maua, kiingilio kama fremu ya mlango kwa mfano wa vibao vya kupishana au hata chuma, milingoti miwili iliyozungushiwa mimea mitambaazi na hata geti la chuma na kadhalika na kadhalika. Uwezekano ni mwingi na upeo ni mwisho wa ubunifu wako. Vizuri, kitu muhimu cha kufahamu ni kuwa ni eneo la mwanzo linaloonekana kabla ya kuingia kwenye bustani, anasema Tatu. Eneo hili linatoa tamko la papo kwa papo la utambulisho wa mwenye bustani na linaleta mguso wa eneo lingine lote la bustani lililobakia.

Mbao na chuma zinaweza kuchanganywa kwa uzuri na kufanya eneo la kuingia. Vifaa vya ujenzi navyo vinafanya wigo mpana wa kuchagua mtindo wa muonekano wa eneo hilo. Kama unadhani mbao zinaonekana kuoza sana ndani ya muda mfupi basi tumia chuma peke yake.
Pamoja na hayo ni muhimu kufahamu kuwa sio kila eneo la kuingia kwenye bustani liko mbele ya nyumba. Wengine hupendela kugawa bustani kwenye vyumba na hivyo kuwa na maeneo tofauti ya kuingia katika kila chumba.

Kuzungushia hiyo fremu ya eneo la kuingia kwa mimea na maua inaonyesha ubunifu zaidi. Mgeni anayepita chini ya kivuli anafunikwa na kijani na hivyo kujisikia burudani kwa hewa safi.
Hii yote inatokana na ladha ya mwenye nyumba, muonekano na bajeti. Eneo la kuvutia la kuingia kwenye bustani ni utambulisho wako kwa mapambo yako ya nyumbani.

Sasa unaanzaje kupata mawazo ya jinsi ya kutengeneza eneo la kuingia? Bi Tatu anajibu swali hili kwa kusema kuwa anza kubuni kwa kuangalia kwanza bustani yako kwa ujumla. Ni wapi ungependa kuweka eneo la kuingilia? Wakati mwingine uamuzi unatokana na eneo lililozoeleka kupitwa hapo kabla, na pia ni jinsi gani ungependa wageni waifikie nyumba yako? Je unapenda kubuni njia ya moja kwa moja kutoka kwenye bustani kuingia kwenye nyumba ama kuwe na kona ya kuingia kwenye bustani kwanza kabla ya kufikia mlango wa mbele wa nyumba?
Halafu jifanye kama wewe ni mgeni kwenye makazi yako mwenyewe. Jiulize kama ungefika mahali hapo kwa mara ya kwanza ni wapi ungepitia kufika bustanini. Sasa weka baadhi ya maelezo haya kwenye mawazo yako ya kuamua ni wapi utengeneze sehemu ya kuingia kwenye bustani yako.
Hakikisha kuwa utatumia njia yako ya kuingilia kwenye bustani. Hii ina maana kuwa kama utaitengeneza mahali ambapo huvutiwi kupitia basi ni dhahiri kuwa utaitumia kwa mara chache sana au hata inawezekana hutaitumia kabisa. Kwa hiyo kabla hujatengeneza njia hakikisha kuwa utaitumia.

Muonekano wa eneo la kuingilia uwe ni muendelezo wa mapambo mengine ya nyumba yako. Kama nafasi inaruhusu tengeneza eneo la kutosha kwa ajili ya kupitia watu kadhaa. Eneo la kuingilia la upana mdogo zaidi ni mita moja na nusu kwa bustani ya wastani hadi mita mbili na nusu kwa bustani kubwa, anasema Bi Tatu.

Mwisho fikiria bajeti; haihitaji hela nyingi kutengeneza eneo la kuingia kwenye bustani. Kama mbunifu alivyosema kuwa hata vyungu viwili vilivyooteshwa maua vikawekwa mkabala vinaweza kufanya eneo la kuingia kwenye bustani, au hata boda za maua zilizozunguka bustani zinaweza kuachwa nafasi ya eneo la kuingilia na ikawa ndio hicho tu unachohitaji. Ni rahisi tu kama hivyo wala haihitaji mambo makubwa.
Wawezeshe wageni wako kupunguza mwendo wanapofikia bustani yako kwa kuweka njia ya kuingilia, watafurahia kwa undani maua mazuri na mimea laini ya bustani yako.
Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Wednesday, April 23, 2014

my everyday life....hapa na pale baada ya weekend ndefu..

marafiki zangu waukweli wamerudi shule


kuelekea kwenye mishe..mambo mazuri yanakuja..
kwa nini unachukua pima joto yangu..

Tuesday, April 22, 2014

block pavers na mvua ni kama zimepigwa deki!

makoko yote yameng'olewa na mvua...ni zaidi ya kupiga mashine ya pressure
p
vitofali viking'aa na miguu inang'aa

Thursday, April 17, 2014

makala ya kabati la sebuleni ilibamba zaidi...

hakika wasomaji wengi wanavutiwa na makala ya kabati la sebuleni.
makala hii imekuwa ikipotelea na kurudi kila mara kwa ajili ya wasomaji wapya kuivuta tena na kuisoma na hata wengine wanadhani kuwa nauza haya makabati.
ukitaka kabati la staili yoyote ni kiasi cha kuteta na fundi anayejua kazi yake, kumnunulia vifaa na anakutengenezea kwa ladha yako mwaya..

Tuesday, April 15, 2014

my article for newspaper: umuhimu wa dressing table nyumbani

Kumpenda mwingine, ni muhimu kujipenda mwenyewe kwanza. Mtu anatakiwa kujithamini utu wake mwenyewe na kujifurahia alivyo. Kila mmoja anajiona mzuri mbele ya kifaa kinachoitwa kioo, ambacho kinatuonyesha sura zetu zilivyo. Wengi wanapenda kutumia muda mwingi ndani ya sehemu ya nyumba palipo na kioo kwa maana ya kuwa sehemu ya kuvalia yenye kioo. Hapo mahali ni kwenye dressing table! Meza ya kuvalia kwa lugha nyingine dressing table ikiwa imeambatanishwa na droo, kioo na kiti ni fenicha muhimu mno ndani ya nyumba ya kuishi.
Kuna aina kadha wa kadha za fenicha ambazo ni kama zimepuuzwa katika baadhi ya nyumba. Meza ya kuvalia ni le aina ya fenicha ambayo ni muhimu sana kuwa katika kila nyumba ambapo sio tu kwamba inaongeza uzuri na rehema ndani ya nyumba bali pia inaonyesha ushirikiano mkubwa  katika matumizi yake.
Vioo vilivyoko kwenye meza ya kuvalia vinasaidia mno kwa kuwezesha wewe mwanamke mzuri na mwanaume bomba kujiandaa vyema wakati wa kuvaa na hivyo kutoka nyumbani ukiwa unajiamini. Kiti kidogo ama kistuli cha meza ya kuvalia kinakusaidia kukaa na kujiandaa kwa kuvaa, kutupia na kuweka vipodozi vyako bila wasiwasi huku ukijitazama kwenye vioo. Hasa wanawake huwa tunachukua muda wa kujiandaa na kupaka vipodozi, kiti kinahtajika sana wakati huo. Pia fahamu kuwa hiki kiti au kistuli cha meza ya kuvalia huwa ni kidogo kwa hivyo hakisababishi mrundikano kwenye chumba chako.
Droo za meza ya kuvalia hutumika kuhifadhi vitu mbalimbali hivyo kuwa rahisi kupata kile unachohitaji mara moja.
Kwa kawaida huwa meza ya kuvalia ina droo 3 hadi 4 ambazo hutumika kuhifadhia vitu kadhaa. Meza hii inaakisi utambulisho wa mtu anayeitumia. Kwa mfano, bachela atajaza meza yake kwa kila aina ya deodoranti, pafyumu, nguo za ndani, mikanda na wakati mwingine hata mipira ya kiume miwili au mitatu! Mwanamke naye anaweza kuhifadhi vitu kama vile nguo (kwenye droo zake), kuhifadhi vipodozi na manukato, kuhifadhi vitupio kama bangili, shanga, mikufu na hereni. Meza hii pia huwa hutumika kuhifadhi vitu vya faragha kama nguo za ndani kwa vile mara nyingi huwa inawekwa chumba cha kulala.

Meza za kuvalia zinapataikaan za aina na mitindo mbalimbali. Zipo za mbao, chuma na hata plastiki ngumu na kadhalika. Unaweza kununua yeyote ambayo inafaa kwa nyumba yako na inaendana vyema na mapambo yako mengine ya ndani. Gharama pia zitatofautiana kuendana na kifaa kilichotumika kutengenezea meza na pia aina ya kioo, anasema seremala Musa Hussein. Meza nyingine huwa zina vioo viwili ambapo unaweza kujiona nyuma na mbele.
Unaweza kununua meza iliyotengenezwa tayari au unaweza kupeleka oda yako kwa fundi akakutengenezea. Kama fundi atafanya kazi nzuri meza ya kuvalia ya kubuni mwenyewe inaweza kukupa burudiko la kudumu. Kufahamu mitindo iliyopo tembelea mitandao na soma majarida mbalimbali yanayohusu mapambo ya nyumbani. Wakati wa kuoda au kununua ni vyema kuzingatia sehemu au chumba utakachoweka seti yako hiyo. Kila mmoja ana ladha yake binafsi linapokuja swala la kununua fenicha za nyumbani, ila ni vyema kupokea ushauri wa wanafamilia wengine ama hata wabunifu wa ndani kabla ya kuamua kununua aina fulani ya meza ya kuvalia.
Kwa kawaida meza hii inakaa chumba cha kulala ingawa baadhi ya wabunifu wa fenicha wanashauri iwekwe bafuni kama una eneo kubwa, na hata zipo meza za kisasa zaidi zilizounganishiwa umeme kwa ajili ya kutumia vikaushia vywele na visafisha uso vya mvuke.
Meza ya kuvalia ilivumbuliwa kukusaidia kujiandaa ukiwa huru na amani tele kwenye chumba chako mwenyewe cha kulala. Unaweza kujiremba na kujipendezesha kwa raha zako kwenye meza hii.

Unaweza sasa ukatafakari ni kwa jinsi gani unaweza kuwa mbunifu kwa kutumia dressing table na droo zake maridadi bila kusahau kioo na kiti chake cha staili. Ni fenicha muhimu mno kuwa nayo. Pia usisahau kuwa meza ya kuvalia ni kituo cha vitu vyako vingi ambavyo vingeweza kuwa vimewekwa maeneo mengine chumbani na kuleta muonekano wa mrundikano. Chumba cha kulala kinasemekana hakijakamilika bila kuwa na eneo hili la kuvalia kwenye ukuta wake mmojawapo.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Friday, April 11, 2014

friday finest

mvua za hapa na pale leo zimefanya hali ya hewa iwe ya kiubaridi ila madimbwi sasa...kukaa ndani kunalipa ukiwa umejivalia soksi na kujikunyata kiaina...weekend njema wapendwa..


Tuesday, April 8, 2014

my article for newspaper: chumba cha binti - tumboni hadi 18


Karibu msomaji kwenye makala ya leo ambayo nitaongelea jinsi ya kupamba chumba cha kulala cha binti yako miezi michache kabla hajazaliwa hadi akiwa na umri wa miaka 18.  Fuatana nami kwenye makala hii.
Sasa basi ni miezi michache imebaki kabla binti yako hajazaliwa. Kutokana na teknolojia kuwa juu mama mjamzito amepewa uwezo wa kujua jinsia ya mtoto wake aliye tumboni kama atapenda kufanya hivyo. Endapo basi wazazi watakuwa wanatarajia kuna binti yao anakuja duniani basi moja kwa moja wanaanza kufikiria kitanda cha mtoto na nguo na mapambo ya rangi za pinki, njano na kijani ambazo zitatawala chumba cha kijacho. Wakati ukiwa kwenye maandalizi hayo ni vyema ukaandaa kwa kufikiria miaka mitano hadi kumi mbeleni.

Kutokana na ukali wa maisha jaribu kuweka vitu ambavyo ni vya kudumu kwa kukumbuka kuwa kila kitu unachoweka kwenye chumba hiki ni chake na atakitumia kwa miaka 18 inayofuata  na hata kama ni mabadiliko yawe madogo yasiyo na gharama kubwa. Sasa utaniuliza je, kitanda cha mtoto kitatumika kwa miaka 18?  Endelea kujisomea ili upate jibu la hili swali. Rangi za pinki, njano na kijani nazo pia ni sawa kwa chumba cha mtoto wako wa kike mchanga lakini jaribu kutumia rangi ambazo zinakaa kati. Kwa mfano ukitumia pinki iliyokolea na njano ya mwanga wa jua kama rangi za ukuta wa chumba cha binti yako vitadumu hata atakapokuwa mkubwa na ataipenda pinki hii kuliko ile nyepesi ya kitoto!

Kununua fenicha ambazo zina matumizi zaidi ya moja na ambazo zinaweza kukaa kwenye chumba hicho kwa muda mrefu inaweza kuwa changamoto kuliko swala la rangi. Unahitaji kutembelea maduka mbalimbali ya fenicha na pia karakana za waseremala. Wote tunajua kile kitanda cha kichanga binti yako hawezi kukitumia kwa miaka 18 ijayo. Ni sawa kuwa na kitanda cha mtoto kwa ajili kina vizuizi pembeni ili asianguke. Ila ili kuweza kuwa na matumizi ya kitanda hiki kwa umri wote wa utoto wa binti yako tafuta kitanda cha bebi ambacho kinaweza kugeuzwa na kuwa cha binti hapo baadaye. Kuna baadhi ya maduka ya fenicha ambayo unaweza kupata kitanda kama hiki. Vinginevyo unaweza kwenda kwenye karakana za waseremala na kuagiza utengenezewe kitanda cha kikubwa ila kiwekwe vizuizi ambavyo vitafanya kazi kama ile ya kitanda cha bebi.
Hapo baadae kadri binti yako anavyokua unapamba chumba chake upya ambapo utaondoa vizuizi na kitabakia kuwa kitanda cha binti na sio bebi tena. Mzazi siku hizi usitafute kitanda cha bebi kinachosimama peke yake. 

Tafuta ambacho bebi yako pia atakitumia akiwa binti, kwa njia hii utakuwa umetumia pesa yako kwa busara. Usitumie hela nyingi na uchumi huu kununua vitu ambavyo utaviondoa tena miaka michache itakayokuja. Kama unataka kuongeza kitu kwenye chumba cha mtoto wako ambacho anafurahia sasa lakini sio hapo baadaye hakikisha sio cha gharama kubwa na ni rahisi kukiondoa.

Chumba cha kulala cha binti yako ni sehemu ambayo atatumia muda mwingi zaidi wakati akiwa msichana mdogo, atakuwa analala hapo pia wakati mwingine atacheza na madoli yake hapo. Kuwa mbunifu kwenye kupamba chumba hiki na utumie gharama za kawaida. Weka zulia la rangi moja ambalo utaweza kutupia kizulia kingine kidogo cha rangirangi juu yake pale pembeni ya kitanda. Kizulia hili kidogo rangi kuu ziwe zinaendana na rangi nyingine za hapo chumbani hata kama ni pazia ama shuka ama ukuta. Zulia litasaidia kuweka miguu ya bintiyo kwenye joto na hata akiwa amekaa chini na pia linaongeza uzuri wa muonekano wa chumba. Mwekee shuka, mito na pazia zinazooana na rangi ya mandhari uliyochagua. Chagua pazia na shuka za kike na pia zenye rangirangi kama maua au nyota au hata rangi za upinde wa mvua.

Hatimaye binti yako mdogo anaanza chekechea; muda unakimbia. Weka mpangilio wa chumba kivingine ili kutengeneza nafasi kubwa ya kucheza na matoi na kusuka madoli yake. Kadri binti anavyokua, ladha yake inabadilika kwa kasi siku hadi siku achilia mbali mwaka hadi mwaka. Unaweza ukatetea kutumia hela kwa umakini kwa ajili ya chumba chake kwa kujua ni nini cha kununua na jinsi ya kukitumia.

Unapamba chumba chake tena kwa awamu nyingine ya kikubwa. Chagua mandhari itakayotokana na vitu na rangi anazopendelea binti yako kabla ya kumshtukiza na kuanza kupanga na kuweka vitu upya chumbani kwake. Pia unaweza kupamba nae pamoja. Anza kwa kupaka tena rangi na baada ya hapo ongeza fenicha ambazo bintiyo atahitaji ambazo ni kimeza na kiti chake , meza ya kuvalia, kisofa kidogo na kishelfu cha vitabu. 

Rangi ya vitu hivi iendane na mandhari uliyochagua. Kwa mfano kama mandhari ni rangi ya pinki, usiweke sofa ambalo halioani na pinki. Pia sasa ni wakati wa kuondoa zile mbao za kuzuia asianguke na kitanda kubakia cha binti mdogo sio kile cha kichanga tena.

Kwenye droo za hiyo meza ya kuvalia hifadhi vitu vyake vya michezo na vitu vidogovidogo viwekwe humo visitupwetupwe. Kwenye droo hizo weka kwa mpangilio ili asipate shida kuona vitu. Kama kutakuwa na nafasi ya ziada pia weka kiti cha kubembea. Mabinti wanaokua wanakipenda kukalia wakati wa kusoma kitabu cha hadithi, gazeti au jarida. Kwa ajili miaka imeenda kile kizulia cha rangirangi ulichotupia juu ya lile zulia la rangi moja unaweza ukakibadilisha kwa  kumnunulia kingine. Maadam sasa ni mkubwa ataweza kuchagua rangi anazopenda ambazo zitaoana na zingine hapo chumbani.

Baada ya hapo unaweza ukaenda na bintiyo kweye maduka ya mapambo ya ndani akachagua vitu vidogodogo vya kuongezea kama taa za vivuli fremu za picha, kifungashio cha kalamu na penseli kwenye deski lake, mishumaa na kibox cha kuweka hereni na mikufu na vitu vyake vingine vya urembo. Na pia kama atapenda waweza mwekea vioo vya ukutani. Sasa kitu pekee anachohitaji kwenye lile deski ni kompyuta. Mzazi usione bintiyo anataka kutumia kompyuta yako ukamfukuza. Ni muda wake nae kuwa na yake kwake.

Kwa majumuisho, pamba kwa jinsi ambayo chumba kinakuwa na mwanga wa kutosha na sehemu kubwa ya kuhifadhi vitu ili asitupetupe vitu chini kwa madai ya kuwa hakuna nafasi ya kuweka. Mwanga wa kutosha na deski ni kwa ajili ya kujifanyia kazi zake za shuleni. Na kama unapenda binti yako ajenge tabia ya kujisomea basi usidharau umuhimu wa kumwekea shelfu la vitabu kwenye chumba chake kuweka vitabu vyake vya zamani na vipya mahali pamoja.

Hongera! Umefanikiwa kupamba chumba cha binti yako toka akiwa bebi hadi miaka 18 bila usumbufu mkubwa, muda au pesa nyingi!

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk