Friday, June 5, 2015

KICHEKO!... Wananchama DECI kupewa "mbegu" zao walizopanda

Waziri wa fedha, Saada Mkuya
Serikali imesema kuwa inafanya utaratibu wa kuwalipa fedha takribani Sh. bilioni 19 za waliokuwa wanachama wa Taasisi ya Development Entrepreneurship Community Initiative (Deci).
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, alisema fedha hizo zimehifadhiwa katika akaunti ya Benki Kuu (BoT) na kwamba kinachofanyika sasa ni uangalizi wa kiasi cha michango iliyochangwa na wanachama ili waweze kulipwa kwa usahihi.

“Bado fedha zinashikiliwa BoT uchambuzi unaendelea kufanywa kwa umakini wa hali ya juu, utakapokamilika wanachama wote waliochanga fedha watalipwa,” alisema Mkuya.

Aidha, Waziri Mkuya alisema siyo jambo litakaloweza kuchukua muda mfupi kukamilisha mchakato wa malipo ya wanachama hao, kwani linahitaji muda wa kutosha kufanyiwa kazi kikamilifu, ingawa hakutaja kiasi kilichopo.


Mwaka 2009 serikali ilisitisha shughuli za Deci na kuwafungulia mashtaka wakurugenzi watano wa taasisi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam na Agosti 19, mwaka 2013, walihukumiwa.

No comments:

Post a Comment