Thursday, March 14, 2013

My article for newspaper: Sofa Sahihi


Jinsi ya kupata sofa zitakazokufaa

Kama unataka kupata kiusingizi cha mchana, kuangalia filamu au hata kujisomea kitabu, sofa mara nyingi ni sehemu panapopendwa zaidi kwa wanafamilia. Sofa ni fenicha muhimu nyumbani kwako na mara uinunuapo utakaa nayo walau kwa miaka mitano au zaidi. Kwa hivyo ni muhimu kuchagua sofa sahihi unapoamua kununua moja. Makala hii itakupa dondoo za kukuwezesha kununua sofa sahihi! Endelea kusoma.

Kila nyumba ni matokeo ya ndoto ya anayeimiliki, ambapo maslahi na ladha za mmiliki huyo zitaonekana kila kona ya nyumba hiyo. Iwe ni rangi au kifaa cha fenicha kitakuwa kimepata baraka za mmiliki kuwa ndani ya nyumba yake. Ni ukweli kuwa kila chumba kinaweza kuwekwa katika hali ya juu kabisa kwa kuwekwa fenicha na samani sahihi. Sofa linachukua sehemu muhimu kubadilisha chumba kilichozubaa kuwa cha muonekano wa kuvutia. Kuna aina nyingi ya sofa ambazo unaweza kuchagua kuanzia za kuweka sehemu iliyonyooka hadi sehemu ya mduara na kwenye kona, na kazi yako haitakuwa rahisi kama unataka sofa sahihi za kuendana na ndani mwako, kufanya sebule  yako au chumba kingine rasmi kiwe cha kuvutia. Kuchagua sofa sahihi haiwezi kuwa kazi ngumu kwako kama unajua baadhi ya miongozo muhimu.

Kabla hujapanga kununua sofa, unatakiwa ujue ukubwa wa chumba ukoje na unataka sofa ichukue nafasi kiasi gani. Jiulize kama sofa husika zitatosha familia yako yote ama laa. Matumizi ya nafasi ni kipaumbele kati ya vipengele vya kuzingatia kabla hujanunua sofa.
Wakati unapoenda kutafuta sofa za kununua, tafuta zile zenye muonekano na mtindo ambao utaoana vyema na samani nyingine zilizopo hapo chumbani. Kuna chaguzi kadhaa kutoka sofa za kitamaduni hadi za kisasa. Unaweza ukapata zilizotengenezwa tayari au unaweza kutoa oda kwa waseremala wakakutengenezea kwa kadri ya hitaji lako. Sofa yoyote iwe ni ndefu, ama ya kona ama ya mtindo wa sofa kitanda inaweza kuleta mvuto kwenye chumba chako.

Rangi na michoro ya sofa vinahusu, mara nyingi rangi ya sofa inapendekezwa iwe sawa na ya ukuta wa chumba. Hata hivyo kama unataka kuongeza mtindo na staili chagua sofa zenye rangi na michoro iliyokolea. Hii itafanya macho yavutwe kuzitizama badala ya kuwa tu kama mojawapo ya fenicha chumbani. Zingatia ladha na matamanio yako binafsi vilevile.

Chagua sofa zenye kitambaa kinachoendana na maisha unayoishi. Kwa mfano usithubutu kuchagua kitambaa cheupe kama una watoto wadogo. Kuwa na wanyama kama vile paka na mbwa ndani ya nyumba ni mapenzi ya mtu binafsi na kama wewe ni mmoja wa wenye mapenzi hayo si busara kuchagua sofa za kitambaa cheupe kwani wanyama hawa wanaweza kuleta maafa kwenye sofa zako za gharama. Kwa hivyo zingatia rangi na ubora wa kitambaa cha sofa kabla ya kufanya manunuzi.

Kabla ya kununua sofa zijaribu kwa kuzikalia wewe mwenyewe. Tafuta mawazo ya mtu wa pili kama itahitajika. Kama wakati wa kukaa sofa zinatoa mlio ni dalili kuwa hazijatengenezwa vizuri. Angalia kama kiti kinaendana na urefu wa miguu yako na eneo la kuegemezea mkono. Hata hivyo kadri sofa inavyotumika ndivyo inavyokaa vyema na kukidhi mahitaji.

Wakati wa kuchagua sofa hakikisha kuwa fremu zake ni imara na gundi za mbao zimesambazwa na kugundishwa vyema. Ubora wa mbao ni jambo la kuzingatia sana hasa kama unaweka oda ya  kutengenezewa. Mara kadhaa waseremala wanaweka mbao za matenga ya nyanya na kwakweli mbao hizi si imara kwa matumizi ya sofa. Kwa hivyo mara baada ya kukabidhiwa sofa zako na kuzipeleka nyumbani kwa ajili ya matumizi hazikai hata miezi mitatu zinavunjika vunjika.

Mito ambayo haijaunganishwa kwenye sofa ni mizuri zaidi kwa starehe na pia urahisi wa kuvua foronya na kuzifua. Mito iwe imejazwa ujazo sahihi ili isibonyee na kusinyaa kadri siku zinavyoenda.

Mwisho wa yote kumbuka kuwa usinunue sofa kwa ajili tu ya kukalia, bali pia kwa ajili ya starehe!
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23

No comments:

Post a Comment