Wednesday, September 28, 2016

Hatua za kusafisha milango na madirisha ya kioo


Kusafisha madirisha na milango ya kioo nyumbani ni moja ya kazi ambayo inawezekana unaipa wasafishaji wa nje waifanye kwa kuhofia kuwa ni ngumu. Japo kiukweli haipaswi kuwa kazi ngumu, kama unajua mbinu na hatua sahihi za kupitia ili kufanikisha kwa urahisi. Zifuatazo ni hatua za kupitia ili kufanikisha kusafisha maeneo yenye vioo yang’ae kabisa.

·        Pangu muda wa kusafisha
Safisha muda ambao jua halipigi moja kwa moja kwenye kioo.
Jua kali linakausha dirisha mapema mara unapoanza kuliloanisha kabla ya
kulisuuza ambapo inaacha ukungu wa dawa ya kusafishia au matone ya maji na hivyo kukulazimu kurudia tena zoezi hilo. Ili kuepuka hali hiyo, safisha asubuhi na mapema kabla jua halijawa kali au subiri hadi siku yenye mawingu.

·        Andaa vitendea kazi
Vimiminika vya kusafishia vyaweza kuwa vya aina mbili, ya kwanza ikiwa ni ile dawa maalum iliyotengenezwa kwa lengo la kusafishia vioo na aina ya pili ikiwa ni kutumia maji. Endapo unatumia maji yachanganye na kiasi kidogo cha vinega kwa uwiano wa kipimo kimoja cha vinega kwa vipimo kumi vya maji. Vifaa vingine ni sponji, kitambaa kikavu cha pamba au magazeti, brashi ndogo laini na ngazi ndogo endapo madirisha yako umbali mkubwa toka ardhini.

·        Safisha kuanzia juu kushuka chini
Ikiwa kweli unataka usafishe eneo lenye kioo litakate na kung’aa, basi safisha kuanzia juu kushuka chini. Kufanya hivyo kutakuhakikishia kuwa hakuna uchafu utakaodondokea kwenye sehemu ambayo umeshasafisha tayari.

Kama eneo la kioo unalotaka kusafisha ni chafu sana kwa mfano kuna vumbi jingi au utando wa buibui, inakupasa kutumia kitambaa kikavu kuondoa uchafu huo kwanza. Kwenye kona kuna kawaida ya uchafu kuzama kwahivyo tumia brashi laini kuuondoa.

·        Loanisha kioo
Kwa kutumia sponji lenye maji loanisha kioo huku ukiepuka kuweka maji mengi kiasi cha kuchuruzikia kwenye fremu ya mlango au dirisha la kioo unalosafisha. Suuza na kausha kioo kwa kutumia kitambaa kikavu halafu mwishoni ng’arisha kwa kufuta na kipande cha gazeti.
Endapo unatumia dawa za kusafishia kioo basi inakupasa kuipulizia kidogo kidogo moja kwa moja kwenye kioo huku ukifuta haraka haraka kabla haijakaukia. Tumia gazeti au kitambaa cha pamba ambacho hakitoi nyuzinyuzi.
Pia ni vyema kufahamu kuwa baadhi ya dawa za kusafishia vioo zinaharibu mbao. Kuwa makini kama fremu ya eneo la kioo unalosafisha imetengenezwa kwa mbao, puliza dawa kidogo kidogo na epuka kuigusisha na fremu.

·        Safisha fremu na kona kwa kitambaa tofauti
Haijalishi ni ngumu kiasi gani unaweza kuondoa uchafu kwenye eneo la kioo, lile la kona na fremu ndio linabeba uchafu mwingi zaidi kama huna vifaa sahihi. Safisha maeneo haya kwa kutumia kitambaa au fulana zee ya pamba, inanyonya uchafu wote na kuacha fremu safi.



Madirisha ya kioo inapaswa yawe yanasafishwa kwa kina angalau mara moja kila mwezi au walau kila baada ya miezi miwili.

No comments:

Post a Comment