Thursday, January 16, 2014

My article for newspaper: chumba cha kufulia


Eneo la kufulia liwe na muonekano na vifaa hivi.

Ni mara ngapi kwa juma ambazo unafua nguo? Familia ya watu wanne kwa mfano, inaweza kuwa inafua kati ya mara 3-4 kwa juma. Kwa maana hiyo ni vyema kuwa na chumba ama eneo maalum la kufulia nguo ambalo lina vitu muhimu vinavyotakikana kuwepo ili kufanikisha kwa haraka na kwa urahisi mchakato mzima wa kuondoa nguo kutoka kwenye uchafu hadi kuiweka katika hali ya kufaa kuvaliwa tena.

Asilimia kubwa ya kaya katika nchi zinazoendelea hakuna mahali au chumba maalum cha kufulia na badala yake hasa maeneo ya mijini mahali pa kufulia ni juu ya shimo la maji taka! Hii sio sawa kwa mfuaji kwani muda wote anaokuwa anafua pale anavuta hewa chafu inayotoka shimoni humo hivyo kuhatarisha afya. Kwa wenzetu walioendelea na baadhi ya familia katika nchi zinazoendelea, kwenye makazi yao wana chumba au eneo maalum la kufulia linalokidhi viwango vya vifaa na mahitaji. Si sawa kuwa na eneo tu la nje karibia na chanzo cha maji kwa ajili ya kufulia kwani kuna vitu muhimu ambavyo vinafanikisha zoezi la kufua na kwa kweli huwezi kuvihifadhi nje tu kwenye eneo hilo.

Eneo ama chumba cha kufulia kitafaa zaidi kikiwa kiko maeneo ya uani. Ili kuwa na eneo sahihi la kufulia ambalo utaokoa muda na nguvu zako na kukufanya uvutiwe na kazi hiyo fikiria shughuli zitakazofanyika hapo: kuchambua nguo, kufua, kukausha, kunyoosha, kutundika na kukunja. Weka mpangilio wa kuwezesha vifaa vyako viendane na mtiririko huo. Wala hutakiwi kuwa na eneo kuubwa kwa kazi hii, dogo liwavyo, eneo hili litawezesha nguo zitoke kwenye sinki iwapo unafua kwa mikono au kwenye mashine kwenda kukaushwa/kuanikwa, na kupelekwa meza ama kaunta ya kunyooshea na kukunjwa ama kutundikwa kuendana na hitaji la kila nguo.

Nchi yetu imejaaliwa kuwa kwenye ukanda wa jua la kutosha ambapo hatuna haja ya kuwa na mashine za kukaushia nguo. Rasilimali ya jua tuliyonayo inatutosha hatuhitaji kukausha kwa mashine za umeme. Kinachotakiwa tu ni kuwa na kamba za kukaushia karibia na mahali pako hapo pa kufulia.
Ni lazima kuwa na mahali pa kutundikia nguo zinazonyooshwa ambazo hazitakunjwa. Fimbo za kutundia mahali pa kufulia zinahusu. Fimbo hizi ziwe mbali kidogo na ukuta ili nguo zilizokwisha nyooshwa zisiuguse. Fimbo hizi ni za kutundika nguo kwa muda tu wakati wa kunyoosha kabla hasijasambazwa katika makabati ya nguo husika. Zile nguo zinazokunjwa baada ya kunyooshwa nazo zinahitajika mahali pa kuhifadhia kwa muda katika chumba cha kufulia kabla hazijasambazwa kwenye droo zinazohusika. Kwa maana hiyo pamoja na fimbo ya kutundikia, pia unahitaji kuwa na shelfu. Huu mpangilio ni kwa ajili ya kurahisisha mchakato wa kuondoa nguo kwenye kutoweza kuvalika kutokana na uchafu hadi kuiwezesha kuvalika tena; kwa hiyo ni kwa kaya yoyote na wala usidhanie ni maisha ya watu wa daraja fulani tu.
 Gawa sakafu ya eneo lako la kufulia katika maeneo mawili. Lile la maji maji kwa mfano kwenye sinki na lile kavu kwa mfano pale pa kunyooshea. Utajikuta hili eneo kavu halipati maji kabisa na waweza kupamba hata kwa kizulia. Kama una mashine ya kufulia weka upande sawa na wa sinki ili hata imuwie rahisi fundi bomba endapo kutakuwa na tatizo lolote kwani bomba zote zitakuwa eneo moja na kufanya zile shughuli za maji maji kuwa pamoja. Tenga la nguo chafu liwe jirani kwa ajili ya urahisi wa kubeba na kuweka kwenye mashine au kwenye sinki.
Eneo la kamba za kukaushia lisiwe mbali na panaponyooshewa ili iwe rahisi kuanua nguo na kupeleka moja kwa moja kwenye kaunta ya kunyooshea. Ili kutumia eneo dogo mara nyingi baadhi ya wenye nyumba wanapenda kujenga kaunta ya kunyooshea juu ya mashine ya kufulia. Inakuwa ni busara kutumia eneo hili la juu ya mashine badala ya kuliacha bure na badala yake kwenda kuweka kimeza cha kunyooshea kwingine. Na kwa bahati nzuri mashine za kufulia kwa ajili ya majumbani zina urefu chini kidogo ya meza ya kunyooshea kwa hivyo hakuna ubaya kujengea hii kaunta ya kunyooshea juu yake. Pia kaunta iliyojengwa kwa zege kwa ajili ya kunyooshea ni imara na inadumu maisha kulinganisha na meza.
Kuweka vifaa katika mpangilio kunarahisisha mambo. Kusanya sabuni na dawa zako zote za kufuli katika shelfu mojawapo ili kila kitu kiwe kwenye ncha ya vidole vyako pale unapokihitaji. Hakikisha baadhi ya madawa na blichi zinakuwa eneo la juu ambalo watoto wadogo hawawezi kufikia, kama vipi weka loki kabisa.  
Mahali pako pa kufulia pawe na mwanga wa kutosha. Mwanga mwingi wa asili ni mzuri zaidi hasa wakati wa kufua kwa mkono na kunyoosha. Mwanga pia unakuonyesha ndani ya mashine kukuridhisha kuwa hakuna nguo iliyosahaulika.
 Sakafu inayofaa bafuni na jikoni inafaa pia eneo la kufulia. Sakafu ya marumaru ni rahisi kusafisha, haipitishi maji na ikitokea kumwagika haiharibiwi na blichi.
Kufua haitakiwi kuwa kazi ya kuchukiza. Weka mpangilio huu mahali pako pa kufulia  na kamwe hutachukia mchakato mzima wa kufua na kunyoosha nguo.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa magari, nguo na mazulia; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment