Thursday, April 4, 2013

My article for newspaper: Mito ya sakafuni


Tumia mito ya sakafuni kwa kukalia na kama pambo

Mto wa sakafuni ni kusheni kubwa linalotumika sakafuni kama pambo au mahala pa kukalia. Mto huu huwa umejazwa zaidi na ni mgumu kuliko mito ya kawaida ya kwenye sofa ili kuweza kuhimili uzito wa mwili. Mara nyingi mito hii ni mikubwa na hutumika kukalia wakati wa burudani kama vile wakati wa kutazama  luninga na pia ni nyongeza ya mahali pa kukalia kwenye vyumba vya michezo ya watoto.

Mto wa sakafuni unaweza kuwa na umbo lolote liwe ni duara, boksi ama mraba. Weka mito yako mitatu juu ya kizulia chako cha kutupia na mara utagundua kuwa umetengeneza sehemu ya nyongeza ya kukalia wakati wa burudani au mahali poa pa kusoma na kustarehe. Chagua mito ambayo itaendana na kizulia chako. Mpangilio wa kizulia hicho na mito yenye rangi za kukolea utaleta mvuto. Pia unaweza kupendezesha sakafu yako ya marumaru au mbao kwa kutupia mito ya sakafuni. Chagua rangi za ladha yako kuendana na rangi ya sakafu ili kuleta muonekano wa mapambo ya kisasa.

Mito ya sakafuni ni pambo rahisi ambalo kila nyumba inaweza kuwa nalo. Kama wazo lako la mito ni kuweka kwenye sofa  tu; basi unahitaji kuchukua muonekano mwingine. Mito hii inakuja kwa saizi mbalimbali kwa jinsi ambayo inaweza kumfurahisha kila mtumiaji awe ni mtoto, kijana ama mtu mzima. Unakutana na matumizi mengi ya mito mikubwa ya sakafuni na utashangaa ni kwa vipi unaweza kuishi bila hiyo. Hata kwa kukaa tu na kutulia kutafakari maisha au kucheza karata karibu na meza ya kahawa, mito ya sakafuni inafanya kukaa sakafuni kuwa ni raha na shughuli zako kuwa za starehe zaidi

Watoto wanaipenda! Ni muhimu wakati wa kucheza na watoto. Ukiwa unakaa karibu na watoto mara kwa mara utaanza kugundua ni muda mwingi kiasi gani wanaoutumia sakafuni.  Na pia ni muda mwingi kiasi gani wanapenda ukae nao hapo sakafuni! Kama una mtoto mdogo utakugundua kuwa mto mkubwa wa sakafuni ni sehemu tosha kwa usingizi kwa mchana.
Pia kwa swala la usalama, watoto wadogo hawako makini kihivyo; na hasa wanapokuwa wanakimbia na kuishia kujirusha kwenye sofa. Ndio hapo wapohitaji mto mkubwa wa sakafuni kuangukia. Na hata wanapong’ang’ania kubembea kwenye mikono yako hadi unaposikia kama mikono inataka kung’oka, basi sehemu ya kuwatulizia ni kwenye mito ya sakafuni.
Kwa kuhurumia magoti yako idadi ya mito inavyoongezeka ndio na uzuri wake unavyoongezeka. 

Kwa nini ukae tu juu ya kizulia uumizwe na sakafu wakati kuna mto mkubwa wa kunesa ambao ungeweza kuukalia? Wakati familia yako ikiendelea kukua na sehemu ya kuweka fenicha imeshajaa, mito mikubwa ya sakafuni ni mbadala tosha wa viti. Kwa mikutano ya familia na marafiki wakati ambapo hamna viti vya kutosha hufurahii wale wanaoshia kukaa sakafuni wapate starehe (hata kama ni watoto?)

Mito ya sakafuni inayokunjika ni chaguo zuri. Hii ina sehemu tatu, kunjua wote kama unataka kulala kwa tumbo; halafu kama unataka kukaa kwa muda; ukunje zile sehemu mbili ili usaidie mgongo na sehemu ya tatu kalia. Mito ya aina hii pia ipo ya kufanana kama fenicha kabisa ambayo ina hadi sehemu za kupumzisha mikono.

Je una kimnuso cha binti yako mdogo nyumbani? Ni nini kinachoweza kuwa rahisi zaidi ya kuweka nusu dazeni ya mito hii kwenye sakafu ya sebule yako. Wacha waangalie katuni hadi wasinzie halafu waache hapo, ukijua kuwa wana kitanda na mto pamoja! Kwa hivyo kama isivyo kwa mapambo mengine ya ndani, mito ya sakafuni inawekwa kwenye matumizi ya kukalia na mapambo kwa wakati mmoja.

Mito ya sakafuni inaweza kuwa kwenye kitambaa chochote utakacho hadi kwenye ngozi na hata plastiki kwa ajili ya ile ya kwenye varanda. Baadhi ya watu wanapenda kuoda mito ili watengenezewe kuendana na mapambo yao mengine ya ndani au hata mapambo ya chumba husika. Ingawa hii inaweza kuwa gharama zaidi lakini inakuwezesha kupata foronya za rangi upendayo na utakazoweza kubadilisha kadri upendavyo.
Kama unataka kuburudisha nje ya nyumba kwenye varanda yako tafuta mito ya sakafuni ya nje. Mito hii ya sakafuni ya kwenye varanda inatengenezwa kwa foronya za kudumu kwa mfano za kanvasi, ngozi ama plastiki, ili kujikinga na unyevu maji na hata kuzuia kupauka kirahisi. Wakati usioihitaji ihifadhi stoo ili kuiwezesha idumu.

Mito ya sakafuni inatumika kama pambo na mahali pa kukaa pale ambapo urefu wa kiti ama usaidizi wa kina wa mgongo hauhitajiki. Kama unavyoweza kuona, jinsi ambavyo mto wa sakafuni unavyoweza kutumika kama pambo au kama fenicha nyumbani kwako ubunifu tu ndio unahitajika. Wageni wako watu wazima wanaweza kuunganisha mito ya sakafuni kadhaa wakavuta shuka na tayari kuwa kitanda bandia  cha mgeni Kwa hivyo unasubiri nini kuwa na mito ya sakafuni?

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi anajishughulisha na usafi wa mazulia na nguo aina zote; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda viviobed@yahoo.co.uk au 0755 200023

Wednesday, March 27, 2013

My article for newspaper: Jinsi ya kufanya zulia lidumu


Jinsi ya kuwezesha zulia lako lidumu na kuwa maridadi kila wakati

Kwa jinsi ambavyo utaweza kuweka zulia lako safi ndivyo litakavyoweza kudumu. Kwa madhumuni ya makala hii zulia litamaanisha lile la kufunika ukuta kwa ukuta na vitupio vya zulia ama vizulia ni yale mazulia madogo madogo ya kuweka maeneo yaliyoainishwa kwa mfano chini ya meza ya kahawa na kadhalika.

Sasa basi ingawa zulia safi na maridadi ni sehemu muhimu sana ya muonekano wa nyumba, kuweka jipya mara kwa mara ni gharama kubwa. Makala hii itakuonyesha ni kwa jinsi gani unaweza kufanya zulia na vizulia vyako vidumu na kuonekana vipya kwa muda mrefu.
Uchafu unafanya nyuzi za zulia lako zichakae. Safisha kwa mashine ya upepo ili kunyonya mchanga na vumbi kwenye zulia lako kila siku kwenye zile sehemu zinazokanyagwa kila wakati na walau mara moja au mbili kwa wiki kwenye zile sehemu zisizokanyagwa mara kwa mara. Asilimia 80 ya uchafu kwenye zulia ni taka kavu kwahivyo zinadakwa moja kwa moja na aina hii ya usafishaji wa zulia. Wakati wa kutumia mashine hii hakikisha unatumia brashi sahihi kuendana na unene na urefu wa manyoya ya zulia lako na pia iwe imesetiwa kwa urefu sahihi kwani kama utaipitisha juu juu tu haitakuwa inasafisha ipasavyo na kama iko chini sana inaweza kuharibu zulia kwa kung’oa manyoya. Kumbuka kusafisha mfuko wa taka wa mashine ili kuiwezesha kufanya kazi vizuri. Maeneo ya mlangoni weka vizulia vidogo vya kukanyagia kabla mtu hajaingia ndani. Utunzaji huu wa mara kwa mara utaboresha muonekano mzima na kuongeza maisha ya zulia lako .

Teua maeneo ya kulia chakula. Matone ya vyakula yanaleta mafuta kwenye zulia ambapo haya mafuta yanavuta taka nyingine na kufanya zulia lipoteze mvuto. Kwa jinsi ambavyo vyakula vinaliwa maeneo yasiyokuwa na zulia ndivyo kunavyokuwa na nafasi kubwa ya kuepuka matone matone kwenye zulia. Weka sera ya  kwamba vitafunwa vyote vitaliwa jikoni au mezani ili hata kama ni kwa watoto wadogo wakae mezani mabaki yadondoke mezani na sio juu ya zulia. Hata kama familia yako itaandamana kuhusu sera hii, bado ni njia pekee kuzuia matone yasifanye madoa kwenye zulia lako. Kama una watoto hakikisha kuwafahamisha wakujulishe mara wamwagapo kitu kwenye zulia ili usafishe mara moja. Michuzi, chokoleti na juisi ni mauaji kwenye zulia lako la thamani. Kama chakula kitapata njia ya kuelekea kwenye zulia basi hakikisha unasafisha mara hiyo hiyo. Tumia povu la shampoo ya kusafishia zulia ili kuepuka kulilowesha chepechepe na sugua kwa brashi laini kuondoa uchafu wote. Mabaki yoyote yatavuta uchafu mwingi zaidi.

Usiruhusu uchafu kuingia ndani. Weka mazingira ya nje ya nyumba na njia zote za kuingilia ndani safi. Hii itapunguza sana kiasi cha uchafu unaoweza kuingia ndani ya nyumba. Uchafu wote ubaki nje ya nyumba kwani uchafu unazeesha zulia. Ingawa unaweza kujisikia ugumu wa kuwaambia wageni wako wavue viatu kuingia ndani, kuacha viatu mlangoni kunapunguza kiasi kikubwa cha uchafu ambao ungeingia ndani. Kuvua viatu kabla ya kuingia ndani ni tabia nambari moja ambayo sio tu itapunguza ratiba za kusafisha zulia bali pia kuongeza maisha ya zulia lako. Chukua muda kuweka njia za kuingilia ndani safi.

Ni vyema kuhamisha fenicha zako kila baada ya muda fulani fulani ili kupunguza shurba kwa yale maeneo yanayokanyagwa mara kwa mara. Zulia linachakaa haraka zaidi maeneo watu wanapokanyaga kila mara. Badilisha muonekano wa vyumba ambapo utaleta njia mpya za kupitia ili kupumzisha baadhi ya maeneo kwahivyo zulia lako kuwa jipya maeneo yote na sio tu maeneo kadhaa. Weka vizuizi kwenye miguu ya fenicha hasa zile nzito  kuzuia zisiharibu zulia. Kama ukihamisha fenicha na kukuta kuwa imeweka alama kwenye zulia chukua kipande cha barafu weka juu ya hilo eneo  acha iyeyuke na polepole sugua kwa brashi laini. Kutegemea na jinsi nyumba yako ilivyo bado pengine kuna maeneo ambayo yanabakia kukanyagwa zaidi hata kama ungebadisha badilisha fenicha kiasi gani. Hivyo basi maeneo haya yanayokanyagwa zaidi tupia vizulia.
Maeneo ya zulia chini ya mlango wa kutokea nje huwa yanajenga mstari wa uchafu. Hii ni kwa ajili nje kuna uchafu mwingi wa mavumbi na udongo ambao ukinyonywa na zulia hufanya mstari huo. Ukienda kwenye maduka ya vifaa vya usafi wa majumbani utapata dawa maalumu za mazulia za kuondoa uchafu wa aina hii. Wekeza kwenye zulia nzito za kukanyagia mlangoni kuzuia uchafu wa ziada usiingie ndani.
Uji wa mishumaa hung’ang’ania sana kwenye zulia kwa hivyo epuka mshumaa unaowaka kudondosha uji wake moja kwa moja kwenye zulia.
Kuondoa uzi au nyoya lililochomoza tumia mkasi kukata badala ya kuvuta ambapo kwa kuvuta unaweza vuta zaidi ya uzi mmoja hivyo kuharibu zulia.
Maeneo ya zulia yanayopigwa na jua moja kwa moja, usiweke pazia wazi ili kuzuia kupauka au kufanya rangi ya kahawia.
Tembea kwenye zulia ukiwa umevaa soksi. Wakati kutembea bila viatu itafanya zulia lidumu, hutakiwi kutembea kwenye zulia lako miguu mitupu. Mafuta na majasho yanayotoka kwenye ngozi ya miguu yanang’ang’ania kwenye zulia na kuvuta takataka zaidi.
Pamoja na yote hayo hapo juu ya kuwezesha zulia lako liwe maridadi kila wakati na lidumu, jinsi lilivyowekwa pia inahusu. Hakikisha unatafuta wawekaji wenye ujuzi wa kuweka zulia hasa lile la ukuta kwa ukuta. Safisha zulia lako usafi wa kina wa mashine ya umeme ya mvuke ya kusafishia mazulia walau mara moja kwa mwaka. Huduma hii utaipata kwa wataalam wa usafi wa mazulia na wala huna haja ya kuwekeza kwenye mashine hii kwa kuwa utahitaji huduma yake mara moja tu kwa mwaka.
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie viviobed@yahoo.co.uk , simu 0755 200023

Thursday, March 14, 2013

My article for newspaper: Sofa Sahihi


Jinsi ya kupata sofa zitakazokufaa

Kama unataka kupata kiusingizi cha mchana, kuangalia filamu au hata kujisomea kitabu, sofa mara nyingi ni sehemu panapopendwa zaidi kwa wanafamilia. Sofa ni fenicha muhimu nyumbani kwako na mara uinunuapo utakaa nayo walau kwa miaka mitano au zaidi. Kwa hivyo ni muhimu kuchagua sofa sahihi unapoamua kununua moja. Makala hii itakupa dondoo za kukuwezesha kununua sofa sahihi! Endelea kusoma.

Kila nyumba ni matokeo ya ndoto ya anayeimiliki, ambapo maslahi na ladha za mmiliki huyo zitaonekana kila kona ya nyumba hiyo. Iwe ni rangi au kifaa cha fenicha kitakuwa kimepata baraka za mmiliki kuwa ndani ya nyumba yake. Ni ukweli kuwa kila chumba kinaweza kuwekwa katika hali ya juu kabisa kwa kuwekwa fenicha na samani sahihi. Sofa linachukua sehemu muhimu kubadilisha chumba kilichozubaa kuwa cha muonekano wa kuvutia. Kuna aina nyingi ya sofa ambazo unaweza kuchagua kuanzia za kuweka sehemu iliyonyooka hadi sehemu ya mduara na kwenye kona, na kazi yako haitakuwa rahisi kama unataka sofa sahihi za kuendana na ndani mwako, kufanya sebule  yako au chumba kingine rasmi kiwe cha kuvutia. Kuchagua sofa sahihi haiwezi kuwa kazi ngumu kwako kama unajua baadhi ya miongozo muhimu.

Kabla hujapanga kununua sofa, unatakiwa ujue ukubwa wa chumba ukoje na unataka sofa ichukue nafasi kiasi gani. Jiulize kama sofa husika zitatosha familia yako yote ama laa. Matumizi ya nafasi ni kipaumbele kati ya vipengele vya kuzingatia kabla hujanunua sofa.
Wakati unapoenda kutafuta sofa za kununua, tafuta zile zenye muonekano na mtindo ambao utaoana vyema na samani nyingine zilizopo hapo chumbani. Kuna chaguzi kadhaa kutoka sofa za kitamaduni hadi za kisasa. Unaweza ukapata zilizotengenezwa tayari au unaweza kutoa oda kwa waseremala wakakutengenezea kwa kadri ya hitaji lako. Sofa yoyote iwe ni ndefu, ama ya kona ama ya mtindo wa sofa kitanda inaweza kuleta mvuto kwenye chumba chako.

Rangi na michoro ya sofa vinahusu, mara nyingi rangi ya sofa inapendekezwa iwe sawa na ya ukuta wa chumba. Hata hivyo kama unataka kuongeza mtindo na staili chagua sofa zenye rangi na michoro iliyokolea. Hii itafanya macho yavutwe kuzitizama badala ya kuwa tu kama mojawapo ya fenicha chumbani. Zingatia ladha na matamanio yako binafsi vilevile.

Chagua sofa zenye kitambaa kinachoendana na maisha unayoishi. Kwa mfano usithubutu kuchagua kitambaa cheupe kama una watoto wadogo. Kuwa na wanyama kama vile paka na mbwa ndani ya nyumba ni mapenzi ya mtu binafsi na kama wewe ni mmoja wa wenye mapenzi hayo si busara kuchagua sofa za kitambaa cheupe kwani wanyama hawa wanaweza kuleta maafa kwenye sofa zako za gharama. Kwa hivyo zingatia rangi na ubora wa kitambaa cha sofa kabla ya kufanya manunuzi.

Kabla ya kununua sofa zijaribu kwa kuzikalia wewe mwenyewe. Tafuta mawazo ya mtu wa pili kama itahitajika. Kama wakati wa kukaa sofa zinatoa mlio ni dalili kuwa hazijatengenezwa vizuri. Angalia kama kiti kinaendana na urefu wa miguu yako na eneo la kuegemezea mkono. Hata hivyo kadri sofa inavyotumika ndivyo inavyokaa vyema na kukidhi mahitaji.

Wakati wa kuchagua sofa hakikisha kuwa fremu zake ni imara na gundi za mbao zimesambazwa na kugundishwa vyema. Ubora wa mbao ni jambo la kuzingatia sana hasa kama unaweka oda ya  kutengenezewa. Mara kadhaa waseremala wanaweka mbao za matenga ya nyanya na kwakweli mbao hizi si imara kwa matumizi ya sofa. Kwa hivyo mara baada ya kukabidhiwa sofa zako na kuzipeleka nyumbani kwa ajili ya matumizi hazikai hata miezi mitatu zinavunjika vunjika.

Mito ambayo haijaunganishwa kwenye sofa ni mizuri zaidi kwa starehe na pia urahisi wa kuvua foronya na kuzifua. Mito iwe imejazwa ujazo sahihi ili isibonyee na kusinyaa kadri siku zinavyoenda.

Mwisho wa yote kumbuka kuwa usinunue sofa kwa ajili tu ya kukalia, bali pia kwa ajili ya starehe!
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755 2000 23

Thursday, March 7, 2013

My article for newspaper: Feni ya Stovu


Umuhimu wa feni ya stovu

Jiko ni kitovu cha nyumba ya kisasa. Jinsi nyumba inavyozidi  kuwa za kisasa, ndivyo inavyokuwa na jiko lenye vifaa na muonekano wa kisasa pia. Katika makala hii jiko litamaanisha chumba chenyewe na stovu itamaanisha pale panapobandikwa sufuria. Ili kufanikisha uingizaji wa hewa jikoni nyumba za kisasa zina vifaa vya jiko vya kisasa. Mojawapo ya vifaa hivi ni feni ya stovu.

Feni ya stovu ni kifaa kinachofungwa juu ya stovu kwa ajili ya kukusanya moshi, harufu, mvuke na ghasia nyingine zizalishwazo hewani wakati wa kupika. Kwa ufanyaji kazi wa kuridhisha feni ya stovu inatakiwa kuwa na upana sawa na wa stovu yenyewe. Kuna feni ambazo zinanyonya moshi na mvuke na kutoa nje ya nyumba na kuna ambazo zimetengenezwa kwa jinsi ambayo moshi na harufu zinanyonywa ndani kwa ndani hata kama mfumo wa kutoa nje ya nyumba haupo. Kwa hiyo usijali kuwa jiko lako halina mfumo wa kukuwezesha kutoa uchafu huo wa mapishi nje ya nyumba, bado unaweza kufunga feni hii aina ya pili yaani ya kuvuta uchafu ndani kwa ndani.

Ndio, nyumba yako inaweza kuwa na harufu za mapishi ambazo hazikukoseshi faraja lakini ni ukweli kuwa harufu hizo sio nzuri kwa afya yako. Wakati unapopika, mvuke, gesi na moshi zinaachiliwa hewani kama uchafu na kwenda kutulia kwenye fenicha, makabati, nyavu za jiko na hata ukutani. Uchafu huu unaharibu samani za nyumba yako na pia hewa ya jikoni.
Inawezekana jiko la bibi yako lilikuwa kwa jinsi ambayo uingizaji wa hewa ulikuwa rahisi, lakini kwa nyumba za kisasa zenye jiko humo humo uingiaji wa hewa jikoni unaweza kuwa wa taabu. Kwa maana hiyo ni vyema kufunga feni ya stovu ili kuwezesha hewa safi ndani ya nyumba.  Kwa jinsi ambavyo nyumba zetu zinakuwa kubwa, jiko linakuwa ndio sehemu ya kuwezesha starehe ndani ya  nyumba kuanzia kuandaa chakula cha wageni jumapili na vyakula vingine vyote vya familia. Jifunze njia sahihi za kuwezesha uwepo wa hewa safi ndani ya jiko lako mara zote.

Hewa safi jikoni wakati wa kupika ni usafi, na ni afya kwa wakaaji na hufanya  mazingira na harufu safi ya nyumba kwa ujumla. Wakati wa kupika kwa gesi, hewa ukaaa inazalishwa hewani kama uchafu kutokana na kuungua kwa hiyo gesi ya kupikia. Hewa hii inaweza kusababisha matatizo kadhaa kama maumivu ya kichwa na hata kifo. Kwa hivyo leo hii kuna njia nyingi za uwekaji wa hewa safi ndani ya jiko na mojawapo ni hii ya kufunga feni ya stovu. Ukienda kwenye maduka ya vifaa vya umeme ukaulizia feni ya stovu huenda usieleweke kirahisi. Jina ambalo limezoeleka na ni maarufu kwa wauzaji wa vifaa hivyo ni “hood” na huwa zipo za ukubwa mbalimabali kuendana na ukubwa wa stovu yako. Kama nilivyosema awali feni hizi zipo ambazo uwekaji wake unatakiwa uwe ulikuwa kwenye mpango wa ujenzi wa jiko ambapo hizi ni zile zenye bomba maalumu la kutoa moshi na harufu nje ya nyumba, na zipo zile ambazo harufu mvuke na moshi hunyonywa ndani kwa ndani  na chujio maalumu zilizojengewa kwenye feni hiyo kwa hivyo hata kama mpango wa jiko haukuweka mfumo wa feni ya stovu bado utaweza kuifunga feni yako.

Feni ya stovu inafungwa kwa jinsi ambayo gesi, mvuke, moshi na mafuta vinavyotoka kwenye hiyo hewa ya moto wakati wa kupika zinadakwa na feni hiyo. Upana wa feni unavyozidi upana wa jiko ndivyo uchafu mwingi unavyodakwa. Moja ya nyanja muhimu sana kwenye kuwa na hewa safi ndani ya nyumba ni kwa kudhibiti kiasi cha unyevu. Kwa kuwa ni unyevu mwingi unaotokana na mapishi ni vyema kukumbuka kuwasha feni yako kila unapopika. Mfumo wa uingizaji hewa kwenye nyumba yako kwa jinsi ulivyowekwa  wakati wa ujenzi kwa maana ya madiridha na kadhalika unaweza kudhibiti kiasi fulani cha unyevu, lakini kama huna feni ya stovu utaanza kusikia kiwango cha hewa safi ndani ya nyumba kikishuka wakati wa kupika. Unyevu ukiruhusiwa kujijenga unazalisha vumbi, ukurutu wa mafuta, uozo na hata fangasi ambavyo huweza kusababisha maradhi ya ngozi, macho na hata matatizo kwenye mfumo wa kupumua wa binadamu.

Ingawa kufungua madirisha inaweza kusaidia kuondoa moshi na harufu kwa kiwango fulani, bado haitoshi kutoa uchafu wote uzalishwao hewani wakati wa kupika na kuleta hewa safi jikoni.
Ili kufanya kazi vyema mfumo wako wa uingizaji hewa jikoni inabidi uwe unasafishwa mara kwa mara. Chujio za feni zisafishwe kila baada ya miezi mitatu na mfumo mzima usafishwe mara moja kwa mwaka.

Karibia hood zote zina taa, kwa hivyo hii inasaidia pia kuongeza mwanga kwenye sufuria yako wakati wa kupika na kuwezesha kuona chakula kilicho chini ya feni. Fanya mazingira na hewa ya ndani ya jiko na nyumba yako kwa ujumla yawe safi kwa kuweka feni ya stovu leo!
Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Kwa maoni niandikie barua pepe viviobed@yahoo.co.uk au kwa simu 0755200023

madenti wanaelekea skuli



alhamisi njema wadau...

Wednesday, March 6, 2013

new and improved me!


ready kwenda kufua maguo na kuosha magari.. hivi can it be new and improved..kidogo hii lugha inanitatiza hapa kwa ajili nadhani new ni new na kama ni improved basi sio new..we unaonaje?