Saturday, May 30, 2015

KUANDIKA WOSIA SIO UCHURO KAMA WENGI MNAVYODHANI..

Wazri Mkuu Mizengo Pinda amewataka Watanzania wote wajenge tabia ya kuandika wosia ili kuondoa matatizo ya mirathi pindi mwenza au mme anapoaga dunia.

 Alitoa wito huo jana  wakati akizindua kampeni ya kuandika wosia
kwenye maadhimisho ya miaka 25 ya Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (Tawla) yaliyofanyika, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada ya kushuhudia uandishi wa wosia mbele ya wakili, Waziri Mkuu alisema uandishi wa wosia ni suluhisho la migogoro mingi inayosababishwa na wanandugu ambao wakati mwingine wala hawakushiriki kuchuma mali wanayogombea.

 “Kuandika wosia siyo uchuro kama ambavyo watu wengi wanadhani… ninatoa kwa Watanzania kuandika wosia mapema kwani inasaidia kuondoa matatizo ya mirathi baada ya mmoja wao kuondoka duniani,” alisema.

“Mtu anapaswa kutamka mali nilizonazo ni kadhaa na endapo nitakufa mali hii apewe fulani, na hii fulani na nyingine fulani. Hati hii inapaswa kutunzwa kwa mwanasheria, benki au kwa Kabidhi Wasii. Tusipolifanya hili, matatizo yataendelea kuwakumba wajane na watoto walioachwa na marehemu,” alisema. Aliipongeza Tawla kwa kuchukua jukumu la kuhamasisha umma kuhusu suala la uandishi wa wosia lakini pia akawataka wanachama wake  wajikite zaidi kwenye kutetea haki za makundi maalum kama walemavu wa ngozi, vikongwe na watu kutoka makabila madogodogo.

 “Haya makundi yana shida zao ambazo hazifanani na watu wengine. Nendeni vijijini, mkatoe elimu, jueni changamoto wanazokabiliana nazo, wasikilizeni shida zao na muone ni njia gani mnaweza kuwasaidia,” alisema.


CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment