Sunday, May 31, 2015

MTOTO WA MIEZI MITATU ANYAKULIWA NA FISI AKIWA MGONGONI KWA MAMA YAKE

Watu wawili wamefariki dunia mkoani Simiyu katika matukio tofauti akiwamo mtoto wa miezi mitatu aliyenyakuliwa na fisi akiwa mgogoni mwa mama  yake.
Kamanda wa Polisi  wa  mkoa wa Simiyu, Gemin Mushy  jana alisema  kuwa mtoto Ng’wanza Samwel, akiwa amebebwa na  mama  yake alinyakuliwa na fisi Mei 25, majira ya saa 1;30 jioni katika kijiji cha Ngugunu,Tarafa ya Kisesa wilayani Meatu.

Alisema katika kufuatilia tukio hilo, mabaki ya mtoto huyo yalipatikana mita 200 tu fisi kutoka eneo alilonyakuliwa huku kichwa, kifua, tumbo, mikono na miguu  ikiwa haipo.

Katika tukio jingine mpanda baiskeli aliyefahamika kwa jina la Magina Supa(20), mkazi wa Nyaumata mtaa wa Kisiwani wilayani Bariadi, aliuawa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali shingoni na bega la kushoto na mtu aliyekuwa amempakiza kama abiria wake.

Akifafanua, Kamanda  Mushy alisema kuwa tukio  hilo lilitokea Mei 26 majira saa 1;00 jioni katika mtaa wa Izunya, kata ya Somanda tarafa ya Ntuzu wilayani Bariadi kwa mtuhumiwa wa mauaji hayo anayedaiwa kuwa abiria wa mpanda baiskeli huyo aliyekuwa  anajishughulisha na biashara ya daladala ya baiskeli.

Kamanda huyo alisema kuwa mara  baada ya mauaji hayo, mtuhumiwa ambaye hajafahamika na anasakwa baada uhalifu huo alitoroka. Chanzo cha mauaji hayo  hakijafahamika.


NIPASHE

No comments:

Post a Comment