Tuesday, March 1, 2016

Namna ya kubadilisha muonekano wa nyumba na kuleta mvuto kwa gharama nafuu

Baada ya miaka kadhaa ya kuishi kwenye nyumba hiyo hiyo,  nyumba wengi wanatamani kubadilisha mionekano ya nyumba zao hizo. Na mara nyingi wazo linalowajia ni marekebisho ya jengo na kubadilisha fenicha. Hata hivyo hii inamaanisha gharama kubwa na kushirikisha wataalam wa kutekeleza jambo hilo.

Lakini je, kwanini mwenye nyumba asifikirie kufanya mabadiliko ya gharama nafuu kama vile badala ya kununua fenicha mpya akafanya maboresho kidogo ya zilizopo na zikaleta mvuto kabisa.

Makala zangu nia yake ni kukupa mawazo lukuki ambayo unaweka kutumia kuboresha maisha ya nyumbani kwako kwa gharama nafuu. Endapo mwenye nyumba utaamua kufanya utafiti kidogo na kufuata ushauri unaweza kufanikisha kazi yako kirahisi na kwa gharama nafuu sana. Kwani utakuwa umeshaelewa picha nzima ya unachotakiwa kufanya na kwa wewe kushirikiana na watendaji wachache utafanikisha lengo lako.

Matumizi tofauti ya rangi, karatasi za ukutani, vitambaa na malighafi nyingine zilizotengenezea fenicha zako vinaweza kubadilisha kabisa muonekano na kukupa wa kuvutia.
Zipo rangi za kung’aa kama polishi na zipo zisizong’aa za mati unazoweza kutumia kuboresha fenicha zako. Kwa mfano kupaka rangi upya kabati la luninga,  miguu ya kiti au meza kunabadilisha kabisa muonekano wake. Vile vile bila kusahau kubadilisha kitambaa kilichotengenezea viti au sofa endapo kuna umuhimu wa kufanya hivyo.

Dondoo nyingine ni kubadili vitu kidogodogo kama vile tai na fimbo za pazia. Ni ukweli kuwa vitu vya nymbani vinabadilika kila baada ya kipindi kifupi. Huenda tai zako za pazia za miaka mitano iliyopita ni tofauti kabisa na zilizopo kwenye mitindo sasa. Cha muhimu ni kuangalia hivi vitu vidogo visivyo vya gharama kubwa ambavyo ukivibadili vinapendezesha nyumba yako zaidi.

Eneo lingine ni la kwenye mito ya makochi. Kuwa na foronya mbalimbali na badilisha mara kwa mara. Vilevile kwa upande wa bakuli la taa, balbu siku zote ni hiyohiyo kinachobadilika ni jumba lake. Endapo utabadili jumba la taa kama vile taa ya jikoni au chumba cha chakula na kuweka ya kisasa zaidi bila shaka utakuwa umeboresha muoneakno kwa gharama nafuu kabisa.
Tukienda kwa upanda wan je ya nyumba huenda ukataka kuboresha kwa kupaka rangi upya na pia kuongeza taa za ulinzi. Unapopaka rangi zingatia kuboresha zaidi yale maeneo yaliyomeguka meguka. Kwa mfano nimeona watu wakitengenezea mikanda kuzunguka madirisha ambapo mwanzoni haikuwepo. Matokeo ya hii mikanda ni kufanya nyumba kuwa ya kisasa zaidi kwa nje na vilevile kuficha zile kona zilizokuwa zimemeguka.

Kwa upande wa bustani huenda mwanzoni miaka ya nyuma uliweka njia ambazo sasa huzihitaji tena kwa maana ya kwamba hazitumiki. Ni wakati wa kuziondoa na kufanya eneo lote liwe na ukoka. Pia kuna wakati vitofali vinakuwa vimemeguka aidha kwa sababu ya maji ya chumvi au ni kwamba tu vimekaa muda mrefu. Kutokana na hali yake unaweza kuvipaka rangi au laa kuviondoa na kuweka  sakafu ya malighafi nyingine bora zaidi iliyopo sokoni kwa kipindi hicho. Wakati huohuo usisahau kuboresha stendi na  vyungu vyako vya maua aidha kwa kuvipaka rangi (kazi ambayo unaweza kufanya mwenyewe) au kuotesha maua mazuri zaidi.

Hizi ni dondoo za maeneo kadhaa unayoweza kuangalia ili kuboresha muonekano wa nyumba yako uwe wa kisasa zaidi na mahali pazuri pa kuishi. Na kama wewe ni mpenzi wa vitu vizuri hii inaweza kuwa ni tabia yako kila baada ya miaka kadhaa.


Vivi anakuwezesha kupendezesha nyumba yako kwa gharama nafuu kabisa, atakushauri na aidha utatekeleza wewe mwenyewe au atakuunganisha na watendaji wa maeneo hayo. Kwa maelezo zaidi simu 0755200023

No comments:

Post a Comment