Monday, March 21, 2016

Zingatia haya unapojiuliza uchague kitambaa cha sofa chenye michoro au cha rangi moja.

 
Kuna vingi vya kuchagua pale ambapo unaamua  kupamba nyumba yako kwa jinsi unayotaka wewe.  Aina na mitindo mbalimbali ya fenicha, pazia na mazulia zipo sokoni za kumfaa kila mmoja na vivyo hivyo kwa vitambaa vya sofa.

Baada ya kusema hayo, kutokana na kuwa na machaguo mengi inaweza kukuwia vigumu kuchagua kitambaa sahihi cha sofa kwa ajili ya
nyumba yako kutokana na wigo mpana wa rangi na michoro ambayo ni pamoja na maua. Kuamua kama uchague kitambaa kisicho na michoro au chenye michoro ni jambo linalotatiza wengi.  Dondoo zifuatazo zitakusaidia kufanya uamuzi sahihi:

·         Kitu cha kwanza ni kufikiria mazingira ya chumba ambacho unaenda kuweka sofa zako ili kuona kama zenye michoro au za rangi moja ndio zitafaa zaidi. Sofa zenye michoro zinapendeza kwenye chumba ambacho kina rangi moja.  Rangi moja tunayosema ni pamoja na ukutani na pazia. Si kwamba zinafanana ila ni kuwa rangi za vitu hivyo hazina michoro. Kwa kawaida chumba cha rangi moja huwa kinapooza, kwahivyo kwa kuweka sofa yenye michoro, bila shaka utakuwa umekichangamsha na vilevile kulifanya sofa kuwa kitovu cha chumba.


·         Wakati huohuo michoro mingi inaweza kutoa matokeo ya chumba kuonekana hakijatulia. Kwahivyo kama una pazia zenye michoro, zulia lenye michoro na pengine karatasi za ukutani zenye michoro nazo, kwenye chumba cha namna hii ni muhimu kuwa na sofa za rangi moja na hii itasababisha macho kuelekea kwenye vitu vyenye michoro badala ya kwenye sofa. Michoro kila mahali inaweza kuharibu muonekano wa chumba na kumpa aliyepo hisia za uchovu. Huenda ulishawahi kuingia kwenye nyumba fulani na kutokana na rangi na michoro iliyopo ukajisikia vibaya/kuchefukwa na uchovu hata ukamuomba mgeni wako mkae nje kutokana na hali hiyo ya ndani. Kama ilishawahi kukutokea basi utakuwa unaelewa ninachosema.

·         Inawezekana ukawa na vitu vingine vyenye michoro na hapohapo ukapenda kuwa na sofa zenye michoro. Inawezekana kabisa kuchanganya michoro, kwa mfano unaweza kuwa na pazia za michoro ya nyeusi na nyeupe na ukalandanisha michoro hii kwa kuwa na sofa za michoro ya kijivu na nyeupe.

·         Dondoo ya mwisho ni kwamba michoro mara zote inatakiwa iendane na ukubwa wa kitu michoro hiyo iliyopo. Sofa kubwa zinapendeza na michoro mikubwa, wakati sofa ndogo zikipendeza na michoro midogo.

Ninaamini kwamba dondoo hizi zitakusaidia unapochagua kuwa na kitambaa cha sofa cha rangi moja au chenye michoro.


Makala hii imeandaliwa na Vivi Obed ili kukuwezesha kupendezesha nyumba yako. Simu 0755 200023

No comments:

Post a Comment