Thursday, July 3, 2014

my article for newspaper: kutandika kitanda

Jinsi ya kutandika kitanda ili kionekane nadhifu na maridadi

Linaweza kuonekana ni jambo rahisi ila kufahamu mbinu za kutandika kitanda kionekane nadhifu na maridadi ni faida ya kila mmoja iwe ni mtu wa umri mdogo au wa makamo na awe ni mwanaume au mwanamke. Kuwa na kitanda kilichotandikwa vyema sio tu kinaonekana nadhifu, bali pia unajisikia vizuri wakati ukifunua shuka kwa ajili ya kulala usiku. Kitanda nadhifu kinaleta burudiko la moyo vilevile, kwa ajili kinaleta hisia ya utulivu na muonekano wa kuwa na mapangilio chumbani. Kitanda kilichotandikwa nadhifu pia, ni nadra kuanza kuhangaika kupanga shuka wakati wa kulala na hii inamaanisha amani zaidi na muda mchache wa kupambana na shuka na blanketi.

Awali ya yote ondoa malazi yote ( shuka na blanketi au komfota) pamoja na mito kitandani. Chukua shuka safi ambazo zinafiti ukubwa wa kitanda chako. Kama shuka zako ni zile za seti ya shuka moja ya kufitisha (hii ni ile yenye mipira kwenye kona zake) na ya pili ni flati (haina mipira), basi chukua hii ya mipira na ifitishe kwenye kona nne za godoro. Shuka hizi za kufitisha zinarahisisha sana utandikaji wa kitanda hasa kama saizi ya shuka na godoro ni sawasawa. Huna haja ya kunyoosha kusawazisha mikunjo kwani huwa inajisawazisha yenyewe ukishavalisha kwenye kona za godoro. Kama ni saizi sawa na godoro itafiti vizuri kabisa.

Baada ya hapo juu ya shuka ya kwanza tandaza ya pili ambayo ni ile flati kwa jinsi ambayo upande wenye pindo kubwa unakuwa kichwani na ule wa pindo dogo unakua miguuni. Hakikisha shuka hii inaning’inia ukubwa sawa kwenye pande zote za kitanda ikifuatiwa na kuichomekea kwenye godoro sehemu za miguuni wakati maeneo la kichawani na pembeni yakiachwa bila kuchomekewa.

Tandaza blanketi juu ya shuka ya flati ukilinyoosha vizuri kwa kadri unavyosogea. Ruhusu urefu kiasi wa blanketi kwa ajili ya kuchomekea miguuni. Kunja blanketi eneo la kichwani ukiwa umelishikisha pamoja na lile shuka la flati urefu wa saizi ya upana wa mto mkubwa wa kitandani. Baada ya kukunja chomekea kwa pamoja blanketi na shuka kwenye pande mbili ndefu za kitanda.Kama kitanda kinatumika kila siku utandikaji huu ni njia rahisi kwa mlalaji kufunua upande anaopandia kitandani, shuka ya juu iliyokunjiwa na blanketi na kuingia kitandani kulala. Ila kama kitanda husika hakitumiki mara kwa mara, kwa mfano kama ni kitanda cha chumba cha mgeni unaweza kufunika  kwa kuchomekea kote kote na juu yake kuweka kava la kuzuia vumbi hadi mgeni atakapotembelea.

Sasa basi endapo kitanda tunachotandika ni kwa ajili ya matumizi ya kila siku njia ya kukunja shuka na blanketi ni utandikaji utakaofaa zaidi. Eneo la kichwani mahali ambapo pamekunjiwa blanketi, lile shuka la kufitisha litakuwa linaonekana kwa hivyo chukua mito na weka juu yake.  Huenda unahitaji mito miwili tu kwa ajili ya kulalia, ila unaweza kuongeza mito kadhaa midogo midogo kama mapambo kukipa kitanda mvuto.Unaweza kuweka mito mitano hadi sita kuendana na ukubwa wa kitanda chako. Kanuni ya kuweka mito kitandani ni kuwa lile eneo la kichwani lisibaki na uwazi wa ukubwa wa mto. Kwa maana ya kwamba kama kuna uwazi wa kutosha mto uliobakia basi ongeza mto. Kwa mmoja namna hii ya utandikaji inaweza kuwa mwisho na akajiridhisha kitanda kimekamilika na kina mvuto, ila kwa mwingine anaweza kupenda kuongezea komfota.

Kwa hivyo kama wewe ni mmoja wa wanaopenda kutandika komfota kitandani basi litandaze juu ya blanketi huku ukilinyoosha vizuri kuondoa mikunjo yote inayoweza kutokeza. Huna haja ya kuchomekea komfota na huwa lenyewe ni njia mojawapo ya kupamba kitanda – liache tu likining’inia urefu unaolingana kwenye pande zote za kitanda na hapo kitanda kinakuwa kimemalizika kutandikwa.

Kuna baadhi yetu ambao hatuoni umuhimu wa shuka ya pili. Uzoefu wa kutumia shuka moja (ikiwa ni ile ya kufitisha ni bora zaidi) na komfota pekee inafanya utandikaji wa kila siku wa kitanda uwe rahisi, ila kiukweli ni kuwa hii shuka ya pili inaulinda mwili wa mlalaji usikwaruzwe na ugumu wa blanketi au komfota na pia husaidia kuweka blanketi au komfota safi na bila kusahau kuongezea mwili joto. Ni rahisi zaidi kufua shuka mara kwa mara kuliko blanketi au komfota, na pia makava haya ya kitanda yanadumu zaidi yakifuliwa mara chache.

Kutumia shuka ya flati ambayo ina ukubwa wa kutosha inafanya kitanda kiwe rahisi kulalia na kutandika tena asubuhi ya pili. Tumia shuka na blanketi zenye ukubwa wa kutosha kiasi kwamba havitachomoka chomoka ukiwa umelala. Kama una blanketi dogo ni bora kulikunja na kuliweka chini ya mito na ukawa unalikunjua na kujifunika wakati wa kulala tu kwa maana ya kwamba wakati wa kutandika unalikunja kwani ukiamua kuchomekea blanketi dogo litakusumbua kwa kuchomoka kila mara.

Zaidi ya kutandika safisha chumba chako cha kulala ili kuonyesha zile juhudi zako za kutandika. Kitanda pekee kikiwa maridadi ilhali sehemu ya chumba iliyobaki ni mrundikano unadhifu hauwezi kuonekana. Kutandika kitanda kunakuwezesha kuanza siku yako vizuri na kunakufanya ujiikie kuwa na mpandilio zaidi mapema mwa siku yako.


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

Tuesday, July 1, 2014

usiruhusu magugu kushamiri yaharibu bustani yako...

ukiona kote kijani kwa undani magugu yamejificha

muhimu kuyang'olea kwani yakishamiri yataharibu bustani

unaona kama hiyo ndago hapo kati ilivyotulia

magugu yote kwenye ndoo kwa ajili ya kutupiliwa mbali

gugu majani yake ni mapana zaidi

majani bila gugu

Friday, June 27, 2014

fabulous friday

ha ha haaa...tunamalizia mchakamchaka wa mitihani...



Thursday, June 19, 2014

my article for newspaper: Jinsi ya uchaguzi , uhifadhi na utunzaji wa visu vya jikoni

Jinsi ya kuchagua, kuhifadhi na kutunza visu vyako vya jikoni

Visu ni vifaa muhimu zaidi jikoni. Kwanza tuangalie muonekano wa jumla wa kisu kinachofaa jikoni ambacho tunaweza kukiita ni kisu cha mpishi. Kisu hiki ni kile ambacho walau unakitumia kwa kila shughuli unayofanya hapo jikoni. Ni muhimu sana kufahamu urefu na upana endapo utakuwa unataka kununa kisu hiki. Kisu cha mpishi kina urefu wa kati ya inchi 8 hadi 12 na upana wa kati ya inchi 1 ½ hadi 2.

Kisu cha mpishi kikiwa na urefu huu wa inchi 8 ni mwake kwa matumizi mengi tofauti tofauti kwani kikiwa kirefu sana huenda usiweze kutumia ncha yake vizuri. Mkono wa kisu cha mpishi unaweza kuwa umetengenezwa kwa vifaa na miundo mbalimbali. Vifaa na miundo ya aina fulani ni rahisi kushikika mkononi kuliko aina nyingine. Mikono mingine ya visu hivi inaweza kuwa inateleza wakati wa kukata chakula na hivyo kuleta usumbufu kwako. Sasa haya yote yakiwa yameshasemwa, basi ni juu yako kuchagua kisu cha mpishi ambacho utajisikia huru, burudani na rahisi kwako wewe mpishi kukitumia. Unajua jinsi panavyokuwa na visu kadhaa jikoni lakini unakuwa na kimoja ambacho unakipenda zaidi kwa maana ya kwamba unaona kinakufaa zaidi kwa matumizi.

Unapaswa kuwa na kati ya visu 3-5 jikoni kwako. Aina hizi tofauti tofauti zinapatikana kwenye seti ya visu. Hakikisha unachunguza kwa makini aina ya visu iliyopo kwenye seti endapo utakuwa unanunua kwa seti. Mara nyingi utakuta kule kwenye seti kuna aina ya kisu ambacho utakitumia mara chache sana ua hata labda hutakitumia kabisa. Kama ni hivyo basi ni bora kunua kimoja kimoja badala ya seti. Hata hivyo, faida mojawapo ya kununua visu kwa seti ni kuwa unapata na kihifadhio chake ambacho unaweza kutunzia visu vyako.

Kama unafanya kazi nyingi na nyama yenye mifupa au samaki wazima wazima basi fikiria kuwa na kisu kile ambacho sehemu ya kukatia ni kama msumeno kwa ajili ya kupenya kwenye mifupa na kingine kilicho laini kwa ajili ya kukatia minofu iliyotenganishwa toka kwenye mifupa.
Usalama na usahihi wa kuhifadhi visu vyako ni jambo la muhimu mno unalopaswa kuzingatia. Visu vikali kamwe visihifadhiwe vimesambaa  kwenye droo la kabati la jikoni vikiwa vinagongana na vyombo vingine kwa sababu kuu mbili:

Kwanza ni hatari kuingiza mkono wako kwenye droo kuchukua kisu kwani kinaweza kukukata, na pili msuguano wa visu na vyombo vingine kwenye droo vinaweza kusababisha visu kuwa butu.
Kitufe cha kuhifadhia visu au kipande cha sumaku kilichowekwa ukutani ni njia sahihi zaidi za kuhifadhi visu vyako vya jikoni. Kama hauna eneo la kaunta kwa ajili ya kuwekea kitufe cha visu au labda hauna ukuta kwa ajili ya kuwekea hiki kipande cha sumaku basi kwenye droo pekee ndio mahali unapoweza kuhifadhi visu vyako. Yaani droo liwe ni chaguo la mwisho baada ya kitufe na sumaku kushindikana. Kwa hali hii inabidi uwe na zuio la visu ukiwa umevalisha kwenye kila kisu au droo la mbao liliogawanywa visehemu vidogo dogo  ndani kwa ajili ya kila kisu kuhifadhiwa kwenye kisehemu chake.

Kwa hivyo tumeona kwamba utunzaji wa visu unaenda sambamba na uhifadhi sahihi. Visu vinatakiwa kusafishwa kwa mikono na kufutwa kabla ya kuhifadhiwa. Kwa vyovyote vile kisu chochote kitahitajika kunolewa baada ya kipindi fulani. Unaweza kufanya shughuli hii kwa kumshirikisha mtaalam. Baadhi ya wataalam huwa wanapita mitaani na baiskeli wakiwa wamebeba mashine zao za kunolea huku wakitangaza wananoa visu.Vinginevyo unaweza kuamua kufanya kazi ya kunoa visu vyako mwenyewe nyumbani. Kama utaamua kufanya mwenyewe basi kifaa kingine cha kufikiria ni hicho cha kunoa visu vyako. Wengine huwa hata na jiwe la kunokea visu ambalo linatumia ama mafuta au maji kama kilainishi wakati wa kunoa. Lakini aina nyingine za vinoleo vinavyouzwa madukani havihitaji vilainishi na vinoleo hivi ni rahisi zaidi kutumia kuliko jiwe.

Natumai umejifunza jambo kuhusu ununuzi, matumizi na uhifadhi wa visu vyako vya jikoni. Tukutane tena wiki ijayo.


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

Thursday, June 12, 2014

my article for newspaper: jinsi ya kutunza na kusafisha godoro

Kila mmoja anapenda usingizi wake, na tunategemea godoro kutupatia mahali safi na nyororo pa kulala. Ni nini kinafanyika pale godoro lako linapokuwa chafu? Ni kwa namna gani unazuia mavumbi na wadudu kuweka makao kwenye godoro lako na kukubughudhi na usingizi wako? Ni ratiba gani ya matunzo na usafi godoro inahitaji?

Kama inavyofahamika kwamba binadamu anatumia theluthi moja ya maisha yake akiwa amelaza mwili mlalo na tena wengi wetu juu ya godoro, basi ungetegemea kwamba kusafisha godoro ingekuwa ni orodha namba moja kati ya vitu vinavyopewa kipaumbele kwenye orodha ya kusafisha, lakini utashangaa wala siyo. Ni mara chache tunafikiria juu ya kusafisha godoro.

Tatizo ni kuwa, unaondoa shuka zote, unabakiwa na godoro ambalo limeshionewa foronya ambayo huwezi kuivua sio – kama vile kuna zipu unayoweza tu ukafungua kirahisi ukavua foronya na kwenda kuifua – hapana, ukweli wa masikitiko ni kuwa – wakati tunatoa shuka zote, tunakuwa kama tumeziba macho kwa uchafu mwingine wowote uliopo juu ya godoro lenyewe.

Godoro linaweza kuhifadhi uchafu wa vimiminika, madoa, vumbi na mbaya zaidi hata wadudu kama chawa na kunguni  – kwahivyo kuwa na godoro safi ni muhimu kwa sababu kadhaa zaidi ya kufahamu kuwa mwili ambao umevalishwa nusu unalilalia kukiwa na shuka pekee iliyotenganisha mwili huo na godoro.

Kusafisha godoro kwa mashine ya kunyonya vumbi ni muhimu kwa ajili ya kuondoa vumbi, seli za ngozi zilizokufa na uchafu mwingine unaotua kwenye godoro lako na ambao unajilimbikiza kadri muda unavyokwenda. Fikiria kusafisha godoro kwa namna hii kwa walau mara mbili kwa mwaka. Sasa kumbuka kuwa kwa vile mashine hii ya kusafishia kwa upepo ina vichwa kadhaa, utapaswa kutumia kile kichwa cha kusafishia viti na sio kile cha kawaida cha kusafishia zulia kwa huwa kinazoa kila aina ya uchafu kwa hivyo usingependa kukipitisha hicho kwenye godoro lako. Wakati wa kusafisha godoro ni vyema kusafisha pia mvunguni.

Vile vile kila baada ya miezi sita iwe ni wakati wa kugeuza godoro lako juu kwenda chini na miguuni kwenda kichwani. Fikiria kwa mfano mwenzi wako na wewe mna zaidi ya kilo mia, kwa hivyo kwa kugeuza na kuzungusha godoro inamaanisha kuwa mnaongeza uhai wake na kuleta uwiano wa uchakavu . Kulingana na ukubwa wa godoro, hii kwa kirahisi kabisa inaweza kuwa kazi ya watu wawili.

Madoa kama ya mapatapishi, jasho, damu, mkojo na vimiminika vingine toka mwilini huwa kuna wakati vinatua kwenye godoro. Kama ilivyo ada kwa doa lolote, ni vyema kulichangamkia liondoke mapema kabla halijakomaa zaidi. Madoa ya vimiminika yanatakiwa kwanza yafutwe kwa maji baridi, na kitambaa chenye unyevu. Na baadaye unyevu wa ziada unakaushwa na kitambaa kikavu. Kumbuka kufuta kwa kukandamiza badala ya kuzungusha mduara ili kuondoa uwezekano wa kuchana kitambaa cha godoro. Madoa haya ya viminika toka mwilini asili yake ni protini kwa hivyo tumia maji ya baridi pekee wakati wa kuondoa madoa haya.

Funika godoro lako kwa foronya ya kuvulika ili kulinda maeneo ya godoro. Chagua foronya ambayo inaosheka kirahisi ambayo ni rahisi kuvalisha na kuvua kwenye godoro lako. Foronya nyingine zimebuniwa maalum kwa kazi ya kuzuia kushika vumbi kwa hivyo kukupunguzia kazi ya kunyonya godoro vumbi mara kwa mara.

Kama maeneo ya godoro yamepatwa na tope au udongo ondoa kwa shampoo ya kusafishia sofa na mazulia. Safisha tu lile eneo lililochafuka kwa kutumia sponji. Suuza eneo hilo kwa sponji jingine la maji ya moto na kandamiza eneo hilo kwa kitambaa kikavu ili kunyonya unyevu. Unaweza kuruhusu eneo hilo kukauka kwa kuwasha feni au hata kutoa godoro nje kwenye jua kali. Usiruhusu maji kuzama sana ndani kwenye kiini cha godoro kwani maji na godoro sio marafiki.

Endapo godoro litakuwa makazi ya wadudu kama chawa na kunguni jambo hili si dogo eti wadudu hawa waondolewe tu na watu hapo nyumbani ambao sio wataalam wa kazi hii. Changamka mapema na mwite mtaalam. Watakusafishia na kupuliza dawa godoro lako chumba, na hata maeneo mengine ya makazi yako ambayo yatakuwa yamedhurika na wadudu hawa. Kama umefikiwa na wadudu hawa unataka waondoke na wataalam wanajua jinsi ya kufanya kazi yao.

Hongera kwa kuwa na dogoro safi ambalo litadumu muda mrefu!


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

Thursday, June 5, 2014

my article for newspaper: bustani za kwenye vyungu

Mwongozo wa bustani za maua za kwenye vyungu
Hata kama una eneo dogo kiasi gani lakini unapenda bustani za maua, unaweza ukatimiza tamanio lako hilo kwa kutengeneza bustani za maua za kwenye vyungu.
Au pengine labda una eneo la kutosha kuwa na bustani ya ardhini lakini bado kuna yale maeneo kama ukutani, ndani ya nyumba au kwenye varanda ambapo ungependa kuwa na maua, basi suluhisho ni bustani za kwenye vyungu.

Bustani hizi zinakuwezesha kutengeneza bustani maalum kwa ajili ya eneo lolote. Unaweza kuotesha humo maua yako ya upendeleo ambayo usingependa kuotesha kwenye eneo kubwa la bustani ya ardhini kwani labda yatamezwa na mimea mingine iliyopo kwenye bustani husika. Mtunza bustani wa bustani za kwenye vyungu kikomo chake ni ubunifu wake pekee, anasema landscaper Aisha Idd.

Kwenye makala hii bi Aisha atatufunza jinsi ya kuchagua vyombo vya kuoteshea, uwekaji wa mbolea, udongo na umwagiliaji wa bustani zako bila kusahau maua yanayofaa kuotesha kwenye vyungu na mengine mengi!
Baadhi ya vyombo vinavyoweza kutumika kwenye bustani za kwenye vyungu ni vyungu vidogo vya kuning’iniza na vile vikubwa vya kuweka chini pamoja na maboksi ya mbao.                                                                                                                                       

Aisha anatupa mwongozo wa namna ya kuchagua vyungu kwa ajili ya bustani yako hiyo. Anasema epuka vyungu vyenye midomo myembamba. Pia vyungu vya plastiki nyembamba sana vinaweza kuharibiwa na jua na vitafanya ua lililoko ndani kukaukiwa na maji mara kwa mara. Kama utachagua vyungu vya udongo fahamu kuwa udongo unapitisha maji hivyo kiasi cha mji kitakuwa kinapotea kupitia kuta za chungu. Vyungu vya seramiki na saruji ndio vizuri zaidi kwenye kuhifadhi maji ila vinatakiwa kuwa na matundu kadhaa.                                                                                                                                    

Maboksi ya mbao huenda yakaoza, mbao nyekundu na za aina ya cedar huwa haziozi na zinaweza kutumika bila tatizo. Maboksi ya mbao zilizowekwa dawa ya kuzuia kuoza au kuliwa na wadudu si mazuri kwani kemikali zlizopo kwenye dawa hizo huwa zinaweza kuunguza maua. Uzuri wa mabokisi ya mbao ya kuoteshea maua ni kuwa yanaweza kutengenezwa kwa umbo na ukubwa utakaofiti eneo linalohitajika kuwekwa.

Vyungu viwe na ukubwa wa wastani kwani vikiwa vidogo sana vitazuia mizizi ya mmea kutambaa vizuri na pia huwa vinakauka maji mapema sana. Ukubwa na idadi ya mimea inayooteshwa itatokana na ukubwa wa chungu kitakachotumika. Maua yenye mizizi inayoenda chini inahitaji vyungu virefu. Hakikisha kuwa vyungu vyako vinapitisha maji vizuri na tandika magazeti chini ili kuzuia udongo usiwe unakimbia chungu wakati wa kukimwagilia. Sasa utajiuliza hayo magazeti si yataloa? Ni kweli ila hata kama yakiloa yatatengeneza kizuizi chini kwani hama tujuavyo ni kuwa karatasi haiozi. Kwa upande wa vyungu vidogo vya kuning’iniza hakikisha ya kuwa hutundiki kwenye ukuta wenye jua la moja kwa moja kwani vitakuwa vinakaukiwa maji mara kwa mara.

Hakikisha kuwa chombo chako cha kuoteshea bustani za kwenye vyungu kinapitisha maji mapema lakini kinahifadhi unyevu wa kutosha kuweka mizizi katika hali ya maji. Mboji inafanya udongo mzuri sana wa kwenye vyungu. Ila ni muhimu kujua hitaji la mmea kwani usijezidisha udongo wenye mbolea kali, na pia mbolea nyingine kama ya kuku ina tindikali sana kwahivyo inahitaji maji kwa wingi pindi unapoiweka. Kadri utakavyokuwa unamwagilia mmea wako ndivyo utkavyokuwa unaweka mbolea kwani huwa maji yanaondoa baadhi ya vimeng’enyo. Pia kuna mbolea za dukani za maji maji ambazo waweza tumia kwa kupata maelezo ya kitaalam toka kwa wauzaji.

Umwagiliaji wa bustani yako ya kwenye vyungu ufanyike pale mmea unapohitaji maji kwa maana ya ikiwa dalili za hali ya kunyong’onyea zitaanza kujitokeza. Baadhi ya mimea inaweza kuvumilia na inahitaji ukame kiasi kwamba ukiimwagilia mara kwa mara unaisababishia kuwa na unyevu wakati wote kwa maana hiyo itakufa. Ielewe mimea uliyo nayo, anasema Aisha. Kuna mimea mingine ya kwenye vyungu kwa mfano, kama iko ndani ya nyumba inaweza kumwagiliwa vikombe viwili tu kwa juma zima. Kumwagilia kuwe ni hitaji na sio jambo la kila wakati na kanuni kuu ya kujua kuwa mmea unahitaji maji ni kujaribu udongo wake. Kama inchi moja au zaidi ya udongo ni mkavu basi mwagilia.

Kwenye mazingira ya uwazi, mimea ya kwenye vyungu inapoteza maji mapema. Wakati wa kiangazi bustani zilizowekwa kwenye mazingira haya huenda zikahitaji kumwagiliwa kila siku.   Sasa basi, ni muhimu kufahamu kuwa sio kila maua au mmea unafaa kuoteshwa kwenye vyungu. Mimea inayokubalika zaidi kwa bustani hizi ni ile yenye mizizi michache na mifupi. Pindi uendapo kwenye bustani za wauza maua zilizojaa maeneo mengi kando kando ya barabara kuu watakufahamisha.                             

Umaarufu wa bustani za kwenye vyungu umetisha.

Mimea kwenye vyungu inaonekana kila mahali, kutoka kwenye makazi ya watu hadi maofisini, mahotelini, kwenye ma mall na hata barabarani. Udongo mbaya au hakuna eneo la kuweka bustani sio kisingizio tena cha kutokuweza kufurahia kijiraha cha kuwa na bustani!

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Friday, May 30, 2014

my article for newspaper: jinsi ya kufanana na mazingira yako

Jinsi ya kufanana na mazingira ya nyumbani kwako

Kila mtu anachagua ni vipi anataka mazingira ya nyumbani kwake yawe. Ingawa tunaweza tusijali kuhusu uchaguzi huo lakini mazingira yetu ni dili kubwa kutuhusu. Una nafasi ya kutengeneza mazingira ambayo yatarahisisha maisha yako ama yatayafanya  yazidi kuwa magumu.

Kuna kanuni ya kwanza ya msingi kuwa katika kila kitu kilichopo kwenye eneo linalokuzunguka kina nguvu fulani iwe kitu hicho kina uhai ama hakina. Ni kama watu wa kale walivyoamini kuwa kila kitu kina uhai. Kanuni ya pili ni kuwa kila kitu kwenye mazingira yetu kinahusiana na kitu kingine. Inawezekana kwa mtizamo wa kiroho au wa kisayansi. Na kanuni ya tatu ni kuwa kila kitu kinabadilika kila wakati.

Sasa basi kama kila kitu kwenye mazingira yako kina uhai na kimeunganishwa na wewe basi mabadiliko yakitokea kwenye eneo lako nawe unaguswa. Mazingira yako yanakugusa nawe unayaakisi. Hii ni kama usemi kuwa kila kitu kwenye mazingira yako kinaongea na wewe. Je vitu vya mazingira yako vinasema yale ambayo unapenda kusikia, je vinakusaidia kupata kile unachotaka kupata katika maisha.

Fikiria jinsi unavyoingia nyumbani kwako na kukumbuka usemi kuwa unachokutana nacho mwanzo kinakugusa zaidi . Kama unaingilia varanda iliyojaa makorokoro kila mara unapoingia nyumbani kuna uwezekano mkubwa wa kuchoka hapo hapo nje hata kabla hujafika ndani. Vilevile kama unatembea kuelekea karibia na kizuizi unaanza kujifikiria kuwa inahitaji nguvu kupita pale. Pia kama unafungua mlango wa ofisi asubuhi na kukutana na meza iliyojaa nyaraka, unaweza kujisikia kama siku yako tayari imejaa na hakuna nafasi ya kuanza kitu kipya kwa siku hiyo.

Tembelea kila chumba nyumbani kwako. Je kuna kitu kinakuambia kuwa maisha ni mazuri na yamejaa fursa? Au una picha usiyoipenda, fenicha ambayo haijakaa sawa au rangi ya ukuta ambayo inakupa ukakasi kuitazama? Kila mara unapooana vitu kama hivi, unapotembelea chumba hiki unapata ujumbe hasi. Hata kama akili yako itazoea kuona hivyo lakini dhamira itakuwa inakereka.

Mkusanyiko wa picha unaweza kuwa chanzo cha ujumbe hasi. Hakikisha ni za kumbukumbu na hisia nzuri za watu hao kwako. Zinaweza kuwa ni picha nzuri sana kwa kuonekana kwa macho lakini kama mojawapo inakukumbusha tukio au wakati wa huzuni basi iondoe.  Weka zile zinazokufanya uwe na tabasamu. Watu mara nyingi wana picha kwenye kuta zao kwa sababu tu hawana kitu kingine cha kuweka hapo na sio kwamba ni kwa kuwa wanakipenda kilichopo. Sanaa ukutani inaweza kuwa nzuri sana ila kama ukiitazama haikubariki haina faida kwako. Badala yake inakupa ujumbe hasi na kukunyonya nguvu kila unapoiona. Ni vyema kuiondoa na kuacha nafasi kwa kitu ambacho kinakupa mtizamo chanya katika maisha.

Kuchukua hatua hii mbele zaidi, fikiria ni nini unakipenda kwenye maisha. Mfano mzuri ni mtu anayetaka kuwa na uhusiano. Mara nyingi picha atakazoweka nyumbani kwake na hasa chumba cha kulala ni za akiwa singo. Chumba hicho kitakuwa na taa moja tu ya kivuli na hata kimeza cha kando kimoja. Vyote hivi vinatoa ujumbe kuwa mhusika hana mtu. Badala ya vitu vilivyopo kwenye seti kwa mfano picha yenye watu wawili, na taa mbili za vivuli vinaleta alama za mahusiano.

Mazingira ya mahali unapoishi yanahusika katika kila eneo la maisha yako. Kama unahitaji akili tulivu hakikisha kuwa mazingira yako hayakupi kinyume na matakwa yako kwa kuwa na vitu ambavyo haviko mahali pake. Pia kama unataka kuwa mbunifu zaidi angalia kama je kuna nafasi zaidi ya kuweza kuwa hivyo? Kama unahitaji miundo mbinu safi je njia ya kuendea mlangoni kwako ni wazi, safi na inakaribisha?

Unavyotembea kwenye mazingira ya nyumbani kwako angalia kila kitu kwa jicho la ziada. Ondoa kila kitu ambacho huwezi ukasimama na kushuhudia kuwa unakipenda na ni kitu ungependa kuwa nacho. Unaweza usiwe na kiti kingine cha kuweka kwenye hiyo sehemu ulipotoa kile usichokipenda, lakini kama kinakuletea tukio la huzuni bado,  potelea mbali kitoe tu. Kinaziba kile unachokipenda na pia hicho usichokipenda kinakuletea hisia mbaya. Kwa kuamini utapata kingine unatengeneza uwezekano. Kuwa makini na hivyo vitu vinavyoongea na wewe furaha na kuvipa nafasi ya heshima nyumbani kwako.

Katika nyakati hizi za mihangaiko mingi, ni muhimu kuwa mazingira yako hayakuongezei vikwazo kwenye dunia yako. Hii inahusu hata taarifa za habari kwenye matukio ya mauaji, ajali na mengi ya kutisha. Fuatilia ni nini kiko kwenye vyumba vya watoto. Kama mazingira ya vyumba vyao yanaongea amani, watakua wakiwa wanajifunza amani.

Kwa kuwa makini na kila kitu kwenye mazingira yako unatengeneza makazi ambayo yanafanana na wewe kwa kukupa ujumbe chanya na zenye kukutia nguvu. Kuwa kitu kimoja na makazi yako unakuwa na mtizamo chanya zaidi katika maisha. Mtazamo chaya unagusa kila kitu kwenye maisha yako. Yasikilize mazingitra yako.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Thursday, May 22, 2014

my article for newspaper: jinsi ya kuhifadhi vyombo makabatini

Jinsi ya kupanga vyombo kwenye makabati ya jikoni

Je vyombo vyako vinataka kuporomoka wakati ukifungua makabati ya jikoni? Kama ndivyo basi ni wakati wa kupanga na kuhifadhi upya na makala hii ni sahihi kwako.  Njia bora zaidi ya kupangilia vyombo na vifaa kwenye makabati yako ya jikoni ni kufikiria ni kwa vipi unavitumia vyombo vyenyewe. Ni vyombo na vifaa vipi unajikuta ukivitumia kila siku, na ni vipi vinakaa tu kabatini. Tosa vile ambavyo unaweza kuendesha shughuli zako za hapo jikoni bila kuwa navyo na elekeza nguvu kwenye kufanya makabati yako yaonekane yanafanya kazi, masafi na yana mvuto. Mara utakapopanga ndani ya makabati yako basi utajisikia furaha tena kuingia jikoni.

Ili kuweza kufanikisha zoezi la kuhifadhi vyombo kwa unadhifu kwenye makabati yako ya jikoni kwanza kabisa ondoa kila kitu kwenye makabati. Ni rahisi kuanza mradi wowote wa kupanga upya kwa kuanza na eneo safi, na kwa makabati ya jikoni ni hivyo hivyo. Songa mbele na toa kila kitu kwenye makabati kuanzia sahani, glasi, vikombe, sufuria, vikaangio na kila kitu kingine chochote ulichohifadhi kwenye makabati yako hayo. Panga kila kitu juu ya kaunta zako za jiko au hata kama una meza ya jikoni ili kuweza kutathmini ni nini unacho na ni kipi unahitaji. Kuondoa vile usivyohitaji kutasaidia kuondoa mrundikano hivyo kukuwezesha kuhifadhi vyema vile unavyohitaji. Na kama utajigungua kuwa kuna chombo ama kifaa unakihitaji lakini huna basi hakikisha unakinunua kwanza kabla ya kuweka mpangilio wako. Kama ukisubiri itakuwa ngumu kupata eneo la kukihifadhi baadaye.

Fikiria kugawa vyombo vya zamani na vile usivyohitaji kwa wanaohitaji zaidi, au hata kupeleka kwenye mnada wa vyombo vilivyotumika endapo viko katika hali nzuri. Kufahamu kuwa vifaa vyako vya zamani vinaenda kwenye jiko lingine itakupa amani zaidi ya kuvitupa tu bila mpangilio.

Futa makabati yako ambayo hayana chombo chochote kuanzia juu hadi chini. Tumia sabuni nzuri za kusafishia pamoja na kitambaa cha kufutia na safisha kila mahali hadi kwenye milango yote ile ya mbao na hata kama ya kioo ipo. “Kama utataka kutumia kemikali za kusafishia,tumiavinega iliyochanganywa na maji kidogo,” anasema Bi Mwajuma Issa ambaye ni mmiliki wa kampuni ya kufanya usafi majumbani.  Kemikali hii ya asili ya kusafishia imefanikiwa sana kwenye makabati ya jikoni ila kama makabati yako yametengenezwa kwa mbao ambayo haijapakwa rangi basi hakikisha unatumia sabuni za kusafishia ambazo hazitaharibu mbao. Kwa namna hii unaweka makabati yako tayari kwa ajili ya mpangilio mpya wa vyomba na vifaa vingine vya hapo jikoni. Kusafisha makabati yako kwa mtindo huu kutaangamiza makazi ya wadudu na kufanya nyombo, vifaa na vyakula utakavyohifadhi humo kuwa freshi.

Nunua vihifadhio vya kukusaidia katika mpangilio wa jikoni kama vile vitrey vinavyotumika kuweka baadhi ya vyakula vikavu kama vitunguu na viungo , kitufe cha visu kwa ajili ya kuhifadhia visu vingi kwa wakati mmoja na pia kurahisiha matumizi na vitu vingine vidogodogo kama vya kuwekea vijiko kadhaa na uma ambazo zinatumika kila siku. Kwa kawaida vihifadhio hivi husimamishwa kwenye kaunta za jiko. Pia makontena kwa ajili ya kuhifadhia vyakula kama mchele, unga na sukari vitakusaidia kuweka mpangilio jikoni

Baada ya kabati kukauka unyevu wote sasa ni wakati wa kutandika karatasi za kwenye makabati ya vyombo kabla ya kupanga vyombo vyako. Sasa una makabati yako yakiwa masafi na yameshatandikwa, ni wakati wa kufikiri ni kwa namna gani unataka kuweka mpangilio wa vyombo unavyotaka kuhifadhi ndani. Tathmini hivyo vyombo na vifaa unavyotaka kuhifadhi. Weka kila chombo kwenye kundi lake kutokana na aina ya chombo. Wakati wa kupanga makabati ya jikoni inaleta mantiki kupanga vyombo vinavyoendana pamoja.

Hifadhi vyombo vya thamani na kuvunjika kwenye kabati za juu ya kaunta ambapo ni ngumu kwa watoto kufungua na kuvunja.
·         Hifadhi pamoja vyombo vya kuvunjika kama vile glasi za kunywea maji, glasi za juisi na glasi nyingine zozote za matumizi ya kila siku.
·         Hifadhi pamoja glasi za mvinyo na shampeni.
·         Hifadhi pamoja sahani zako za kuvunjika na mabakuli. Ila hapa ieleweke vizuri kuwa sio sawa kuweka sahani na mabakuli kwenye mstari mmoja kama njia ya kuhifadhi nafasi kwani inaweza kusababisha kuvunjikiana.
·         Tofautisha sahani na bakuli za matumizi ya kila siku na zile za matumizi ya msimu.
·         Kama makabati yako ya jikoni yana milango ya kioo fikiria ni vyombo vipi ungependa vionekane kwa nje kwani makabati haya ni kwa matumizi na umaridadi.

Hifadhi sufuria na vikaangio kwenye kabati za chini karibia na jiko. Kila mmoja ana jiko la tofauti, lakini kwa mara nyingi makabati ya chini (chini ya kaunta) ndio sahihi kwa sufuria na vikaangio. Vyombo hivi huwa ni vizito na mara nyingi kuokoa nafasi sufuria moja inaingizwa ndani ya nyingine kuendana na ukubwa kwa hivyo inaleta mantiki kuvihifadhi eneo ambalo haitakuwa na haja ya kuvitoa tokea juu. Zile sufuria na vikaangio unavotumia mara kwa mara viweke karibia na mlango ili kuchukua kirahisi na zile ambazo unatumia kwa nadra zihifadhi mwishoni  mwa makabati. Pia unaweza kuona ni rahisi kuhifadhi sufuria na vikaangio vya kutumika mara kwa mara kwenye raki yake inayoning’inizwa ukutani mbele ya makabati yako. Hii inasaidia kuning’iniza kila moja peke yake badala ya kubebana.

Panga vijiko, uma na visu vya ziada kwenye droo flati,ukiwa umegawanyisha kila kimoja kwenye mahali pake. Vile vinavyotumika mara kwa mara hifadhi kwenye kihifadhio cha vijiko na uma kilichowekwa juu ya kaunta na kitufe cha visu. Pia weka droo moja la flati kwa ajili ya kuhifadhi vitambaa na vitaulo vya kufutia vyombo.

Tafuta eneo kwa ajili ya kuhifadhia vifaa kama blenda na tosta ambapo vile ambavyo unatumia kila siku waweza hifadhi juu ya kaunta. Kama blenda ni ya juisi ambayo inatumika mara chache kwa juma basi hifadhi kwenye kabati

Hifadhi sabuni na vifaa vya kusafishia ndani ya kabati lililo chini ya sinki.

Sasa umemaliza kuhifadhi vyombo kwenye kabati zako za jikoni, zicheki mara kwa mara kuhakikisha kuwa bado vyombo na vifaa vyako vipo kwenye mpangilio uliochagua. Unaweza kuwa unaweka vidonge vya kuua wadudu kama mende mara moja kila baada ya miezi sita.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

Sunday, May 18, 2014

super sunday...

maisha ni haya haya wajameni...ha ha haaa...tuendako baada ya hapa hakuna uzoefu kwa hivyo enjoy hapa hapa kwa sana kadri uwezavyo.....




Tuesday, May 13, 2014

pilika mitaani nikakutana na showroom iliyonitumbuiza..

showroom ilinivutia nikapiga picha kwenye hii dressing table.
imetengenezwa kwa mdf ila miguu ni mkongo

ki kiti cha dressing table
TV cabinet

Sunday, May 11, 2014

happy mothers day from my son

wala sikuwa aware...kesho shule nikamwambia mtu wangu mdogo do your homework..nikashangaa ananitolea na kikadi cha mothers day...shule hizi...nami nasema happy mothers kwa wamama wote wasomaji wangu... 


Thursday, May 8, 2014

my article for newspaper: mpangilio wa chumba cha kulala cha wakuu wa familia

Huenda wewe na mwenza wako mnaishi maisha yenye kazi nyingi (busy) ambayo mara nyingi yanapingana na kuwa na muda mzuri wa kukaa pamoja. Hakika mnajua hisia zenu zinavyokuwa kwa ajili ya kukosa muda huo muhimu. Ndio maana ni vyema kuwa na chumba cha kulala ambacho mkiwa pamoja kama wanandoa itawezekana kufurahia ule muda mchache mnaokuwa pamoja. Kwa lengo la makala hii chumba cha wakuu wa familia ni kile cha  baba na mama wa familia – ni koloni lao hapo nyumbani kama wengine wanavyoweza kusema. Wazazi mkiwa ndio nguzo ya familia basi mnahitaji chumba cha kipekee. Mnaokaa kwenye chumba hiki ndio mnaolipa bili na kufanya kazi kwa bidii ili mfanikiwe katika hilo. Kwa nini chumba chenu kisiwe maalumu? Wakuu wa familia mnastahili chumba hiki!

Je wewe mkuu wa familia unakipenda chumba chako cha kulala? Chumba hiki kiwe kama mahali patakatifu kwa wanandoa au yeyote anayelala mule. Chumba kiheshimiwe kisiwe ni ofisi ya nyumbani. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni sehemu ya kupumzika hivyo vitu kama kompyuta havina nafasi kwenye chumba hiki. Ni nini cha kwanza unachokiona mara baada ya kufungua mlango wa chumba hiki, na ni nini unachokiona cha kwanza mara baada ya kufungua macho asubuhi. Chumba hiki kiwe ni sehemu huru pasipo na usumbufu kama wa kufua, ndoo za maji, kompyuta au midoli ya watoto. Chumba hiki sio stoo!                          

Midoli imekuwa ni tatizo kwenye chumba cha kulala hasa kwa wazazi wanaokimbia mchakamchaka wa maisha ya kila siku. Midoli inaishia chumba cha wazazi na hata kitandani.  Kuwa wazi  na kuweka mipaka juu ya chumba hiki na hata midoli ya watoto isijazane chumbani kwako na kitandani. Kwa ujumla watoto wawe na sehemu ya kucheza na kuweka midoli yao. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia ni cha watu wazima ndani ya familia.

Fenicha kuu kwenye chumba hiki ni kitanda. Kimsingi, kitanda kina lengo moja kuu: kufagilia usingizi wenye afya. Chumba cha kulala cha wakuu wa familia kinahitaji kitanda chenye kukidhi vigezo vya usingizi bora. Kama matangazo tuseme ya magodoro yanavyoonyesha ni kuwa tunatumia theluthi moja ya maisha yetu kulala. Sasa kwa nini godoro, malazi na fremu ya kitanda visiwe maalumu. Kuna njia nyingi ya kupata kitanda bora kwa bajeti yeyote. Kitanda chenye fremu ya chuma tuu kilichosogezwa karibia na ukuta hakikidhi vigezo. Kila kitanda kinahitaji bodi la kichwani (makala zijazo tutaongelea umuhimu wa bodi hili) ambayo yanapatikana kwa saizi na mitindo mbalimbali.

Kwa kuwa msisitizo wa chumba hiki ni kwa wanandoa,  kama kuna sehemu kubwa weka sofa au viti viwili vya kukalia badala ya kimoja. Mara zote fikiria vitu viwili viwili. Kama wewe ni mwanaume au mwanamke uliye singo lakini ndio mkuu wa familia weka picha ya peke yako kusisitiza utambulisho wako kuwa huna mtu. Kama mnaolala humo mko kwenye mahusiano basi mambo ni kwa seti kama vile taa za vivuli mbili, vimeza vya kando viwili na hata kama mishumaa basi miwili.  Kumbuka unatengeneza mandhari ya kupumzika na kuondoa msongo wa mawazo wa siku nzima. 

Chagua sanaa inayoelezea uhusiano wenu iwe ni picha ya ngalawa, ndege au hata maneno ya kimahaba. Sio sawa kuweka picha za marafiki, mababu na hata wanafamilia wengine kwenye chumba hiki. Tatizo ni kuwa chumba kinaanza kuonekana kinguvu kimezidiwa na vitu. Watu wote hawa wana haja gani chumbani kwako. Pambeni chumba cha kulala kwa picha zenu nyie wanandoa mnaolala humo.
Chumba hiki kamwe kisiwe na mrundikano, weka kero za maisha ya kila siku mbali na mahali hapa patakatifu. Kama kabati lako la nguo limefurika, punguza ubakize zile ambazo haswa unazivaa. Pia fikiria kupunguza kiasi cha fenicha ili kuwe na nafasi chumba kisionekane kusongamana. Sakafu ionekane peupe isijazane vitu.  

Zingatia kile unachokiona kwanza mara baada ya kuingia chumba chako cha kulala. Kanuni inasema kuwa mlango usiwe usawa mmoja na kitanda, kwa maana ya kuwa ukiwa umelala kitandani uuone mkango lakini ukifungua mlango macho yasione kitanda moja kwa moja. Mlango ukiwa namna hii unawapa walalaji kujiamini zaidi kuwa wanamiliki chumba na usingizi unakuwa mwororo.
Vifaa vya umeme leo hii ni changamoto kwenye chumba cha kulala. Kompyuta, luninga na vifaa vingine vya umeme vinatuzunguka na kutunyonya nguvu kwa  kuleta nguvu ya uvutano mithili ya sumaku ambayo baadaye inaleta msongo wa mawazo. Ili kupumzisha mwili na kuuweka katika afya njema basi ni vyema kuwa mbali na vifaa vya umeme katika chumba cha kulala. Kama hamna jinsi kuwa ni lazima vifaa hivi viwepo chumbani basi sio tu vizime na kuacha vijitaa vinawaka bali chomoa kabisa kwenye umeme wakati wa kulala.

Kumbuka kuwa kila kitu kwenye nyumba tunazoishi kinatupa ujumbe. Chumba chako cha kulala wewe mkuu wa familia kinakupa ujumbe gani? Je kinakukumbusha majukumu yote unayohitajika kukamilisha au kinakupa hisia za utulivu na kukukaribisha kupumzika? Je kinakushawishi kuwasha luninga au kinakuleta kwenye faragha? Je kinaongeza msongo wa mawazo kwenye maisha yako? Au kinakupa pumziko la nafsi hata kama uko singo? Kama ndio basi umeweka mpangilio wa chumba cha kulala ambacho ni kama mahali patakatifu.

Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

nukuu ya leo: mapenzi & maudhi

"mapenzi yakiwa na maudhi ndio yanaota mizizi"

Wednesday, May 7, 2014

nukuu: kasheshe homa ya dengue...

“Kwa ufupi, mbu sasa ni hatari kuliko ilivyokuwa awali kwa sababu hawa wanaoambukiza homa ya dengue huuma wakati wa mchana, tofauti na wale wanaoambukiza malaria ambao huuma usiku na watu walikwishajua kujikinga kwa chandarua au dawa,