wakati wa sikukuu tunachapa lapa kama hivi...usisahau chimbuko lako mdau...watu wangu wadogo washasepa zao xmas hiyoooooo yaja...
Sunday, December 21, 2014
Saturday, December 20, 2014
Thursday, December 11, 2014
my article for newspaper: kuhifadhi taulo na ugeni
Jinsi
unavyoweza kuhifadhi taulo za bafuni kwa ajili ya wageni watakaokutembelea
msimu huu wa sikukuu.
Moja ya faida za kipindi cha sikukuu ni fursa ya kufungua nyumba yako kwa wageni
ambao hamjakaa pamoja mwaka mzima. Kama utakuwa
na wageni nyumbani msimu huu wa sikukuu, makala hii inakuhusu. Mahoteli yanafanya
wageni wao wajisikie spesho kwa ajili wanafahamu jinsi ya kuwafanya
wajisikie nyumbani kwa kuwapatia
mahitaji muhimu. Wewe pia unaweza wafanya wageni wako wajisikie kama wameshukia
kwenye hoteli ya kitalii wanapokuwa nyumbani kwako, kwa ajili tu ya buduriko
wanalopata wanapokuwa kwenye chumba au vyumba vyao vya wageni hapo kwako.
Ni bafu
chache zenye sehemu ya kutosha kwa ajili ya kuhifadhi taulo za wenyeji na
wageni kwa wakati mmoja, na huenda unafikiria ni jinsi gani utahifadhi taulo za
wageni wako watakapokutembelea. Lakini usijali kwani hata kama bafu lako ni
dogo namna gani njia mojawapo kati ya hizi itakufaa kutundika ama kuhifadhi
taulo za wageni wako.
Kuweka fimbo za kutundika taulo kwenye ukuta wa bafu
ama nyuma ya mlango (uwe wa mbao kwa uimara) ni njia rahisi zaidi ya kuhifadhi taulo
za bafuni. Fimbo hizi hazichukui nafasi kubwa na wala hazina marembo kwahivyo ni
suluhisho tosha kuhifadhi taulo kavu na hata zile zenye unyevu. Fimbo za taulo zinaruhusu
taulo kukauka kwa usafi zikiwa zimetundikwa kwa kukunjwa nusu. Fimbo za bafuni za
kuwekea taulo zinasaidia mambo makubwa mawili: kwanza, zinaweka taulo kavu na safi
kwa jinsi ambayo ni rahisi kuchukua na kutumia; pili, zinatandazwa taulo zenye unyevu
na kuzifanya kukauka kirahisi, hivyo kuzuia kuota kwa ukungu.
Licha ya kufungwa bafuni fimbo za taulo zinaweza kufungwa
pia jikoni kwa ajili ya kuwekea taulo za mkononi.
Muonekano wa fimbo za taulo ni kawaida sana. Ni
fimbo iliyosimikwa ukutani ama nyuma ya mlango kwa kutumia mashine ya kutobolea
ukuta na taulo huwekwa hapo, hutolewa kutumika na hurudishwa tena hapo baada ya
kutumika kwa ajili ya kukauka. Ni muhimu fimbo hizi zimewekwa imara kwakuwa kama
tujuavyo taulo zikiwa mbichi zinakuwa nzito na pia mara nyingine fimbo hizi hutumika
na watoto kwa utundu wao wa kupenda kubembea kila wapoona panafaa, na pia wazee
kujishikilia wakiwa bafuni. Kwahivyo siwezi kuacha kusisitiza kuwa fimbo za taulo
ni lazima zifungwe kwenye ukuta wa tofali ama mlango wa mbao kwa ajili ya uimara.
Fimbo za taulo sizo tu zinazoweza kuhifadhi taulo kwa
usafi na kuruhusu zile zenye unyevu kukauka. Kulabu (hook) za taulo, susu
(rack) za kusimama wima, bangili na ngazi za taulo nazo ni njia nyingine za kuhifadhi
taulo za bafuni. Bangili iliyotobolewa ukutani ambapo taulo kadhaa zinatundikwa
ni maarufu sana siku hizi na kwenye maduka ya fenicha wanaziita bangili za taulo.
Ngazi za taulo ni chuma kingine kinachoonekana kama ngazi
ndogo ambacho hutumika kuwekea taulo, ni
njia mojawapo ya kuhifadhi taulo za bafuni. Je una nafasi kwenye ukuta wa chumba
cha kulala cha wageni wako ambapo unaweza kuweka ngazi hii? Ni kiasi cha
kuishikilia na braketi juu ili isianguke na unaweza kuhifadhi kwa kutandaza taulo
za kuogea. Uzuri wa ngazi ya taulo ukilinganisha na fimbo ni kuwa wakati kwenye
fimbo unaweza kuweka taulo zisizozidi 2 kwenye ngazi ya taulo unaweza kuweka hadi
taulo 6.
Lakini kuna njia nyingine ambazo hazitakufanya uusumbue
ukuta wako ambazo zinaonekana za kimapambo zaidi kwa mfano kuweka susu ya kusimama
inayojitegemea kama ile ya kutundika makoti ofsini. Kama chumba cha kulala cha
wageni wako kina nafasi kidogo ya ziada basi simamisha susu ya koti kwa ajili ya
kutundikia taulo za bafuni. Susu inaweza kutundikwa taulo kadhaa kwa wakati mmoja.
Fikiria kuiweka sehemu ambayo inaingiza hewa au vinginevyo wageni wako wawe wanazigeuza
mara kadhaa kuwezesha kukauka. Kama susu hii inatundika taulo za wageni tofauti
tofauti basi wawe na taulo za rangi tofauti kwa kila mmoja. Hakuna anayependa kushirikiana
taulo.
Badala ya ile susu ya kusimama kuna hii nyingine inayofanana
na ya kuhifadhia chupa za mvinyo. Kama unataka wageni wako wajisikie kama wako
kwenye hoteli yenye hadhi ya nyota tano nenda kistaili zaidi kwa kuhifadhi taulo
zao safi zilizobiringishwa vizuri kwenye susu ya taulo. Susu za taulo zina muonekano
wa kuvutia kwahivyo kwa upande mwingine ni kama pambo. Taulo safi zinabakia zimebiringishwa
vizuri ndani ya susu hadi wakati wa kutumiwa, na hii inachukua nafasi kidogo kuliko
ile ya kusimama. Kuhifadhi taulo kwa kutumia susu ya taulo inakubidi uwe ni mtu
wa kutumia taulo mara moja tu na kulifua.
Kama ulijisikia kwamba bafu lako ni dogo kiasi kwamba
huna mahali pa kuhifadhi taulo za wageni wako msimu huu wa sikukuu hatimaye leo
umefahamu njia kadhaa za kuweza kuhifadhi na kutunza taulo wakati huo huo ukiwa
unazitumia. Wekeza katika njia mojawapo kati ya hizi ilikurahisisha maisha bafuni
sikuzote na hata msimu wa wageni.
Wednesday, December 10, 2014
ideas za makabati ya bafuni
Kila mmoja wetu ana ladha na mahitaji mbalimbali tofauti na mwingine. Wakati baadhi yetu tukiamini kuwa muonekano wa sebule ndio kipaumbele namba moja kwenye makazi yetu, wengine wanajali zaidi ni kwa namna gani mabafu yao yanaonekana, kwahivyo makabati ya bafuni kwa watu hawa ni kitu muhimu zaidi kwao kwa uzuri na kwa matumizi ya bafu.
Wenye nyumba wengi wanaona uhaba wa eneo la kuhifadhi vitu bafuni kama vile shampoo na vipodozi. Sasa basi yawezekana ulikumbuka hivi wakati wa ujenzi na hivyo kuwa na mababati yaliyojengewa humo humo. Vinginevyo yapo hata ya kusimama peke yake, kama makabati ya bafuni ni jambo muhimu kwako bado hujachelewa, pata mionekano ya makabati haya ambapo staili mojawapo yaweza kukuvutia.
Friday, December 5, 2014
....my babies....
ulishahudhuria msiba ambapo marehemu ana miaka 80 lakini ukashangaa jinsi wanae wanavyomwaga chozi...kumbuka usemi wa kiswahili kuwa mtoto kwa mama hakui...lol
Thursday, December 4, 2014
my article for newspaper: ubora wa tile za bafuni
Umuhimu wa kujali
ubora wakati wa kununua marumaru za bafuni
Bila
shaka kila mmoja anataka apate bidhaa au huduma kwa thamani ya hela aliyotoa
wakati wa ujenzi wa nyumba yake, lakini chaguo la marumaru za bafuni inahitaji
kuwa makini zaidi ya hilo. Katika makala hii nitakuwa na Mhandisi David ambaye
atatujuza umuhimu wa kuzingatia ubora zaidi ya gharama wakati wa kununua
marumaru za bafuni.
Unaweza
kuwa umepata marumaru za bei nafuu, lakini zisizokuwa na kiwango. Marumaru za
aina hii zitakugharimu kwa kiasi kikubwa muda wote utakaokuwa unaishi kwenye
nyumba yako hiyo.
Linapokuja
swala la marumaru za bafuni, malighafi, rangi, uimara, mtelezo, na usimikaji ni
mambo muhimu zaidi ya kuzingatia, anasema David. Hakikisha kuwa unapata ushauri
kwa fundi mwenye uwezo kabla ya kufikia kufanya uamuzi.
Marumaru
za bafuni zipo za kuanzia maumbo madogo zenye nyongeza ya border za aina na michoro mbalimbali. Wajenzi wanatafuta marumaru
za maumbo tofauti tofauti kutoka umbo la
pembe nne lililozoeleka hadi malighafi nyingine kama mawe ya asili na vioo. Wanapenda
pia mabafu yao yawe na muonekano wa kazi
za sanaa zaidi, anasema David. Ila marumaru za bafuni zinafanya kazi kubwa,
zinatakiwa kufanya mvuke usisambae vyumba vingine na kulinda kuta zisiharibiwe
na ukungu na hali ya umajimaji. Zinatakiwa zizibwe vyema na grout maeneo ya miungio na ziwe na
usalama kutembea juu yake zinapowkuwa zimeloa, anasema mhandishi.
Pamoja
na mawe ya asili, marumaru bado zitabaki kuwa chaguo maarufu zaidi kwa ajili ya
kuta na sakafu za bafuni. Marumaru ngumu zina rangi sawa kwenye unene wake
wote, ingawa zina gharama zaidi, na hapa ndipo mnunuzi anapopaswa kuwa makini.
Ujue kutofautisha kama unanunua marumaru zilizopakwa rangi kwa juu tu, na hizi
ni zile nyepesi na bei yake iko chini. Aina hii ni kuwa baada ya muda si mrefu
rangi inatoka kutokana na kukanyagwa mara kwa mara, kwa kuwa rangi imepakwa
kwenye eneo la juu la marumaru kwa unene kiasi tu na sio unene wote. Hizi
zilizopakwa rangi inakuwa eneo la juu tu mfano barafu kwenye mlima au kwenye
keki! Hizi za aina hii zinafaa zaidi kwa mapambo pengine kutengenezea ua la
ukutani lakini sio kwa kuhimili shurba za sakafu ya bafuni. Marumaru ambazo zina rangi hiyo hiyo hadi ndani kwenye
kiini na unene wote wa marumaru ni imara zaidi kwa matumizi ya sakafu ya bafuni.
Kwa
hivyo muhimu zaidi ni kutumia marumaru hizi ngumu zenye rangi sawa kila mahali
kwa ajili ya sakafu na kuchagua za bei rahisi zinazoendana na zile ngumu kwa
ajili ya ukuta, anasema David. Usimikaji wa marumaru ni kazi ya sanaa kwahivyo
inahitaji fundi mwenye uwezo nayo.
Zaidi
ya kuweka marumaru bafuni unaweza kuweka pia jiwe la asili kama vile marble lakini iliyo ngumu. Ubora wa jiwe
na usimikaji wake ni muhimu sana. Uwekaji wa jiwe la asili ni wa kitaalam.
Kunaweza kuwa na shida ya kufitisha slabu kubwa ya jiwe hilo kwenye maeneo ya
kutolea maji machafu na kuingiza maji safi, na muhimu zaidi ya yote sio kila jiwe la asili
linafaa kwenye mazingira ya mvuke na majimaji ya bafuni, anasema mhandisi. Mawe
mengine ya asili yananyonya maji na mwishowe kuwa na mipasuko.
Marumaru zitaongeza
thamaini ya nyumba yako, kwahivyo kuwa tayari kutumia muda na pesa. Kwa bafu la
kisasa na muonekno wa kifahari chagua marumaru zenye rangi za mwanga kama vile
nyeupe ukutani huku ukiweka miisho na mpangilio fulani wenye mvuto kwa baadhi ya maeneo ya ukuta.
Haijalishi
ni mtindo gani wa marumaru utakaochagua kwa ajili ya bafu lako, zingatia ubora
na usimikaji wa kitaalam kabla ya kufanya maamuzi yoyote. Dondoo muhimu kuliko
zote, kabla hujaanza kutengeneza bafu lako angalia thamani ya nyumba yako. Ubora
wa bafu uendane na thamani ya nyumba. Kwa kuzingatia hilo utafanya uamuzi
sahihi kwa kushirikisha wataalam watakaokufanya usijutie maamuzi yako hapo
baadaye.
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Thursday, November 20, 2014
my article for newspaper: jinsi ya kupamba bedroom
Jinsi ya kupamba chumba cha kulala
Kwa nyumba nyingi chumba
cha kulala ni chumba binafsi zaidi. Ni chumba pia ambacho
kina vitu vingi zaidi binafsi. Kinaweza kuwa kama kiota cha mahaba au mahali
patakatifu pa kulala na kupumzika. Pia kinaweza kuwa chumba cha kuchangamka na
kutuliza kwa watoto, kwa jinsi wanavyokuwa wakigundua kuwa wanamiliki chumba
chao wenyewe.
Kupenda
kufurahisha marafiki, majirani na wageni; wenye nyumba wengi wanamalizia nguvu
zao kupamba vile vyumba vya kuonekana na hadhara ndani ya nyumba. Umefika
wakati wa kuwa mchoyo na kuelekeza nguvu zako kwenye chumba cha kulala. Juu ya
yote ni kuwa kabla ya kuoga kujiaandaa kutoka ni lazima kwanza utokee
kitandani.
Kwanza
kabisa anza na kitanda kwa ajii kitovu cha chumba chochote cha kulala ni kitanda.
Ni wazi kuwa kitu cha kwanza cha kuzingatia kwenye kitanda itakuwa ni godoro,
lakini usisahau ubao wa kichwani. Ni ngumu kudharau umuhimu wa sababu za
kisaikolojia katika kupata usingizi mwororo. Hisia na hata muonekano wa kitanda
chako wakati unapoingia humo inaweza kuelezea ni namna gani unavyojisikia wakati
unapotoka humo.
Kwa upande wa sakafu chaguo zuri zaidi kwa ajili ya chumba cha kulala ni
zulia na mara zote imekuwa hivyo. Hamna kitu kizuri kama kuamka na kuweka miguu
yako kwenye sakafu ambayo inaelekea kuwa na hisia kama za kitandani kwa kupata
joto lile lile mithili ya la kitandani. Wengine hupenda kuweka sakafu za
marumaru na mbao lakini eneo la pembeni mwa kitanda wengi wanapenda kuweka
zulia.
Wazo la mwanga katika chumba cha kulala kwa baadhi linadharauliwa. Taa zisizokuwa
na maridadi na balbu za juu ya kichwa tu zimeanza kupoteza mvuto kwenye chumba
cha kulala cha kisasa. Taa za vivuli za kuweka juu ya vimeza vya kando mwa
kitanda na za ukutani za maridadi ndio zinaendana na wakati kwa chumba cha
kulala, kwa ajili ya mwanga wa chumba hiki kwa matumizi ya wakati wowote iwe ni
mchana, jioni au usiku.
Taa ndogo zinaweza kuwekwa kwa ajili ya kutumia muda maalum ambapo hutaki
kuwasha taa zote kwa mfano wakati wa kusoma au kushikisha kifungo.
Kwa vyumba vidogo vya kulala mara nyingi vinafaidika na uwepo na makabati
ya nguo, madroo na shelfu kwa kusaidia kuhifadhi na kuweka mpangilio. Baadhi ya
vitu vidogo dogo na nguo vinapoukuwa vimewekwa kwenye sehemu hizi za kuhifadhia, chumba kinaonekana nadhifu.
Mara
nyingi rangi za mwanga zinashauriwa
zaidi kwenye chumba cha kulala kwa ajili zinaleta hisia ya mapumziko. Rangi za
vitambaa vya malazi viendane na rangi nyingine hapo chumbani na hata zile za
samani. Shuka za rangi na maua ya kuvutia zinunuliwe ili kuongeza uzuri wa
chumba.
Komfota
lenye rangi nzito litaendana na samani au ubao wa kichwani wa mbao. Hii pia ni
kweli kwa mapazia.
Wakati
huo huo kumbuka kuweka samani zenye ukubwa na wingi wa kuendana na ukubwa wa
chumba. Kabla hujanunua samani hizo ni vyema kwanza kufahamu mpangilio wa
sakafu na ukubwa uliopo.
Kutengeneza bajeti ni muhimu kwa mradi wowote wa maboresho ya nyumbani. Kujipa wastani wa gharama inayohitajika itakusaidia kuamua ni nini kinachoweza kufanyika na kipi si kipaumbele. Baadhi ya shughuli kwenye mradi huu unaweza kufanya mwenyewe, kwa baadhi itakubidi utafute mtaalam. Kama kipaumbele chako ni ukuta kwa mfano, basi unaweza kutafuta mtalam wa rangi akapaka, ilihali ukitandika zulia mwenyewe. Vyovyote utakavyoamua, ni wakati wa kufanya chumba chako kuwa chako tena.
Kupamba chumba cha
kulala ni shughuli mojawapo ya maboresho ya nyumbani ambayo inaweza kuhuisha
tena afya yako na mahali unapoishi.
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
...picha hizi za mapambo haya yamenitumbuiza...
![]() |
| Hii picha nimefurahishwa zaidi na jinsi ya kupamba kwa mto ya soseji. Angalia hilo sofa kati kaweka soseji na iliyokuwa sandwiched na square, so nice... |
![]() |
| Hii fremu unaweza iweka jikoni hasa kama mlango wako wa jikoni ni wa kuingilia toka nje pia. Ni pambo na ukaribisho vilevile |
haya tena ni ubunifu tu
![]() |
| lovely |
Kama unakaa nyumba ya ghorofa ona hapa chini ya ngazi unavyoweza kufanya mambo.
Monday, November 17, 2014
designs simple za majiko kwa wanaoanza familia
Kuna aina nyingi za majiko ambazo wewe mdada unayeanza familia unaweza kuchagua kulifanya jiko lako kuwa na mashiko na kufanya kazi iliyokusudiwa kwenye nyumba. Siku hizi imekuwa rahisi kupata mawazo kwa kuchungulia dondoo mbalimbali kwenye majarida, kudesa la jirani au rafiki, kuangalia video na mitandao mbalimbali kwa mfano unavyosoma hapa sasa.
Muonekano wa jiko kwa asilimia kubwa unachukuliwa na tile na makabati. Tile za floor na ukuta wa jiko, zipo za kumwaga, ni wewe tu kuamua rangi na muundo upi unataka na kwa finishing ipi.
Kitu kingine unatakiwa kuzingatia kwenye design ya jiko ni makabati. Hard wood eg mkongo, mninga ndio mambo yote na ni muhimu sana, usidanganyike kwa urembo wa soft wood kwani si lolote si chochote kwa jikoni. Jiko litolee gharama lidumu.
Friday, November 14, 2014
Thursday, November 13, 2014
my article for newspaper: vioo vya mapambo
Boresha muonekano wa ndani ya nyumba kwa kuweka vioo vya
mapambo.
Vioo vina kitu kwakweli ambacho ni maalum ndani yake.
Vinakusaidia kukujulisha unaonekanaje na pia kukuwezesha kujiweka jinsi ambayo
unataka uonekane. Zaidi ya haya maandalizi binafsi na kujiridhisha na muonekano
wako kabla hujatoka, vioo vinasaidia pia kwenye kupamba ndani na hivyo kufanya
muonekano wa nyumba kuwa maridadi na nadhifu zaidi kwa kila mgeni
anayekutembelea.
Kama
kuna pambo la ndani ambalo wenye nyumba hatakiwi kulikosa, basi ni kioo.
Havitumiki tu kujiangalia unapoingia, bali vina mahadhi yake kwenye kuongeza
staili ya chumba au muonekano wa kupagawisha kwa kumfanya mgeni kuduwaa. Sababu
nyingine kuu hapa ni kuwa vioo vinaweza kuwa
na bajeti rafiki. Ni kweli kuwa kuna vioo ambavyo ni lazima viwepo
nyumbani kwa matumizi kuwa watu wanahitaji ili kuhakikisha kuwa wanaonekana
jinsi wanavyotaka kuonekana, lakini leo kwenye makala hii tunaongelea vioo kama
mapambo ambavyo unaweka kwenye ukuta wa nyumba yako ili kuongeza staili na
ukubwa.
Utagundua
kuwa leo, sokoni kuna aina nyingi na tofauti za miundo na aina za vioo.
Watengenezeaji wa vioo vya mapambo wanakuja juu kwa kuongeza ubunifu hasa wa
fremu wanazofungia vioo hivi. Unaweza kuvipata vioo hivi vikiwa kwenye fremu ya
kila malighafi unayohitaji kwa mandhari unaotaka kutengeneza.
Fremu nayo ni kigezo muhimu cha kioo kuwa kifaa cha mapambo. Unaweza
kuagiza kioo kwa umbo unalotaka kwa mfano unaweza kuwa na kioo kwenye ukuta wa
sebule ambacho kinatoa sura kwenye taswira nne kwa jinsi ambayo ukijitazama
unaona uso nne zinazofanana.. Haijalishi staili unayotaka au bajeti uliyonayo,
kuna uhakika wa kupata kioo ambacho ni sahihi kwa mradi wako.
Sababu
ya kuweka vioo hivi ndani ya nyumba ni ukweli rahisi kuwa unataka kutumia ile hali
ya kujiona ndani ya kioo kwa faida ya kimapambo. Baadhi wananunua vioo na
kuvitundika kama sanaa nyingine za ukutani, kwa maana ya kuwa wanakitundika
katikati ya picha na fremu nyingine, au wanakiweka kwenye ukuta ambao hauna
kitu kingine ambacho kingefaa hapo. Hata hivyo unaweza kutumia vioo vya mapambo
kuakisi mwanga na vifaa. Kwa mfano unaweza kuwa na ujia (corridor) ambao una
mlango upande mmoja lakini mwingine hauna. Pambo lako hapo linaweza kuwa mmea
wa kijani (uwe hai au mfu) pale kwenye ukuta usiokuwa na mlango pamoja na kioo.
Kioo kitauakisi ujia kwa kuukuza uonekane mpana na mrefu. Kupamba kwa vioo kunafanya eneo dogo lionekane kubwa na
mbinu hii inatumika na wataalam wengi wa ubunifu wa ndani nyumba.
Kupamba kwa vioo kunaongeza mwanga
wa chumba. Chumba kilichopakwa rangi ya giza kinaweza kuonekana kidogo,
kuongeza vioo kwenye kuta zake kutaboresha mwanga. Njia sahihi zaidi ya kuongeza
mwanga wa jua bila kuongeza taa ni kufunga vioo vitazamane na madirisha. Vioo
vinadaka mwanga wa jua toka dirishani na kuusambaza chumba kizima. Hii inaweza
kuwa njia mojawapo pia ya kubana matumizi badala ya kuwasha taa mchana.
Kupamba kwa vioo vya mapambo hakuhitaji mtaalam. Mtu akiwa na vifaa vya toolbox anaweza kufunga vioo ukutani na kutengeneza chumba chenye muonekano mzuri kwa gharama nafuu.
Chagua vioo vyenye maumbo ya kuvutia,
pembe nne ni nzuri ila vioo vyenye maumbo yasiyozoeleka vinafanya umaridadi
zaidi. Tafiti aina na maumbo mbalimbali ya vioo kabla hujamua ni vipi unataka.
Ili kukifanya chumba kisicho na
uwiano kionekane kuwa nao, funga vioo vya mapambo ukutani. Vioo hivi viwekwe
kuakisi vitu fulani kwenye chumba ili kufanya ionekane kama vitu hivi viko
katika kila upande wa chumba, kwahivyo pale unapoingia uone kama chumba kina
uwiano na ni kikubwa.
Baadhi ya wenye nyumba wanatamani
waboreshe muonekano wa ndani wa nyumba zao. Marekebisho yana gharama kubwa,
hata hivyo wewe mwenye nyumba usizime tamanio lako. Unaweza kunyanyua uso wa
ndani ya nyumba yako kwa kutumia vioo vya mapambo badala ya marekebisho
makubwa.. Mradi huu mdogo wa kunyanyua uso kwa kutumia vioo unaweza kukupa
matokeo usiyotarajia. Kupamba kwa vioo ni moja kati ya njia nyepesi na rahisi
za kuboresha muonekano wa ndani ya nyumba.
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ni mjasiriamali upande wa usafi wa nguo, mazulia na magari;
pia ana mapenzi makubwa ya muonekano wa nyumba. Kwa maoni au maswali tuma
kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Saturday, November 8, 2014
tv cabinet ni moja kati ya post zangu iliyopendwa kuliko...
nakuongezea hapa dondoo chache za muhimu kabla hujanunua kabati la tv, twende kazi...
kabati hili ni moja kati ya fenicha ya msingi hapo sebuleni ambapo unakutana na marafiki zako, kula dinner na kuangalia tv. Wakati unapotaka kununua kabati la tv, ukubwa wa tv yako unahusu.
wakati wa kununua usifikirie tv tu. fikiria pia vitu vidogodogo ambavyo vinatakiwa kuwa hapo lakini vihifadhiwe, kwa mfano remote, kwahivyo nunua kabati lenye droo moja au mbili na hata likiwa pia na shelfu itakuwa poa zaidi.. kwahivyo kumbuka kuwa usifikirie tv tu.
la mwisho lakini si dogo unatakiwa uamue malighafi na rangi za kabati lako. kuna makabati mengi ambayo machoni yanavutia lakini kwa ubora si lolote si chochote. kwa swala la rangi hakikisha una research hadi uone kitu kinachokuvutia ndio ununue. Good luck!
super saturday na marafiki zangu wa ukweli...
hapa na pale leo na watu wangu wadogo...
pozi la kibaunsa..sungusungu wangu
pozi zikazidi hadi rafiki akalamba chini
akanyanyuka akijongea tartiiibu
Friday, November 7, 2014
njia rahisi kabisa ya kupamba sebule
kwa vile sebule ni sehemu muhimu ndani ya nyumba inahitaji kutupiwa jicho zaidi ya nyingine zote na ni lazima ipambwe kwa njia mbalimbali ili iwe na mvuto mbele ya kila mgeni anayekutembelea, na hii wala si ngumu.
kwanza kabisa weka fenicha zenye mvuto ambazo ni sofa, vimeza vya kando, kimeza cha kati, meza ya chakula na viti vyake.
weka taa maridadi na zenye mwanga wa kutosha kumulika sebule yote. weka taa za vivuli juu ya meza na sakafuni ili kuleta matokeo makubwa. kama wewe ni mshabiki wa wallpaper chagua ukuta wa tv ubandike, ning'iniza picha na fremu ukutani na hata vikapu vidogodogo vikiwa na maua ya kutengeneza.
weka vyungu vikubwa vya maua juu ya meza au sakafuni kwenye kona. weka kioo kikubwa katika ukuta wowote na upambe boda zake kwa fremu za kuvutia. unaweza pia kuweka sanamu kwenye kona na pembe za sebule yako.
Thursday, November 6, 2014
my article for newspaper: fenicha za kwenye bustani na varanda
Zingatia haya
kabla ya kununua fenicha za nje ya nyumba
Fenicha
za nje ya nyumba pia zinajulikana kama fenicha za kwenye bustani au varanda. Aina hii ya fenicha huwa imetengenezwa kwa
malighafi inayozuia maji kupenya, kwa kuwa ni kwa ajili ya matumizi ya nje.
Fenicha za nje ya nyumba zimekuwa
zikitumika toka enzi za himaya ya Roma.
Fenicha
za nje ya nyumba ni muhimu kwa mikutano
wakati unapokuwa na kikundi cha watu kwa ajili ya siku maalum kama vile siku ya
kuzaliwa na kadhalika. Hakuna kinachofurahisha zaidi kama kuwa na kiusingizi
kwenye upepo mwanana wa kwenye varanda au bustani. Kuwa na chakula cha usiku na
mwenzi wako wakati nyota ziking’aa angani inakuwa ni mahaba zaidi ya ndani ya
nyumba.
Ila
kuna jambo linalofanya aina hii ya fenicha kuwa tofauti na zile za ndani;
malighafi ya fenicha za nje ya nyumba ni lazima iwe imara kwa sababu fenicha zitapambana
na mvua kubwa, jua kali, upepo na baridi kali. Je hali ya hewa ya unapoishi ni
joto na ukame, au unaishi karibia na pwani? Mvua ni za mara kwa mara? Haya yote
ni maswali muhimu ya kupatikana majibu kabla ya kununua fenicha za nje ya
nyumba. Hapa ni sababu, hali ya joto na ukame inafanya mbao kupasuka. Upepo
mkali unaweza kufanya fenicha za aluminiam zipeperushwe.
Ndio
maana ni muhimu sana kuhakikisha kuwa fenicha unazotumia kwenye mazingira ya
nje ya nyumba ni sahihi kwa matumizi hayo.
Kwa
malighafi, fenicha nyingi za kutumia nje ya nyumba zimetengenezwa kwa plastiki,
mbao aluminiam na chuma cha pua. Amua ni malighafi ya aina gani unataka kwa
ajili ya fenicha zako za nje. Vitu vitatu ambavyo vitakusaidia kuamua ni hali
ya hewa, utunzaji na muonekano.
Baadhi ya
malighafi kama vile aluminiam hazihitaji utunzaji wa kina. Chuma cha pua
kinaweza kudumu kwa muda mrefu sana na kinamudu joto na unyevu. Hapa
ni muhimu kufahamu kuwa fenicha za nje za mbao sio imara kama nyingine, kwa
hivyo inatakiwa kuziweka dawa mara kwa mara, anasema mseremala Rajab Hamis.Bottom of Form
Fenicha za nje ya nyumba
zinakusaidia kuongeza ukubwa wa makazi yako, unapata eneo zaidi la kupumzika
hasa wakati ule ambao jua sio kali sana au mvua sio nyingi. Kwa hivyo fenicha
hizi zinakamilisha ahadi ya mapumziko, burudani na raha kwa ujumla. Uchaguzi wa
fenicha za nje unazingatia hatua zilezile za kununua fenicha za ndani. Japo
kunahitajika umakini wa ziada kwa ajili ya tofauti kati ya fenicha hizi mbili.
Fikiria ni eneo kiasi gani ulilonalo
na lina umbo la namna gani. Je ni varanda ndefu na nyembamba au ni fupi pana? Tumia
eneo na umbo la varanda au bustani yako kufahamu ukubwa wa fenicha zako za nje.
Hakikisha unaacha nafasi ya kutosha kati ya fenicha zako ili uweze kupishana
kirahisi. Tumia utaratibu ule ule wa kupanga fenicha za ndani. Kwa eneo dogo
meza za ukubwa wa kwenye mgahawa na stuli zitafaa zaidi kwani zitachukua nafasi
ndogo.
Ni wapi
utakapoweka fenicha zako za nje, je kwenye bustani yako kuna eneo la kukaa
ambalo lina paa? Na pia je fenicha zako zitakaa juu ya sakafu laini ya udongo
na majani au zitakaa juu ya sakafu ngumu? Hii itakusaidia kuchagua malighafi ambayo
itaoana na mazingira yako.
Hakikisha
kuwa ukikalia fenicha zako unapumzika vyema. Hata kama viti haviji na mito unaweza
kutengenezesha mito yako mwenyewe na uwe unaihifadhi ndani majira ambayo
hutumii fenicha za nje. Jaribu fenicha za nje kabla ya
kununua na hata kuzilaza kwa jinsi ambayo ungetaka viwe kama vitanda vya
mchana.
Yote hayo yakiwa yameshasemwa bajeti
yako ndio itaamua ni nini unachoweza kununua. Siwezi nikasisitiza ni kwa namna
gani ni muhimu kununua fenicha imara zaidi unazoweza kumudu. Kama uchumi
unagomba, bado kuna namna unayoweza kupata fenicha za nje zilizo imara kwa hela
uliyonayo. Unaweza kupata fenicha za nje nzuri na imara kwa bei nafuu kabisa
kwa kununua zile zilizotumika. Fenicha zinazouzwa kwenye minada ya wafanyakazi
wa kimataifa wanaomaliza muda wao na hivyo kurejea kwao, ukizifanyia maboresho
kidogo na kuzisafisha zinaonekana kama mpya, na huwa hizi zinakuwa na ubora
unaokubalika. Unaweza pia kufikiria kubadilisha mito na makusheni kwa ajili ya
kuhuisha fenicha za nje za zamani.
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ni mjasiriamali upande wa usafi wa nguo, mazulia na magari;
pia ana mapenzi makubwa ya muonekano wa nyumba. Kwa maoni au maswali tuma
kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Subscribe to:
Posts (Atom)























