Tuesday, February 2, 2016

Zijue aina 4 maarufu za mitindo ya kupamba ndani ya nyumba


Unapoanza kupamba ndani ya nyumba iwe ni mbunifu au ni mwenye nyumba mwenyewe, anajiuliza ni mtindo upi nichague? Je mandhari gani ninayotaka kutengeneza? Ni mtindo upi utavutia kwenye hiyo nyumba? Iwe unapamba chumba kimoja au nyumba nzima maswali haya yote yanaamua  matokeo ambayo baadaye utajisikia vizuri katika mazingira hayo.

Kwa ujumla kuna aina 4 zilizo maarufu zaidi katika
mitindo ya kupamba ndani ya nyumba. Hata hivyo mitindo mipya inabuniwa kila leo lakini kwa hii minne utapata uelewa wa msingi na tofauti kati ya mtindo mmoja na mwingine kimuonekano.

Huenda wewe ni mbunifu na mteja wako anataka mtindo wa saresare, huwezi kumbadilishia na kumfanyia wa kisasa kwa ajili anaamini anachokitaka ndicho ladha yake na ndicho atakachoweza kuishi nacho vizuri. Ifuatayo ni mitindo mine maarufu zaidi:

1.     Mtindo wa kisasa (modern/ contemporary)
Tabia kuu za mtindo huu ni kuwa na vitu vichache muhimu ambavyo kila kimoja kinatumika. Yaani kinachoangaliwa ni uwepo wa kitu chumbani kwa ajili ya matumizi na sio kuwepo kama pambo pekee. Kuta hazipakwi rangi nzito na msisitizo ni uwepo wa vitu vichache sana na upambaji wake ni mrahisi. Eneo kubwa la chumba linakuwa wazi, safi na hakuna vitupio vidogodogo kama kwenye mitindo mingine. Kitu chochote ambacho ni pambo tu na huwezi kukitumia hakina nafasi kwenye mtindo wa kupamba kisasa.

Mtindo huu unatumika na kufaa zaidi kwenye vyumba/nyumba ndogo. Kuna baadhi ya watu wanahisia kwamba kupamba kwa mtindo wa kisasa kumerahisishwa sana na ni mtindo wa kichoyo. Ila watu wanaopenda utulivu na hasa nyumba zenye watu wa makamo wanapendelea mtindo wa kisasa.

Sasa,  ni vyema kufahamu kuwa maneno haya mawili (modern na contemporary) yanatumika kuelezea upambaji wa kisasa lakini  kuna tofauti ndogo sana kati yake. Upambaji wa contemporary ni kwamba pamoja na vitu vichache ila ni vile vilivyoko kwenye chati kwa kipindi hicho tu wakati upambaji wa modern ni vitu vichache  vilevile lakini inawezekana visiwe kwenye chati kwa wakati huo.


2.     Mtindo wa saresare (classic)
Mtindo wa saresare unasisitiza mpangilio na uwiano. Tabia kuu ya mtindo huu ni kuwa na eneo la kitovu cha chumba ambapo ndio macho yanaelekea ufikapo chumbani hapo, kwa mfano eneo ilipo luninga. Baada ya kuwa na eneo hilo kinachofuata ni kupamba kwa kugawa chumba pande mbili na kila kitu kwenye upande mmoja kinafanana na upande wa pili. Vitupio vingi kama mito ya vitambaa vya pamba, silki au velveti  na picha za ukutani za kanvasi vinatumika katika mtindo huu.  Chumba kinakuwa sawasawa pande mbili kiasi kwamba ungekigawa katikati, vitu vilivyoko upande mmoja ndivyo vitakuwepo upande wa pili huku eneo la kitovu likiwa limeainiswa. Nyumba nyingi za kisasa za Kitanzania zinaangukia kwenye mtindo huu.

3.     Mtindo wa kiutamaduni
Katika mtindo huu fenicha na mapambo ni mazuri na yana muonekano wa utamaduni wa watu fulani ila mapambo si mengi. Sehemu kubwa ya mapambo kama pazia na michoro ya ukutani ni ya kiutamaduni na fenicha zimekaa kisanaa zaidi.

4.     Mtindo wa mchanganyiko
Katika kutumia mtindo huu mpambaji au mbunifu anachanganya mapambo ya mitindo mitatu ya juu na kutengeneza huu mtindo wanne.

Kazi kwako mpambaji, naamini umenufaika kiasi cha namna ya kuweza kuchagua mtindo hata mwenye nyumba akikuambia nataka unipambie kwa muonekano fulani kwa mfano contemporary basi huna haja ya kubabaika tena. Kupitia makala hii yeyote anayetaka kupamba awe ni mpambaji mtaalam au mwenye nyumba mwenyewe amejua kipi ni kipi na anaweza kuamua mtindo mmojawapo kati ya hii huku akijua matokeo yataleta mandhari gani.

Je wewe msomaji wangu umepamba kwa mtindo upi kati ya hii? Mawasiliano 0755200023

1 comment:

  1. natfuta hizo vitambaa vya kanvasi kwa hapa dar ntapata wap?

    ReplyDelete