marafiki zangu wa kweli wamerudi shule...
ukiniuliza best skill yangu ni ipi nitakujibu cleaning..yani iko moyoni. i love to make things and places spotless...
Monday, August 25, 2014
Thursday, August 21, 2014
my article for newspaper: makosa wakati wa kununua sofa
Makosa makubwa ya kuepuka wakati wa kununua sofa
Moja ya umuhimu wa makala kama hii ni kusaidia wadau kuchagua kilicho chema kwa ajili ya nyumba zao. Sofa ni fenicha ambayo muda mwingi wa maisha ya nyumbani unakuwa pale hivyo inatakiwa ikidhi viwango vya nyumba na maisha unayoishi. Kuhakikisha unapata sofa sahihi, epuka makosa haya makubwa unayoweza kufanya wakati wa kuinunua. Habari njema ni kuwa makosa haya yanaweza kuepukwa kama kutafanyika maandalizi kabla ya manunuzi. Makosa haya makubwa basi, ni yapi ambayo mara kwa mara wanunuzi wanayarudia?
Kusahau kupima ukubwa wa sebule yako
Unatakiwa
kujua ukubwa wa chumba kabla ya kukua sofa ili kuwa na uhakika kuwa fenicha
hiyo mpya itafiti. Usikimbilie kununua fenicha kabla ya kuwa na uhakika wa
ukubwa wa chumba, zingatia itakavyokaa kwa kujali milango na madirisha.
Kama
eneo husika kuna mwanga mwingi unaoingia zingatia rangi ya kitambaa kwani vipo
vinavyopaushwa na jua. Sofa inatakiwa iendane na ukubwa wa chumba, isiwe kubwa
sana wala kiduchu. Usitegemee kumbukumbu wakati ukiwa kwenye chumba cha
maonyesho ya sofa, huwa inadanganya kuona kuwa sofa ni ndogo kwenye chumba hicho
kwani eneo ni kubwa, pia sofa iwe na uwiano na fenicha nyingine sebuleni.
Kutokuwa makini
na rangi
Je
unafahamu kuwa rangi ya sofa inayoonekana kutokuwa na nguvu kwenye chumba cha
maonyesho inaweza kuwa kinyume kwenye sebule yako? Nenda na mto wa sofa
unaoupenda na kuutupia kwenye sofa unayotaka kununua ili kuona itakuwaje ndani
mwako.
Mvinyo mwekundu unaenda kumwagika kwenye sofa zako, kama una wanyama wa ndani kama paka nao wanaenda kufanya mambo kwenye sofa yako, mwenza na watoto wanaenda kula bisi kwenye sofa zako; hata uwakataze mara ngapi. Kwa kuwa maisha halisi yanaendelea kila siku, unahitaji sofa ya kuweza kubeba madhila yote haya.
Kuchagua aina mbaya ya kitambaa cha sofa ni kosa la gharama. Chagua rangi na aina ya kitambaa kutokana na jinsi sofa inavyoenda kutumika. Kama sebule inatumika sana na ukanunua sofa ya kitambaa laini au rangi za mwanga, inaenda kuharibiwa hata kabla hujaifurahia. Rangi ya sofa iendane na fenicha, samani, rangi ya ukuta na taa.
Rangi nyeupe, maziwa au nyingine ya mwanga isiwe chaguao lako kama kwenye makazi yako kuna uwezekano wa tope na mikono michafu kufikia sofa. Siku zote chagua rangi ambayo unaipenda na unaweza kuishi nayo, usichague kwa kuangalia mitindo ya nyakati. Utaishi na hiyo rangi uliyochagua kwa miaka.
“Siwezi kukuambia ni mara ngapi nimefanya kazi na wateja ambao wanataka kubadili kitambaa cha sofa zao ambacho bado kiko vizuri bali ni kwa sababu tu wameichoka rangi yake”, anasema mtengeneza sofa Hamis Rajabu. Bahati mabaya ni kuwa haichukui muda kuchoka vitambaa vya maua maua, vyenye mistari mikali na vile vya rangi za giza, anasema Hamis. Ushauri wangu ni kuwa, chagua rangi ya kitambaa ambayo itashirikiana na rangi nyingi. Kama unapenda rangi nilizosema zinachosha mapema basi weka japo kwenye kiti kimoja cha pembeni lakini siyo kwa sofa nzima, anashauri Hamis
Kutokuomba ushauri
kwa wauzaji
Ongea
na watu wanaouza watakupa mawazo ambayo yatakupelekea kufanya maamuzi ya busara.
Hata hivyo unamuizi wa mwisho ni wako ila unapenda kuwauliza wataalam usikie
wanasemaje.
Kutofikiria sofa
ina burudiko kiasi gani
Utakubaliana
na mimi kuwa mara nyingi unaweza kushindwa kupata usingizi kitandani, ila ukija
kwenye sofa ukaegesha aidha ukiangalia muvi au kusoma kitabu haraka sana
unapata usingizi. Ni muhimu kuwa sofa unayotaka kununua ikawa ya matumizi na
burudani.
Kununua sofa
kabla ya kuijaribu
Kama
ambavyo sofa haitakiwi kuwa ndogo sana au kubwa sana kwenye chumba, vilevile
isiwe ndogo sana au kubwa sana kwako. Kama ni mrefu, hakikisha ukikaa miguu
yako itakaa vizuri. Kamwe usinunue sofa kabla ya kuijaribu, ikalie, ilalie,
ijaribu kwa kila namna ambayo utaitumia nyumbani. Kama unapenda kupata usingizi
wa mchana kwenye sofa hakikisha mikono yako iko vizuri kwenye sofa unayotaka
kununua.
Haya ni makosa makubwa ya kuepukwa wakati wa kunua sofa. Endapo utafanya makosa haya utaishia kutoridhika na sofa uliyonunua.
Tukutane wiki ijayo!
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Tuesday, August 19, 2014
Sunday, August 17, 2014
Thursday, August 14, 2014
my article for newspaper: maeneo tunayosahau kusafisha
Wakati ukiwa unasafisha makazi yako
mwishoni mwa wiki hii, kumbuka kufanya usafi wa uhakika. Mara nyingi huwa
tunasafisha maeneo na vitu vinavyoonekana. Makala hii itakujuza baadhi ya
sehemu na vitu ambavyo kwa wengi ni rahisi kusahaulika kusafishwa na mwishoni
utasema, ee kweli hapa huwa sisafishi.
Tunakumbuka kusafisha ndani ya
jokofu, lakini je juu na chini yake? Ndani ni kwasababu huenda kila
tunapofungua mlango wa jokofu harufu mbaya na macho yanatuashiria kuwa sasa ni
wakati wa kusafisha. Juu ya jokofu kunabeba vumbi ambalo sio rahisi kuliona
vinginevyo uwe ni mrefu sana. Nyuma na chini ya jokofu vile vile kunaweza kuwa
kumebeba vumbi sawa na lile la juu. Na chini sio vumbi tu hata mabaki ya vyakula
vinavyodondoka kwenye sakafu ya jikoni. Kinachotakiwa ni kusimama juu ya kiti
na kusafisha juu wakati kwa chini
unachotakiwa ni kuomba mtu wa kukusaidia kulisogeza ili usiharibu sakafu yako
kwa kuburuza. Jokofu likishakuwa limesogezwa, ni kiasi cha kufagia na kudeki. Baada ya hapo lirudishe mahali pake.
Tunategemea
feni majumbani mwetu kwa ajili ya kuleta mpepea wa ubaridi. Kwa kadri feni
inavyotumika, ndivyo inavyojaa vumbi. Feni hasa za darini ni maarufu kwa kujaza
tabaka la vumbi. Njia rahisi ya kuzisafisha ni kufuta kwa kutumia ufagio uwe wa
kawaida au wa buibui uliofungiwa kitaulo kilicholoa kwenye brashi zake.
Kulingana na majira na matumizi, feni zisafishwe walau mara moja hadi mbili kwa
mwezi .
Ni
kichekesho cha muda mrefu kuwa ndani ya nyumba sofa ndio eneo linalomeza vitu
vidogodogo. Kwa sababu hii mito ya sofa (ile ya kukalia na kuegemea) inapaswa kuondolewa
na ndani ya sofa kusafishwe. Japo kwa nyumba nyingi ndani ya sofa ni rahisi
kusahaulika kusafishwa hadi pale vitu kama hereni, kalamu ama opener inapopotea
ndio eneo hili linakumbukwa kua huenda mtoto kaficha humo. Kulingana na aina na
ukubwa wa familia yako pengine huhitajiki kusafisha ndani ya sofa mara kwa
mara. Usafi huu ujumuishe na kufua foronya za mito, ni kazi rahisi japo huwa inasahaulika.
Ndoo
za taka za ndani ya nyumba zinaashiria kuwa zinahitajika kusafishwa ila pipa la
nje linakosa kiashiria hiki kutokana na eneo lililopo. Ukiona jirani anaanza
kuguna kila unapofungua pipa lako la nje la taka basi ni wakati wa kufikiria
kulisafisha kiaina. Kwa kawaida mapipa ya taka ya nje yanahitaji kutupiwa jicho
la usafi zaidi wakati wa kiangazi kuliko wa masika.
Kama una taa za vivuli ndani ya nyumba yako, kumbuka kusafisha kile kifaa kinachosababisha kivuli. Kuendana na jinsi kilivyotengenezwa iwe ni kwa kitambaa, kioo au plastiki zinaweza kusahaulika kufunguliwa na kusafishwa.
Majani ya mimea iliyooteshwa ndani ya nyumba husahaulika kufutwa vumbi. Haishangazi kukuta mmea wa ndani iwe ni nyumbani au mgahawani ukiwa na majani yaliyojaa vumbi.
Vipasha vyakula (microwave) vinachafuka sana ndani kwa kuwa wengi wanapasha vyakula ambavuo havijafunikwa. Uchafu huu wa matone ya michuzi unaorukia kwenye kuta za microwave hubaki na kukaukiana na ajili unapata moto kila vyakula vingine vinapopashwa. Haishangazi kukuta microwave ambayo kwa jinsi ilivyo ndani unapata ukakasi kupashia chakula.
Ingawa wengi hawana taabu ya kukumbuka kusafisha vioo iwe ni vya madirisha au vya kujitazama, kioo cha luninga ni eneo ambalo kwa wengi linasahaulika kusafishwa. Endapo luning hii inatumiwa na watoto wadogo ni rahisi kuona alama za vidole kwenye kioo pale inapokuwa imezimwa. Chukua muda kufuta vumbi luninga yako weekend hii ili kufanya kioo king’ae tena.
Vumbi linajikita kwenye vitabu. Chukua dasta kufuta vumbi vitabu vyako.
Ingawa tunaweza tusione uchafu na utando ulio kwenye vitasa vya milango ya nyumba zetu lakini upo. Na tunapovisafisha tunaweza tusihisi tofauti, lakini unajisikia vizuri kushika kitasa kisafi. Na zaidi ya yote kukinga nyumba yako na vijidudu vinavyotoka kwenye mikono michafu inayofungua milango kwa kushika vitasa hivi.
Ni nini na wapi unapofikiri watu wengi wanasahau kusafisha? Je kuna popote nimesahau?
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Wednesday, August 13, 2014
Friday, August 8, 2014
house tour: Here's the $20M SoCal Mansion Kim and Kanye Just Bought
hebu tusafishe macho mdau tuone mambo hapa...
wenye nyumba, kim & kanye
ukifungua geti unakutana na muonekano huu wa mbele
yasemekana ina vyumba 8 vya kulala
vegetable garden nayo haijakosekana
floor ni ya mbao...huenda baby north atalala hapa
kanye naye atakuwa anajilia raha za kisamaki hapa kwenye hii pool
Thursday, August 7, 2014
my article for newspaper: kusafisha vifaa vya kusafishia
Jinsi ya
kusafisha vifaa vya kufanyia usafi
Hatusafishi
vifaa vyetu vya kusafishia sio? Hata ukikataa, kubali tuu kuwa wengi
hawasafishi. Wengi tunajua umuhimu wa kusafisha na kutunza vitu….ila vifaa
vyetu vya kusafishia mara nyingi vinasahaulika. Haijalishi wewe ni msafi kiasi
gani, haiwezekani kuweka nyumba safi kama vifaa vyako vya kusafishia
havisafishwi! Makazi ya vijidudu vingi ni kwenye maeneo machafu. Angamiza
vijidudu kwa kusafisha sponji na vifaa vyako vingine vya kusafishia!
Kwa
sababu tu kinatumika kusafishia sio kuwa kinajisafisha chenyewe. Kiukweli vifaa
vya kusafishia vinaweza kuwa makao ya uchafu, vijidudu, tope na harufu kama
havitunzwi vizuri. Jinsi vifaa vinavyotunzwa ndivyo hela yako ya kununua vipya
itakavyobaki mfukoni. Ufagio mchafu unachafua zaidi sakafu na pia uchafu huo
unaweza kukwaruza sakafu yako. Mashine ya kusafishia kwa upepo ambayo haijasafishwa
haifanyi kazi yake vizuri. Weka vifaa vyako katika hali ya usafi ili kuwa na
matokeo mazuri.
Kuna ule usafi wa kawaida wa kusafisha vifaa vya kusafishia japo kwa sabuni
na maji na kuviacha vikiwa safi tayari kwa kuanza usafi mwingine. Brashi za
kusafishia bafuni zishafishwe kwa dawa za kuua vijidudu japo mara moja kwa
mwezi. Brashi za kusugulia zaweza kusafishwa kwa maji na sabuni ya kawaida. Brashi
zenye taka zilizojishikilia waweza kuchukua kijiti na kuondoa taratibu taka
zote ziwe ni tope au nyuzi nyuzi.
Ndoo
zako za kupigia deki usiziache zikiwa na uchafu wa aina yoyote hata kama ni
maji yaliyotumika tayari. Ziache zikiwa kavu aidha kwa kuzigeuza juu chini.
Sponji
la kuoshea vyombo uwe unaliosha kwa maji ya moto walau kila juma. Ikiwezekana
hata kulichemsha jikoni itakubwa bora zaidi, wengine wanaenda hatua ya mbali
zaidi ya kuliweka kwenye kipasha vyakula (microwave).
Ila kama utafanya hivi hakikisha sponji
limeloa chepechepe kabla ya kuliweka kwenye microwave.
“Asimilia 70 ya bacteria huishi kwenye sponji chafu”, anasema dokta Mbuya.
Tokea
ukiwa mdogo, kulikuwa na kitambaa cha kufutia vumbi nyumbani. Ukichukua kitabu
chenye vumbi unachukua kitambaa unakifuta. Vitambaa hivi vya kufutia vyumbi
ambavyo wengi wetu wanaviita dasta
vinapaswa kufuliwa kiumakini kama tunavyofungua nguo nyingine. Tofautisha kati
ya vile vyenye uchafu mkubwa wa kudiriki kutengeneza utando na vile vyenye
uchafu mwepesi.
Vichwa
vya mop na madekio mengine vinapaswa
kusuuzwa baada ya kufanyika usafi na kuachwa vikauke. Kabla ya kusuuza
hakikisha kuwa unaondoa udongo wote, mchanga na hata majani yanayoweza kuwa
yamejishikilia ndani. Sio sawa baadhi walivyozoea kuacha dekio linakanyagiwa
mlangoni. Pale ni sehemu ya kuweka tandiko la mlangoni na sio dekio. Sabuni ya
kawaida ya kufulia inatosha, huhitaji kuweka dawa za kusafishia kwenye vifaa
hivi. Ila ni muhimu vikuke kwani vinaweza kutoa harufu ya uvundo.
Kusafisha
mifagio..mmh ni wachache wanaofikiria kufanya hivyo! Unaweza kufungua ile
sehemu ya brashi ukaitenganisha na fimbo na ukaiweka kwenye ndoo ukasafisha na
brashi zako nyingine za kusafishia. Jambo la kuzingatia ni kuondoa matope
kwanza kwa kuwa sehemu ya ufagio ya brashi ni maarufu kwa tope na uchafu
uliojizunguishia kwenye vibrashi vyake.
Mashine
za kusafishia kwa upepo zinatofautiana kiumuundo ila kuna dondoo kadhaa za
kukuwezesha kuisafisha. Tafuta kama una kitabu ulichonunulia kitakuongoza jinsi
ya kuisafisha. Hakikisha unamwaga mfuko wa kukusanya vumbi mara kwa mara. Kutegemea
na jinsi unavyotumia mashine yako fua mfuko wa vumbi kila baada ya miezi
mitatu. Uanike ili ukauke kabisa kwani ukiiurudisha ukiwa na unyevu
utasababisha vumbi kufanya tope na hivyo kuiharibu mota kwa kuilazimisha ifanye
kazi kubwa ya kusukuma kushindana na ukuta wa tope. Kama unasikia harufu ya
vumbi inatoka ndani ya mashine yako ni kwa kuwa mfuko wa vumbi umejaa.
Ingawa hutumii mashine yako ya kufulia kwa kitu kingine zaidi ya nguo bado kuna wakati inakubidi ufungulie maji kuisafisha yenyewe bila kuweka nguo ndani.
Tumejuzana
namna ya kusafisha vifaa vya usafi ambavyo tunatumia mara kwa mara nyumbani.
Inaweza kuwa shughuli sahihi ya kufanya kwa muda wowote wa ziada ulio nao weekend hii!
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
alhamisi ya rasha rasha...
rasha rasha za leo za hapa na pale za kupunguza vumbi kwa tuliopo mazingira ya vumbi. hali ya hewa si joto wala baridi ni safi kabisa...
Thursday, July 31, 2014
my article for newspaper: kusafisha bafuni
Hakuna anayetaka kusafisha bafuni, lakini ukisafisha
kila unapotumia, kazi inakuwa na maumivu kidogo kuliko kuacha hadi wakati wa
usafi mkubwa. Makala hii itakujuza ni jinsi ya kuweka kuta, bafu, sinki, bomba,
eneo la kuogea na bakuli la choo nadhifu kila wakati.
Unapoanza kusafisha bafuni, kwanza ondoa vitu vyote
vya kuhamishika kama vile vizulia, tenga la nguo chafu, kimeza au kikabati na
kindoo cha taka.
Baada ya hapo ondoa buibui kwenye
kona za dari ikifuatiwa na kufuta vumbi mlango kwa nje na ndani. Kwa ujumla
wakati wa kusafisha chumba anzia juu kushuka chini. Ruhusu taka za vumbi na
buibui zimwagike sakafuni kwa ajili utasafisha mwishoni. Kitambaa cha kufutia
kinafaa sana kwa kazi hii japo pia waweza kutumia fagio.
Mimina blichi ama sabuni za
kusafishia kwenye bakuli la choo na iache iondoe uchafu taratibu.
Weka dawa ya unga wa kusafishia zile sehemu ambazo
zina uchafu. Kama kuna uchafu umejijenga kwenye lile eneo la kuogea, sinki ama
pembeni na bomba weka unga wa kusafishia halafu sugua taratibu kwa brashi.
Ukiacha unga huu ukae kati ya dakika 10 hadi 15 wakati ukifanya jambo jingine itaruhusu
kulainisha uchafu. Hakikisha unasoma maelezo ya dawa ya kusafishia ili kuwa na
uhakika unatumia kiasi sahihi ambacho hakitaharibu maeneo yako. Pia ni vyema
kujaribu dawa eneo dogo kabla ya kusafishia eneo kubwa.
Paka sabuni au dawa nyingine za kusafishia kwenye kuta
za bafu kama ni za marumaru. Kwa kutumia sponji ama brashi sugua sehemu uliyoweka
sabuni. Isuuze vizuri kuondoa michirizi yoyote michafu na kama ukuta ni wa
karibia na sinki ama bakuli la choo ukaushe kwa taulo. Ukuta wa sehemu ya
kuogea unaweza kuuacha bila kuukausha. Ni vyema kuvaa glovu wakati wa kusugua
kwani baadhi ya madawa na sabuni zinaweza kuchubua ngozi.
Safisha bomba la kuogea ambalo sio siri kuwa
wasafishajiwengi huwa hawakumbuki kusafisha. Bomba inatumika tu kusafishia
kwingine ila yenyewe inasahaulika kusafishwa. Ni kama msemo wa mshumaa kujiunguza
kumulikia wengine! Kwa sababu hiyo utakuta kwenye bomba na vichwa vyake
kunakuwa na uchafu wa sabuni zilizogandian. Hali huu huweza ikasababisha makazi
ya vijidudu.
Pazia la bafuni huwa linaandamwa na ukungu eneo
linalogusana na sakafu. Ni vizuri zaidi ukalifungua na kulifua kwenye maji ya
moto kwa kiasi kidogo cha sabuni na blichi. Kumbuka adui nambari moja wa ukungu
ni blichi. Kiasi kidogo kitaondoa uchafu bila hata kusugua.
Angalia eneo la sinki na sugua mabaki ya sabuni na
dawa za mswaki kwa sabuni kidogo pamoja na sponji au brashi. Mswaki wa zamani
unaweza kutumika kuondoa uchafu kutoka eneo la kati ya bomba na mishikio yake. Kuwa makini kuwa brashi
la kusugulia bakuli la choo lisitumike kusugulia sinki. Hii inaweza kusambaza maradhi kwa
kuruhusu vijidudu vya kwenye choo kuingia kwenye sinki la mswaki. Kuzuia hali
hii isitokee, brashi la bakuli la choo liwe la peke yake. Ni muhimu kutumia
blichi kusafishia bafuni ili kusaidia kuua vijidudu.
Safisha kioo kwa kutumia ama maji na taulo au dawa
ya kusafishia vioo na taulo.
Safisha nje ya choo ukianza na ile sehemu ya juu ya
kuvuta maji, taratibu endelea kusafisha eneo lote la nje ya choo ambalo ni
pamoja na mfuniko na eneo la chini ya pale pa kukalia na futa kwa taulo. Kumbuka
kitaulo hiki kimetengwa kwa kusafishia choo pekee.
Sugua ndani ya bakuli la choo kwa brashi yake halafu
vuta maji. Huna haja ya kusugua kwa nguvu nyingi. Acha sabuni na dawa ya
kusafishia ikufanyia kazi hiyo.
Sasa ni wakati wa kusafisha sakafu ukinanzia na zile
sehemu zilizojifisha hadi zile za wazi. Safisha mavumbi yote na uchafu wote
ulio chini na pale eneo la choo lilipounganika na sakafu. Eneo hili kwa kawaida
huwa ni chafu sana na lile bomba la nyuma linajaa mavumbi. Malizia kwa kusuuza kwa
maji masafi kuondoa sabuni itakayoweza kubaki na kusababisha utelezi.
Subiri kidogo sakafu ikauke ndipo urudishe vile vitu
ulivyoondoa awali.
Ili kuweka bafu lako katika hali ya usafi na
kupunguza kutumia nguvu kubwa ya kusafisha unatakiwa uwe unasafisha maeneo
mbalimbali ya bafu mara baada ya kuyatumia. Kwa mfano safisha bakuli la choo
kila baada ya kulitumia, vile vile eneo la kuogea pamoja na sinki. Hata kama
sehemu hizi hazionekani kuchafuka safisha tu kwani madini yaliyoko kwenye maji
nayo yaweza kufanya alama. Kama utafanya hivi, usafi mkubwa utakuwa na maumivu
kidogo kwani uchafu hautakuwa umejijenga.
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Thursday, July 24, 2014
my article for newspaper: mpangilio wa chumba cha kulala
Chumba chako cha kulala ni
sehemu ambayo unalala, kwahivyo ni muhimu pawe katika mazingira ya kupumzikia.
Wakati huohuo unataka pawe eneo la kufanyia shughuli mbalimbali zinazotakikana
kufanyikia hapo kwa mfano kujiandaa kwa ajili ya kutoka asubuhi. Jinsi ambavyo
fenicha zimepangwa italeta matokeo chanya au hasi kwa mazingira ya chumba chako
cha kulala. Kitanda ni fenicha nambari moja kwa chumba chochote cha kulala na
kwa asili ndio kitovu cha jicho linakotazama.
Vyumba vya kulala
vinavyotumika na watu wa kundi fulani vina mahitaji ya kipekee kwa kundi hilo.
Iwe unapanga chumba cha kulala cha wakuu wa familia, cha mgeni au cha watoto
makala hii itakupa dondoo za jinsi unavyoweza kupangilia.
Iwapo
unapanga chumba cha kulala cha wakuu wa familia (kumbuka kuwa chumba hiki sio
lazima kiwe ni kikubwa zaidi kama wengi wanavyodhani) kinachotakiwa tu ni kuwa
na vifaa muhimu vinavyohitajika mule. Na kama chumba chako ni kidogo zaidi ya
ambavyo ungependa, fikiria mbinu za kukifanya kiwe kikubwa kama vile kuondoa
mrundikano na kuweka fenicha, pazia na malazi yenye rangi za mwanga kwani zinafanya
chumba kionekane kikubwa.
Tukiachana na ukubwa wa chumba cha kulala cha wakuu
wa familia, dondoo hizi zitakusaidia kukifanya kiwe sehemu bora zaidi ya
mapumziko. Weka vimeza vya pembeni mwa kitanda vyenye ukubwa wa kuendana na
eneo lako. Kama unatazama luninga ukiwa kitandani utagundua kuwa vimeza hivi
vitakusaidia. Tafuta eneo japo kwa kiti kimoja au viwili vya kukalia. Viti
vinasaidia sana siku ya ugonjwa, kupumzika mchana au wakati wa kusoma. Fikiria
kuweka zulia sakafu yote ya chumba hiki ili kuondoa kelele za fenicha na nyayo kwenye
chumba. Kama una nafasi si mbaya kuweka deski kwa ajili ya kukaa na kuandika
chochote.
Kwa upande wa watoto wanaoingia
kwenye rika la ujana huwa wanajua ni nini wanachotaka kwenye chumba chao cha
kulala, na hawachelewi kukuambia wewe mzazi au mlezi wanahitaji sehemu ya
kuhifadhia vitabu na muziki ama eneo lao lingine la kuhifadhia vitu vyao
vingine vyovyote unavyoweza kudhani.Wana mawazo yao kuhusu mpangilio na rangi,
kwa hiyo waulize!
Pilika nyingi zaidi ya kuperuzi
mitandao na burudani zinafanyika kwenye chumba cha kulala cha watoto wa rika
hili la kuingia kwenye ujana. Viti vya ziada na vimeza vitawezesha eneo la
wageni wao. Weka fenicha zitakazotumika na rahisi kutunza.
Vyumba vya
kulala vya watoto wadogo viwekwe fenicha kwa kufikiria miaka yao ijayo. Ila
mwanzoni, hakikisha unaweka eneo la kuwabadilishia karibia na kitanda. Kwenye
chumba hiki hakikisha usalama unapewa kipaumbele. Usiweke kitanda karibia na
dirisha kama dirisha hilo linafunguliwa mara kwa mara. Mara nyingi kuweka
kitanda katikati kama chumba kina nafasi kubwa huwa ndio mpangilio mzuri zaidi. Ila kama nyumba yako
ina viyoyozi na madirisha hayahitajiki kufunguliwa basi unaweza kuweka kitanda
chini ya dirisha.
Hakikisha mtoto hawezi kuanguka toka
kitandani. Hakikisha droo za chumba
hiki ni laini kufunga, kwa mfano endapo mtoto atakuwa amefungua kwa bahati
mbaya basi reli zitateleza zenyewe na droo kufunga. Zikiwa ni droo ngumu
kufunga mtoto anaweza akanyanuka droo ikiwa wazi na kona yake ikamtoboa
kichwani. Vitasa vya milango na mikono ya makabati visiwe na ncha kali kwenye
chumba hiki. Ikiwezekana funika swichi za umeme na nyaya zisisambae sakafuni.
Kuwa na chumba
cha mgeni kunamfanya mgeni wako kuwa huru zaidi ugenini na hata wewe mwenyeji
wake. Unaweza kupanga chumba cha kulala cha mgeni kwa kitanda sahihi na vifaa
vinavyohitajika na kukisahau. Hakikisha kuwa mgeni wako ana sehemu ya kutosha
ya kuhifadhia, seti mbili za shuka, mito na komfota au kava la duveti.
Kwa
kufanya haya utakuwa umeweka mpangilio wa kufaa kwa kila chumba cha kulala kwa
watu wa kada mbalimbali walioko ndani ya familia yako.
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
--vitu vizuri-- urembo wa Tanga stone kwenye nguzo
Tanga stone kwa vile yanatokea Tanga...yanaweza kukatwa ukubwa unaolingana ama unaweza kuyatumia bila kuyakata. Pia unaweza kuyaongezea urembo kwa kuya polish. Jiwe hili la asili limewashika sana WaTZ na wasio na kuwa maarufu sana kwenye majengo mengi nchini.
Saturday, July 19, 2014
Friday, July 18, 2014
Thursday, July 17, 2014
my article for newspaper: kung'arisha nguo nyeupe
Jinsi ya kung’arisha nguo nyeupe
Sababu kadhaa zinaweza kufanya nguo nyeupe zipoteze
weupe wake. Huenda utafuata kanuni za utunzaji wa nguo nyeupe, lakini bado
zinaweza kubadilika na kuwa na rangi ya njano baada ya muda. Unjano mara nyingi
unatokea kwenye nguo ambazo hazijahifadhiwa vizuri kwa kugusana na mbao au bodi
za kabati.
Haiepukiki kuwa baada ya muda nguo hupata udongo na kuanza
kuonyesha uchakavu. Nguo nyeupe ni chambo cha madoa, na madoa hayo huonekana
zaidi ya nguo yenyewe. Habari njema ni kuwa nguo nyeupe hata iwe imendamwa na
madoa kwa kiasi gani, bado inaweza kuokolewa.
Soma makala ifuatayo ambapo Aisha Idd ambaye ni mtaalam wa kufua
anatujuza namna tunavyoweza kurudisha tena uhai wa nguo nyeupe. Anasema kuna
njia kadhaa za kuweza kuzing’arisha tena. Baadhi ya njia zinaweza kuharibu
vitambaa laini kwa hivyo kuwa makini.
Unatakiwa kufua nguo nyeupe mara kwa mara. Madoa yanavyokaa
kipindi kifupi, ndivyo ilivyo rahisi kuyaondoa. Hii hasa inahusu kwa njano ya
kikwapa itokanayo na kutokwa jasho na deodoranti. Weka dawa ya kuondoa madoa
kwenye maeneo haya na mengine yenye madoa kabla ya kufua nguo nzima.
Njia ya kwanza na iliyozoeleka na wengi ya kung’arisha nguo
nyeupe ni kuweka blichi wakati wa kufua. Blichi ya klorini inashauriwa kutumika
zaidi kwa kipimo kilichoelekezwa kwenye chupa na kwenye nguo za pamba. Itumie
tu kwa nguo nyeupe na ambazo zinaruhusu blichi. “Hakikisha unasoma lebo ya nguo
kabla ya kuamua kutumia njia fulani ya kuing’arisha,” anasema Aisha. Kuna nguo
hata kama ni nyeupe ila lebo yake inasema usitumie blichi.
Pia blichi ikizidi inaweza kuharibu nguo na wakati mwingine
kuleta mistari ya njano kwenye nguo nyeupe kwa hiyo kuwa makini na kiasi cha
blichi kinachotakiwa kuchanganywa na maji. Wakati mwingine yapasa kuloweka nguo
zako kwenye maji yenye blichi kwa usiku mzima.
Unaweza kuweka rangi ya bluu kwenye maji ya kusuuzia
ili kufanya nguo zako nyeupe zing’ae.
Unachotakiwa ni kufuata maelekezo kwenye chupa ya bluu. Bluu inaongeza
ubluu kwenye nguo ambao unaifanya ionekane nyeupe zaidi na ing’ae. Bluu
inatakiwa kuwekwa na maji ya baridi.
Kuanika nguo nyeupe zikauke juani ni njia mojawapo pia ya
kuzingarisha. Kwenye jua kuna mionzi ya UV ambayo inafanya nguo nyeupe izidi
kuwa nyeupe, anasema Bi Aisha. Bila shaka! Mwanga wa jua ni zana mojawapo kuu
ya asili tuliyonayo ya kufanya nguo nyeupe zizidi kuwa nyeupe bila kutumia
kemikali.
Vinega;
ndio vinega hii hii unayoifahamu pamoja na sabuni yako ya kufulia vitang’arisha
nguo zako nyeupe. Vinega ni kilainishi na marashi ya nguo, hii inawekwa kwenye
maji wakati wa kusuuza. Usijali harufu kwani nguo zako hazitanukia kama vinegar
bali harufu itapotea juani wakati wa kukaushwa.Vinega hii nyeupe pia inasaidia
kuondoa mabaki ya sabuni kwenye nguo. Onyo: Kamwe usichanganye vinega na blichi
kwani inafanya kemikali hatari kwa nguo zako, anasema Aisha.
Juisi
ya ndimu ni njia nyingine ya asili ya kung’arisha nguo nyeupe. Weka nusu kikombe
cha chai na sabuni kwenye maji ya kufulia (hata kama unafua kwa mashine) na
endelea kufua nguo nyeupe kama kawaida. Itumie tu kwenye nguo nyeupe kwani
inaweza kuharibu nguo za rangi.
Magadi soda (Baking Soda)
nayo inaleta matokeo ya ajabu kwenye kung’arisha nguo nyeupe bila kutumia
blichi. Hii pia weka nusu kikombe cha chai pamoja na sabuni yako ya kufulia.
Nguo zitatoka nyeupe na zitang’aa kuliko.
Usishange hii ni moja ya viambato kwenye dawa za meno, ni kwa ajili ya
kuongeza weupe.
Hizo hapo juu ni njia mbalimbali za kufanya nguo nyeupe ziwe
nyeupe zaidi. Zingatia kuchagua sabuni za kufulia ambazo zimetengenezwa kwa
ajili ya kung’arisha na zitumie mara kwa mara kwa matokeo mazuri. Fua nguo nyeupe
kwa maji ya baridi ili kufanya madoa na unjano usizame na kung’angania zaidi
kwenye nyuzi za nguo. Usichanganye njia moja na nyingine pamoja kwani unaweza
kutengeneza kemikali itakayoharibu nguo zako.
Kwa hivyo kwa matokeo mazuri, fua nguo zako nyeupe kwa sabuni za
kawaida za kufulia ukiongeza moja ya njia za kung’arisha hapo juu tulizojuzwa
na Bi Aisha. Halafu tundika nguo zikauke juani. Utashangazwa ni kwa namna gani
zimeng’aa. Bottom of Form
Makala hii
imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa
makazi na pia ni mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au
maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Tuesday, July 15, 2014
housekeeping: jinsi ya chap chap ya kusafisha pavers
Vitofali vya paving zaidi ya kuongeza mvuto kwenye landscape ya makazi yako, pia vinaleta muonekano wa uimara na usafi wa eneo iwe ni drive way, au njia ya miguu au uani. Vyovyote vile unavyotumia vitofali hivi kuendana na mahali ulipoviweka huwa vinachafuka na kuonekana kuchakaa hasa pale gari zinapoingia na tairi zenye tope na pia mimea ya mosi inayoota maeneo ya kati ya kitofali kimoja na chenzake pale masika inapofuliliza. Sasa basi njia za chap chap za kurudisha mvuto ni kuvisafisha ama kwa mashine ya presha au kama hauna mashine hiyo waweza kukwangua kule katikati ya kitofali kimoja na kingine (kwenye vifereji) ili kuondoa ukungu (mosi) wanaokuwa wameota na baada ya hapo ukafagia kwa mfagio mgumu na mpira wa maji.
Kufanya hivi hasa baada ya masika kunafanya vitofali vyako ving'a e tena na kuingia kwenye kiangazi free of makoko. Endapo hutafanya hivyo (kusafisha kuondoa hayo makoko), kiangazi kinapotinga baada ya masika jua linayakausha na kutoka yenyewe na ndipo huleta sura mbovu kwenye vitofali. Kwa hivyo vifaa utakavyohitaji endapo huna pressure washer ni mpira wa bustani, kisu cha kukwangulia, na mfagio mgumu. Dondoo hii ni ya kusafsha chap chap bila gharama kubwa ili kurudisha landscape yako kwenye mvuto wa awali.
Kufanya hivi hasa baada ya masika kunafanya vitofali vyako ving'a e tena na kuingia kwenye kiangazi free of makoko. Endapo hutafanya hivyo (kusafisha kuondoa hayo makoko), kiangazi kinapotinga baada ya masika jua linayakausha na kutoka yenyewe na ndipo huleta sura mbovu kwenye vitofali. Kwa hivyo vifaa utakavyohitaji endapo huna pressure washer ni mpira wa bustani, kisu cha kukwangulia, na mfagio mgumu. Dondoo hii ni ya kusafsha chap chap bila gharama kubwa ili kurudisha landscape yako kwenye mvuto wa awali.
Friday, July 11, 2014
housekeeping: kisulisuli kimepamba moto
kwakweli upepo wa kipupwe hiki umetisha. Kwa wanaoacha milango wazi, kwa kipindi hiki ni bora tuu kuifunga kwani mavumbi yanajaa ndani na kwa wenye miti inayododosha ukifagia ama kuokota baada ya nusu saa ni vululuvlulu kila mahali.
mti huu inaitwa Dodoma tree, huwa ni kijani kipindi chote cha mwaka. inadondosha majani machache mno hata pamoja na kisulisuli hiki.
Dodoma tree inafaa sana kuoteshwa eneo unalotaka lifunge na unaweza kuielekeza utakavyo. Kwa mfano unaweza kuikatia urefu fulani ili isiende juu zaidi au kuicha ikawa mikubwa kabisa, yote hayo ni wewe tu na jinsi roho yako ilivyopenda. Kama uko karibia na barabara vumbi, dodoma tree inasaidia kudaka vumbi lote na pia mizizi yake huwa ni midogo sana kiasi kwamba haipasui kuta nyufa. Ukiiotesha hutajuta, inapatikana kila mahali kwenye bustani za maua ila kuwa makini usibambikiwe. Ukishafanya hivyo urudi kunishukuru kwa desa!
mti huu inaitwa Dodoma tree, huwa ni kijani kipindi chote cha mwaka. inadondosha majani machache mno hata pamoja na kisulisuli hiki.
Dodoma tree inafaa sana kuoteshwa eneo unalotaka lifunge na unaweza kuielekeza utakavyo. Kwa mfano unaweza kuikatia urefu fulani ili isiende juu zaidi au kuicha ikawa mikubwa kabisa, yote hayo ni wewe tu na jinsi roho yako ilivyopenda. Kama uko karibia na barabara vumbi, dodoma tree inasaidia kudaka vumbi lote na pia mizizi yake huwa ni midogo sana kiasi kwamba haipasui kuta nyufa. Ukiiotesha hutajuta, inapatikana kila mahali kwenye bustani za maua ila kuwa makini usibambikiwe. Ukishafanya hivyo urudi kunishukuru kwa desa!
rafiki yangu wa ukweli apanda udzungwa
ha ha haaa...mambo ya schoo trip haya. Mwalimu wake ananiambia kajitahidi kupanda mlima kilomita 3 hadi Udzungwa falls! Akirudi kitambi chote kitakuwa kimeyeyuka nadhani...
Monday, July 7, 2014
vitu vizuri: vizulia vya katani
bibi Pili ni mtaalam wa kutengeneza vizulia vizuri mno vya katani. leo nimemtembelea nijionee namna vitu hivi vizuri vinavyotengenezwa na matumizi yake ndani ya nyumba. karibu msomaji ujionee...
| nikiianza safari |
| kizulia cha katani hicho bi Pili amekanyagia akitupa desa |
| vizulia vya rangi mbalimbali kwa ladha ya mteja |
| doormat ya mkonge hiyo...mwisho wa matumizi yake ni mwisho wa ubunifu wako |
| hii unaweza kuitumia kama bedside..ni mchanganyiko wa nyuzi za katani na za pamba |
| mwanzoni chote kinakuwa cheupe kwa ajili ndio rangi halisi ya katani. rangi watia baadaye ukipenda |
| hapa kizulia cha katani kimetumika kutengenezea mgongo wa kiti cha uvivu |
| kwenye karakana |
| nikajipatia kimoja nikakitupia jikoni kama hivi. nikiwa napika taratiibu miguu inatekenywa |
Thursday, July 3, 2014
my article for newspaper: kutandika kitanda
Jinsi ya kutandika kitanda ili kionekane nadhifu na maridadi
Linaweza kuonekana ni jambo rahisi
ila kufahamu mbinu za kutandika kitanda kionekane nadhifu na maridadi ni faida
ya kila mmoja iwe ni mtu wa umri mdogo au wa makamo na awe ni mwanaume au
mwanamke. Kuwa na kitanda kilichotandikwa vyema sio tu kinaonekana nadhifu,
bali pia unajisikia vizuri wakati ukifunua shuka kwa ajili ya kulala usiku.
Kitanda nadhifu kinaleta burudiko la moyo vilevile, kwa ajili kinaleta hisia ya
utulivu na muonekano wa kuwa na mapangilio chumbani. Kitanda kilichotandikwa
nadhifu pia, ni nadra kuanza kuhangaika kupanga shuka wakati wa kulala na hii inamaanisha
amani zaidi na muda mchache wa kupambana na shuka na blanketi.
Awali ya yote ondoa malazi yote (
shuka na blanketi au komfota) pamoja na mito kitandani. Chukua shuka safi
ambazo zinafiti ukubwa wa kitanda chako. Kama shuka zako ni zile za seti ya shuka
moja ya kufitisha (hii ni ile yenye mipira kwenye kona zake) na ya pili ni flati
(haina mipira), basi chukua hii ya mipira na ifitishe kwenye kona nne za
godoro. Shuka hizi za kufitisha zinarahisisha sana utandikaji wa kitanda hasa
kama saizi ya shuka na godoro ni sawasawa. Huna haja ya kunyoosha kusawazisha
mikunjo kwani huwa inajisawazisha yenyewe ukishavalisha kwenye kona za godoro.
Kama ni saizi sawa na godoro itafiti vizuri kabisa.
Baada ya hapo juu ya shuka ya kwanza
tandaza ya pili ambayo ni ile flati kwa jinsi ambayo upande wenye pindo kubwa
unakuwa kichwani na ule wa pindo dogo unakua miguuni. Hakikisha shuka hii inaning’inia
ukubwa sawa kwenye pande zote za kitanda ikifuatiwa na kuichomekea kwenye
godoro sehemu za miguuni wakati maeneo la kichawani na pembeni yakiachwa bila
kuchomekewa.
Tandaza blanketi juu ya shuka ya
flati ukilinyoosha vizuri kwa kadri unavyosogea. Ruhusu urefu kiasi wa blanketi
kwa ajili ya kuchomekea miguuni. Kunja blanketi eneo la kichwani ukiwa umelishikisha
pamoja na lile shuka la flati urefu wa saizi ya upana wa mto mkubwa wa
kitandani. Baada ya kukunja chomekea kwa pamoja blanketi na shuka kwenye pande
mbili ndefu za kitanda.Kama kitanda kinatumika kila siku utandikaji huu ni njia
rahisi kwa mlalaji kufunua upande anaopandia kitandani, shuka ya juu iliyokunjiwa
na blanketi na kuingia kitandani kulala. Ila kama kitanda husika hakitumiki
mara kwa mara, kwa mfano kama ni kitanda cha chumba cha mgeni unaweza
kufunika kwa kuchomekea kote kote na juu
yake kuweka kava la kuzuia vumbi hadi mgeni atakapotembelea.
Sasa basi endapo kitanda
tunachotandika ni kwa ajili ya matumizi ya kila siku njia ya kukunja shuka na
blanketi ni utandikaji utakaofaa zaidi. Eneo la kichwani mahali ambapo pamekunjiwa
blanketi, lile shuka la kufitisha litakuwa linaonekana kwa hivyo chukua mito na
weka juu yake. Huenda unahitaji mito
miwili tu kwa ajili ya kulalia, ila unaweza kuongeza mito kadhaa midogo midogo kama
mapambo kukipa kitanda mvuto.Unaweza kuweka mito mitano hadi sita kuendana na
ukubwa wa kitanda chako. Kanuni ya kuweka mito kitandani ni kuwa lile eneo la
kichwani lisibaki na uwazi wa ukubwa wa mto. Kwa maana ya kwamba kama kuna
uwazi wa kutosha mto uliobakia basi ongeza mto. Kwa mmoja namna hii ya utandikaji
inaweza kuwa mwisho na akajiridhisha kitanda kimekamilika na kina mvuto, ila
kwa mwingine anaweza kupenda kuongezea komfota.
Kwa hivyo kama wewe ni mmoja wa
wanaopenda kutandika komfota kitandani basi litandaze juu ya blanketi huku
ukilinyoosha vizuri kuondoa mikunjo yote inayoweza kutokeza. Huna haja ya
kuchomekea komfota na huwa lenyewe ni njia mojawapo ya kupamba kitanda – liache
tu likining’inia urefu unaolingana kwenye pande zote za kitanda na hapo kitanda
kinakuwa kimemalizika kutandikwa.
Kuna baadhi yetu ambao hatuoni
umuhimu wa shuka ya pili. Uzoefu wa kutumia shuka moja (ikiwa ni ile ya
kufitisha ni bora zaidi) na komfota pekee inafanya utandikaji wa kila siku wa
kitanda uwe rahisi, ila kiukweli ni kuwa hii shuka ya pili inaulinda mwili wa
mlalaji usikwaruzwe na ugumu wa blanketi au komfota na pia husaidia kuweka blanketi
au komfota safi na bila kusahau kuongezea mwili joto. Ni rahisi zaidi kufua
shuka mara kwa mara kuliko blanketi au komfota, na pia makava haya ya kitanda
yanadumu zaidi yakifuliwa mara chache.
Kutumia shuka ya flati ambayo ina
ukubwa wa kutosha inafanya kitanda kiwe rahisi kulalia na kutandika tena
asubuhi ya pili. Tumia shuka na blanketi zenye ukubwa wa kutosha kiasi kwamba
havitachomoka chomoka ukiwa umelala. Kama una blanketi dogo ni bora kulikunja na
kuliweka chini ya mito na ukawa unalikunjua na kujifunika wakati wa kulala tu
kwa maana ya kwamba wakati wa kutandika unalikunja kwani ukiamua kuchomekea blanketi
dogo litakusumbua kwa kuchomoka kila mara.
Zaidi ya kutandika safisha chumba
chako cha kulala ili kuonyesha zile juhudi zako za kutandika. Kitanda pekee
kikiwa maridadi ilhali sehemu ya chumba iliyobaki ni mrundikano unadhifu
hauwezi kuonekana. Kutandika kitanda kunakuwezesha kuanza siku yako vizuri na kunakufanya
ujiikie kuwa na mpandilio zaidi mapema mwa siku yako.
Makala hii imeandaliwa na Vivi
Machange ambaye ana mapenzi makubwa juu ya muonekano wa makazi na pia ni
mjasiriamali wa usafi wa magari, mazulia na nguo. Kwa maoni au maswali tuma
kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com
Tuesday, July 1, 2014
usiruhusu magugu kushamiri yaharibu bustani yako...
Subscribe to:
Posts (Atom)












