Friday, December 20, 2013

My article for newspaper: Meza ya chakula msimu wa sikukuu


Wakati wa sikukuu za mwisho wa mwaka uko karibu sana na kama wengi wetu walivyozoea ni wakati wa familia kukaa pamoja kwa ukaribu zaidi kwa kipindi walau kisichozidi wiki mbili. Kwa mfano baba mama na watoto hukutana pamoja na familia za watoto wao wakubwa ambapo huwa ni pamoja na wajukuu na kama Mungu amewaweka wazazi hawa huenda na vitukuu wakawepo. Pia ndugu jamaa na marafiki hutembelea na kusheherekea sikukuu pamoja. Sasa basi kwa vile wanafamilia ndani ya nyumba wanakuwa wengi inabidi kuwa na maandalizi ya mahali pa kulia chakula. Na mahali hapo ni kwenye chumba cha chakula. Kwa maana hiyo wakati huu chumba cha kulia chakula inabidi kiwe tayari kwa ajili ya familia na wageni watakaotembelea kukaa pamoja. 

Chumba cha chakula ni mahali ambapo patatumika kwa mlo wakati huo wote wa sikukuu.
Kwa kawaida mara nyingi milo ya kila siku familia huwa sio rasmi, isipokuwa wakati wa milo ya sikukuu maalum. Hata hivyo milo na wageni inaweza kukurusha roho wewe mwenye nyumba. Kwa maana hiyo maandalizi ni hayakwepeki kipindi hiki.

Kwa kuwa chumba cha kulia chakula kilicho rasmi kinaweza kisiwe burudani kwa milo ya kawaida, watu wengi wanapamba chumba hiki kwa kuwa na muonekano rasmi pale tu wanapokuwa na eneo la pili la kulia chakula. Lakini kama una chumba kimoja cha kulia chakula ambacho unategemea kwa ajili ya milo yote miwili yaani ile rasmi na isiyo rasmi bado unaweza kufurahia dunia zote hizi mbili.

Kwanza kabisa tuangalie muonekano halisi wa chumba cha kulala. Meza na viti vya kulia chakula ndio utambulisho rasmi wa chumba cha chakula. Meza hii yaweza kuwa ya umbo la duara, yai au pembe nne. Meza za umbo la yai na duara huwa sio rasmi sana kama zile za pembe nne. Najua msomaji ya kuwa unaona shughuli zote rasmi huwa meza zinazowekwa ni za pembe nne. Meza za duara na yai zinampa kila mtu uhuru sawa, na zinawezesha mazungumzo kirahisi kwa kila mmoja mezani wakati zile za pembe nne  ni rasmi zaidi na huwa zinawaweka wakaaji katika ngazi tofauti tofauti, kama vile eneo la mwenyeji au mgeni  rasmi na kadhalika. Andaa meza ya chakula ya ukubwa ambao utatosha wageni wako.

Kitamaduni, viti vya mikono vinatumika kwenye miisho ya meza za pembe nne. Viti visivyokuwa na mikono vinaruhusu upenyaji wa kirahisi. Andaa meza yako vyema kwa kuwa na kitambaa cha meza na kama kitambaa hicho kikiwa na rangi za msimu itakuwa bora zaidi. Tukumbuke kuwa rangi za msimu huu wa sikukuu ni nyekundu, nyeupe na kijani. Vesi ndogo ya maua hata kama ni kutoka kwenye bustani yako itaongeza mvuto. Kila wakati wa mlo hakikisha kuwa mezani kuna napkin hasa zile za kipambaa – zinatumika muda wote wa tukio kwa kufuta alama za vyakula, glasi baridi, matone na mengine mengi. Hizi za kitambaa ni nzuri zaidi kuliko zile za karatasi na hata ni rafiki zaidi kwa mazingira.

Andaa kuta na sakafu za chumba hiki kwa ajili ya ujio wa familia kubwa. Paka kuta zake rangi za kuvutia zitakazoongeza hamu ya kula chakula na kutengeneza sehemu ya kukaa na kuongea. Zulia sakafuni ni upendeleo wa mtu binafsi, wengine huona kuweka zulia chuni ya meza ya chakula ni changamoto hasa kama kuna watu wadogo ambao wanaweza kuwa wanadondosha vyakula wakati wa mlo. Hata hivyo kuna aina nyingi za mazulia ambazo ni rahisi kusafishika kwa dawa zilizopo na hivyo kufanya kazi ya usafishaji iwe rahisi na zulia kuonekana jipya kila wakati.

Chanzo cha mwanga kwenye chumba cha kulia chakula huwa ni ile taa maalum ya kwenye chumba cha chakula. Hata hivyo taa hii sio lazima iwe chanzo kikuu kama sio ya kuweza kurekebisha kiasi cha mwanga kwani wakati umekaa na wageni wako waweza kuhitaji kupunguza ukali wa mwanga. Kwa hiyo kama kuna taa nyingine za mwanga hafifu basi zitumie wakati huo ili kupunguza msongo wa mwanga mkali kwenye macho na pia kujenga mandhari yenye mvuto.

Fremu za picha za ukutani  sio muhimu chumba cha kulia chakula. Zile rangi maridadi za kuta zinatengeneza mvuto wa kutosha kwenye nyumba hasa kwa kuwa kitovu kitakuwa ni wageni walioko mezani.

Mwisho kabisa weka mazingira ya burudani wakati wa milo. Watu wanataka burudani kwa hivyo hawatapendelea kukaa muda wote kwenye viti vya meza ya chakala hasa pale kwenye tumazungumzo twa hapa na pale. Wanafamilia wengine wanaweza kukaa kwenye sofa ila hii haimaanishi kutofuata utaratibu wa wakati wa mlo pamoja. Mfanye kila mmoja wa wanafamilia wako afurahie kulia sikukuu ya kipindi hiki nyumbani kwako kwa kuweka mazingira ya starehe wakati wa mlo kwa jinsi itakupendeza wewe mwenyeji wao.

Makala hii imeandaliwa na Vivi O. Machange. Vivi ni mjasiriamali upande wa usafi wa magari, nguo na mazulia; pia ana mapenzi makubwa ya mitindo na mapambo ya nyumbani. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au viviobed@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment