Monday, June 27, 2016

Zijue faida na changamoto za paa la zege

Teknlojia inawapa fursa zaidi wanaojenga kuchagua aina ya paa wanalotaka kuezekea nyumba zao. Mhandisi David Sembuyagi anatujuza faida na changamoto za paa la zege.

Ingawa paa la zege linaweza kuwekwa kwa mitindo mbalimbali, kwenye makala haya tutaangalia paa la zege lililo flati.

Paa la zege ni mchanganyiko wa saruji, mchanga, kokoto na
maji kwa uwiano unaokubalika.
Hata hivyo paa la zege kwa Watanzania sio maarufu hasa kwenye nyumba za makazi.  Hii huenda ni kwa sababu wengi hawana uelewa juu ya paa hili na wengine wanaogopa gharama japo kiukweli hawajatafiti kujua gharama halisi na pia wapo ambao hawajashawishiwa kujua faida za paa la namna hii au kuona miundo yake mbalimbali ya kuvutia kuliko hata mapaa mengine kama ya  bati na vigae.

Hebu tuangalie faida na changamoto za paa la zege ili tulifahamu zaidi na kama unatarajia kujenga uweze kufanya uamuzi sahihi kwa kuona ni paa lipi linakufaa.

Faida namba moja ya paa la zege ni kuwa linadumu miaka mingi hadi miaka 50 hasa pale linapokuwa limewekwa vizuri. Halihitaji matengenezo ya mara kwa mara na linaondoa wasiwasi wa kushika moto.

Paa la zege haliwezi kuezuliwa na upepo ukilinganisha na paa la bati. Hii ni faida hasa kwa wale walio maeneo yanayokumbwa na upepo mkali kwenye majira fulani ya mwaka.

Ni rahisi kusafisha. Kupanda juu ya paa la zege na kusafisha kwa maji yenye msukumo mkubwa kuna usalama zaidi kuliko kwenye mapaa mengine kama yale ya vigae. Paa la zege haliharibiwi kwa kulikanyaga.  Ila changamoto ya paa la zege lililo flati ni kwamba linakusanya takataka zaidi hasa kama nyumba iko chini ya miti kulinganisha na mapaa mengine ambayo takataka zinateleza na kudondoka .

Paa la zege halisababishi joto ndani ya nyumba na pia mvua ikinyesha halipigi kelele.

Unaweza kutumia eneo la juu ya paa la zege kwa ajili ya matumizi mengine kama vile kukaa na kubarizi, na pia kuwekea matanki ya maji ya akiba.

Paa la zege linahitaji msingi na kuta za nyumba husika ziwe imara kwa vile zege ni zito sana kwahivyo vilivyo chini yake vinatakiwa kuwa na nguvu ya kulibeba.

Japo wanaojenga wamekuwa wakiogopa kuwa gharama za paa la zege ni kubwa, kiuhalisia inawezekana isiwe kweli. Kwani paa hili linajitosheleza, halihitaji malighafi nyingine zozote kama vile gypsum na nyinginezo za kupaulia. Kwahivyo utaona kwamba kwa malighafi za kisasa na kupaua ni kama vile gharama sawa na paa la zege.


Mawasiliano 0755 200023

No comments:

Post a Comment