Wednesday, July 1, 2015

INASIKITISHA JINSI MMILIKI WA SHULE ALIVYOUAWA....WAUAJI MBARONI

POLISI Kanda Maalumu ya Dar es Salaam inawashikilia watu watatu kwa tuhuma za kumuua mmiliki wa shule ya Mtakatifu Zion, Anna Mizingi (48) kisha kumtumbukiza katika shimo la choo cha shule hiyo.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Kamishna wa Kanda hiyo, Suleiman Kova alisema, Februari, mwaka huu mtoa taarifa alifika katika kituo cha Polisi na kueleza kuwa Mwalimu Anna aliondoka tangu Desemba 26, mwaka jana akiwa na mmoja wa watuhumiwa na hakuonekana tena.

Kutokana na taarifa hizo polisi walifungua jalada la uchunguzi, ambapo wakati wakiendelea na uchunguzi zilipatikana taarifa zilizosaidia kukamatwa kwa watuhumiwa hao huko Uchira Mawaleni, wilaya ya Moshi, Kilimanjaro.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa watuhumiwa hao walipokamatwa na kuhojiwa mmoja kati yao alikiri na kutoa maelezo kuwa siku ya tukio aliondoka na Anna kuelekea katika shule ya Mt Zion.

Kwamba walipofika shuleni hapo walivamiwa na watu wapatao wanne na kuanza kupigwa lakini yeye alifanikiwa kutoroka na kujificha katika uzio wa shule hiyo.

“Akiwa katika uzio huo aliwaona watu hao wakiendelea kumpiga Mwalimu Anna na kisha kumtupa katika shimo la choo. Baada ya kitendo hicho watu waliotenda uhalifu huo waliondoka na gari la Mwalimu Anna na kutokomea kusikojulikana,” ilieleza taarifa hiyo.

Kamanda Kova alisema, Juni 22, mwaka huu mabaki ya mwili wa marehemu yalipatikana eneo la Ununio baada ya Polisi kwa kushirikiana na kikosi cha Zimamoto kubomoa shimo la choo cha shule hiyo.

Aliwataja waliokamatwa kuwa ni Daniel Mkilindi (25) mganga wa kienyeji mkazi wa Uchira, Said Omary maarufu kama Said Ntimizi (34) mfanyabiashar ana mkazi wa Mbweni na Erick Mziray (40) mfanyabiashara mkazi wa Kurasini.

“Watuhumiwa hawa wanaendelea kuhojiwa ili kupata undani wa tukio hili, ikiwa ni pamoja na kuwatafuta na kuwakamata watuhumiwa wengine wanaohusiana na tukio hili. Mara baada ya uchunguzi kukamilika jalada la shauri hili litapelekwa kwa mwanasheria wa serikali kwa hatua zake za kisheria,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

HABARI LEO

No comments:

Post a Comment