Friday, July 10, 2015

Majina Matano CCM Ngoma bado Nzito


  • Mizengwe yatawala hadi usiku wa manane Kamati Kuu kufyeka waliodaiwa kuanza kampeni mapema.

Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imejikuta ikiwa katika kibarua kizito cha kuteua watia nia watano kati ya 38 wa nafasi ya urais mjini Dodoma jana usiku baada ya kuwapo kwa msuguano mkali juu ya watu wa kuwaondoa kwa tuhuma za kuanza kampeni mapema.
Taarifa kutoka chanzo kimoja cha uhakika ndani ya CCM kilieleza kwamba kulikuwa na mizengwe ya kuwapo kwa barua kutoka kwa vigogo wenye ushawishi mkubwa ndani ya chama hicho kushinikiza kuondolewa kwa baadhi ya wagombea kwa madai kuwa walianza kampeni mapema na hivyo kuhatarisha hatma ya ushiriki wa chama hicho katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu.

Hali hiyo inaelezwa kwamba ndiyo kigezo ambacho wajumbe wa Kamati Kuu waliokutana kwenye ofisi moja nyeti mjini Dodoma waliendelea kuishikilia kwa lengo la kuwaondoa wagombea wenye dosari hizo.

Kwa mujibu wa chanzo hicho, baadhi ya wajumbe walikuwa kwenye mjadala mkali kutokana na hofu kuwa wakiteuliwa watia nia walioanza kampeni mapema watakiweka chama chao katika hatari ya kuwa na mgombea aliyepoteza sifa kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi mkuu zinazosimamiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

Hadi kufikia mishale ya saa 7:31 usiku hakukuwa na taarifa zozote za matokeo ya majina matano yaliyopitishwa na Kamati Kuu kati ya 38 ya waliorejesha fomu ili yapelekwe kwenye kikao cha Nec kwa mchujo zaidi ili wabaki wanafainali watatu.

USIRI MKUBWA  WATAWALA                                          
Kama ilivyotarajiwa, kikao hicho cha Kamati Kuu, kilifanyika kwa usiri mkubwa kiasi cha kuwafanya waandishi wa habari kuwa na wakati mgumu kupata taarifa zilizokuwa zikiendelea ndani yake.

Awali kabla ya Kamati Kuu ya chama hicho kukutana kwa kazi hiyo, siri nzito ilitenda juu ya maamuzi yaliyofanywa na kikao cha Kamati ya Usalama na Maadili ya CCM kilichoketi juzi usiku chini ya Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Kikwete. Kikao hicho cha Kamati ya Usalama na Maadili ya CCM, kilikaa kupitia mafaili ya wagombea 38, waliorejesha fomu za kuomba kuteuliwa na chama hicho kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Kabla ya kikao cha Kamati Kuu, Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alipotafutwa na NIPASHE jana kwa njia ya simu kutoa ufafanuzi iwapo kikao cha Kamati ya Usalama na Maadili kilifanyika kama ilivyokuwa imepangwa awali, alisema: “Nianze na hili la Kamati Kuu (CC), mimi pia sijui kinafanyika wapi na saa ngapi. Halafu hata hicho kikao cha Kamati ya Usalama na Maadili unachoniuliza hapa; hakikufanyika.”

Kabla ya Rais Kikwete kuongoza Kikao cha Kamati Kuu kwa ajili ya kufyeka majina 33 ya wagombea wanaoomba kuteuliwa kuwania kiti cha urais na kubaki matano; alifanya kazi kubwa mbili katika siku ya jana, ikiwamo kuzindua jengo jipya na la kisasa la CCM, maarufu kama Dodoma Convention Centre na baadaye jioni kwenda kulivunja Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Jumla ya makada 42 wa CCM walichukua fomu kwa ajili kuomba ridhaa kwa chama hicho kiwateue kuwania urais.
Hata hivyo, kati hao 42, makada 38 ndiyo waliorejesha fomu huku wanne `wakiingia mitini' na fomu hizo.

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment