Wednesday, December 30, 2015

MIKAKATI 8 YA KUISHI PASAFI 2016

Mara baada ya sikukuu za mwisho wa mwaka kuanza kumalizika na mapambo yake kuanza kuondolewa ni wakati wa kuweka mikakati ya namna ya kuishi mahali pasafi kwa mwaka huu mpya. 

Na sio jambo la kushangaza kuwa wengi wanaweka mikakati ya mwaka mpya kwahivyo bila shaka moja ya hiyo ni kuhusu mahali unapoishi. Hii ni mikakati ya kukuwezesha kusafisha na kutunza mazingira ya nyumbani kwa mwaka 2016. Jitahidi ufanikiwe katika hili.

1. Tenga fungu kwa ajili ya usafi na matunzo ya nyumba. Bila shaka maisha  ni magumu na wengi wanafikiria mbinu mbalimbali za kubana matumizi, na hili halina ubishi hata kwa nyumbani. Pamoja na hayo ni vyema tukumbuke kuwa mazingira safi kwa ubora wa afya zetu ni kipaumbele namba moja. Unaweza kutumia njia mbalimbali za kuwa katika mazingira mazuri ya nyumbani kwa kubana matumizi, na mojawapo ni kufanya mambo kadha wa kadha bila kumuita fundi au nguvukazi ambayo itaongeza gharama. Kwa mfano, wanafamilia wanaweza kushiriki kutunza bustani na maua bila kuhusisha mtunza bustani wa nje. 

Pia unaweza kuweka majani ya kuhifadhi unvevu kwenye bustani yako ya maua na kukufanya uwe na matumizi kidogo ya kumwagilia. Kwa upande wa kusafisha kama vile vyombo, kutumia maji ya uvuguvugu kutapunguza matumizi makubwa ya sabuni kwahivyo unakuwa umeshabana matumizi. Tumia sabuni za kusafishia ambazo zina matumizi zaidi ya moja na tunza vizuri vifaa vya usafi.

2. Jifunze kusafisha haraka zaidi. Ni watu wachache dunia hii ambao wanapenda kutumia muda mwingi kusafisha nyumba zao. Kwa wengi wetu ambao tuna majukumu mengi ambayo ni lazima tuyakamilishe kwa siku, kujifunza kusafisha haraka haraka ni mkakati mzuri. Ili ufanikiwe katika kusafisha kwa haraka hakikisha unahifadhi vifaa vyako vya usafi eneo moja. Haifai unataka kudeki huku unaanza kutafuta dekio na kukasirika hulioni kiasi kwamba hata ari ya usafi inaondoka. Pia anza na eneo ambalo sio chafu sana na usipoteze muda kusafisha sehemu ambayo sio chafu. Kwa mfano umesafisha jokofu wiki iliyopita basi wiki hii usihangaike kusafisha tena. Kuepuka kurudia rudia safisha kuanzia juu kushuka chini.

3. Epuka mrundikano. Nyumba iliyovurugwa inahitaji kitu zaidi ya usafi. Kuwa na mkakati wa kupunguza vitu ndani ya nyumba yako ili kuepuka  mrundikano. Kuondoa mrundikano ni njia kuu ya kukufanya uweze kusafisha kwa haraka bila kupoteza muda. Nyumba isiyokuwa na mrundikano ni rahisi kusafisha kuliko ya kinyume chake.

4. Kuwa na mpangilio. Mara mrundikano unapoondioka, hatua nyingine kubwa inayofuata ni kupanga vizuri vitu vilivyobakia. Mara kila kitu kinapokuwa na makao yake ndani ya nyumba yako mrundikano unakuwa sio hoja tena na kusafisha kunarahisishwa.

5. Andaa ratiba ya kusafisha. Kila dakika kuna kitu cha kusafisha, lakini huwezi kusafisha kila dakika. Kuwa na ratiba ya usafi kunawezesha urahisi wa kusafisha kwa siku, kwa juma na kwa mwezi. Ratiba ya kusafisha ina faida ya kuu kuwa hupotezi muda wako kusafisha vitu ambavyo haviko kwenye ratiba ya kusafisha siku hiyo.

6. Hamasika zaidi kusafisha. Kuna wakati hamasa ndio kitu kinakosekana kwenye utunzaji wa nyumba zetu. Sio rahisi kila wakati kuhamasika kusafisha, lakini kuna vitu rahisi ambavyo vinaweza kukuhamasisha. Hamasa ya kusafisha inafanya usafi uende haraka. Tafuta hamasa inayokufanya usafishe, labda unataka upige picha baada ya kusafisha au unataka uache nyumba safi au unapenda ugeni wa mara kwa mara, au ni kujaribu sabuni mpya ya kusafishia au ni kupanga upya chumbani na kadhalika.

7. Shirikisha wana familia wote kwenye kusafisha. Kugawa majukumu ya kusafisha hata kwa wale wanafamilia wadogo kabisa ni mkakati mzuri wa kufanya mazingira ya nyumbani yawe masafi. Mtu anaposafisha anaelewa ugumu wake kwahivyo hata kuchafua anapata ukakasi. Na kwa wale wanaoweza kusafisha vizuri wanasaidia zoezi zima limalizike kwa uzuri na haraka.

8. Nyumba safi ni pamoja na kufanya ukarabati. Hakikisha pale panapohitaji ukarabati panarekebishwa mapema iwezekanavyo.


Na wewe msomaji wangu nishirikishe mikakati unayotumia kuhakikisha unaishi mahali pasafi. Nijulishe kwa simu/whatsapp 0755 200023

No comments:

Post a Comment