Wednesday, December 16, 2015

ZINGATIA HAYA PAZIA ZAKO ZIVUTIE

Kuwa na pazia zinazovutia inaweza kuwa changamoto.Kuna mambo mengi unayopaswa kuzingatia kuhakikisha kwamba pazia husika zinaoana na rangi na mapambo ya chumba chako na mpangilio wake. Baadhi ya mambo hayo ni haya yafuatayo:

·       Kwanza kabisa weka pembeni suala la muonekano kwani lengo namba moja la pazia ni kufunika dirisha. Kwa sehemu kubwa lengo hili ndilo litakubana kwa njia nzuri unapochagua pazia zako. Kama unataka pazia zinazoleta faragha au giza kabisa, unatakiwa kuwa na pazia zenye kitambaa cha pili (lining) kwa ndani. Kitambaa hiki kitaongeza gharama lakina kina faida nyingi kama vile: kuzuia kile kitambaa cha nje cha pazia (ambacho ndio maridadi) kisiharibiwe na jua na hivyo kudumu muda mrefu. Kitambaa cha ndani pia kinaongeza uzito wa pazia na hivyo kulifanya limwagike vizuri na kutulia bila kuhamahama hata kama umewasha pangaboi. Na vilevile lining linafanya pazia kuonekana la kifahari. Pazia za hivi nyingi ni za kushonesha, huzikuti zikiwa zimeshonwa tayari.

Ni vizuri ifahamike kuwa pazia zinaweza kutofautiana kimatumizi kati ya chumba na chumba. Kwa mfano kwenye chumba cha chakula pazia zinaweza kuwa na lengo la kimuonekano zaidi, ikimaanisha nyembamba, nyepesi na zenye urembo mwingi wa matobotobo. Kama unalala chumba ambacho kina dirisha linalopokea mwanga mwingi wa asubuhi, pazia zenye rangi za giza zitakusaidia kuzuia jua na kuongeza muda zaidi wa kulala siku za mwishoni mwa wiki bila jua kukusumbua wakati umelala.

·       Zingatia rangi za pazia unazotaka kununua ukilinganisha na mapambo mengine ya ndani. Kwa mapambo ya ndani rangi ya pazia ikiwa ya giza kuliko ile ya ukuta inafanya chumba kipendeze zaidi. Kwa mfano kama ukuta una rangi ya bluu iliyofifia basi pazia ziwe na bluu iliyokolea. Pia ukichagua rangi ya pazia ambayo haijashamiri kwenye rangi nyingine zilizoko hapo chumbani huwa  chumba kinaleta mvuto zaidi. Ile rangi ya kipekee (iliyokolea tofauti na nyingine zote) ya pazia inaleta mshtuko wa uzuri.
·       Urefu wa pazia. Pazia la kufika sakafuni ndio sahihi, vinginevyo kuwe na sababu ya kipekee. Na uzuri pazia nyingi zilizoshonwa tayari zinakidhi urefu huu. Kama unanunua kwa mita pima kutoka sakafuni hadi kwenye fimbo utakayotundikia pazia. Kama linazidi kumwagika sakafuni ni bora kulipunguza kwa sindano ya mkono kuliko pazia fupi.

·       Pazia liwe pana kiasi gani? Ili pazia liwe na marinda na limwagike vizuri linatakiwa kuwa na upana mara mbili hadi mbili na nusu zaidi ya upana wa dirisha. Isipokuwa kama unaweka pazia kwa ajili tu ya kufunika dirisha basi hata upana wa zaidi ya mara moja na nusu ya dirisha utafaa. Pazia pana lililojaa marinda ndio halali ya dirisha.

·       Umbali wa kutundika pazia toka juu ya dirisha uwe wa kutosha. Angalao kuwe na inchi 4 hadi 6kutoka kwenye dirisha hadi pale pazia lilipoanzia. Lakini vilevile lisikabe dari. Kwahiyo kumbuka kuhesabia urefu huu wa ziada wakati unaponunua au kushonesha.

·       Kuhusu muonekano wa juu linakoanzia pazia. Kwenye ule ukanda wa juu kabisa wa pazia ndiko kunasemea uzuri wa pazia zima. Ingekuwa pazia ni mwanamke hapa ndipo tungesema ni uso wa pazia. Marinda, vyuma na kulabu katika eneo hili zinatakiwa kukaa vizuri maridadi na katika umbali wa kulingana. Hapa ndipo panafanya ufunguzi na ufungwaji wa pazia uwe rahisi au mgumu.

·       Pazia linapotundikwa. Je, linatundikwa kwenye boksi ama fimbo za pazia. Na je likifunguliwa linafungwa kwa tai au linajiachia lenyewe? Yote haya unatakiwa kuyafahamu kabla hujaanza huo mradi kwa kufunga pazia. Na je tai ni zile zimejengewa ukutani au ni zile za vitambaa? Unapaswa kufahamu yote haya ili pazia zikidhi malengo ha wakati huohuo  zikionekana maridadi.

Makala hii imeandaliwa na Vivi.
Je, unauza bidhaa au huduma inayohusu nyumba na bustani ambayo unataka Watanzania waijue? Nijulishe simu/whatsapp 0755200023. www.vivimachange.blogspot.com


No comments:

Post a Comment