Friday, March 27, 2015

MKE WA SUMAYE, ESTER SUMAYE KUNYANG'ANYWA MASHAMBA.............YADAIWA NI BAADA YA KUSHINDWA KUYAENDELEZA

WAZIRI MKUU WA ZAMANI, FREDRICK SUMAYE
Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha, mkoani Pwani, imewataja vigogo wanaohodhi maeneo makubwa ya ardhi bila ya kuyaendeleza na kuwapa siku 90 kuhakikisha  wanayaendeleza, kinyume chake yatachukuliwa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya  Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Tatu Suleiman, ilisema vigogo hao walinunua mashamba katika eneo hilo na kisha kuyaacha kwa muda mrefu bila kuyaendeleza akiwamo mke wa Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye, Mama Ester Sumaye ambaye
anamiliki mashamba mawili, moja likiwa na ukubwa ekari 145.5 likiwa na namba 6069 na 6070 na shamba la pili lenye ukubwa wa ekari 103. 25 likiwa na namba 6071 na 6075, yote yakiwa Misufini, Kibaha vijijini.

Taarifa hiyo inawataja watu wengine maarufu ambao wameshindwa kuyaendeleza mashamba hayo kuwa ni,  Phillipo Marmo ambaye ni Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani anayemiliki shamba 6159-6164 maeneo ya Kikongo, Nicodemus Banduka ambaye ni mkuu wa mkoa mstaafu wa mikoa ya Pwani, Iringa na Mtwara anaye miliki shamba namba 1707 eneo la Vikuge ambalo alilipata mwaka 2,000 na  Kipi Warioba aliyewahi kuteuliwa kugombea Ubunge Jimbo la Kawe ambaye anamiliki eneo Mperamumbi lenye ukubwa wa heka 4000.

Taarifa hiyo inaonyesha kuwa, watu wengi walichukua mashamba katika eneo hilo kuanzia miaka ya 1986 na kushindwa kuyaendeleza na kusababisha kuwa mapori hali iliyopelekea halmashauri hiyo kufuata sheria na kanuni zinazohusiana na umiliki wa ardhi.

Kufuatia mashamba hayo kutelekezwa, halmashuri ya wilaya hiyo inapanga kuwasilisha taarifa hiyo kwa wizara husika ili miliki zake zifutwe endapo wahusika watashindwa kuyaendeleza     kwa    muda   waliopewa.

Tatu, alisema mwaka jana waliwataka watu wote waliochukua mashamba hayo kuyaendeleza baada ya kufanyiwa uhakiki na baadhi ya watu walijitokeza kuyaendeleza, lakini watu zaidi ya 40 hawajitokeza.

“Kutokana na kukahidi kuyaendeleza mashamba hayo, tumeshapeleka majina  ya wamiliki Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi  na wizara  imetutaka tutoe tena siku 90 kama hawatatekeleza kwa kipindi hicho, watajua nini cha kufanya,’’ alisema.

Gazeti hili lilipowasiliana na Waziri Mkuu wa zamani, Sumaye kwa njia ya simu ili kuzungumzia taarifa za mkewe kushindwa kuyaendeleza mashamba hayo kwa kipindi kirefu, alisema hana taarifa zozote za mkewe kushindwa kuyaendeleza mashamba hayo anayomiliki.


‘‘Wewe ndiyo nakusikia, sisi hatujaliona hilo tangazo, wala mke wangu hana hizo taarifa ila baadaye tutakapoziona tutakupigia simu tuwasiliane,’’ alisema Sumaye. 
CHANZO NIPASHE

No comments:

Post a Comment