Tuesday, March 31, 2015

GWAJIMA AONGEA.......ASEMA ALIAGIZA BASTOLA KUJILINDA PALE HOSPITALINI

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda (kushoto) akizungumza na Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima,
Josephat Gwajima alipokwenda kumjulia hali katika Hospitali ya TMJ, Dar es Salaam jana.
 
Kauli ya Gwajima

Akizungumza kwa shida akiwa amejishika tumbo, Gwajima alisema alipopata taarifa za uvumi kwenye mitandao ya kijamii kuwa amefariki dunia, aliagiza wachungaji waende hospitalini kwa ajili ya kumlinda, lakini wakaishia mikononi mwa polisi wakidaiwa kutaka kumtorosha.

Alisema alihofia kuwapo kwa watu wabaya ambao wangeweza kumdhuru halafu wakasingizia kitendo hicho kufanywa na polisi kwa kuwa alipata tatizo akiwa mikononi mwao.

“Usiku wasiwasi ulizidi, huku kila mmoja akiwa hafahamu kwa nini ujumbe wa namna ile unasambazwa kwenye mitandao, msambazaji ni nani, ana nia gani, nikaamua kuwaagiza waniletee silaha yangu iliyokuwa kwenye begi ili likitokea lolote niweze kujilinda,” alisema Gwajima.

Alisema alishangaa kukamatwa wachungaji wake na kuchukua silaha iliyokuwa ndani ya begi na hadi jana hakuwa ameulizwa chochote kuhusu umiliki wa silaha hiyo.

“Kabla sijazungumza na waandishi kueleza ukweli wa kinachodaiwa kuwa nilitaka kutoroshwa na wachungaji wangu, nilitaka kuzungumza na ZCO (Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu), lakini hajaja, kadi ya ile silaha ninayo,” alisema Gwajima.

Alisema madai kuwa alitaka kutoroka ilihali polisi alikwenda mwenyewe akitokea Arusha baada ya kusoma katika vyombo vya habari kuwa anatafutwa.

Alifafanua kuwa hata alipofika polisi kwa ajili ya mahojiano hakuwa na shaka hata kidogo, lakini alishangaa kuona anaishiwa nguvu kila baada ya muda na alipoona kichwa kinamuuma, akawaomba wampeleke hospitali ili mambo mengine yafuate baadaye, kitu ambacho hakikufanyika kwa wakati.

Makonda amtembelea

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda ambaye alikuwa amemwandikia Gwajima barua akimwita ofisi kwake, jana mchana alimtembelea hospitalini hapo kwa ajili ya kumjulia hali kiongozi huyo lakini akasisitiza kuwa nia yake bado ipo palepale.

“Nilimtaka leo aripoti ofisini kwangu lakini kwa bahati mbaya anaugua na amelazwa. Nitakwenda kumuona ili nijue hali yake ikoje,” alisema Makonda kabla ya kufunga safari kwenda hospitali alikolazwa.

Alisema pia atataka kiongozi huyo wa kiroho amweleze anavyoelewa maana ya uhuru wa kuabudu unaoelezwa katika Katiba, usajili wa taasisi yake na katiba ya taasisi hiyo. “Mimi ni mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kinondoni. Niliagiza polisi wamkamate na baadaye wakimaliza kumhoji aje kwangu pia atahojiwa na jopo la watu 20,” alisema Makonda.

Maaskofu wahoji mambo manne

Wakati huohuo; maaskofu na wachungaji kutoka makanisa mbalimbali wametoa tamko wakihoji maswali matatu kuhusu tukio lililompata Askofu Gwajima.

Akitoa tamko hilo, Askofu wa Kanisa la Pentekoste Agizo Kuu, Dk Mgullu Kilimba alisema wanajiuliza ilikuwaje Gwajima aende akiwa mzima atoke akiwa mahututi?

“Tumeshindwa kuelewa nini kimempata mwenzetu huyu. Tunajiuliza je, vyombo vya usalama vimekuwa siyo sehemu salama kama zamani?” alihoji.
Kuhusu tuhuma za kutoroshwa kwa Gwajima, maaskofu hao wamehoji: “Kama alikuwa anaona ugumu wa kutoroka akiwa mwenye afya tele, itakuwaje rahisi kutoroshwa akiwa mahututi na kwenye ulinzi mkali wa polisi?”

Pia walihoji kuhusu mlalamikaji wa kesi dhidi ya Gwajima aliyetajwa kwa jina la Aboubakar,  wakisema si mtu sahihi kwa sababu hawezi kuonyesha ameumizwa kiasi gani na matamshi ya Gwajima. Hata hivyo, Kova alisema hawamtambui mtu huyo wala hajui lolote kuhusiana na mlalamikaji huyo aliyetajwa.


Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment