Tuesday, January 5, 2016

KUTOKA KWANGU:.... Mwelekeo wa Mapambo ya Ndani kwa Mwaka Huu

Nimetafiti maeneo mbalimbali na kuongea na wadau kuhusu mwelekeo wa mapambo ya nyumbani utakavyokuwa 2016 kwa nyumba za Watanzania walio wadau wa mapambo ya nyumbani. Kuna mawazo mengi ya nini kitashamiri mwaka huu, na kwa hivyo si rahisi kuorodhesha kila kitu na kwahivyo nimekuwekea maeneo 6 kuonyesha mwelekeo utakavyokuwa.

Karatasi za ukutani yaani wallpaper – Kwa mwaka 2015 karatasi hizi zimekuwa kivutio sana na  hasa zile zenye michoro ya mawe ya mtoni na vitofalitofali.  Pamoja na kwamba michoro hii imevuma sana kwa mwaka jana, mwaka huu inaelekea wallpaper za maua za aina ya 3D ndio zitashika kasi. Hii ni kwa ajili wenye nyumba wengi wameshaanza kuwa na wasiwasi kwamba hizi mbili za 2015 ziko walau kwenye kila nyumba yenye wallpaper.


Kuepuka mimea kugusana na nyumba - Wengi wa wadau wa eneo hili wanabainisha kuwa bustani za kushikana na ukuta wa nyumba zinaenda kupotea kuanzia mwaka huu na kuendelea. Hii ni kwa  vile wenye nyumba wa kisasa wamegundua bustani hizi zinachangia kuchafua na kuozesha eneo la chini la ukuta wa nyumba. Badala yake sasa, ukanda huu wa kuzunguka nyumba umetengwa kama kawaida ila badala ya kuoteshwa mimea na maua unawekwa vitu kama mawe meupe ya mapambo ama wapo wanaoweka vigae na wengine wanaweka marumaru za nje. Wachache bado wanaweka maua ila ni ya kwenye vyungu vichache vilivyo mbalimbali. Vyungu hivi vimewekwa juu ya sakafu ngumu na kwa mantiki hiyo hakuna udongo unaogusana na ukuta.

Meza za marble kuzidi kushamiri -  Meza za marble hasa zile za chakula zilianza kushika kasi toka mwaka jana na mwaka huu kasi yake inaongezeka. Hii imechangiwa na uimara wake na kuwa za gharama nafuu na urahisi wa kusafisha na kuzitunza. Vilevile meza hizi ni ndogo ambapo zimewavutia wengi ambao hawana eneo kubwa la kulia chakula. Na hata wale wenye eneo kubwa bado wamevutiwa kwakuwa wanataka sehemu ya nyongeza ya kuweka kabati la vyombo kwenye chumba cha chakula. Kupanda sana kwa gharama ya mbao ngumu nayo ni sababu ya meza za marble kushika kasi.

Hitaji la vitanda vya chuma kuongezeka – Vitanda vya chuma na baadhi ya fenicha nyingine za chuma zina mwelekeo wa kushika kasi sana mwaka huu. Vitanda hivi vimekuwa mkombozi wa karibia kila mtu kuanzia vijana waliotoka vyuoni wanaoanza maisha hadi familia changa. Sababu ni zilezile kuwa ni imara, bei nafuu na utunzani usiokuwa na changamoto nyingi.

Marumaru za mapambo – Kama tujuavyo sakafu za marimaru zimejipatia umaarufu kwa nyumba za watanzania walio wengi wenye uwezo wa kuzinunua. Tegemea kuona marumaru zenye maua kwa wingi ambapo nyingine zinabuniwa kama vile ukiona kwa mbali utafikiri ni zulia lakini ukikanyaga kumbe ni marumaru. Mwaka huu kutakuwa na ongezeko la marumaru za maua hasa kwenye sakafu za sebuleni.

Vitendea kazi jikoni  -  Mwaka huu tegemea vitendea kazi vingi vya jikoni kuongezeka. Licha ya kipasha na kisaga chakula, maisha ya jikoni yanazidi kurahisishwa kwa vitendea kazi vipya mbalimbali kama vile kitendea kazi cha kuchanganya na kukanda unga wa chapati na maandazi, kitendea kazi cha kusaga vitunguu swaumu, kitendea kazi cha kuchoma mahindi, mishikaki na kadhalika
Naamini maelezo haya yamekupa mwelekeo wa baadhi ya mapambo ya nyumbani kwa mwaka huu mpya wa 2016.

Vivi ni mshauri wa mapambo ya nyumba na bustani. Kwa maswali au maoni piga/whatsapp 0755200023


No comments:

Post a Comment