Sunday, January 17, 2016

KUTOKA KWANGU:...ILI KUPATA FUNDI RANGI MZURI FANYA HIVI..

Sehemu kubwa ya uzuri wa muonekano wa nyumba ni rangi yake. Haijalishi ukubwa wa eneo unalotaka kupaka rangi bali kupata fundi sahihi itaokoa muda, nguvu na pesa zako kwa kipindi kirefu kitakachofuata.

Nimeongea na Mkandarasi Kassim Ally na amesema kabla hujampa kazi ya kupaka rangi fundi au mkandarasi anayekidhi vigezo vyako, hakikisha yafuatayo:

·        Uzoefu. Ni muda gani
fundi huyo amekuwa katika kazi hiyo? Hakikisha kuwa unampa kazi fundi ambaye ameshakuwa kwenye kazi hiyo kwa miaka miwili na zaidi.
·        Wafanyakazi. Je huyo fundi/mkandarasi unayetaka kumpa hiyo kazi ana wafanyakazi wake? Kazi ya  kupaka ukuta rangi inahitaji hatua nyingi za maandalizi ya ukuta kabla ya rangi ya mwisho kwahivyo inahitaji nguvu kazi kubwa na ifanyike kwa muda mfupi ili kuepuka madhara yoyote yanayoweza kutokea kwa mfano ujio wa mvua na kadhalika.
·        Leseni. Ni vyema kuhakikisha fundi unayetaka kumuajiri kwa ajili ya kazi yako ya rangi ana leseni ya kazi hiyo. Hii ni muhimu sana hasa pale itakapotokea ajali kwa mfano mfanyakazi wake anaweza kuanguka na kuumia vibaya au hata kusababisha kifo kama ameanguka toka juu jingo refu. Leseni itamlinda yeye na wewe kisheria kwani kazi inafanyikia kwenye eneo lako.
·        Rufaa: Fundi rangi unayemtaka anaweza kukupa orodha ya watu kadhaa alowafanyia kazi ya rangi kabla? Wapigie na hata ikiwezekana watembelee ongea nao na angalia kazi fundi husika aliyofanya kabla hujaamua kumpa fundi huyo kazi yako.
·        Taaluma: Je fundi husika anaweza kupendekeza ni malighafi zipi zitafaa zaidi kwa ajili ya kazi yako? Awe ni mtaalam anayeenda na wakati, anayejua ni rangi na teknolojia gani mpya zaidi iliyopo sokoni kwa wakati huo. Ashauri rangi na nakshi mbalimbali. Uzoefu hapa unahusika.
·        Makadirio rasmi. Hakikisha fundi unayetaka kumpa kazi anaweza kukupa makadirio ya muda na vifaa vyote vinavyohitajika vikiwa kwenye maandishi.
·        Garantii. Mbali na garantii zinazotolewa na viwanda vya rangi, fundi rangi anatakiwa aweze kukupa garantii ya kazi yake. Maana yake ni nini? Ni kwamba fundi atapaka rangi kipindi cha kiangazi, anamaliza kazi yake na inaonekana kuvutia kabisa machoni. Lakini mvua zikianza mwezi mmoja au wiki kadhaa baadaye unaweza kushangaa ukuta wa nje ulioloa maji ya mvua rangi yake inavimba malengelenge na inabanduka eneo kubwa. Sasa hapo sababu inaweza kuwa huenda fundi hakusimamia wafanyakazi wake vizuri na kwa hivyo wakapaka rangi ukuta wenye vumbi. Ama wakati wa kuchanganya malighafi zinazohitajika vipimo havikuzingatiwa matokeo yake rangi inabanduka chini ya mwezi mmoja. Kwa swala kama hili ndipo tunaposema ni vyema kuwa na fundi mwenye uwezo wa kugarantii kazi yake hata kama ni kwa miezi mitatu tu.
·        Gharama. Kwa asili, gharama ni swala linalotiliwa mkazo kwenye kazi nyingi. Kupata fundi wa bei nafuu kisiwe ni kigezo chako namba moja. Unataka kupata fundi mwenye ujuzi, uzoefu, leseni, makini kwenye swala la usalama na mchapa kazi. Ni ukweli kuwa mtu wa hivi hatakuwa wa bei chee. Na hatahivyo hatakiwi kuwa wa gharama ya juu zaidi kwamba eti ndio atafanya kazi nzuri. Cha muhimu tu hakikisha haumpi fundi rangi kazi kwa kuangalia bei yake.  Tafuta gharama za mafundi watatu tofauti ili ulinganishe.
Angalia picha nzima, inasikitisha kusikia mwenye nyumba anampa kazi saidia fundi. Rahisi ni gharama.

Msomaji wangu kama ulishawahi kusimamia kazi ya kupaka rangi nirushie picha tuone nyumba ilivyopendeza na tuambie ulimpataje fundi. Ukishea ujuzi unajisikia vizuri, kila tunachofahamu leo kuna mtu wa mwanzo alishea..Nawe karibu ushee na sisi..Piga/Whatsapp 0755 200023


No comments:

Post a Comment