Wednesday, January 6, 2016

KUTOKA KWANGU:...Hatua 8 za Kuondoa Mrundikano Katika Chumba Chochote

                          
1.     Weka malengo
Malengo ni muhimu kwani yanatufanya tushikilie kwenye fikra zetu kile tunachotaka kukamilisha. Malengo yako ya kuondoa mrundikano ni binafsi, lakini yanaweza kuwa katika mfumo wa sentensi kama hivi. Nitaondoa mrundikano na kuweka mpangilio kwenye chumba changu cha kulala ili iwe rahisi kupata kitu na  kiwe nadhifu kukitazama. Au nitaondoa mrundikano kwenye kabati langu la nguo ili iwe rahisi kujua ni zipi za kugawa. Au nitakunja nguo zangu
vizuri ili zisiporomoke zote pale ninapochukua moja. Umuhimu wa malengo ni ile sehemu ya kusema unaenda kufanya nini na kwa nini. Kumbuka kuchukua picha kabla hujaanza malengo yako ya kuondoa mrundikano mahali au chumba fulani.

2.  Weka vifaa vyako pamoja
 Vifaa vya kuondoa mrundikano ni vya kawaida. Unahitaji vikusanyio vinne ambapo mchanganuo wake ni kikusanyio cha uchafu, cha vitu vya kugawa au kuuza, cha vitu vya kuhifadhi na cha vitu vya kuweka mbali. Unaweza kuweka majina kwenye vikusanyio hivi na vinaweza kuwa mifuko, maboksi, matenga au chochote kile kitakachokuwezesha kutenganisha mafungu haya manne ya vitu. Hivi ndio vifaa pekee ambavyo unahitaji.

3.  Chagua chumba au eneo
 Sasa ni wakati wa kuchagua chumba au eneo la kuanza kufanyia zoezi lako la kuondoa mrundikano. Unayeijua nyumba yako zaidi ni wewe. Kama hujawahi tena kufanya zoezi hili, chumba kizima kinaweza kukuwia ngumu. Chagua eneo moja, kwa mfano kama umeamua wiki hii unaondoa mrundikano jikoni, basi jumatatu  anza na droo za vijiko, uma na visu. Weka jumanne kiporo kwa ajili ya masufuria na vikaangio. Endelea jumatano na vikontena. Endelea kidogokidogo na maeneo mengine na hadi umalize wiki jiko lote linakuwa limekamilika.

4.  Tafuta Muda
Inaweza kuwa ngumu kupata muda. Kila mtu ana pilika. Kupanga muda wa kuondoa mrundikano ndani ya nyumba kuna wakati inahusisha hata kujua muda  wa wanafamilia wengine. Kwa mfano, huwezi kufanya zoezi la kuondoa mrundikano ukiwa na mtoto mdogo kabisa kwani atakuwa na kazi ya kusambaza upya vitu ulivyotenganisha. Wakati mzuri ni akiwa amelala au vinginevyo kuwe na dada anamwangalia na kaka naye eneo la mbali na unapofanyia zoezi lako. Kama unafanya kazi siku tano kwa wiki basi siku za mwisho wa wiki zinaweza kukufaa zaidi kwa zoezi hili. Unaweza kupanga siku nzima maalum kila baada ya miezi michache kwa ajili ya kuondoa mrundikano. Au unaweza kuchukua dakika chache ndani ya siku kuondoa mrundikano, kwenye raki ya viatu tuseme vyako na vya watoto wako wadogo haikuchukui zaidi ya dakika 20 hasa kama haupotezi muda kwenye kufanya uamuzi.

5.  Anza Kuchambua
 Kuondoa mrundikano kunaanza sasa kwa kuchambua vitu eneo ulilochagua na kuviweka katika yale makundi manne. Fungu la vya kutupa/takataka unaweka vitu ambavyo wewe wala yeyote hatavitumia tena. Inapendeza pale vifaa vingi vinapotumbukia kwenye fungu hili. Fungu la vya kugawa au kuuza ni lile la vitu ambavyo hutavitumia tena nyumbani kwako lakini bado vina thamani. Kuwa makini usiweke vitu vingi kwenye fungu hili ambapo huenda ungevitazama kwa mara ya pili ni kwamba unavihitaji. Fungu la tatu ni la vitu wa kuhifadhi mbali. Hivi ni vile ambavyo hutumii mara kwa mara lakini kuna wakati unavitumia. Mfano mzuri ni kwenye nguo. Kuna majira mavazi ya baridi kama sweta yanahitajika sana na kuna majira ya joto ambapo huhitaji sweta. Kwahivyo unahifadhi mbali pindi unapohitaji unachukua na kutumia tena. Kwa kawaida fungu hili huwa ni dogo. Fungu la nne na la mwisho ni la vile vitu unavyotumia kila siku ambapo ndio vya kuhifadhi karibu. 

6.  Weka kila kitu panapostahili
Baada ya kufanikiwa kuchambua kila kitu kwenye fungu lake anza kuondoa na kutupa vile vya fungu hilo.Vitupe haraka sana ili usije ukabadili mawazo. Ule uamuzi wa mwanzo ndio uamuzi sahihi. Beba vitu vya kugawa au kuuza na vipeleke kunakostahili. Vile vya kuhifadhi mbali weka kwenye maboksi au mabegi na masanduku kwa ajili ya kuhifadhi. Na vya kutumika mara kwa mara vihifadhi vinapostahili kuwepo. Usipoteze muda kwani vitu vinaweza kujichanganya na ukashangaa unaanza kuchambua tena.  

7.  Furahia mafanikio yako
 Ni wakati wa kupiga picha na kutuma kwa wale unaowapenda ili wafurahi na wewe. Kaa na utazame hicho chumba ulichoondoa mrundikano. Umefanya kazi nzuri unahitaji muda wa kujipongeza.

8.  Anza tena
 Ukiwa umemaliza eneo moja unajipanga upya kwa ajili ya wakati mwingine na kuchagua tena chumba au eneo lingine na kufanya zoezi lilelile la mwazo. Sasa unakuwa umeshajua mbinu kwa hivyo inakuwa rahisi.

Vivi ni mshauri wa mapambo ya nyumba na bustani. Kwa maoni au maswali Piga/whatsapp 0755200023. Pia wewe msomaji wangu niandikie njia ambazo unatumia kuondoa mrundikano hapo nyumbani kwako. Huenda maelezo yako yakachapishwa kwenye makala zijazo!

No comments:

Post a Comment