Tuesday, June 9, 2015

Membe amesema hana undugu wa damu na JK

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, amekana kuwa na undugu wa damu na Rais Jakaya Kikwete.

Membe (62) ambaye
Juni 8 mwaka huu alitangaza nia ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) na kisha jana kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea kiti hicho, alisema ingawa amekuwa akifananishwa na Rais Kikwete mara kadhaa; hakuna ushahidi wowote wa kibailojia unaothibitisha kwamba wana uhusiano wa kindugu.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuchukuwa fomu hiyo kwenye makao makuu ya CCM mjini Dodoma jana, Membe alisema baadhi ya watu wamekuwa wakimfananisha na Rais Kikwete lakini hawana undugu wowote baina yao.

“Kungekuwa na aibu gani au hasara gani kuficha kwamba mimi ni ndugu wa damu wa Rais Jakaya Kikwete. Mimi siyo ndugu wa mheshimiwa Rais, lakini  binadamu tunafanana…rangi yangu, sura yangu na ufupi wangu nimeuchukua kwa mama yangu,” alisema Membe na kuongeza:

”Aliyekuwa Rais wa Malawi Bingu wa Mutharika (sasa marehemu) wakati fulani pia aliwahi kunifananisha na Rais Kikwete. Naomba nitamke wazi kwamba sina undugu wa damu na mheshimiwa Rais.” 

Alisema hali hiyo pia iliwahi kumkuta baada ya Wamarekani weusi (Afro Americans) kumkaribisha Marekani wengi walimuomba kupiga naye picha wakidhani ni Rais Kikwete lakini baadaye aliwaeleza ukweli kwamba yeye hakuwa Rais Kikwete.

Hadi kufikia jana mchana makada wa CCM waliotangaza nia ya kugombea nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama hicho na kisha kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa kuwania kiti hicho walifikia 20.

NIPASHE

No comments:

Post a Comment