Wednesday, June 10, 2015

WANAFUNZI WAANDIKA BARUA KUOMBA KUACHA SHULE...KISA IKO MBALI

Serikali ilianzisha mpango wa kujenga shule za sekondari za kata moja ya mikakati  ikiwa kupunguza adha ya umbali kwa wanafunzi na kusogeza huduma za elimu jirani na wananchi ili kila mtoto apate haki ya kupata elimu.

Pamoja na mpango huo kutekelezwa kwa asilimia kubwa, bado adha ya umbali wa shule kwa baadhi ya wanafunzi iko palepale, hali inayosababisha wanafunzi wengi kuacha masomo.

Shule ya Sekondari Shantamine katika Kata ya Mtakuja, Geita mjini ni miongoni mwa shule nyingi mkoani Geita  na maeneo mengi nchini ambayo bado  wanafunzi wana changamoto ya umbali wa kuifuata elimu au kurudi nyumbani.

Zaidi ya wanafunzi 27 wameacha masomo kwenye shule hiyo katika kipindi cha miezi mitano tangu kuanza kwa mwaka huu.
Taarifa zinaonyesha kuwa kati ya wanafunzi 200 walioanza kidato cha kwanza  katika shule hiyo, waliomaliza kidato cha nne mwaka jana ni wanafunzi 50.

Takwimu hizo zinamaanisha kwamba wanafunzi 150 waliacha shule huku sababu kubwa ikiainishwa kuwa ni umbali, pia mimba kwa wasichana.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ofisa Elimu wa Mkoa wa Geita, Eufransia Buchuma aliyoitoa mwaka 2013, wanafunzi 8,606 sawa na asilimia 50.2 kwa katika Mkoa wa Geita hawakumaliza kidato cha nne mwaka  huo kati ya wanafunzi  17,113 walioanza kidato cha kwanza mwaka 2010.

Mwalimu mkuu wa shule hiyo  Kakila Swillah anabainisha kwamba  tatizo hilo ni kubwa katika shule yake akieleza kuwa limesababisha wanafuzi wawili kuandika barua ya kuomba kuacha shule mwanzoni mwa mwezi Mei mwaka huu.

“Hii inaonyesha ni jinsi gani tatizo hilo ni kubwa. Nimekuwa mwalimu mkuu katika shule nyingi, lakini sijawahi kuona mwananfunzi kwa hiari yake mwenyewe anaomba kuacha masomo kwa kigezo cha umbali. Hili ni tatizo,”anasema mwalimu huyo.

MWANANCHI

No comments:

Post a Comment