Thursday, January 29, 2015

MAHUSIANO: Kwanini asimfunge kizazi?


‘Mume kanikimbia kisa nazaa sana’
“Sitasahau siku niliyokimbiwa na mume wangu baada ya kumzalia pacha kwa mara ya tatu mfululizo.” Hii ni kauli ya Salome Paul Mhando, mama wa watoto sita ambao ni pacha, aliowazaa kwa nyakati tofauti katika kipindi cha miaka sita iliyopita, wakipishana miaka miwili miwili.

Salome, alitelekezwa nyumbani na mumewe huyo baada ya kujifungua pacha kwa mara ya tatu, huku wakiwa hawana sehemu maalumu ya kuishi, achilia mbali njaa iliyotokana na umaskini wa kipato.
Baada ya kutelekezwa, msamaria mwema alijitolea kumhifadhi katika shamba lake lililopo eneo la Mabwepande nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, kabla ya kupata msaada wa nyumba ya kuishi.

Mama huyo anayekumbuka tukio hilo kwa uchungu, anasimulia kuwa mumewe aliyemtaja kwa jina moja la Ali, alimtoroka saa saba mchana na kumwacha akiwa na pacha hao.
Anabainisha kuwa tukio hilo lilitokea baada ya familia hiyo kukaa na njaa kwa siku kadhaa kutokana na umaskini wa kipato.

“Siku hiyo, ambayo tarehe yake siikumbuki, mume wangu alirudi nyumbani akiwa tena hana chakula na kunieleza kuwa anaumwa. Nilipomwuuliza sasa tunafanyaje kuhusu chakula, alitoka nje,” anaeleza mama huyo na kuendelea:
“Nikaamua kumfuata na kuanza kumsema nikimdai chakula. Baadaye (mumewe) akaniuliza mbona unanisema? Mimi nikamjibu; naulizia masuala ya chakula, tunafanyaje leo? Akasema; basi niache naenda kukitafuta.”
Salome anaeleza kuwa kinyume na ahadi hiyo, tangu wakati huo alipoondoka hajaonekana nyumbani hadi sasa. “Niliamua kwenda kulala, lakini nikiwa na wasiwasi kuhusu usalama wake. Nikapatwa na hofu nikijiuliza; nini kimempata mwenzangu na kuanza kuwapigia simu ndugu zake ambao pia hawakupatikana.”

Salome anasema jitihada za kuwatafuta ndugu wa mumewe ziligonga mwamba na hadi sasa hana mawasiliano yoyote na familia hiyo ya mumewe.
Anaeleza kuwa kutokana na mumewe huyo kutorudi tena nyumbani, alilazimika kwenda kwenye vyombo vya habari kuomba msaada wa malezi ya watoto hao.
“Nilikwenda kwanza ITV ambako mbali na kunisaidia katika mahitaji ya msingi ya chakula, walinitangaza pia kwenye luninga kuwa ninahitaji msaada na tukio hilo ndilo limenisaidia kupata msaada wa kudumu.

Hali ikoje?
Salome anahusisha kutoroka nyumbani kwa mumewe na ugumu wa maisha unaoikabili familia hiyo.
“Nina watoto pacha sita; wawili wana umri wa miaka sita, wawili wengine wana umri wa miaka minne na wawili wa mwisho wana umri wa miezi 12. Nasikitika kukimbiwa na mume kwa sababu ya ugumu wa maisha, lakini zaidi akidai kuwa ninazaa sana. Maisha ni magumu na ninashukuru kwa misaada ninayoendelea kuipata kutoka kwa jamii, hasa kupatiwa msaada wa nyumba ya kuishi na wanangu,” anasema.

Akifafanua kuhusu ugumu wa maisha, Salome anasema ameshindwa hata kuwapeleka shule watoto wake wakubwa... “Hakuna anayesoma, wote bado wako nyumbani.”

Msaada wa nyumba
Hata hivyo, ugumu wa maisha wa Salome umeigusa Benki ya Covenant ya jijini Dar es Salaam, ambayo imejitokeza kumnunulia nyumba ya kuishi na watoto hao eneo la Mabwepande.

Mkurugenzi mtendaji wa benki hiyo, Sabetha Mwambenja anasema mbali na msaada huo, anatamani kuona mume huyo aliyemtelekeza anapatikana na kuchukuliwa hatua za kisheria.
Anasema benki yake ilitambua mahitaji ya mama huyo kupitia vyombo vya habari na kuamua kumpa msaada wa kumnunulia nyumba ya kuishi yenye thamani ya Sh25 milioni, ambayo alikabidhiwa juzi.

“Tumemkabidhi, nyumba, tukamnunulia magodoro, vitanda vinne, mashuka na taa za sola na familia nzima tumeikatia bima ya afya itakayowawezesha kutibiwa katika hospitali yoyote inayotoa huduma kupitia bima hiyo,” anaeleza mkurugenzi huyo.

“Sisi hatuna kitengo wala idara inayojishughulisha na matatizo ya jamii, tumeguswa tu na tatizo la mama huyo aliyekimbiwa na mumewe sababu ya kumzalia pacha. Natoa wito kwa benki nyingine na wadau mbalimbali wa maendeleo kuguswa na matatizo ya jamii inayowazunguka na kusaidia pale inapowezekana,” anasema.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa benki hiyo, Balozi Salome Sijaona anasema baada ya kuona mateso aliyokuwa akiyapata mwanamke huyo kwa kukosa makazi, chakula na mahitaji mengine ya kibinaadamu, waliona ni vyema kujitolea kumsaidia ikiwa ni moja ya kutimiza majukumu yake kwa jamii.

“Tumeguswa na mateso aliyokuwa akipata Salome Mhando, yeye pamoja na watoto wake, baada ya kutelekezwa na mumewe kwa kigezo ha kuzaa watoto pacha mfululizo. Tuliguswa na kuamua kujitolea kumnunulia nyumba ambayo ataimiliki mwenyewe,” anasema Balozi Sijaona na kuongeza:
“Nyumba hii tumemkabidhi pamoja na samani za ndani ambazo sasa zitamwezesha kuishi maisha ya amani na furaha akiwa kama wanawake wengine na kufurahi pamoja na watoto wake.”

Shukrani
“Ninaishukuru Benki ya Covenant kuniwezesha kumiliki nyumba yangu, ninawashukuru na ninaomba waendelee na moyo huo wa kuwasaidia kina mama wenye matatizo kama haya kwa sababu siko peke yangu,” alisema Salome na kuongeza:

“Kina mama tumekuwa na wakati mgumu katika ndoa zetu hususan katika masuala ya uzazi. Ninawashukuru watu wote ambao walijitolea kunisaidia chakula na nguo katika wakati wote nilipokuwa sina sehemu maalumu ya kukaa, hadi sasa ninamiliki nyumba yangu.”

No comments:

Post a Comment