Thursday, January 22, 2015

MY ARTICLE FOR NEWSPAPER: Amri 10 za kuweka mpangilio wa vitu mahali unapoishi

worth reading again and again

Umeshawahi kutamani kuona kwa haraka kile unachokitafuta? Je vitu vyako mara kwa mara viko hovyo hovyo vimesambaa kila mahali? Kama ndivyo basi, jifunze jinsi ya kuweka mpangilio wa vitu nyumbani kwako kwa kusoma amri hizi kumi tunavoelekezwa na mjasiriamali na mbunifu wa ndani Bi Alma Said.

1. Weka vitu vinavyofanana pamoja. “Unapopangilia vitu vyako weka vinavyoendana pamoja ili kuleta mtiririko na mantiki. Kwahivyo acha kuweka chochote popote, inaweza kusaidia ndani ya muda mfupi lakini ikafanya eneo lote lionekane mvurugano.

2. Fikiria kabla ya kununua. Kununua kwa mhemko ni kifo cha mpangilio wowote. Unataka kununua kitu? Kinahitaji makazi. Kuwa na uhakika na mpangilio wako kabla hujaleta chochote kipya nyumbani kwako. Inasikika kama msongo eeh? Ndio, panga kabla ya kununua: hiki kitakaa wapi? Je una nafasi, kama majibu ni sijui na hapana  basi acha usinunue (jumlisha na kuwa utakuwa umehifadhi hela yako).

3. Kila kitu kina mahali pake, kiweke hapo. Kwa lugha nyingine ni kuwa na eneo kwa kila kitu. Zaidi ya kuweka vitu mahali pake ni kuwa pia kila kitu kinatakiwa kiwe na mahali pake kabla hujakiweka hapo!

Eneo kwa kila kitu kwa mfano ufuatao, eneo la:
Hiyo kalamu wakati ambapo huiandikii.
Waya za kuchaji kamera na simu wakati ambapo hazitumiki.
Barua ambazo hazijasomwa.
Soksi ambayo mwenzake haonekani anasubiriwa kutafutwa.
Vipeperushi na magazeti ambayo utasoma utakapopata muda, na vitu vingine vingi vingi hapo nyumbani.
Unataka kufahamu ni vitu gani hapo nyumbani vinahitaji eneo lake maalum? Anza kwa kutizama kwenye kaunta yako ya jiko. Kama kuna chombo kipokipo tu ni kwa sababu hujakitafutia eneo maalum.

4. Zishukuru kumbukumbu zako halafu ziage. Hapana, sikushauri ulitose hilo gauni lako la harusi. Kumbukumbu nyingine ni muhimu mno na zinahitaji eneo kwenye nyumba yako maisha (wengine hadi wanazikwa na magauni yao ya harusi). Lakini hizo CD na mikannda ya filamu? Fikiria mara mbili kabla hujabaki na hiyo kumbukumbu unayotaka kuhifadhi maisha.

5. Weka nguo zako mbali. Ndio najua unaguna, lakini fanya hivyo, hakuna msamaha kwa hili. Nguo sio za kuwepo kila mahali. Tundika zilizo safi, kunja za kukunja, fua zinazotakiwa kufuliwa na loweka za kuloweka. Mwisho wa hadithi. Mrundikano wa nguo ni janga la nyumba nyingi. Kutumia muda mchache kila siku kushughulikia swala la kuweka nguo panapotakiwa  itafanya mahali unapoishi paonekane nadhifu na hivyo kurahisisha maisha yako kwa muda mrefu.

6. Tumia vikontena vilivyopo kwa lengo lingine pindi vimalizapo lengo moja. Kwa maana nyingine ni kuwa tumia kile ambacho tayari unacho. Nimeona watu wanaotumia vikopo vilivyoisha biskuti ama chokoleti kwa ajili ya kuhifadhia vitu kama hereni na vipodozi.

7. Weka kituo cha amri . Manake ni kwamba kituo hiki ndicho kinachokaa vile vitu kama funguo, mifuko, yani vile vitu ambavyo vinatumika mara kwa mara kwenye pilika za kila siku. Hutakuwa na haja ya kutafuta ama kuanza kuuliza kama utakuwa na kituo cha amri nyumbani kwako.

8. Weka ratiba ya siku. Na hakikisha unaifuata. Ratiba ni uti wa mgongo wa mipangilio. Hakikisha kila siku unatenga muda wa kurudisha vitu pale vinapotakiwa kuwa, faili ripoti za watoto za shule na karatasi nyingine muhimu, tandika kitanda na kadhalika ni kuwa nyumba yako itakushukuru. Kumalizia siku na nyumba yenye mpangilio ni kweli kuwa unajisikia vizuri ajabu.

9. Anza kidogo kidogo. Kama huna karama ya kuweka vitu kwenye mpangilio anza kidogokidogo na vitu vidogodogo kama vile hicho kituo cha funguo, taratibu utashika kasi na kufika hadi kwenye kabati za nguo. Furahia kimpangilio kidogo unachoanzia ambapo kitakupa stamina ya kusonga mbele.

10. Usichoke. "Kumbuka kuwa wewe ndio msimamizi wa nyumba na vitu vyako. Kama utaiambia akili yako nataka kuishi mahali penye mpangilio, muda si muda haitajisikia kuchoka. Umesongwa? Sawa, chukua mapumziko kidogo.

Sasa msomaji wangu umeelimishwa juu ya amri kumi za kuweka mpangilio wa vitu nyumbani, je wewe ni mmojawapo wa wale wenye vitu ambavyo havina makao bado? Niandikie ukinijulisha ni kwa namna gani umefaidika na makala hii kwa kuvipa eneo vitu hivyo leo!


Makala hii imeandaliwa na Vivi Machange ambaye ana mapenzi makubwa ya muonekano wa nyumba. Kwa maoni au maswali tuma kwenda 0755 200023 au christines.daughter@yahoo.com

No comments:

Post a Comment