Thursday, May 21, 2015

Mbunge Amjia juu DC Kuhusu Sakata la Wanawake wa Rombo Kukodi Wanaume toka Kenya ili Wafanye nao Mapenzi....Amesema Kauli Imewadhalilisha na Ambao Hawahusiki

Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini amewajia juu Mkuu wa Wilaya ya Rombo, Lemrise Kipuyo na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya hiyo, Anthony Tesha akiwataka wajiuzulu nyadhifa zao kwa kushindwa kusimamia sheria wilayani humo.

Selasini alitoa kauli hiyo
jana alipokuwa akizungumzia taarifa ya wanawake wa Rombo inayodai kwamba wanakodi wanaume kutoka Kenya ili wafanye nao tendo la ndoa.

Juzi, gazeti hili liliripoti habari iliyomkariri Mkuu wa Wilaya kuwa baadhi ya wanawake wilayani humo, hukodi wanaume kutoka Kenya kwa ajili ya kufanya nao tendo la ndoa baada ya waume zao kupoteza nguvu kutokana na ulevi.

Eneo ambalo limeathirika zaidi na unywaji wa pombe haramu na zinazotengenezwa kiholela bila viwango ni la Kikelelwa lililopo mpakani mwa Kenya na Tanzania.

Taarifa hiyo ilimnukuu Kipuyo wakati wa ufunguzi wa kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo na kuitaja Kikelelwa kama eneo linalohitaji kutazamwa kwa jicho la pekee.

“Imefikia mahali wanaume wengi wanashindwa kumudu kufanya tendo la ndoa na kuwalazimu wanawake wao kukodi wanaume kutoka nchi jirani ya Kenya kwa ajili ya tendo hilo,” alisema Kipuyo.

Kauli hiyo iliungwa mkono na baadhi ya wanawake waliozungumza mbele ya mkuu huyo wa wilaya katika operesheni ya kukamata pombe haramu ya gongo kijijini hapo iliyofanyika wiki mbili zilizopita.

Jana, Selasini alikanusha vikali taarifa hizo akidai kuwa siyo sahihi kuwajumuisha wanaume wote wa jimbo lake na ulevi huo au wanawake wote.

“Hiyo kauli haina utafiti wala haijaonyesha ni wanaume wangapi Rombo wana tatizo hilo au ni wanawake wangapi waume zao wana shida hiyo. Siyo sahihi kutoa kauli ya jumla,” alisema.

Alisema, “Haiwezekani mtu mmoja aliyehojiwa akawakilisha wanaume au wanawake wenye matatizo hayo. Kauli hiyo imewadhalilisha wanaume na wanawake ambao hawahusiki na tatizo hilo.”

“DC ndiye mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama aliyepaswa kusimamia sheria. Mwenyekiti wa halmashauri, naye anawajibika. Kama wameshindwa kazi waachie ngazi.

“Siungi mkono unywaji holela wa pombe ambazo hazina viwango vya TBS. Kama kuna mtu ana tatizo la tendo la ndoa ajitokeza tumjue. Hili jambo limenifanya nipokea simu nyingi sana,” alilalamika Selasini.
Selasini alisema inawezekana hakuna mwananchi wake mwenye tatizo hilo kwa vile hakuna utafiti wala majina ya waathirika na alimtaka Kipuyo kuomba radhi kwa kauli yake hiyo.

Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama naye aliwahi kutoa kauli inayofanana na ya Kipuyo aliposema wapo baadhi ya wanandoa wilayani humo wanalala “mzungu wa nne”.

MWANANCHI

No comments:

Post a Comment