Monday, May 18, 2015

Mfanyabiashara Maarufu Adaiwa Kutapeli Tanzanite

MFANYABIASHARA maarufu wa madini ya Tanzanite, mkazi wa Arusha, Eliakimu Daud Molle (45), amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha akikabiliwa na shtaka la kutapeli na kujipatia madini yenye thamani ya sh. milioni 15 kwa njia ya udanganyifu.

Mshtakiwa alifikishwa mahakamani
hapo mwishoni mwa wiki iliyopita mbele ya hakimu, Nestory Baro ambapo Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Gaudencia Lyimo, aliieleza mahakama hiyo kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Januari 4, mwaka huu, katika Jengo la Ottu.

Alisema mshtakiwa alijipatia madini ya Tanzanite kutoka kwa mlalamikaji, Banai Shininu yenye thamani kiasi hicho baada ya
kumrubuni kuwa ampatie ili akayauze kwa sh. milioni 15 lakini hakufanya hivyo badala yake alitoweka kusikojulikana.

Aliongeza kuwa, mshtakiwa alikuwa akitafutwa muda mrefu na mlalamikaji ambapo anapopatikana, hutoa ahadi za uongo kuwa angelipa fedha hizo lakini hakufanya hivyo hadi alipokamatwa na kufikishwa mahakamani.

Baada ya kusomewa shtaka hilo, mshtakiwa alikana ambapo Baro alisema dhamana ipo wazi kwa masharti ya kuwa na fedha taslimu sh. milioni 7.5 na wadhamini wawili lakini mshtakiwa alishindwa kuyatimiza na kupelekwa gerezani.

Kesi hiyo namba 88 ya mwaka huu, imepangwa kutajwa tena mahakamani hapo Mei 26, mwaka huu.
MAJIRA

PICHA: MITANDAONI

No comments:

Post a Comment