Sunday, May 24, 2015

Zitto amechukua fomu za kugombea ubunge Kigoma Mjini....Amesema ameshatimiza kila kitu Kigoma Kaskazini kwa hivyo haoni sababu za kuwawakilisha tena

Safari ya mbunge wa zamani wa Kigoma Kaskazini kwa tiketi ya Chadema, Zitto Kabwe kurejea bungeni imeanza rasmi baada ya kiongozi huyo wa chama kipya cha ACT-Wazalendo kuchukua fomu za kuwania kuongoza jimbo la Kigoma Mjini.

Uamuzi huo wa kulitaka jimbo
hilo unathibitisha kauli zake ambazo amekuwa akizitoa kwa muda mrefu kuwa hatarudi tena Kigoma Kaskazini kwa kuwa alishawatimizia kila kitu na haoni sababu za kuwawakilisha tena wananchi wa eneo hilo.

Kauli yake iliibua ubashiri kuwa Zitto anataka kubadilishana jimbo na mbunge wa Kigoma Mjini (CCM), Peter Serukamba, uvumi ambao aliukanusha akisema hadhani kama CCM inaweza kupata jimbo Kigoma.
Zitto, ambaye alijiondoa Chadema baada ya kukiuka katiba kwa kufungua mashtaka dhidi ya chama hicho, hakufanya mbwembwe wakati akienda kuchukua fomu kwenye ofisi za ACT Ujiji jana, badala yake aliita viongozi wa kata na matawi bila ya kutaarifu vyombo vya habari.

“Nimeamua kugombea ubunge wa Kigoma Mjini ili niwatumikie ndugu zangu ambao wamekuwa wakipata tabu katika kupigania haki zao za msingi ambazo walistahili kuzipata kama ilivyo katika mikoa mingine,” alisema Zitto alipoongea na mwandishi wa Mwananchi kwa simu.

“Nitakapokuwa mbunge wa Kigoma Mjini nitahakikisha barabara za mitaani zinapitika katika kipindi chote cha mwaka, nitahakikisha watu wanaacha tabia ya kulima mashamba katikati ya mitaa na makazi, lakini nitahakikisha kila mmoja anajiunga na mifuko ya kijamii ili kujiwekea akiba ya uzeeni pamoja na kupata huduma ya matibabu, elimu na nyinginezo zinazopatikana kwa kutumia mifuko hiyo.”

Mwenyekiti huyo wa zamani wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), alisema bonde la Mto Luiche bado halijatumika ipasavyo kuzalisha chakula kwa wingi.

“Nakusudia kuibana Serikali ijenge skimu ya umwagiliaji maji ili wakulima walime kilimo cha mpunga kwa mwaka mzima bila kupumzika, jambo ambalo litainua uchumi wa wakulima na kuongeza chakula hapa Kigoma,” alisema.

Kuhusu umeme wa gridi ya Taifa, Zitto alisema lazima upatikane ili kusaidia jitihada ya ujenzi wa viwanda vya kusindika mazao ya uvuvi na kilimo kwa kuwa hivi sasa mji wa Kigoma Ujiji unategemea umeme wa jenereta ambao hauwezi kuendesha shughuli za viwanda, hali inayochangia mkoa kuendelea kuwa masikini licha ya kuzungukwa na rasilimali nyingi.

Katibu wa ACT wa Jimbo la Kigoma Mjini, Azizi Ally alisema Zitto alichukua fomu hiyo jana kwa malipo ya Sh100,000 mbele ya viongozi 72 wa kata na matawi kutoka jimboni humo.

“Kwa hali ya sasa Kigoma Mjini inahitaji kupata mbunge anayeweza kufuatilia mambo kwa kina ili kuleta maendeleo ya wananchi baadala ya yule anayekwenda bungeni kujifunza,” alisema Ally.

AFRICANJAM

No comments:

Post a Comment